Siku ya Kukumbuka
“Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.”—YOHANA 16:33.
1, 2. Ni siku gani moja katika historia inayotokeza zaidi ya siku nyinginezo zote, na kwa nini?
ULIMWENGU leo una mengi ya kusema kuhusu amani. Mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu 2, amani ilishirikishwa na Siku ya V-E (siku ya ushindi wa majeshi ya Muungano katika Ulaya) na Siku ya V-J (siku ya ushindi wa majeshi ya Muungano juu ya Japani).a Kila mwaka, Krismasi hufanya watu wafikirie ‘amani duniani.’ (Luka 2:14) Lakini kuna siku moja katika historia yote ya kibinadamu inayotokeza zaidi ya nyinginezo zote. Ni ile siku ambayo katika hiyo Yesu alisema maneno yaliyonukuliwa juu. Kati ya zile siku milioni mbili na zaidi ambazo ainabinadamu imekuwapo hapa duniani, ni siku ile moja ambayo imebadili kabisa mwendo wa aina ya binadamu kwa manufaa yayo ya milele.
2 Siku hiyo ya maana sana ilikuwa Nisani 14 kwenye kalenda ya Kiyahudi. Katika mwaka wa 33 wa Wakati Wetu wa Kawaida, Nisani 14 ilianza wakati wa mshuko-jua katika Aprili 1. Acheni tuangalie matukio ya siku hiyo ya maana sana.
Nisani 14!
3. Yesu alitumiaje saa hizo za mwisho?
3 Giza la jioni linapoingia, mwezi mpevu wenye kupendeza wamulika ukiwa ukumbusho wa kwamba Yehova huamua nyakati na majira. (Matendo 1:7) Na ni jambo gani linalotukia katika chumba cha orofani ambamo Yesu na mitume wake 12 wamekusanyika kuadhimisha Sikukuu ya Kupitwa ya kila mwaka ya Wayahudi? Yesu atayarishapo ‘kutoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, awaonyesha upendo watu wake, awapenda upeo.’ (Yohana 13:1) Afanyaje hilo? Kwa maneno na kwa mfano, Yesu aendelea kukaza kikiki ndani ya wanafunzi wake sifa ambazo zitawasaidia kuushinda ulimwengu.
Kujivika Unyenyekevu na Upendo
4. (a) Yesu aliwaonyeshaje wanafunzi wake sifa ya msingi? (b) Tunajuaje kwamba Petro alijifunza umaana wa unyenyekevu?
4 Mitume wanahitaji bado kujiondolea kadiri fulani ya wivu na kiburi ya kujitakia makuu. Kwa hiyo Yesu ajivika taulo kiunoni na kuanza kuiosha miguu yao. Hilo si wonyesho wa unyenyekevu wa kuigiza tu, kama linavyofanywa katika Roma kila mwaka na papa wa Jumuiya ya Wakristo. Bila shaka, sivyo! Unyenyekevu wa kweli ni kujitoa mwenyewe kunakotokana na ‘unyenyekevu wa akili unaohesabu wengine kuwa bora zaidi.’ (Wafilipi 2:2-5, NW) Mwanzoni, Petro akosa kuelewa hilo, akimkataza Yesu asiioshe miguu yake. Anaposahihishwa, amwomba Yesu auoshe mwili wake wote. (Yohana 13:1-10) Hata hivyo, ni lazima iwe kwamba Petro alijifunza somo hilo. Miaka mingi baadaye, twaona kwamba alikuwa akiwashauri wengine kwa usahihi. (1 Petro 3:8, 9; 5:5) Ni jambo la maana kama nini leo kwamba sisi sote tumtumikie Kristo katika unyenyekevu!—Ona pia Mithali 22:4; Mathayo 23:8-12.
5. Ni amri gani ya Yesu iliyoonyesha umaana wa sifa nyingine muhimu?
5 Mmoja wa wale 12 hafaidiki kutokana na shauri la Yesu. Huyo ni Yuda Iskariote. Mlo wa Sikukuu ya Kupitwa unapoendelea, Yesu aanza kufadhaika rohoni, atambulisha Yuda kuwa ndiye msaliti wake, na kumwondosha. Ni baada ya hilo tu kwamba Yesu awaambia wanafunzi wake waaminifu 11 hivi: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35) Hiyo kwa kweli ni amri mpya, iliyotolewa kielezi na mfano bora mno wa Yesu mwenyewe! Saa ya kifo chake cha kidhabihu ikaribiapo, Yesu aonyesha upendo wenye kutokeza. Atumia kila dakika ya thamani kufundisha na kuwatia moyo wanafunzi wale. Baadaye, akazia umaana wa upendo akisema: “Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi. Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.”—Yohana 15:12, 13.
“Njia, na Kweli, na Uzima [Uhai, NW]”
6. Yesu aweka mbele ya wanafunzi wake wa karibu sana mradi gani?
6 Yesu awaambia wale waaminifu 11 hivi: “Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali.” (Yohana 14:1, 2) Mahali hapo patakuwa katika “ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 7:21) Yesu ataarifu jinsi kikundi hicho cha karibu sana cha wanafunzi waaminifu-washikamanifu kiwezavyo kupata mradi wacho. Asema hivi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima [uhai, NW]; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) Hilo latumika pia kwa wale wa ainabinadamu wanaopata uhai wa milele duniani.—Ufunuo 7:9, 10; 21:1-4.
7-9. Ni kwa nini Yesu alijieleza mwenyewe kuwa “njia, na kweli, na uzima [uhai, NW]”?
7 Yesu ndiye “njia.” Njia ile moja na ya pekee ya kumkaribia Mungu katika sala ni kupitia Yesu Kristo. Yesu mwenyewe awahakikishia wanafunzi wake kwamba Baba atawapa chochote waombacho katika jina la Yesu. (Yohana 15:16) Sala zinazotolewa kwa sanamu au “watakatifu” wa kidini au zilizojaa sala za Kumwamkia Maria na kuimba kwa kurudia-rudia—hakuna mojawapo ya hizo inayosikizwa na kukubaliwa na Baba. (Mathayo 6:5-8) Zaidi ya hayo, kuhusu Yesu, twasoma hivi kwenye Matendo 4:12: “Hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”
8 Yesu ndiye “kweli.” Mtume Yohana alitaarifu hivi juu yake: “Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.” (Yohana 1:14) Yesu alikuwa kweli ya mamia ya unabii katika Maandiko ya Kiebrania kwa kuyatimiza. (2 Wakorintho 1:20; Ufunuo 19:10) Aliijulisha kweli kwa kuongea na wanafunzi wake na umati uliosikiliza, katika kubishana kwake na makasisi wanafiki, na kwa mfano wa mwenendo wake wa maisha.
9 Yesu ndiye “uhai.” Akiwa Mwana wa Mungu, Yesu alisema hivi: “Amwaminiye [azoeaye imani katika, NW] Mwana yuna uzima [uhai, NW] wa milele; asiyemwamini [asiyemtii, NW] Mwana hataona uzima [uhai, NW], bali ghadhabu ya Mungu inamkalia.” (Yohana 3:36) Imani iliyozoewa katika dhabihu ya Yesu huongoza kwenye uhai wa milele—uhai usioweza kufa mbinguni kwa “kundi dogo” la Wakristo wapakwa-mafuta na uhai wa milele kwenye dunia-paradiso kwa umati mkubwa wa “kondoo wengine.”—Luka 12:32; 23:43; Yohana 10:16.
Kuvumilia Mnyanyaso
10. Ni kwa nini tunahitaji ‘kuushinda ulimwengu,’ na Yesu alitoa kitia-moyo gani kuhusu hilo?
10 Ni lazima wale wanaotumaini kuishi katika mfumo mpya wa Yehova washindane na ulimwengu ambao “uko katika uwezo wa yule mwovu,” Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19, NW) Basi, maneno ya Yesu kwenye Yohana 15:17-19 ni yenye kutia moyo kama nini! Yeye atangaza rasmi hivi: “Haya nawaamuru ninyi, mpate kupendana. Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.” Wakristo wa kweli wamechukiwa hadi mwaka huu wa 1992, na jinsi tunavyoshangilia katika mifano mizuri ya wale walioendelea kusimama imara, wakipata nguvu kwa unyenyekevu chini ya mkono wa Mungu wenye uwezo! (1 Petro 5:6-10) Sisi sote twaweza kuvumilia majaribu kwa kuzoea imani katika Yesu, anayemalizia mazungumzo yake kwa maneno haya yenye kuchangamsha moyo: “Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 16:33.
Kuanzisha Agano Jipya
11. Yeremia alitoa unabii gani kuhusu agano jipya?
11 Katika jioni hiyo, baada ya mwadhimisho wa Sikukuu ya Kupitwa kuisha, Yesu asema juu ya agano jipya. Nabii Yeremia alitabiri hilo karne nyingi mbeleni, akisema: “Angalia, siku zinakuja, asema BWANA [Yehova, NW], nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda . . . Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. . . . nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yeremia 31:31-34) Katika Nisani 14, 33 W.K., dhabihu inayohalalisha agano hilo jipya itatolewa!
12. Yesu alianzishaje agano jipya, nalo latimiza nini?
12 Yesu awaambia wale waaminifu 11 kwamba ametamani sana kula Sikukuu ya Kupitwa hiyo pamoja nao. Halafu atwaa mkate, ashukuru, aumega, na kuwapa, akisema: “Huu ndio [humaanisha, NW] mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu, fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” Kwa njia iyo hiyo, awapitishia kikombe chenye divai nyekundu, akisema: “Kikombe hiki ni [humaanisha, NW] agano jipya katika damu yangu, inayomwagika kwa ajili yenu.” (Luka 22:15, 19, 20) Agano jipya linafanywa kutenda kazi kwa “damu ya thamani” ya Yesu, iliyo ya thamani kubwa zaidi ya damu ile ya mnyama iliyonyunyizwa katika kuhalalisha agano la Sheria la Israeli! (1 Petro 1:19; Waebrania 9:13, 14) Wale wanaoingizwa katika agano jipya huonea shangwe msamaha kamili wa dhambi. Kwa hiyo, wanaweza kustahili kuwa miongoni mwa wale 144,000, wanaopokea urithi wa milele wakiwa Israeli wa kiroho.—Wagalatia 6:16; Waebrania 9:15-18; 13:20; Ufunuo 14:1.
“Kwa Ukumbusho Wangu”
13. (a) Twapaswa kufikiria nini wakati wa Ukumbusho? (b) Ni nani pekee wapaswao kushiriki mifano, na kwa nini?
13 Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu wa mara ya 1,960 utakuwa Aprili 17, 1992. Tarehe hiyo ikaribiapo, twafanya vyema kufikiria mambo yote ambayo dhabihu kamilifu ya Yesu inatimiza. Mpango huo hukweza hekima ya Yehova na upendo wake wenye kina kwa ainabinadamu. Uaminifu wa kimaadili wa Yesu usio na kasoro, hata hadi kifo chenye maumivu sana, unatetea Yehova dhidi ya dhihaka la Shetani kwamba uumbaji Wake wa kibinadamu una hitilafu na utashindwa chini ya jaribu. (Ayubu 1:8-11; Mithali 27:11) Kwa damu yake ya kidhabihu, Yesu hupatanisha agano jipya, njia ya Yehova ya kuchagua “jamii iliyoteuliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu kwa ajili ya mali ya pekee.” Wakiwa wangali duniani, hao ‘hutangaza kotekote sifa bora’ za Mungu wao, Yehova, ambaye ‘amewaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ (1 Petro 2:9, NW; linganisha Kutoka 19:5, 6.) Kwa kufaa, ni wao tu wanaoshiriki mifano ya Ukumbusho kila mwaka.
14. Mamilioni ya watazamaji wanaimarishwaje sana?
14 Kwenye Ukumbusho wa mwaka jana, 10,650,158 walihudhuria kotekote duniani, lakini miongoni mwa hao ni 8,850 tu—wasiozidi sehemu moja ya kumi ya asilimia 1—walioshiriki mifano. Kwa hiyo, basi, mwadhimisho huo una faida gani kwa mamilioni ya watazamaji? Ni wa maana sana! Ingawa hawashiriki, wanaimarishwa sana kiroho kwa ushirika huo pamoja na ule udugu mkubwa wa duniani pote, wanaposikia juu ya mambo yale yote mazuri ajabu ambayo Yehova hutimiza kupitia dhabihu ya Mwana wake.
15. Wengine zaidi ya wapakwa-mafuta hufaidikaje kutokana na dhabihu ya Yesu?
15 Isitoshe, mtume atuarifu kwenye 1 Yohana 2:1, 2: “Tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho [dhabihu yenye kufunika, NW] kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” Naam, dhabihu ya Yesu, ingawa hufaidi kwanza jamii ya Yohana wanaoingizwa katika agano jipya, huandaa pia msamaha wa dhambi za “ulimwengu wote.” Hiyo ni “dhabihu yenye kufunika” kwa ajili ya dhambi za wote wengine wa ulimwengu wa ainabinadamu wanaozoea imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa, inayowafungulia taraja la furaha la uhai wa milele kwenye dunia-paradiso.—Mathayo 20:28.
“Katika Ufalme wa Baba Yangu”
16. (a) Yesu na warithi washiriki wake wanaonekana kuwa wanashiriki katika nini? (b) Na ni nini kinachohitajiwa leo kwa mabaki ya wapakwa-mafuta na kwa umati mkubwa pia?
16 Akiendelea kuwatia moyo mitume wake, Yesu aelekezea siku ambayo katika njia ya ufananisho atakunywa uzao wa mzabibu mpya pamoja na wanafunzi wake katika Ufalme wa Baba yake. (Mathayo 26:29) Awaambia hivi: “Nanyi ndinyi mliodumu pamoja nami katika majaribu yangu. Nami nawawekea ninyi ufalme, kama vile Baba yangu alivyoniwekea mimi; mpate kula na kunywa mezani pamoja nami katika ufalme wangu; na kuketi katika viti vya enzi, huku mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli.” (Luka 22:28-30) Kwa kuwa Yesu alitwaa mamlaka ya Ufalme mbinguni katika 1914, twaweza kukata maneno kwamba idadi kubwa zaidi ya warithi washiriki wa Yesu, waliokusanywa muda wote wa karne zilizopita, tayari wamefufuliwa, “kuketi katika viti vya enzi” pamoja naye. (1 Wathesalonike 4:15, 16) Siku ya malaika kuachilia zile “pepo nne za nchi” za “dhiki ile iliyo kuu,” yakaribia upesi! Kufikia wakati huo, kutiwa muhuri kwa wale 144,000 wa Israeli ya kiroho na kukusanywa kwa wale mamilioni ya umati mkubwa kutakuwa kumekamilishwa. Ni lazima hao wote waushike uaminifu wa kimaadili, kama Yesu alivyofanya, ili kupokea ile zawadi ya uhai wa milele.—Ufunuo 2:10; 7:1-4, 9.
17 na sanduku. (a) Mmoja wa wapakwa-mafuta akikataliwa kuwa asiye mwaminifu-mshikamanifu, ni nani aweza kuchukua mahali pake kwa kufaa? (b) Makala za Mnara wa Mlinzi katika 1938 zaonyesha nuru gani yenye kupendeza juu ya ujenzi na upanuzi wa baadaye wa tengenezo la kitheokrasi duniani?
17 Vipi ikiwa baadhi ya wale waliopakwa mafuta washindwa kuwa washika uaminifu wa kimaadili? Wakati huu wa kuchelewa mno, bila shaka idadi ya wale wasiokuwa waaminifu-washikamanifu itakuwa ndogo sana. Kwa kufaa, wenye kuchukua mahali pao watatoka, si miongoni mwa wale wenye kubatizwa hivi karibuni, bali kutoka wale ambao wamedumu pamoja na Yesu katika majaribu yake muda wote wa miaka mingi iliyopita ya utumishi mwaminifu. Mimuliko yenye kung’aa sana ya nuru ya kiroho iliyotoka kupitia Mnara wa Mlinzi katika miaka ya 1920 na 1930 yaonyesha kwamba kukusanywa kwa mabaki ya wapakwa-mafuta kulikuwa kwa kweli kumekamilika katika kipindi hicho. Wale ambao ‘wamekuwa wakifua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo’ tangu wakati huo wana tumaini tofauti la shangwe. Kupitia Kristo, roho ya Yehova huwaongoza kwenye “chemchemi za maji yenye uhai” katika dunia-Paradiso.—Ufunuo 7:10, 14, 17.
Sala ya Juhudi Nyingi Sana
18. Tunajifunza masomo gani yenye nguvu kutoka kwa sala ya Yesu kwenye Yohana sura 17?
18 Yesu amalizia kusanyiko lake la Ukumbusho pamoja na wanafunzi wake kwa kutoa ile sala ya juhudi nyingi kwenye Yohana 17:1-26. Yeye asali kwanza kwamba Baba yake aweze kumtukuza aushikapo uaminifu wake wa kimaadili hadi mwisho. Kwa njia hiyo Yehova pia atatukuzwa, jina lake likitukuzwa—likiwa limeondolewa masuto yote. Kwani, kwa kweli, yule mwanamume mkamilifu Yesu athibitisha hakika kwamba uumbaji wa Mungu wa kibinadamu waweza kuwa bila hitilafu, hata chini ya jaribu kali zaidi. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Waebrania 4:15) Zaidi ya hayo, kifo cha Yesu cha kidhabihu hufungulia wazao wa Adamu nafasi tukufu. Asema Yesu: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue [kutwaa kwao maarifa kuhusu, NW] wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” Ni muhimu kama nini kutwaa maarifa sahihi kuhusu Yehova Mungu na kuhusu Mwana wake, Mwana-Kondoo wa Mungu, aliyetoa uhai wake kwa ajili ya utetezi wa Yehova na kwa ajili ya wokovu wa ainabinadamu! (Yohana 1:29; 1 Petro 2:22-25) Je! wewe wathamini dhabihu hiyo yenye upendo mwingi sana kwa kadiri ya kujiweka wakfu kikamili kwa Yehova na utumishi wake wa thamani kubwa?
19. Mabaki na umati mkubwa wawezaje kuonea shangwe umoja wa thamani kubwa?
19 Zaidi ya hayo, Yesu asali kwa Baba yake Mtakatifu kwamba Yeye awalinde wanafunzi wanapojithibitisha wenyewe kutokuwa sehemu ya ulimwengu, wanaposhikamana na neno Lake kuwa kweli, na kudumisha umoja wa thamani kubwa pamoja na Baba na Mwana. Je! sala hiyo haijajibiwa vizuri ajabu hadi siku ya leo wakati mabaki ya wapakwa-mafuta na umati mkubwa wanapotumikia pamoja kwa umoja katika vifungo vya upendo, huku wakidumisha kutokuwamo kuelekea ulimwengu, jeuri yao, na uovu wao? Maneno ya Yesu ya kumalizia kwa Baba yake, Yehova, ni ya thamani kubwa kama nini! “Naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo,” akasema Yesu, “ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe ndani yao.”—Yohana 17:14, 16, 26.
20. Ni kwa nini Nisani 14, 33 W.K., kwa hakika ni siku ya kukumbuka?
20 Akiondoka kwenda kwenye shamba la Gethsemane, Yesu awa na ushirika zaidi wa muda mfupi, wenye kujenga pamoja na wanafunzi wake. Kisha maadui wake wamjilia! Maneno hayawezi kueleza yale maumivu mengi makali ya kimwili ya Yesu, huzuni yake nyingi sana kwa sababu ya masuto yaliyoletwa juu ya Yehova, na mfano mzuri wa uaminifu wake wa kimaadili katika kupitia hayo yote. Yesu avumilia hadi mwisho, muda wote wa usiku na wakati wote wa sehemu kubwa ya saa za mchana za siku hiyo. Yeye aonyesha kwa wazi kwamba Ufalme wake si sehemu ya ulimwengu huu. Na kwa pumzi yake ya mwisho, alia: “Imetimizwa!” (Yohana 18:36, 37; 19:30, NW) Ushindi wake wa ulimwengu umekamilika. Nisani 14, 33 W.K., kwa hakika ni siku ya kukumbuka!
[Maelezo ya Chini]
a Siku ya Ushindi Katika Ulaya na Siku ya Ushindi juu ya Japani.
Ungejibuje?
◻ Yesu alifundisha nini kuhusu unyenyekevu na upendo?
◻ Yesu alipataje kuwa “njia, na kweli, na uzima [uhai, NW]”?
◻ Ni nini kusudi la agano jipya?
◻ Ni umoja na upendo gani unaoshirikiwa na mabaki ya wapakwa-mafuta na umati mkubwa?
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Hekima ya Sulemani Mkubwa Zaidi
Makala zenye kichwa “Tengenezo” katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi (katika Kiingereza) ya Juni 1 na Juni 15, 1938, ziliweka mpango wa msingi wa kitheokrasi unaofuatwa na Mashahidi wa Yehova leo. Zilikuwa kipeo cha kipindi cha ajabu cha marekebisho ya kimafundisho na ya kitengenezo kilichoanza katika 1919. (Isaya 60:17) Katika kulinganisha kipindi hicho cha miaka 20 na ile miaka 20 ambayo katika hiyo Sulemani alijenga hekalu na nyumba ya mfalme katika Yerusalemu, Mnara wa Mlinzi lilisema hivi: “Maandiko huonyesha kwamba, baada ya miaka ile ishirini ya programu ya ujenzi ya Sulemani . . . , alishiriki katika programu ya ujenzi ya taifa lote. (1 Fal. 9:10, 17-23; 2 Nya. 8:1-10) Ndipo akaja malkia wa Sheba ‘kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani.’ (Mt. 12:42; 1 Fal. 10:1-10; 2 Nya. 9:1-9, 12) Hilo ladokeza swali hili: Ni nini kilichoko katika wakati ujao ulio karibu wa watu wa Yehova duniani? Tukiwa na uhakika kamili tutangojea, na tutapata kuona.” Uhakika huo haukuwa wa bure. Chini ya tengenezo la kitheokrasi programu pana ya ujenzi wa kiroho ulimwenguni pote imekusanya zaidi ya watu milioni nne wa umati mkubwa. Sawa na malkia wa Sheba, hawa wametoka pande za miisho ya dunia kusikia hekima ya Sulemani Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo—inayoelekezwa kwao kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”—Mathayo 24:45-47.