Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je! Farao kwa kweli alimwoa Sara, mke wa Abrahamu, kama ionekanavyo kutokana na fasiri ya Mwanzo 12:19 katika tafsiri fulani za Biblia?
La, Farao alizuiwa asimtwae Sara (Sarai) kuwa mke wake. Kwa hiyo, heshima na fahari ya Sara haikuharibiwa.
Tunasaidiwa kuona hilo kwa kuchunguza hali hiyo katika muktadha yayo. Hali ya njaa ilimlazimu Abrahamu (Abramu) atafute kimbilio katika Misri kwa muda fulani. Alihofu kwamba uhai wake ungekuwa hatarini huko kwa sababu ya mke wake Sara, mwenye kupendeza. Abrahamu bado hakuwa amezaa mwana kupitia Sara, kwa hiyo ikiwa angekufa Misri, nasaba ya Mbegu ingevunjika, Mbegu ambayo kupitia hiyo familia zote za dunia zingebarikiwa. (Mwanzo 12:1-3) Kwa hiyo Abrahamu alimwamuru Sara ajitambulishe mwenyewe kuwa dada yake, kwani kwa hakika Sara alikuwa dada-nusu yake.—Mwanzo 12:10-13; 20:12.
Hofu yake haikuwa bila msingi. Mwanachuo August Knobel alieleza hivi: “Abramu alimwomba Sarai ajijulishe mwenyewe kuwa dada yake katika Misri ili [Abramu] asiweze kuuawa. Ikiwa Sara angalionwa kuwa mwanamke aliyeolewa, Mmisri angaliweza kumtwaa tu kwa kumwua mumewe na mwenye kummiliki; ikiwa angalionwa kuwa dada yake, kulikuwa uwezekano wa kumtwaa kutoka kwa ndugu yake kwa njia za urafiki.”
Hata hivyo, wana-wafalme Wamisri hawakufanya mapatano yeyote pamoja na Abrahamu ili Farao amwoe Sara. Walimleta Sara mwenye kupendeza ndani ya nyumba ya Farao tu, na mtawala wa Misri akampa zawadi Abrahamu, aliyedhaniwa kuwa ndugu yake. Lakini baada ya hilo, Yehova aliipiga nyumba ya Farao mapigo. Hali ya kweli ilipofunuliwa kwa Farao katika njia isiyotajwa, alimwambia Abrahamu hivi: “Mbona ulisema, Huyu ni umbu langu [dada yangu, NW] hata nikamtwaa [nikawa karibu kumtwaa, NW] kuwa mke wangu? Basi sasa, huyo mke wako umchukue, uende zako”!—Mwanzo 12:14-19.
Union Version na tafsiri nyinginezo za Biblia hufasiri sehemu hiyo ya italiki iliyo juu ya mstari huo “hata nikamtwaa kuwa mke wangu” au katika maneno kama hayo. Hata ingawa si fasiri isiyo sahihi, mpangilio wa maneno kama huo waweza kutoa maana kwamba Farao alikuwa kwa kweli amemwoa Sara, kwamba ndoa hiyo ilikuwa uhakika uliotimizwa. Yaweza kuonwa kwamba kwenye Mwanzo 12:19 kitenzi cha Kiebrania kinachofasiriwa “kumtwaa” kimo katika hali ya kutokamilika, inayoonyesha kitendo ambacho hakijamalizika bado. New World Translation hufasiri kitenzi hicho cha Kiebrania kupatana na muktadha na katika njia inayoonyesha wazi hali ya kitenzi hicho—“hata nikawa karibu kumtwaa awe mke wangu.”a Ingawa Farao alikuwa “karibu kumtwaa” Sara awe mke wake, hakuwa bado amemaliza taratibu au sherehe zozote zilizohusika.
Abrahamu amechambuliwa mara nyingi kwa ajili ya jinsi alivyoshughulikia jambo hilo, lakini yeye alitenda kwa ajili ya masilahi ya Mbegu iliyoahidiwa na hivyo kwa ajili ya ainabinadamu yote.—Mwanzo 3:15; 22:17, 18; Wagalatia 3:16.
Kwenye pindi kama hiyo iliyoelekea kuwa yenye hatari, Isaka alimwamuru mke wake, Rebeka, aepuke kuijulisha hali yake ya ndoa. Kwa wakati huo mwana wao Yakobo, ambaye kupitia yeye nasaba ya Mbegu ingekuja, alikuwa tayari amezaliwa na kwa wazi alikuwa mwanamume kijana. (Mwanzo 25:20-27; 26:1-11) Hata hivyo, kusudi la kitendo hicho cha unyofu lingaliweza vilevile kuwa sawa na la Abrahamu. Wakati wa njaa Isaka na familia yake walikuwa wakiishi katika eneo la mfalme Mfilisti aliyeitwa Abimeleki. Ikiwa angetambua kwamba Rebeka alikuwa ameolewa na Isaka, Abimeleki labda angalifuata mwendo wa uuaji dhidi ya sehemu yote nyingine ya familia ya Isaka, ambao ungalimaanisha kifo kwa Yakobo. Katika kisa hicho pia, Yehova aliingilia kulinda watumishi wake na nasaba ya Mbegu.
[Maelezo ya Chini]
a Tafsiri ya J. B. Rotherham husomeka hivi: “Mbona ulisema, Yeye ni dada yangu; na kwa hiyo nikawa karibu kumtwaa awe mke wangu?”