Juma Lililobadili Ulimwengu
“Ndiye mbarikiwa, yeye ajaye kwa jina la Bwana [Yehova, NW]”!—MATHAYO 21:9.
1. Ni vikundi gani viwili tofauti vilivyoathiriwa na matukio ya Agosti uliopita?
“SIKU TATU ZENYE KUTAABISHA SANA ZILIZOUTIKISA ULIMWENGU.” Katika Agosti 1991, vichwa vikuu vya habari vya jinsi hiyo vilikazia ukweli wa kwamba ulimwengu waweza kuingia hali ya mchafuko katika siku chache tu. Kwa kweli, siku za mwisho mwisho za Agosti zilikuwa zenye matukio mengi sana si kwa ulimwengu tu bali pia kwa kikundi ambacho kukihusu Yesu alisema: “Wao si sehemu ya ulimwengu.” Kikundi hicho kinajulikana leo kuwa Mashahidi wa Yehova.—Yohana 17:14, NW.
2, 3. (a) Uhuru ulitokezwaje katika Zagreb ingawa kulikuwako hatari ya vita? (b) Imani yenye nguvu ilithawabishwaje katika Odessa?
2 Mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova wa kwanza kabisa kupangwa kwa ajili ya Yugoslavia ulikuwa umeratibiwa kuanza Agosti 16 hadi 18. Vilevile, huo ungekuwa pia mkusanyiko mkubwa wa kwanza wa watu wa Yehova wenye kufanywa katika taifa lililokaribia kuwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe. Mashahidi wa mahali hapo, pamoja na wenye kujitolea kutoka nchi za jirani, walikuwa wamefanya kazi ngumu kwa miezi miwili ili kutengeneza upya uwanja wa kandanda wa HAŠK Građanski katika Zagreb. Ulikuwa safi kabisa, mahali palipofaa kwa ajili ya ule Mkusanyiko “Wapendao Uhuru wa Kimungu.” Maelfu ya wakusanyikaji wa kimataifa walipanga kuhudhuria, kutia na 600 kutoka United States. Hatari ya vita ya wenyewe kwa wenyewe ilipotisha, ilisemekana kwamba: “Waamerika hawatakuja kamwe.” Lakini walikuja, pamoja na wakusanyikaji kutoka nchi nyinginezo nyingi. Hudhurio la 10,000 lilikuwa limetazamiwa, lakini 14,684 walikuwako katika uwanja huo kwenye siku ya mwisho! Wote walibarikiwa sana kwa sababu ‘hawakuacha kukusanyika pamoja.’—Waebrania 10:25.
3 Katika siku tatu zilizofuata mkusanyiko huo wa Zagreb, mapinduzi yasiyofanikiwa yalitokea katika Urusi. Wakati huo, wapendao uhuru wa kimungu walikuwa wakifanya matayarisho ya mwisho mwisho kwa ajili ya mkusanyiko wao huko Odessa katika Ukrainia. Je! mkusanyiko huo ungeweza kufanywa? Wakiwa na imani yenye nguvu akina ndugu walimaliza mambo madogo-madogo ya mwisho ili kukamilisha kazi ya kutengeneza upya uwanja wa michezo, na wakusanyikaji wakaendelea kuja. Kana kwamba kwa muujiza, mapinduzi hayo yaliisha. Mkusanyiko wenye kupendeza ulifanywa Agosti 24, 25, kukiwa na 12,115 waliohudhuria na 1,943—asilimia 16 ya kilele cha hudhurio—wakibatizwa! Mashahidi hao wapya, pamoja na washika uaminifu wa kimaadili wa wakati mrefu, walishangilia kwamba walikuwa wamekuja kwenye mkusanyiko huo wakimtumaini Yehova kikamili.—Mithali 3:5, 6.
4. Mashahidi katika Ulaya Mashariki wamekuwa wakifuata kiolezo gani kilichowekwa na Yesu?
4 Mashahidi hao waaminifu walikuwa wanafuata kiolezo kilichowekwa na Kielelezo chetu, Yesu Kristo. Yeye hakuacha kamwe kuhudhuria zile sikukuu zilizoamriwa na Yehova, hata wakati Wayahudi walipokuwa wakitafuta kumwua. Alipokuwa akija Yerusalemu ili kuhudhuria Sikukuu ya Kupitwa yake ya mwisho, hao walikuwa wamesimama kotekote hekaluni, wakiuliza: “Mwaonaje? Haji kabisa sikukuu hii?” (Yohana 11:56) Lakini alikuja! Hilo lilitayarishia njia juma lililofikia upeo walo katika kubadili mwendo wa historia ya kibinadamu. Je! tupitie sasa baadhi ya mambo makuu ya juma hilo—Nisani 8 hadi 14 kwenye kalenda ya Kiyahudi?
Nisani 8
5. Yesu alitambua nini aliposafiri kwenda Bethania katika Nisani 8, 33 W.K.?
5 Siku hiyo Yesu na wanafunzi wake wawasili Bethania. Hapo, Yesu atatumia masiku sita kwenye nyumba ya rafiki yake mpendwa Lazaro, ambaye amefufua hivi karibuni kutoka wafu. Bethania uko karibu na Yerusalemu. Kwa faragha, Yesu tayari amewashauri wanafunzi wake hivi: “Angalieni, tunapanda kwenda Yerusalemu; na Mwana wa Adamu atatiwa mikononi mwa wakuu na makuhani na waandishi; nao watamhukumu afe; kisha watampeleka kwa Mataifa wapate kumdhihaki, na kumpiga mijeledi, na kumsulibisha [kumtundika, NW] na siku ya tatu atafufuka.” (Mathayo 20:18, 19) Yesu atambua kikamili kwamba ni lazima sasa akabili majaribu yenye kuumiza sana. Hata hivyo, wakati huo wa kujaribiwa sana unapokaribia, ajitahidi sana katika kutumikia ndugu zake. Na sikuzote tuwe na “nia iyo hiyo . . . ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 2:1-5; 1 Yohana 3:16.
Nisani 9
6. Katika jioni ya Nisani 9, Mariamu alifanya nini, na Yesu alimwambia Yuda nini?
6 Baada ya mshuko-jua, Nisani 9 ianzapo, Yesu afurahia mlo kwenye nyumba ya Simoni aliyekuwa mwenye ukoma. Ni hapo ambapo Mariamu dadake Lazaro amimina mafuta yenye marashi ya thamani kubwa sana kwenye kichwa na miguu ya Yesu na kupangusa miguu yake kwa unyenyekevu kwa nywele zake. Yuda anapopinga, Yesu asema: “Mwache aiweke kwa siku ya maziko yangu.” Wakisikia kwamba wengi wa Wayahudi wanaenda Bethania na kutia imani katika Yesu, wakuu wa makuhani wanafanya njama kumwua yeye na Lazaro pia.—Yohana 12:1-7.
7. Katika asubuhi ya Nisani 9, jina la Yehova liliheshimiwaje, na Yesu alitabiri nini?
7 Asubuhi mapema, Yesu afunga safari ya kwenda Yerusalemu. Umati waenda kumlaki, ukipunga matawi ya mitende na kupaaza sauti: “Hosana! Ndiye mbarikiwa ajaye kwa jina la Bwana [Yehova, NW], Mfalme wa Israeli!” Kisha Yesu atimiza unabii wa Zekaria 9:9 kwa kwenda jijini akiwa amepanda punda. Akaribiapo Yerusalemu, yeye alililia, akitabiri kwamba Warumi watalizunguka kwa kujenga boma na kuliharibu kabisa—unabii ambao ungekuwa na utimizo wenye kutokeza miaka 37 baadaye. (Hilo pia lawa ishara ya mambo mabaya kwa Jumuiya ya Wakristo, ambayo imeasi-imani kwa kufuata kiolezo cha Yerusalemu ya kale.) Viongozi Wayahudi hawamtaki Yesu kuwa mfalme wao. Kwa hasira wanasema kwa mshangao: “Tazameni, ulimwengu umekwenda nyuma yake.”—Yohana 12:13, 19.
Nisani 10
8. Katika Nisani 10, Yesu alionyeshaje staha yenye kina kwa ajili ya nyumba ya Yehova ya sala, na ni jambo gani lililofuata?
8 Yesu azuru hekalu tena. Kwa mara ya pili, awatupa nje wafanya biashara wenye pupa na wenye kubadili fedha. Ubiashara—“kupenda fedha”—haupasi kuenea katika nyumba ya Yehova ya sala! (1 Timotheo 6:9, 10) Yesu akaribia kufa. Asema juu ya upandaji wa mbegu ili kutoa kielezi cha hilo. Mbegu ya kwanza hufaa, lakini humea kutokeza bua linalozaa wingi wa nafaka. Vivyo hivyo, kifo cha Yesu kitatokeza uhai wa milele kwa wengi wanaozoea imani katika yeye. Akisumbuliwa na wazo la kifo chake kinachokaribia, Yesu asali kwamba jina la Baba yake liweze kutukuzwa. Kwa kuitikia, sauti ya Mungu inanguruma kutoka mbinguni kwa wote waliopo kusikia: “Nimelitukuza, nami nitalitukuza tena.”—Yohana 12:27, 28.
Nisani 11—Siku Yenye Utendaji
9. (a) Mchana mapema katika Nisani 11, Yesu alitumiaje vielezi katika kuwalaumu Wayahudi waasi-imani? (b) Kupatana na mfano wa Yesu, ni nani ambao wamepoteza nafasi tukufu?
9 Yesu na wanafunzi wake waondoka Bethania tena kuanza siku yenye utendaji mwingi. Yesu atumia vielezi vitatu kuonyesha ni kwa nini Uyahudi wenye kuasi-imani walaumiwa. Njiani, alaani mtini usiozaa matunda na hivyo kuonyesha kulaumu kwake taifa la Kiyahudi lisilo jaminifu, ambalo halizai matunda. Aingiapo hekaluni, aeleza jinsi walimaji wasiostahili wa shamba la mizabibu la bwana-mkubwa mmoja wanavyomwua hatimaye hata mwana na mrithi wa bwana-mkubwa huyo—kufananisha usaliti wa tumaini la Wayahudi kwa Yehova, utakaofikia upeo katika kumwua kwao Yesu. Aeleza juu ya karamu ya arusi iliyopangwa na mfalme mmoja—Yehova—ambaye wageni wake walioalikwa (Wayahudi) watoa udhuru ili wasihudhurie. Kwa hiyo, mwaliko huo watolewa kwa watu wa nje—Wasio Wayahudi—wengine kati yao wakiitikia. Lakini mwanamume mmoja anayepatikana kuwa hana vazi la arusi atupwa nje. Yeye awakilisha Wakristo bandia wa Jumuiya ya Wakristo. Wayahudi wengi wa siku ya Yesu walialikwa ‘bali wachache wateuliwa’ kuwa miongoni mwa wale 144,000 waliotiwa muhuri wanaourithi ule Ufalme wa kimbingu.—Mathayo 22:14; Ufunuo 7:4.
10-12. (a) Ni kwa nini Yesu aliwakemea makasisi Wayahudi, na ni shutumu gani kali alilotoa juu ya wanafiki hao? (b) Hukumu ilitekelezwaje hatimaye juu ya Uyahudi wenye kuasi-imani?
10 Makasisi Wayahudi wanafiki watafuta pindi ya kumkamata Yesu, lakini ajibu baadhi ya maswali yao ya hila na kuwashinda mbele ya watu. Aaah, hao Wayahudi wa kidini waasi-imani! Yesu awakemea waziwazi kama nini! Wanatamani umashuhuri, mavazi ya kuwapambanua, na vyeo vyenye utukufu mwingi, kama vile “Rabi” na “Baba,” sawa na makasisi wengi katika siku yetu. Yesu ataarifu kanuni hii: “Ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa.”—Mathayo 23:12.
11 Yesu kwa ukali ashutumu hao viongozi wa kidini. Mara saba asema kwa mshangao: “Ole wenu”! akiwaita viongozi vipofu na wanafiki. Na kila mara atoa sababu ya wazi ya lawama hilo. Wao wanazuia njia ya kuingia Ufalme wa mbinguni. Wanapomnasa mwongofu, yeye awa mwana wa Gehena mara mbili zaidi, yaelekea akiwa tayari miongoni mwa wale watakaoharibiwa kwa sababu ya dhambi nzito sana ya zamani au ushupavu wa dini wa zamani. “Wapumbavu ninyi na vipofu”! Yesu atangaza rasmi, kwani Mafarisayo wanakazia dhahabu ya hekalu kuliko kudumisha ibada ya kweli huko. Wanapuuza haki, rehema, na uaminifu huku wakilipa zaka za mnanaa, bizari na jira zenye kutamaniwa sana, bali wapuuza mambo mazito zaidi ya Sheria. Kuoga kwa kawaida ya dini hakutaondoa kamwe uchafu wao wa kindani—ni moyo tu wenye kusafishwa kupitia imani katika dhabihu ya Yesu inayokaribia uwezao kutimiza hilo. Unafiki na kuhalifu sheria kwao kwa kindani husingizia hali yao yoyote ya nje ‘iliyopakwa chokaa.’—Mathayo 23:13-29.
12 Naam, ni ole kweli kweli kwa Mafarisayo, kwa kweli ni “wana wao [wale] waliowaua manabii” wa zamani! Nyoka, wao ni wana wa majoka, waliohukumiwa kwenda Gehena, kwani watamwua si Yesu pekee bali pia wale anaotuma. Hiyo ni hukumu itakayotekelezwa “juu ya kizazi hiki.” Kwa utimilizo, Yerusalemu liliharibiwa kabisa miaka 37 baadaye.—Mathayo 23:30-36.
13. Maneno ya Yesu juu ya michango ya hekaluni yanaonyeshwa na hali zipi leo?
13 Kabla ya kuondoka hekaluni, Yesu asema kwa kumsifu mjane mwenye uhitaji anayetumbukiza ndani ya kasha la hazina sarafu ndogo mbili—“vyote alivyokuwa navyo.” Ni tofauti kweli kweli na matajiri wenye pupa, wanaotumbukiza michango isiyo ya nafsi yote! Sawa na mjane huyo mwenye uhitaji, Mashahidi wa Yehova leo hudhabihu kwa nia wakati, nishati, na fedha zao ili kutegemeza na kupanua kazi ya Ufalme ya ulimwenguni pote. Ni tofauti kama nini na wale waevanjeli wa Televisheni wanaokumba mali ya makundi yao na kujenga milki za utajiri wa kibinafsi!—Luka 20:45–21:4.
Nisani 11 Inapoisha
14. Yesu alionyesha huzuni gani, naye alijibuje ule ulizo la ziada la wanafunzi wake?
14 Yesu alilia Yerusalemu na watu walo na kutangaza rasmi hivi: “Hamtaniona kamwe tangu sasa, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana [Yehova, NW]”! (Mathayo 23:37-39) Baadaye, wakiwa wameketi kwenye Mlima wa Mzeituni wanafunzi wa Yesu wa karibu sana wauliza juu ya hilo, na kwa kujibu Yesu aeleza ishara itakayotia alama kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme na umalizio wa mfumo mbovu wa mambo wa Shetani.—Mathayo 24:1–25:46; Marko 13:1-37; Luka 21:5-36.
15. Yesu alitoa ishara gani kuhusu kuwapo kwake kwa ajili ya hukumu, na inatimizwa tangu wakati gani?
15 Akirejezea hukumu ya Yehova itakayotekelezwa karibuni juu ya hekalu, Yesu aonyesha kwamba hilo lafananisha matukio ya wakati ujao yenye msiba mkuu kwenye umalizio wa mfumo wote wa mambo. Wakati huo wa kuwapo kwake utatiwa alama na kutokea kwa vita kwa kadiri isiyo na kifani, na pia njaa, matetemeko ya dunia, na magonjwa yenye kuambukiza, pamoja na ukosefu wa upendo na kuhalifu kwa sheria. Hilo limekuwa kweli kama nini kwa habari ya ulimwengu wetu wa karne ya ishirini tangu 1914!
16, 17. Yesu alieleza juu ya matukio gani ya ulimwengu, na Wakristo wapaswa kuitikiaje unabii huo?
16 Upeo utafikiwa katika “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” Kwa kuwa hiyo itakuwa yenye uharibifu mwingi kama lile Furiko la siku ya Noa, Yesu aonya dhidi ya kujishugulisha sana katika ufuatiaji-fuatiaji wa mambo ya kilimwengu. “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.” Twaweza kufurahi kama nini kwamba Bwana-Mkubwa ameweka rasmi “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” mpakwa-mafuta alitangaze onyo na kuandaa chakula kingi cha kiroho kwa siku hii ya kuwapo kwake!—Mathayo 24:21, 42, 45-47.
17 Katika karne yetu ya 20, tumeona “dhiki ya mataifa wakishangaa . . . watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu.” Lakini Yesu atuambia hivi: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” Naye atuonya hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo.” Ni kwa kukesha tu tuwezavyo kusimama tukiwa na kibali mbele ya Yesu, “Mwana wa Adamu [binadamu, NW],” kwenye kuwapo kwake.—Luka 21:25-28, 34-36.
18. Ni kitia-moyo gani tuwezacho kupata kutokana na vielezi vya Yesu vya wanawali kumi na zile talanta?
18 Katika kumalizia mwono-mbele wake wenye ustadi wa matukio ya siku za leo, Yesu atoa vielezi vitatu. Kwanza, katika mfano wa wanawali kumi, akazia tena uhitaji wa ‘kukesha.’ Halafu, katika kielezi cha watumwa na talanta, aonyesha jinsi kufanya kazi kwa bidii kunavyothawabishwa na mwaliko wa ‘kuingia ndani ya shangwe ya bwana-mkubwa.’ Wakristo wapakwa-mafuta, waliotolewa kivuli katika mifano hiyo, pamoja na kondoo wengine waweza kupata kitia-moya kingi kutokana na maelezo hayo ya wazi.—Mathayo 25:1-30.
19, 20. Ni uhusiano gani wenye kupendeza wa ki-siku-hizi unaotokezwa katika kielezi cha Yesu cha kondoo na mbuzi?
19 Kielezi cha tatu charejezea kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme baada ya kuwasili na kuketi juu ya kiti cha ufalme chake cha kimbingu chenye utukufu. Ndio wakati wa kuhukumu mataifa na kutenga watu wa duniani katika vikundi viwili, kimoja kikiwa na watu wasikivu wenye mfano wa kondoo na kile kingine, cha wale washupavu wenye mfano wa mbuzi. Kondoo hujitahidi kujionyesha wenyewe kuwa wenye kutegemeza ndugu za Mfalme—wale wapakwa-mafuta waliobaki duniani wakati huu wa mwisho wa ulimwengu. Kondoo hao wanathawabishwa na uhai, hali mbuzi wasioonyesha shukrani waondoka kuingia uharibifu wa milele.—Mathayo 25:31-46.
20 Ni uhusiano mzuri ajabu kama nini tuonao kati ya kondoo wengine na ndugu za Mfalme wakati huu wa umalizio wa mfumo wa mambo! Ingawa mabaki wapakwa-mafuta ndio waliokuwa na daraka kubwa la kazi mwanzoni mwa kuwapo kwa Mfalme, mamilioni ya kondoo wengine wenye bidii hufanyiza sasa asilimia 99.8 ya watumishi wa Mungu duniani. (Yohana 10:16) Na wao pia wamejionyesha kuwa na nia ya kuvumilia ‘njaa, kiu, uchi, magonjwa, na kutiwa gerezani’ wakiwa waandamani wa wale wapakwa-mafuta wenye kushika uaminifu wao wa kimaadili.a
Nisani 12
21. Ni jambo gani lililosonga mbele katika Nisani 12, na jinsi gani?
21 Njama za kumwua Yesu zasonga mbele. Yuda azuru wakuu wa makuhani hekaluni, akikubali kumsaliti Yesu kwa vipande 30 vya fedha. Hata hilo lilikuwa limetolewa unabii.—Zekaria 11:12.
Nisani 13
22. Ni matayarisho gani yaliyofanywa katika Nisani 13?
22 Yesu, ambaye aendelea kubaki katika Bethania, yaelekea ili kusali na kutafakari, atuma wanafunzi wake waingie Yerusalemu ili wampate “mtu fulani.” Katika nyumba ya mtu huyo, katika chumba cha orofani, wanatayarisha Sikukuu ya Kupitwa. (Mathayo 26:17-19) Jua lituapo katika Nisani 13, Yesu ajiunga nao hapo kwa ajili ya mwadhimisho wenye matukio mengi zaidi katika historia yote. Ni jambo gani linalongojea kutukia katika Nisani 14? Makala yetu ifuatayo itaonyesha.
[Maelezo ya Chini]
a Makala ifuatayo itatusaidia tuthamini hata zaidi ule uhusiano wa karibu sana kati ya lile kundi ndogo la wapakwa-mafuta na wale kondoo wengine.
Ungetoaje Muhtasari?
◻ Wengine walimwonyesha Yesu ukarimu na ukaribishaji gani kuanzia Nisani 8 hadi 10?
◻ Yesu alifunuaje makasisi wanafiki katika Nisani 11?
◻ Yesu alitoa unabii gani mkubwa, nao unatimizwaje leo?
◻ Matukio yaliendeleaje hadi kufikia upeo katika Nisani 12 na 13?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Yesu amsifu yule mjane maskini aliyechanga sarafu ndogo mbili—vyote alivyokuwa navyo