Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 3/1 kur. 8-15
  • Nisani 14—Siku ya Kukumbukwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nisani 14—Siku ya Kukumbukwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Siku ya Kukumbukwa
  • Kulitokea Nini? Yalikuwa na Maana Gani?
  • Utukufu, Upendo, na Umoja
  • Sababu kwa Nini Mlo wa Jioni wa Bwana Una Maana Kwako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kwa Nini Tuadhimishe Mlo wa Jioni wa Bwana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Mlo wa Jioni wa Bwana Huadhimishwaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Ukumbusho (Mlo wa Jioni wa Bwana)
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 3/1 kur. 8-15

Nisani 14—Siku ya Kukumbukwa

“Endeleeni kufanya hivyo kwa kunikumbuka mimi.”​—1 WAKORINTHO 11:24, NW.

1. Yesu aliushindaje ulimwengu?

“IWENI na ushujaa! Mimi nimeushinda ulimwengu.” Kwa maneno hayo ya kufariji na kutia moyo, Yesu aliwatia nguvu mitume wake 11 waaminifu usiku ule kabla hajafa. Yesu alikuwa amejithibitisha kuwa mshindi wa ulimwengu! Alikuwa amefaulu kushinda kila jaribio la Adui yake, Shetani Ibilisi, la kutaka kuvunja ushikamanifu wake kwa Yehova. Na sasa, akiwa anakabili kifo juu ya mti wa mateso baada ya saa chache, yeye alikuwa na uhakika wa kudumisha mwendo wake wa ukamilifu wa uaminifu mpaka mwisho kabisa.​—Yohana 16:33, NW; Waebrania 12:2.

2. Kwa sababu gani Yesu alianzisha “chakula cha jioni cha Bwana”?

2 Tukio hilo la umaana wa kuhusu ulimwengu wote mkubwa lilitokea miaka elfu moja mia tisa na hamsini na miwili iliyopita siku ya 14 ya Nisani, mwezi wa kwanza wa kalenda takatifu ya Kiyahudi. Siku hiyo ingekuwa siku ambayo haingesahauliwa kamwe na wafuasi wake waliojitoa wenye kufuata hatua zake. Ili kuhakikisha kwamba wafuasi wake washikamanifu hawangepuuza umaana wa mambo ambayo yangetokea wakati huo, Yesu alianzisha chakula cha jioni cha ukumbusho cha pekee, kinachoelezwa na mtume Paulo kuwa “chakula cha jioni cha Bwana.” Kwa kuongozwa na roho ya Mungu Paulo alisimulia kwamba katika pindi hiyo Yesu aliwaamuru wanafunzi wake waliokuwapo wakati huo hivi: “Endeleeni kufanya hivyo kwa kunikumbuka mimi.” (1 Wakorintho 11:20, 24, NW) Ikiwa unahangaikia kuwa mmoja wa wafuasi wa Yesu, je, wewe unathamini ni kwa sababu gani aliamuru hivyo, amri hiyo inakutaka ufanye nini, na inaweza kumaanisha nini kwa wakati ujao wako?

Siku ya Kukumbukwa

3. Ni kwa sababu gani, na ni chini ya hali gani, Nisani 14 ikafanywa kuwa siku ya kukumbukwa?

3 Hiyo haikuwa mara ya kwanza katika historia ya wanadamu kwamba Nisani 14 iliwekwa kando kuwa siku ya kukumbukwa. Mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova, kupitia mtumishi wake Musa, aliwaamuru Waisraeli hivi: “Siku hii [Nisani 14] ni lazima itumike kuwa ukumbusho kwenu, na ni lazima mwiadhimishe kuwa sikukuu kwa Yehova katika vizazi vyenu vyote. Ni jambo gani lililofanya kuwa sherehe hiyo huko nyuma? Yehova mwenyewe alijibu hivi: “Ni dhabihu ya kupitwa kwa Yehova, aliyepita juu ya nyumba za wana wa Israeli katika Misri alipopiga Wamisri.”​—Kutoka 12:14, 27, NW.

4. Ni masuala gani ya maana yaliyohusika katika kukombolewa kwa Israeli kutoka Misri?

4 Wokovu huo wenye kuogopesha sana katika Misri wa kila mzaliwa wa kwanza, wa watu na wanyama, ulitokea usiku huo wa Nisani 14. Ulikuwa upeo wa mapigo saba yaliyotangulia juu ya miungu ya kishetani iliyoabudiwa na Wamisri, na kukazia kusudi la Yehova lililokuwa limetanguliwa kusemwa kwa Farao mwenye kiburi: “Nilikusimamisha wewe kwa sababu ii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote.” Siku chache baadaye jina na uweza wa Yehova vilionyeshwa kwa njia kubwa zaidi wakati alipowaokoa mamilioni ya Waisraeli na kundi kubwa la watu waliochangamana kwenye Bahari Nyekundu (Shamu), nayo majeshi hodari ya Farao yakazamishwa naye. Basi si ajabu kwamba Musa na wana wa Israeli waliimba hivi: “Nitamwimbia [Yehova], kwa maana ametukuka sana”!—Kutoka 9:16; 15:1.

5. Ni kusudi gani lililotimizwa na sherehe ya Kupitwa?

5 Baada ya Waisraeli kuikaa nchi aliyoahidiwa babu yao Abrahamu, Kupitwa ilipaswa isherehekewe na taifa lote mara moja kila mwaka katika Yerusalemu, kwa kutii amri katika Kumbukumbu la Torati 16:1-8. Kwa njia hiyo Yehova akapanga kwamba Nisani 14 sikuzote iwe waziwazi katika akili za watu wake halisi. Ingekuwa na kusudi gani? Ingekuwa siku ya kutukuza jina la Yehova, ya kukumbuka matendo yake makuu ya wokovu. Kwa hiyo karne nyingi baadaye umaana wa Kupitwa ungekuwa ndilo jambo kuu katika mioyo na mawazo ya wazazi wa Yesu ambao, tunaambiwa walikuwa ‘wakienda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya [Kupitwa].’ Kulingana na desturi ya Kiyahudi, mwana wao Yesu angekuwa pamoja nao.​—Luka 2:41, 42.

6. Ni kwa sababu gani Yesu alihangaikia kuadhimisha Kupitwa ya 33 W.K. pamoja na mitume wake waaminifu?

6 Baada ya ubatizo wa Yesu katika Yordani na mwanzo wa huduma yake, inaelekea angeendelea kusherehekea Kupitwa pamoja na Mariamu, mamaye wa kidunia, na wanaye, ndugu za Yesu wa baba tofauti. Hata hivyo, wakati wa Nisani 14, 33 W.K., Yesu alipanga kusherehekea karamu hiyo pamoja na mitume wake 12. Masimulizi ya Luka yanatuambia jinsi Yesu alivyohisi kuhusu pindi hiyo: “Nimekuwa nikitaka sana kula chakula hiki cha Kupitwa pamoja nanyi kabla sijateseka!” (Luka 22:15, Today’s English Version) Kwa sababu gani Yesu alikuwa na tamaa yenye nguvu sana kufanya hivyo? Kwa sababu yeye alijua umaana wa matukio ambayo yangetokea baada ya muda mfupi katika siku hiyo ya kukumbukwa iliyokuwa imeanza baada ya jua kushuka. Pia Yesu alijua kwamba matukio hayo yangekuwa yenye maana zaidi ya yale yaliyotokea nyuma mwaka wa 1513 K.W.K. Yangelikweza jina la Yehova juu zaidi ya wakati mwingine uliotangulia na yangeweka msingi wa kubarikiwa hatimaye kwa jamaa zote za dunia. Pia, alikuwa na mengi ya kuwaambia wanafunzi wake kabla hajafa, akatia uhodari ndani yao ili wabaki wakiwa wafuasi wake washikamanifu. Masimulizi ya kirefu ya Injili yanatujulisha mambo yalivyokuwa, kuhusu aliyosema na kufanya Yesu.​—Yohana 12:31; 17:26.

Kulitokea Nini? Yalikuwa na Maana Gani?

7. (a) Ni matukio gani wakati wa chakula cha Kupitwa cha mwisho cha Yesu yaliyoongoza mpaka kwenye kuanzisha kwake Ukumbusho wa kifo chake? (Yohana 13:1-30) (b) Eleza alivyofanya Yesu katika kuanzisha Chakula cha Jioni cha Bwana.

7 Chakula kilipokuwa kikiendelea kuliwa, Yesu aliinuka akasafisha miguu ya wanafunzi wake, kwa njia hiyo akaweka mfano mkamilifu wa unyenyekevu. Halafu Yesu akasema, “Mmoja wenu atanisaliti.” Muda mfupi baadaye, akamgeukia Yuda na kusema, “Uyatendayo yatende upesi.” Masimulizi ya Yohana yanaeleza hivi: “Akatoka mara hiyo. Nako kulikuwa ni usiku.” (Yohana 13:21, 27, 30) Ni baada ya hilo Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake. Ebu tusikie jinsi shahidi aliyejionea Mathayo anavyosimulia mambo yaliyotokea: “Nao walipokuwa wakila, Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu. Nao walipokwisha kuimba, wakatoka nje kwenda mlima wa Mizeituni.”​—Mathayo 26:26-30; ona pia Marko 14:22-26, Luka 22:19, 20, na 1 Wakorintho 11:23-26.

8. Kwa sababu gani ni jambo la maana kuelewa maana ya maneno na matendo ya Yesu katika kuanzisha Ukumbusho?

8 Maana kamili ya yale aliyosema Yesu na kufanya katika pindi hiyo yalikuwa nini? Paulo alikazia jinsi lilivyo jambo la maana kwa wafuasi wapakwa mafuta wote wa Yesu kuthamini hilo, kwa kusema: “Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana.” Bila shaka hakuna ye yote wa wapakwa mafuta angetaka kuwa ‘asiyestahili’ machoni pa Yehova, na kupatwa na hukumu kali yake. Zaidi ya hayo, “mkutano mkubwa” wangetaka kuhesabiwa kuwa wanastahili kuwa wenzi wa mabaki wapakwa mafuta. Basi, kwa kuwa Ukumbusho mwingine unakaribia siku ya Alhamisi, Aprili 4, 1985, huu ni wakati unaofaa kwamba sisi sote tuchunguze tena kirefu jambo hilo pamoja.​—1 Wakorintho 11:27.

9. (a) Ni kwa sababu gani kuonyesha maneno ya Yesu kuwa., “Huu maana yake ni mwili wangu” ni sahihi zaidi ya “Huu ndio mwili wangu”? (Ona maneno ya chini.) (b) Yesu aliweka maana gani ya pekee juu ya mkate? (c) Juu ya divai?

9 Yesu alisema, “Huu maana yake ni mwili wangu.”a (NW) Kwa kusema maneno hayo, Yesu aliupa mkate maana ya pekee​—ulikuwa mfano wa mwili wa nyama wake mwenyewe usio na dhambi aliotoa “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” (Yohana 6:51) Hali moja na hiyo, aliposema kuhusu kikombe cha divai, “Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya . . . ondoleo la dhambi,” yeye alikuwa akitumia divai iliyochachika katika kikombe kuwa mfano wa damu yake mwenyewe. Damu hiyo ingekuwa ndio msingi wa kuanza kutendesha “agano jipya.” Pia damu yake iliyomwagwa ingekuwa njia ya kutoa uandalizi wa “ondoleo la dhambi.”​—Mathayo 26:28; Yeremia 31:31-33; Waebrania 9:22.

10. Kula mkate na kunywa divai kuna maana gani?

10 Basi, ni nini maana ya wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai wakati wa sherehe ya Ukumbusho? Tendo hilo lenyewe linaonyesha wanaokula, na wanaotazama, kwamba tayari wamefaidika na dhabihu ya ukombozi ya Kristo Yesu, lakini kwa njia ya pekee na kwa kusudi la pekee. Inakuwaje hivyo? Kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya Kristo na wakfu wao kwa Yehova, Mungu anawastahilisha kwa ustahili wa dhabihu ya kibinadamu ya Yesu. Kwa kusudi gani? Ili waweze kuhesabiwa wanastahili ukamilifu wa kibinadamu na hivyo wawe na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu. Halafu Yehova anawazaa hao kwa roho takatifu yake na wanakuwa wanaye wa kiroho. Sasa wanakuwa katika hali ya kuweza kutoa haki yao ya kuishi duniani na badala yake wawe na urithi wa kimbingu. Yote hayo yanakuwa yamekwisha kufanyika kabla ya wao kushiriki Chakula cha Jioni cha Bwana.​—Warumi 5:1, 2, 8; 8:15-17; Yakobo 1:18.

11, 12. (a) Ni mambo gani mengine mawili yanayomaanishwa na kunywa divai? (b) Eleza agano ambalo Yesu anafanya pamoja na wale wanaokula na kunywa.

11 Sasa fikiria ni nini maana nyingine ya kunywa divai. Ingawa Yehova amewahesabia wanaye wa kiroho uadilifu na amewafanya kuwa wana, wakiwa wangali na mwili usiokamilika. Bado wanaelekea kufanya dhambi nao wanatambua hilo. Kwa kunywa divai, wanakubali utegemeo wao wa kila siku kwa damu ya Kristo Yesu, ambayo ilimwagwa “kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.”​—1 Yohana 1:9, 10; 2:1.

12 Hata hivyo, kungali jambo jingine linalomaanishwa na kunywa divai. Wenye kunywa wanashuhudia kwamba wameingizwa katika “agano jipya” ambalo Yehova alitabiri zamani sana kupitia nabii Yeremia. Agano hilo lilianza kutendeshwa na damu ya Yesu. Washiriki wa agano hilo ni Yehova Mungu na wanaye wa kiroho, ambao wakiwa pamoja wanafanyiza Israeli wa kiroho. Kila mshiriki anachaguliwa na Mungu. Yesu ndiye Mpatanishi wa agano hilo, ambalo kupitia kwalo anawasaidia washiriki hao wa agano 144,000 wawe sehemu ya uzao wa Abrahamu. (Yeremia 31:31-34; 2 Wathesalonike 2:13; Waebrania 8:10, 12; 12:22-24; Wagalatia 3:29) Hao pia ndio ambao Yesu anaingiza katika ‘agano la ufalme.’ Matokeo ya hilo yatakuwa kwamba, hatimaye watatumiwa pamoja na Mfalme wao Yesu Kristo kuelekeza baraka za Yehova za uzima kwa jamaa zote za dunia.​—Luka 22:28-30; Yohana 6:53; Ufunuo 5:9, 10; Mwanzo 22:15-18.

13. Ni mambo gani yanayopasa kukumbukwa sasa katika Nisani 14?

13 Kweli kweli, tunapochunguza maana ya maneno ya Yesu yaliyosemwa siku hiyo ya kukumbukwa, tunakumbushwa kwa nguvu juu ya upendo wa Yehova kwa kutoa uandalizi wa Mwanaye mpendwa. Pia tunakumbushwa juu ya upendo wa Yesu wa kutoa uhai wake uwe ukombozi kwa ajili ya wanadamu wasioamini. (Yohana 3:16; Warumi 5:8; 1 Timotheo 2:5, 6) Hata hivyo, kuna kweli nyingine zenye thamani ambazo Yesu alizungumza pamoja na wafuasi wake jioni hiyo. Kati ya waandikaji wa Biblia, ni mtume Yohana peke yake aliyeandika mazungumzo hayo ya siri sana.

Utukufu, Upendo, na Umoja

14. (a) Yehova anatukuzwaje na kila sherehe ya Ukumbusho? (b) Upendo unahusikaje katika kumkumbuka Yesu, na hilo linapasa kutokeza uchunguzi gani wa kibinafsi katika akili za wote wenye kushiriki?

14 Yesu alisema: “Sasa ametukuzwa Mwana wa Adamu, naye Mungu ametukuzwa [kwa] yeye.” (Yohana 13:31) Tangu kukombolewa kwa Israeli kutoka Misri, Nisani 14 ilikuwa imeshirikishwa na kuondolewa lawama kwa jina la Mungu, enzi kuu yake, na uwezo wake. Sasa, kwa uaminifu wa Yesu mpaka kufa na ufufuo wake wa utukufu uliofuata kwa uwezo wa Mungu, heshima na utukufu zaidi zilikuwa zikiletwa kwa jina la Mungu. (Linganisha Mithali 27:11.) Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba wangetoa uthibitisho wa uanafunzi wao kwa kufuata “amri mpya,” ya ‘kupendana kama alivyokuwa amewapenda wao.’ (Yohana 13:34, 35) Kina cha upendo wetu wa kidugu ni kionyesho cha kuthamini kwetu upendo ambao Yesu alituonyesha wakati huo.​—1 Yohana 4:19.

15. (a) Ni tumaini gani la uzima linalowekwa mbele ya wote wanaokula na kunywa inavyostahili? (b) Upendo kwa ajili ya Yesu unathibitishwaje?

15 Tumaini la siku moja kuishi katika makao ya kimbingu ni sehemu ya furaha iliyowekwa mbele ya wale waliochaguliwa kuwa watawala wenzi pamoja na Kristo. (Ufunuo 20:6) Yesu anaeleza tumaini hilo, kwa kusema: ‘Mimi naenda kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu.’ (Yohana 14:2-4) Wote wanaobaki wakiwa waaminifu mpaka mwisho wangojea kukaribishwa nyumbani kama nini! Kwa hiyo, Yesu anashauri hivi, “Mkinipenda, mtazishika amri zangu.” Hiyo inamaanisha amri zake zote, kutia amri ya kufundisha na kufanya wanafunzi.​—Yohana 14:15, 21; Mathayo 28:19, 20.

16. (a) Yesu alikaziaje uhitaji wa kuwa na umoja kati ya wafuasi wake, na ni kwa sababu gani umoja huo ni wa maana sana? (b) Ni lazima wafuasi wote wa Yesu wakabiliane na nini, lakini ni nini kinachowasaidia wafanye hivyo?

16 Ni jambo la maana kama nini kwa wafuasi wa Yesu kuwa na umoja pamoja naye na wao kwa wao! Yesu anatumia mfano wa mzabibu na matawi yake kukazia uhakika huo. Umoja unatokeza kuzaa matunda na hilo, nalo, linamtukuza Baba. (1 Wakorintho 1:10; Yohana 15:1, 5, 8) Mateso na upinzani unakabili wafuasi wote wa Yesu. Lakini inatia imani nguvu kama nini kujua kwamba Yesu alidumisha ukamilifu wake akiwa mshindi wa ulimwengu yajapokuwa mashambulio ya Shetani!—Yohana 15:18-20; 16:2, 33.

17. Zungumza baadhi ya maombi ya Yesu katika sala yake iliyoandikwa katika Yohana sura ya 17.

17 Yesu anaileta jioni hiyo kwenye umalizio kwa sala ya kutoka moyoni ya kumwomba Babaye. Kutukuzwa kwa Babaye kunachukua mahali pa kwanza katika ombi lake. Anaomba kwamba wafuasi wake walindwe kutoka kwa yule mwovu, Shetani, wanapobaki wakiwa wamejitenga na ulimwengu. Na pia anaomba kwamba umoja uo huo wa upendo ulio kati yake na Baba uendelee kukua kati ya hesabu yenye kuongezeka daima ya wafuasi wenye kufuata hatua zake.​—Yohana sura ya 17.

18. Kwa kufikiria jumla ya hesabu ya wale waliohudhuria Ukumbusho mwaka wa 1984, ni kwa sababu gani ni wachache sana waliokula mkate na kunywa divai?

18 Tumechunguza kweli na mawazo machache tu yenye thamani ambayo Yesu alishiriki pamoja na wanafunzi wake usiku huo miaka kama 1,952 iliyopita, lakini kwa hakika hayo yanatusaidia kuelewa kwa sababu gani Nisani 14 kweli kweli ni siku ya kukumbukwa. Basi, haishangazi kwamba mwaka jana 7,416,974 wa Mashahidi wa Yehova na marafiki wao waliona umaana wa kukusanyika pamoja kuadhimisha Chakula cha Jioni cha Bwana. Hata hivyo, kati ya umati huo mkubwa, kulikuwako 9,081 tu waliokula mkate na kunywa divai. Kwa sababu gani? Kwa sababu wengi wa Mashahidi wa Yehova leo wanajiona kuwa sehemu ya “mkutano mkubwa” unaosimama “mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo.” Wao wanatazamia kuishi juu ya sayari-Dunia ikiwa makao yao milele, wala si kuishi katika mbingu ambako wale 144,000 “watatawala pamoja [na Kristo] hiyo miaka elfu.”​—Ufunuo 7:9; 20:6; Zaburi 37:11.

19. Ni nini yanayofanyiza msingi wa funzo la juma lijalo, na ni kwa sababu gani ni jambo la maana wote wahudhurie?

19 Hata hivyo, maswali fulani yametokea juu ya uhusiano uliopo kati ya Chakula cha Jioni cha Bwana na “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Basi, inaonekana inafaa kwamba mambo hayo yazungumzwe katika makala inayofuata, ili kusiwe kuelewa vibaya ko kote kwa mtu ye yote sherehe nyingine ya Ukumbusho inapokaribia.​—1 Wathesalonike 5:21.

[Maelezo ya Chini]

a Tafsiri fulani za Biblia zinasema, “Huu ndio mwili wangu.” (Ona Union Version, Habari Njema kwa Watu Wote, na Zaire Swahili Bible.) Lakini, neno la Kigiriki lililotumiwa kuwa “ndio” au “ni” ni neno e·stin, kuonyesha kufananisha, kumaanisha, kuwakilisha. (Ona maneno ya chini juu ya Mathayo 26:26, NW Biblia ya uchunguzi.) Neno ilo hilo la Kigiriki linaonekana katika Mathayo 9:13 na 12:7 na katika visa vyote viwili linatafsiriwa kuwa “maana” (UV, ZSB, na HNWW).

Je! Wewe Unaweza Kukumbuka​—

◻ Ni nani wanaokula mkate na kunywa divai ya Ukumbusho?

◻ Ukumbusho unapasa kutukumbusha mambo gani ya maana?

◻ Kumkumbuka Yesu kila siku kunathibitishwaje?

◻ Ni suala gani la maana ambalo sikuzote linashirikishwa na Nisani 14?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki