Dini Inaweza Kupambana na Ugumu Uliopo?
MAGAZETI yenye mambo yanayopendwa na watu wengi, ya kidini na hata ya utangazaji wa habari yanafanya haraka kueleza “mafanikio” yanayopatikana na makanisa fulani. Yanasema juu ya mikutano ya maombi na sifa inayofanya watu wakaribie Mungu zaidi. Yanasema kwamba mahubiri katika makanisa fulani yanaendelea kuwa ya kiroho badala ya kutaja shughuli za mitaani au za kisiasa. Yanasema kuwe na huduma za kusaidia maskini, kuwe na miisho ya juma ya kujipatia nguvu mpya, kuwa na vikundi vya kujifunza Biblia, mafunzo juu ya dansi za ibada, na kwamba wanakanisa walio na moyo wa kupenda wajaze nafasi zilizo na ukosefu wa mapadri na watawa wa kike. Yote hayo yanaonwa kuwa ishara ya kwamba dini imepata nguvu mpya.
Katika hotuba aliyotolea Shirika la Kitaifa la Wainjilisti mwezi Machi uliopita, Rais Reagan wa United States alitangaza hivi: “Amerika imeanza kuamka tena ili kufuata mambo ya kiroho. Imani na tumaini vinaendelea kurudishwa. Waamerika wanamrudia Mungu tena . . . Nami naamini kwamba Yeye ameanza kuiponya nchi yetu yenye baraka.” Kuonyesha tumaini hakika hivyo kunaunga mkono wazo la kwamba mwishowe yale matatizo mengi yanayoelekea wanadamu wenye taabu nyingi leo yatatatuliwa na hali ya kuamka tena katika mambo ya kiroho.
Huenda yote hayo yakasikika kuwa mambo ya kupendeza sana, lakini “kuamka tena ili kufuata mambo ya kiroho” na ‘kupata nguvu mpya’ kumetimiza nini? Huenda watu wakawa wana maoni mazuri zaidi juu yao wenyewe, lakini je! wamekuwa Wakristo wazuri zaidi? Huenda watu wakajisikia kuwa sasa wana hali zaidi ya kiroho, lakini je! wanapendezwa zaidi na mambo ya kiroho kuliko kufuatia vitu vya kimwili? Ikiwa hali ya kutomwogopa Mungu imekuwa kisababishi kikubwa cha matatizo ya leo, basi je! wao wamesaidiwa kuonyesha utawa? Majibu ya maulizo hayo ni ya maana sana katika kuamua kama dini inaweza au haiwezi kumaliza au kushindana na matatizo ya leo.
Utawa—Ni Nini?
Kufuata mambo ya kimungu, au utawa, kumefafanuliwa kuwa ni kujitolea Mungu kwa bidii au kufanya mambo kwa njia ya Mungu. Basi, hiyo si hali ya kujionyesha kijuujuu tu kuwa una woga wa kimungu au unafuata dini. Mtu aliye na utawa anahangaikia hasa kujua mapenzi ya Mungu na kuyafanya, kuwa na uhusiano wa kindani pamoja naye, si kutosheleza mahitaji fulani ya kibinafsi. Matokeo yanakuwa kwamba maisha ya mtu yanageuzwa kuwa mazuri zaidi kwa sababu ‘utawa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.’—1 Timotheo 4:8.
Je! watu mmoja mmoja wanaogeukia dini kwa sababu tu magumu ya maisha yamewafanya waache kutosheka wanastahili kuhesabiwa kuwa wenye utawa? Au wanaelekea zaidi kuwa kama wale ambao mtume Paulo alisema wana ‘mfano wa utawa, lakini wakikana nguvu zake’?—2 Timotheo 3:5.
Ikiwa mtu anageukia Mungu ili atosheleze tu uhitaji fulani wa kibinafsi badala ya kufanya hivyo kwa kusudi la kujua mapenzi ya Mungu na kumtumikia, anajifanyia mwenyewe utawa huo wala si Mungu, au sivyo? Namna hiyo ya utawa haina nguvu za kugeuza maisha yake yaache kuwa ya kufuatia mambo ya kichoyo yawe ya kutumikia Mungu kwa kujinyima kikweli.
Maneno aliyosema Paulo yalipatana na Mahubiri ya Mlimani yanayojulikana sana ambayo Yesu alitoa. Akionyesha kwamba si wote wanaodai kuwa wafuasi wake wanakubalika kwake, yeye aliongezea hivi: “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.”—Mathayo 7:22, 23.
Hivyo, jambo linalohesabiwa na Mungu kuwa la maana si mtu kujionyesha anafuata dini. Ili apokee uongozi na baraka ya Mungu, ni lazima awe na nia ya kukubali mielekezo ya Mungu katika Biblia na kuifuata katika maisha yake. Ni kama alivyosema mtunga-zaburi: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” (Zaburi 119:105) Je! watu wanaogeukia dini leo wanasaidiwa kuijua mielekezo hiyo na kuifuata?
Mambo ya Uhakika Yanaonyesha Nini?
Uchunguzi uliofanywa karibuni kati ya Wakatoliki 10,000 wanaofuata sana dini yao katika maeneo 60 ya United States ulifunua kwamba asilimia 77 kati yao wanahangaikia litakaloipata nchi hiyo, hali ni asilimia 40 tu wanaohangaikia “masuala ya kuokoka mtu binafsi.” Vivyo hivyo, uchunguzi wa maoni ya watu wengi ulionyesha kwamba kati ya maulizo yote ambayo watu wangependa kuuliza Mungu, lile ambalo wengi wangependa kuuliza ni hili: “Kuna siku ambayo kutakuwako amani yenye kudumu ya ulimwengu?”
Kwa uhakika, katika hizi nyakati za hatari hakuna ubaya wa kuhangaikia wakati wetu ujao. Lakini maoni hayo yanatofautiana sana na vile Yesu alivyoambia wanafunzi wake: “Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Matokeo ya uchunguzi huo yanaonyesha kwamba ingawa imesemwa sana kuwa watu wameamka wakaanza kufuata tena mambo ya kiroho, wasiwasi juu ya wakati ujao unatawala mioyo na akili za watu leo. Namna yao ya dini haikuwasaidia sana wapambane na matatizo ya nyakati zetu za hatari.—Ona Luka 21:26.
Kwa habari ya kufanya wanakanisa wawe watu wenye hali nyingi zaidi ya kiroho, safu ya mhariri katika gazeti Ministry la Waadventisti wa Sabato inatoa maombolezo kwa kusema “mara nyingi mno namna ya maisha yanayofuatwa na washiriki wetu au sisi wenyewe haitofautiani sana na ya watu wasio Wakristo walio karibu nasi.” Badala ya kuwa hivyo, gazeti hilo linaendelea kusema kanisa linawapa washiriki wake maoni yaliyo sawa na ya wasioamini, ya kwamba wana “haki ya kidini ya kuchanganya ufuatiaji wa vitu vya kimwili na maisha ya kupokea tu wala si kutoa.” Linatenda hivyo kwa kufanya Mungu aonekane kuwa mtu “anayetakia watu Wake vilivyo bora zaidi na kukusudia kuhakikisha kwamba wanavipata.”
Vivyo hivyo, baada ya gazeti The Economist la London kuripoti kwamba “kuna ishara fulani ya watu kuendelea (hata kuzidi) kupendezwa na mambo ya kidini,” linadai kwamba “tatizo kwa Kanisa la Uingereza ni namna ya kuhudumia wale wanaotaka kujua juu ya imani hali hilo lenyewe halina uhakika linaamini nini.”
Namna gani upande wa maadili ya kijamaa na kibinadamu? Je! makanisa yameimarisha washiriki wake wapinge mavutano machafu na njia zenye ufisadi za ulimwengu? Je! yametokeza waume, wake, wazazi na watoto walio bora? Uchunguzi wa karibuni kati ya vijana 8,000 na wazazi 10,000 wa jamaa zinazoenda kanisani katika madhehebu 13 unatoa kiwazo fulani juu ya namna mambo yalivyo.
Kulingana na kichapo Christianity Today, uchunguzi huo ulionyesha kwamba asilimia 42 ya vijana wanasema jamaa zao hazizungumzi mambo ya kidini, na asilimia 40 wanasema wanataka mwelekezo zaidi wa wazazi juu ya mambo ya ngono. Kati ya wale wenye umri wa miaka 15, asilimia 53 wametumia pombe, asilimia 20 wametumia kasumba. Uchunguzi wa kabla ya hapo, ulioripotiwa katika kichapo The Ann Arbor News, ulionyesha kwamba asilimia 59 ya wavulana na asilimia 42 ya wasichana walisema walikuwa wamefanya ngono kufikia wakati walipoingia umri wa miaka 18.
Mwisho, je! dini zinasaidia wafuasi wazo kuepuka roho yenye jeuri ya ulimwengu? Kwa kweli, kama dini itakuwa nguvu yenye kuimarisha watu katika nyakati hatari za leo, je! tusingeitazamia angalau ifanye hivyo? Lakini, jambo la kusikitisha ni kwamba watu zaidi na zaidi wamekuja kutambua kwamba dini imeshiriki kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja katika vingi vya vita na mapigano ambayo yameumiza wanadamu. Ukitaja mahali kama Ailandi, Lebanoni na Irani, ni wazo gani linalokuja katika akili? Ijapokuwa barua za uchungaji zimeandikwa na kukawako maandamano ya kutaka amani, je! dini zilizo kubwa hazihusiki sana katika mengine ya mapigano yaliyo ya kumwaga damu nyingi zaidi leo?
Kwa hiyo, tunaweza kusema nini juu ya lile linaloitwa tendo la watu kuamka tena wafuate mambo ya kidini? Labda kuna dalili za kuonyesha watu wameamka tena wafuate mambo ya kidini, lakini haiwezi kusemwa wameamka tena wafuate mambo ya kiroho. Badala ya kujengwa kiroho, kutiwa nguvu wakabili nyakati hizi za hatari, hesabu kubwa ya wale wanaogeukia dini za ulimwengu wanaingizwa katika namna ya ibada iliyo desturi tu. Ni ‘mfano wa utawa lakini wakikana nguvu zake,’ kama mtume Paulo alivyotabiri. Kule ‘kuamka tena’ na ‘kupata nguvu mpya’ kijuujuu tu kunapatana sana na zile hali nyingine zinazozidi kuwa mbaya—uharibifu mkubwa wa maadili, mvunjiko wa jamaa, uhalifu na jeuri, na mengineyo—zinazoonyesha hizi zetu ni nyakati za hatari.—2 Timotheo 3:1-5.
Matokeo Yatakuwa Nini?
Biblia inatumia mji wa kale wa Babuloni uliokuwa wa kidini kama mfano wa kuonyesha kwamba dini ya ulimwengu itapatwa na maangamizi kamili. Kitabu cha Ufunuo kinatabiri hivi: “Malaika mmoja mwenye nguvu sana akainua jiwe mfano wa jiwe kubwa la kusagia, akalitupa baharini akisema, ‘Ndivyo Babuloni utakavyotupwa na kupotea kabisa.’”—Ufunuo 18:21, HNWW.
Lakini, kabla mwisho huo wa haraka sana haujaja, kuna nafasi ya kutii onyo la kimungu lililo katika Ufunuo 18:4: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.” Kuzunguka ulimwengu, katika nchi 205, Mashahidi wa Yehova wametii onyo hilo kisha wakakimbilia Ufalme wa Mungu kuwa tumaini la peke yake kwa wanadamu. (Mathayo 24:14) Je! wewe utakuwa kati ya maelfu wanaojiunga nao katika kukimbilia usalama? Ni juu yako kuamua.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Ijapokuwa barua za uchungaji zimeandikwa na kukawako maandamano ya kutaka amani, je dini zilizo kubwa hazihusiki sana katika mengine ya mapigano yaliyo ya kumwaga damu nyingi zaidi leo?
[Picha katika ukurasa wa 5]
Huenda watu wakajisikia kwamba wanafuata zaidi mambo ya kidini, lakini je! wanapendezwa zaidi na mambo ya kiroho?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Leo mamia ya maelfu wanatii onyo la kuacha dini ya uongo