Dini Imepata Nguvu Mpya au Ina Ugumu wa Kiroho?
“Katika makanisa mengi, kumeacha kuwa na shughuli za kuunga mkono mambo ya kijamii kukawa na mazungumzo juu ya maombi, kutafakari, ibada na kujifunza Biblia. . . . Watazamaji wanasema kwamba maelekeo hayo yanaonyesha kwamba watu wenye imani ya kidini wameanza jitihada mpya ya ‘kutafuta mambo matakatifu’ katika jamii ya watu ambao wamezidi kuiacha misingi yao ya kidini.”—U.S. News & World Report.
“Katika sehemu za Ulaya ya Mashariki, kuna ishara za kwamba dini imepata nguvu mpya . . . . Katika Hungary, Czechoslovakia, Ujeremani ya Mashariki na Poland, viongozi wa kidini na wanachuo wanasema watu zaidi na zaidi wanaendea—au wanarudia makanisa. . . . Vijana wanauliza, ‘Sababu gani tunaishi?’”—The New York Times.
JE! TUNAONA hali ya kiroho ikianza kurudi, tukiamua kulingana na ripoti kama hizo? Ingawa ukuzi katika makanisa umeachwa nyuma na ukuzi wa idadi ya watu, katika miaka michache iliyopita maongezeko madogo-madogo yanaonekana hapa na pale. Wakuu fulani wa makanisa wanaona huo kuwa wonyesho wa kwamba hali ya kushuka kwa makanisa tangu miaka ya 1960 imeanza kumalizika, na sasa maendeleo yameanza kuja. Iwe ndivyo ilivyo au sivyo, tunaweza kuuliza: Kwa sababu gani watu hao wanayageukia makanisa?
Kwa Sababu Gani “Nguvu Mpya”?
“Watu wana njaa ya kweli, maoni ya kwamba wana ukosefu fulani wa kiroho ndani yao,” anasema Tilden Edwards padri Mwamerika wa Episkopali. Ndiyo kusema, inaonekana kuwa watu wengi zaidi wamefunguka macho wakaona upungufu ulio katika maisha ya kufuatia vitu vya kimwili na vya kilimwengu, nao wanatafuta maana na kusudi la maisha. Wengine, kwa sababu ya kushikwa sana na woga juu ya maangamizi yanayoweza kuletwa na silaha za nyukilia au kuogopa uhalifu na jeuri, au kwa sababu tu wamepatwa na msiba fulani wa kibinafsi, wanageukia dini wapate faraja ya moyoni.
Matokeo mengine yasiyotazamiwa ambayo yanaonekana wazi katika maelekeo hayo ni kuanzishwa na kukua kwa dini za Mashariki katika nchi za Magharibi. Mahekalu, majengo matakatifu, misikiti, sehemu za mikutano ya kutafakari, na mahali pengine, yanajengwa katika miji na hata maeneo ya mashambani katika nchi za Magharibi. Vinaonekana sana pia vikundi vya watu wanaojitia adabu kwa mazoea ya kutafakari mawazo yanayoyazidi ya kibinadamu, ya Zen na Hare Krishna. Kulingana na maoni ya wakuu fulani wa kidini, imani hizo “za kigeni” zinaelekea kutolea watu kitu ambacho wengi katika jamii ya Magharibi wanatafuta: mamlaka ya kuwaambia wataamini nini, kusudi la kuongozea maisha yao, kujisikia kwamba wao ni sehemu ya kikundi cha watu wanaojuana vizuri na kuwa na amani ya kindani au kujielewa.
Ni Nguvu Mpya au Ni Ugumu?
Uhakika wa kwamba watu wanageukia dini wapate majibu wakati wanapokabiliwa na nyakati zenye magumu na hatari, au wanasumbuliwa na ukosefu wa kusudi katika njia yao ya maisha, unaonyesha wazi ukweli wa msingi uliotajwa na Yesu Kristo: “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mathayo 4:4) Kufuata njia ya maisha ya utafutaji wa vitu vya kimwili tu hakumpi mtu nguvu na uvumilivu unaohitajiwa ili kushughulika na mengi ya matatizo ya leo.
Kwa kweli, watazamaji fulani wanaamini kwamba ukosefu huo wa hali ya kiroho ndio umeleta kwa kiasi fulani mabaya mengi yaliyo katika jamii ya watu wa kisasa. Alexander Solzhenitsyn mwandikaji Mrusi aliye mashuhuri alisema, “Hali za kupungukiwa kwa kibinadamu, zenye ukosefu wa mambo ya kimungu, zimehusika katika kuleta uhalifu wote mkubwa-mkubwa wa karne hii.”
Kwa sababu ya kuelekeana na ugumu wa kiroho, lazima tuulize hivi: Je! makanisa yanatimiza kazi kubwa ya kutosheleza mahitaji ya kiroho ya wale wanaoyageukia? Je! watu hao wanaweza kupata uongozi wa kiroho na nguvu wanazotafuta? Ikisemwa wazi, je! dini inaweza kumaliza ugumu uliopo leo?