Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 3/1 kur. 26-30
  • Kuufuatia Mradi Uliowekwa Tangu Umri wa Miaka Sita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuufuatia Mradi Uliowekwa Tangu Umri wa Miaka Sita
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kufanyia Kazi Mradi Wangu
  • Hatimaye Gileadi!
  • Wamishonari Katika Moroko
  • Kwenda Hadi Afrika ya Kati
  • Hatimaye, Kwenda Sierra Leone
  • Wazazi Wetu Walitufundisha Kumpenda Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Nina Amani na Mungu Pamoja na Mama Yangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Urithi wa Kikristo Usio wa Kawaida
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kutafuta Ufalme Kwanza Huridhisha na Huleta Furaha Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 3/1 kur. 26-30

Kuufuatia Mradi Uliowekwa Tangu Umri wa Miaka Sita

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA SANDRA COWAN

Wazazi wengi huwachagulia watoto wao kazi-maisha kama vile muziki au kucheza balei (ngoma za kuigiza hadithi), na huanza kuwazoeza tangu umri wa mapema sana. Hilo ndilo jambo ambalo mama yangu alinifanyia. Kuanzia wakati nilipokuwa mwenye umri wa majuma mawili, nilipelekwa kwenye mikutano yote ya Kikristo na katika huduma ya shambani.

NILIPOKUWA na miaka minne, mama alifikiri nilikuwa tayari kuhubiri peke yangu. Nakumbuka kwa dhahiri jaribio langu la kwanza. Tulikuwa tumeendesha gari hadi kwenye nyumba kubwa ya shambani, na wakati mama na wengine walipokuwa wanangojea garini, nilitoka na kutembea hadi mlangoni. Mwanamke mwenye fadhili alisikiliza nilipokuwa nikimtolea vijitabu kumi. Ili kuvilipia, alinipa kipande kikubwa cha sabuni. Ilinibidi nitumie mikono yangu yote miwili kukibeba. Nilisisimuka kwelikweli!

Mwaka uo huo, 1943, Watchtower Bible School of Gilead ilitoa nafasi ya kuzoeza wahudumu mapainia wa wakati wote kwa kazi ya umishonari. Mama alinitia moyo nifanye utumishi wa umishonari uwe mradi wangu maishani. Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa kali sana katika Ulaya wakati huo, na mama alikuwa ananiambia juu ya watoto Mashahidi wachanga katika Ulaya waliochukuliwa mbali na wazazi wao. Alinitaka niwe imara vya kutosha kuvumilia jaribu la aina yoyote.

Katika kiangazi cha 1946, nilibatizwa kwenye mkusanyiko wa kimataifa katika Cleveland, Ohio. Ingawa nilikuwa mwenye umri wa miaka sita tu, nilipiga moyo konde kutimiza wakfu wangu kwa Yehova. Katika kiangazi hicho nilitumikia nikiwa painia kwa mara ya kwanza. Nakumbuka asubuhi moja nikiangusha magazeti 40 kwa watu waliokuwa wameketi kwenye The Plaza katika San Diego, California. Nina uhakika kwamba, kuwa kwangu mdogo na mwenye maneno mengi kulichangia sana jambo hilo.

Mara nyingi tulihubiri karibu na Beth-Sarim, palipokuwa mahali ambapo Ndugu Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Society mwenye kuugua, alikuwa amepitisha nyakati za kipupwe kabla ya kifo chake katika 1942. Tulizuru kwa kawaida na kula chakula cha jioni pamoja na watumishi wa wakati wote huko. Ziara za furaha za jinsi hiyo zilinifanya niamue kwamba hiyo kwa kweli ndiyo ilikuwa aina ya maisha niliyotaka. Kisha nikafanya Shule ya Gileadi na utumishi wa umishonari uwe mradi wangu maishani.

Mwaka uliofuata wazazi wangu walitalikana, lakini hali iliyobadilika ya familia haikupunguza hali yangu ya kiroho. Mama alikuwa painia na alihangaikia sana mazoezi ambayo ndugu yangu na mimi tulipokea. Gari-nyumba letu dogo lilikuwa mahali pachangamfu kukiwa na ziara za ndugu na dada Wakristo. Mama alifanya jitihada ya kipekee ili nikutane na wahitimu wa Gileadi. Wawili wa wahitimu hao walikuwa Lloyd na Melba Barry, waliokuwa wakizuru katika kazi ya kusafiri wakingojea kwenda kwenye mgawo wao wa kigeni katika Japani. Walichukua wakati kunitia moyo—msichana mdogo aliyetamani kuwa mishonari—na hilo lilinivutia sana.

Nilipokuwa mwenye umri wa miaka kumi, mama aliolewa na Shahidi mzuri ajabu aliyekuwa pia mhudumu painia. Alifanya ndugu yangu na mimi kuwa watoto wake si kwenye karatasi tu bali pia moyoni mwake. Kumpenda kwake Yehova na bidii yake kwa ajili ya utumishi ilikuwa yenye kuambukiza.

Mama na baba walifanya kazi kwa umoja kutuongoza sisi watoto wawili kupitia miaka migumu ya utineja. Nyumba yetu ilikuwa mahali pa ustarehe wa kiroho ambapo ninakumbuka kwa uthamini. Halikuwa jambo rahisi kwao kupainia wakiwa na machumo madogo hali wakilea watoto wawili; lilihitaji kujidhabihu. Lakini mama na baba walimtegemea Yehova na kuweka masilahi ya Ufalme kwanza.

Nakumbuka vizuri kama nini ule mkusanyiko wa kimataifa katika New York City mwaka 1950! Baba alipata mkopo kutoka benki, na tulichukua abiria watatu ili wasaidie na gharama. Mama, baba, ndugu yangu, na mimi tuliketi pamoja kwenye kiti cha mbele mwendo wote kutoka San Diego hadi New York, hali wengine waliketi kiti cha nyuma. Kwa sababu mwajiri wa baba alikataa kumpa likizo ya majuma mawili, kuhudhuria kusanyiko hilo kulimfanya apoteze kazi yake. Lakini kama vile baba alivyotuhakikishia, Yehova angeandaa mahitaji yetu, Naye alifanya hivyo. Baba aliuza gari ili kulipia mkopo wa Benki, na kisha akapata kazi bora zaidi. Ono hilo na mengine kama hayo yalithibitika kuwa yenye thamani kubwa sana kwangu baadaye wakati mume wangu nami tulipokabili hali ngumu.

Kwenye safari yetu ya kurudi kutoka New York, tulizuru Kingdom Farm, ambapo nilipata kuona Shule ya Gileadi kwa mara ya kwanza. Nakumbuka nikisimama ndani ya darasa moja na kujiambia mwenyewe, ‘Sijafika miaka 11 bado. Sitapata kamwe kuja hapa. Har–Magedoni itakuja kwanza.’ Lakini ziara hiyo ilinifanya nipige moyo konde zaidi ya wakati mwingine wowote kufanya Gileadi iwe mradi wangu.

Kufanyia Kazi Mradi Wangu

Nilipainia kila likizo la kiangazi muda wote wa shule, tangu kidato cha kwanza na kuendelea. Kisha, majuma mawili baada ya kuhitimu kutoka shule ya upili katika Juni 1957, nikawa painia wa kawaida.

Mkutano wa mkusanyiko wa wilaya kwa wale wanaopendezwa na Gileadi uliofanywa kwenye mkusanyiko wa Los Angeles katika 1957 ulikuwa wa pekee kwangu. Nilipokuwa nikitembea kuingia hema ya mkutano huo, nilikutana na Bill, ndugu kijana ambaye nilikuwa nimemjua tangu nilipokuwa na umri wa miaka sita. Kwa mwaka mmoja uliopita, alikuwa mbali akitumikia mahali penye uhitaji mwingi zaidi katika Louisiana. Tulishangaa kupata kujua jinsi sote wawili tulivyopendezwa sana na utumishi wa umishonari. Miezi sita baadaye tuliamua kufanya huo uwe mradi wa pamoja. Tuliandikia Sosaiti tukiomba mgawo na mwezi mmoja kabla ya arusi yetu, tulipokea mmoja katika Romney, West Virginia.

Tulihamia huko tulipokuwa njiani kwenda kwenye mkusanyiko wa New York katika 1958. Tulipokuwa kwenye mkusanyiko huo, tulihudhuria mkutano wa wale waliopendezwa na Gileadi. Mamia walikuwapo. Tulipoangalia umati huo, tulihisi kwamba mataraja yetu ya kuitwa Gileadi yalikuwa madogo sana. Hata hivyo, tulitoa ombi la kwanza, hata ingawa tulikuwa tumeoana kwa muda wa majuma 11 tu. Mwaka uliofuata kwenye mkusanyiko wa wilaya katika Philadelphia, tulitoa ombi la pili.

Bill na mimi tulijifunza katika Romney kumtegemea Yehova atusaidie kupitia hali ngumu. Romney ulikuwa mji wa karibu wakaaji 2,000. Kazi haikuweza kupatikana. Tuliishi katika gari-nyumba lenye kutengenezwa kwa mkono la urefu wa meta 5 lililobuniwa kufaa hali ya anga ya California. Hatukuwa na maji ya mfereji, wala kipasha-joto, wala friji. Mlikuwa baridi sana ndani hivi kwamba tulihitaji kuvunja barafu katika ndoo ili kupata maji. Ndugu walitusaidia kwa kadiri walivyoweza, wakishiriki chakula ambacho walikuwa wamewinda. Tulikula swala, rakuni, na kindi. Zaidi ya mara moja tulifikiri hatungekuwa na chochote cha kula kwa siku hiyo, halafu tuliporudi nyumbani kutoka utumishi, tulikuwa tunapata matofaa au jibini vimeachwa mbele ya mlango wetu.

Tulijitahidi kwa miezi tisa tukiishi tukiwa na pesa kidogo sana zilizozidi kupungua kila wakati. Hatimaye, tuliamua kwamba lingekuwa jambo la hekima kuhamia Baltimore, Maryland, ambapo Bill angeweza kupata kazi. Tulipoambia ndugu juu ya uamuzi wetu, walilia nasi tukalia. Kwa hiyo tuliamua tuvumilie kidogo zaidi.

Baada tu ya hapo Shahidi mmoja aliyekuwa meneja wa duka kubwa katika Westernport, Maryland, mwendo wa karibu kilometa 60 kutoka hapo, alimtolea Bill kazi isiyo ya wakati wote. Mwezi huo huo mmoja wa wa-nafunzi wetu wa Biblia alitutolea nyumba ndogo yenye kupendeza iliyokuwa na fanicha pamoja na jiko kubwa la makaa. Huo ndio wakati Malaki 3:10 likawa andiko nililopenda zaidi. Yehova alikuwa ametumwagia baraka nyingi kupita matazamio yetu.

Hatimaye Gileadi!

Mojawapo siku zenye kusisimua sana za maisha yetu ilikuwa ile siku, katika Novemba 1959, tulipopokea mwaliko wetu kwenda Gileadi. Tulialikwa kwenye darasa la 35, la mwisho lililofanywa kwenye Kingdom Farm. Niliposimama katika darasa lile lile nililozuru nikiwa mtoto, nilikuwa na hisia changamfu, yenye furaha ambayo hakuna maneno yawezayo kuieleza inavyofaa.

Gileadi ilikuwa mahali pa kiroho penye chemchemi katika jangwa. Ilikuwa kana kwamba kuishi katika ulimwengu mpya kwa miezi mitano. Si mara nyingi maishani tunapopata kwamba jambo fulani tulilongojea kwa miaka mingi latokea kuwa bora zaidi ya vile tulivyotarajia. Lakini Gileadi ilikuwa hivyo barabara.

Tulipewa mgawo kwenda India, lakini hatimaye tukakataliwa viza. Kwa hiyo, baada ya mwaka mmoja wa kungojea katika New York City, Watch Tower Society ikatupa mgawo mwingine kwenda Moroko, Afrika Kaskazini.

Wamishonari Katika Moroko

Tulitumia miaka 24 yenye shangwe katika Moroko, tukipata kuwapenda wale watu mara tulipowasili. Tulijifunza Kifaransa na Kihispania pia, lugha zilizotusaidia kuwasiliana na watu wa mataifa mengi walioishi huko. Ni wale watu hasa kutoka nchi nyinginezo walioitikia ujumbe wa Ufalme.

Mwanamke mmoja niliyejifunza Biblia naye alikuwa Mhispania mwenye kucheza ngoma za flamenko aliyeajiriwa katika mkahawa mmoja Kasablanka. Baada ya kujifunza kanuni za Biblia, alimwacha mwenye mkahawa huo aliyekuwa akiishi naye na kurudi Hispania. Huko alitoa ushahidi kwa wote katika familia yake, na wengine wao walizikubali kweli za Biblia alizoshiriki nao. Baadaye alirudi Kasablanka, ambako alibaki mwaminifu kwa Mungu hadi kifo chake katika 1990.

Miaka yetu michache ya kwanza katika Moroko iliona maongezeko katika idadi ya wahubiri wa Ufalme. Hata hivyo, ilipoanza kuwa vigumu kwa wageni kupata kazi na idhini za kukaa huko, Mashahidi wengi wakaanza kutoka kwenda Ulaya. Wengine wa wale tuliosoma nao wako sasa katika New Zealand, Kanada, United States, Bulgaria, Urusi, na Ufaransa, na wengine wao hushiriki katika utumishi wa wakati wote.

Kwa ghafula, katika Aprili 1973 kazi yetu ya kuhubiri katika Moroko ilipigwa marufuku. Hilo lilikuwa pigo lililoje! Alhamisi jioni, tulikuwa tumekuwa umati wenye furaha kwenye Jumba la Ufalme, tukiongea mpaka taa zilipozimwa kutujulisha kwamba ulikuwa wakati wa kwenda nyumbani. Hatukujua hata kidogo kwamba tusingeona tena kamwe taa hizo zikimulikia ushirika wa Kikristo wa wazi kama huo. Chini ya hali za kupigwa marufuku, mikutano na makusanyiko yetu ya mzunguko yalifanywa katika vikundi vidogo tu katika nyumba za faragha. Ili kuhudhuria mikusanyiko ya wilaya, Mashahidi walisafiri kwenda ama Ufaransa ama Hispania.

Idadi zetu zilipopungua, Mashahidi wale wachache waliobaki Moroko wakawa karibu sana wao kwa wao. Kwa hiyo Watch Tower Society ilipoamua hatimaye kulifunga tawi na kutupa sisi mgawo kwingineko, sisi sote tulilia sana.

Kwenda Hadi Afrika ya Kati

Mgawo wetu mpya ulikuwa Jamhuri ya Afrika ya Kati. Hiyo ilitofautiana sana kama nini na Afrika Kaskazini! Hali Moroko ilikuwa na hali ya anga iliyofanana sana na kusini mwa California, sasa tulijipata wenyewe katika tropiki zenye joto na unyevu.

Kulikuwako matatizo mapya ya kukabili. Kwa mfano, sasa nilihitaji kudhibiti woga wangu wa wanyama watambaazi. Katika pindi tatu mjusi alianguka kwenye kichwa changu nilipokuwa nikitembea kupitia mlango. Nyakati nyingine, nilipokuwa nikiongoza funzo la Biblia, panya angeamua kuungana nasi! Ingawa nilitaka kuruka na kukimbia, nilijifunza kujidhibiti mwenyewe, huku nikiwa siachi kumwangalia Bwana Panya na kuondoa mkoba na miguu yangu kutoka sakafuni mpaka alipoamua kwenda zake. Nilipata kwamba waweza kuzoea jambo lolote ukijitahidi tu.

Tulipokuwa tumekuwa huko kwa miezi sita, tangazo lilifanywa kwenye redio kwamba kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku. Kwa hiyo Majumba ya Ufalme yetu yalifungwa, na wamishonari waliombwa waondoke. Ni sisi na wenzi wengine wa ndoa tu tulioweza kuendelea kubaki kwenye tawi kwa miaka mingine mitatu. Kisha Asubuhi moja ya Jumapili wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi letu, polisi wenye silaha wakaja na kutupeleka kwenye makao makuu ya polisi. Waliwaachilia wanawake na watoto, lakini waliwafunga ndugu 23, kutia na mume wangu Bill. Baada ya siku sita walimwachilia aende nyumbani na kufunga mizigo; siku tatu baadaye, kwa amri ya serikali, tuliondoka nchini, katika Mei 1989. Huo ulikuwa mwachano mwingine wenye huzuni kwenye uwanja wa ndege, ambako wengi wa ndugu zetu wenye upendo walikuja kutuaga.

Hatimaye, Kwenda Sierra Leone

Mgawo wetu wa sasa ni Sierra Leone, Afrika Magharibi, nchi yenye kupendeza iliyo na pwani nzuri zenye mchanga mweupe. Watu ni wenye urafiki sana, na huduma ya shambani hufurahisha. Tunaalikwa kuketi kwenye kila nyumba, mara nyingi chini ya kivuli cha mwembe au mnazi. Watu hupenda kuongea juu ya Mungu na kupata nakala zao wenyewe za Biblia ili wafuatane.

Bill na mimi hufanya kazi kwenye Kao la Betheli la Freetown. Mimi hutumikia nikiwa mpokezi na pia kushughulikia maandikisho na hesabu za kundi. Baada ya miaka 16 nikitumikia katika nchi ambako kazi yetu ya kuhubiri imepigwa marufuku, ni jambo zuri ajabu kuwa katika nchi ambako kazi i huru na yasitawi.

Nilimaliza miaka 30 ya utumishi wa umishonari katika Juni 1991. Kwa kweli, mama aliniwekea mbele yangu mradi uliofaa zaidi! Ikiwa angalikuwa hai bado, ningalipenda kumwambia tena, “Asante mama!” Kwa furaha, ningali naweza kusema, “Asante, baba!”

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mkusanyiko wa New York, 1958

[Picha katika ukurasa wa 29]

35th class—July, 1960

[Picha katika ukurasa wa 30]

Bill na Sandra Cowan, 1991

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki