Mwenyeji au Mgeni Mungu Akukaribisha!
“Alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote.”—MATENDO 17:26.
1. Ni tatizo gani lililomo mahali pengi leo kuhusu kukubaliwa kwa watu kutoka tamaduni za kigeni?
RIPOTI za vyombo vya habari huonyesha kwamba katika nchi nyingi hangaiko linaongezeka juu ya wageni (wasio wazalia), wahamiaji, na wakimbizi. Mamilioni wanatamani sana kuhama kutoka sehemu za Esia, Afrika, Ulaya, na bara na visiwa vya Amerika. Labda wanatafuta kitulizo kutoka katika umaskini mwingi, vita vya wenyewe kwa wenyewe, au mnyanyaso. Lakini je, wao wanakaribishwa kwingineko? Gazeti Time lilitaarifu hivi: “Mchanganyiko wa kikabila wa Ulaya uanzapo kubadilika, nchi nyinginezo zavumbua kwamba hazivumilii tamaduni za kigeni kwa kadiri zilivyofikiria wakati mmoja zilivumilia.” Juu ya wakimbizi 18,000,000 “wasiotakwa,” Time lasema hivi: “Tatizo wanalotolea mataifa yaliyo madhubutu halitaondoka.”
2, 3. (a) Biblia hutoa uhakikisho gani wenye kuburudisha kuhusiana na kukubaliwa? (b) Ni kwa nini twaweza kunufaika kutokana na kuchunguza yale ambayo Maandiko huonyesha kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika na jamii ya watu?
2 Chochote kitakachotokea kwa habari hiyo, Biblia huonyesha kwamba Mungu hukaribisha watu wa kila taifa—mtu awe ni mwenyeji aliyezaliwa kiasili, awe ni mhamiaji, au mkimbizi. (Matendo 10:34, 35) ‘Hata hivyo,’ wengine huenda wakauliza, ‘waweza kusemaje hivyo? Je! Mungu hakuchagua Israeli wa kale tu kuwa watu wake, akiwaacha wengine?’
3 Basi, acheni tuone jinsi Mungu alivyoshughulika na jamii ya watu wa kale. Twaweza kuchunguza pia unabii fulani mbalimbali unaohusu mapendeleo yanayopatikana kwa waabudu wa kweli leo. Kupitia habari hiyo ya kiunabii waweza kupata uelewevu ulio kamili zaidi ambao huenda ukaupata kuwa wenye kutia moyo sana. Kunaonyesha pia, jinsi Mungu awezavyo kushughulika na watu mmoja mmoja “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” baada ya ile dhiki kubwa.—Ufunuo 7:9, 14-17.
‘Mataifa Yote Watajibarikia’
4. Tatizo la utaifa lilisitawije, lakini Mungu alichukua hatua zipi?
4 Baada ya Furiko, familia ya Noa ya karibu ilifanyiza ainabinadamu yote, na wote walikuwa waabudu wa kweli. Lakini umoja huo ulibadilika upesi. Kabla ya muda mrefu, watu fulani, wakipuuza mapenzi ya Mungu, walianza kujenga mnara. Hilo likaongoza kwenye kugawanyika kwa aina ya kibinadamu katika vikundi vya lugha vilivyokuja kuwa jamii za watu na mataifa yaliyotawanyika. (Mwanzo 11:1-9) Hata hivyo, ibada ya kweli iliendelea katika nasaba iliyofika hadi Abrahamu. Mungu alimbariki Abrahamu mwaminifu na kuahidi kwamba uzao wake ungekuwa taifa kubwa. (Mwanzo 12:1-3) Taifa hilo lilikuwa Israeli wa kale.
5. Ni kwa nini sisi sote twaweza kutiwa moyo kutokana na jinsi Mungu alivyoshughulika na Abrahamu?
5 Hata hivyo, Yehova hakuwa akiwaacha watu wengine ila Israeli, kwani kusudi lake lilienea ili kuhusisha ainabinadamu yote. Twaona hilo wazi kutoka kwa lile ambalo Mungu alimwahidi Abrahamu: “Katika uzao [mbegu, NW] wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Hata hivyo, kwa karne nyingi, Mungu alishughulika katika njia ya pekee pamoja na Israeli, kwa kutoa fungu la Sheria ya kitaifa, kupanga ili makuhani watoe dhabihu kwenye hekalu lake, na kuandaa Bara Lililoahidiwa ambamo waliweza kuishi.
6. Mipango ya Mungu pamoja na Israeli ingenufaishaje wote?
6 Sheria ya Mungu kwa Israeli ilifaa watu wa mataifa yote kwa kuwa ilionyesha udhambi wa kibinadamu kwa wazi, ikionyesha uhitaji wa dhabihu kamilifu ili kufunika dhambi ya kibinadamu mara moja kwa wakati wote. (Wagalatia 3:19; Waebrania 7:26-28; 9:9; 10:1-12) Hata hivyo, kulikuwako uhakikisho gani kwamba Mbegu ya Abrahamu—ambayo kupitia hiyo mataifa yote yangejibarikia—ingewasili na kutimiza matakwa ya ustahili? Sheria ya Israeli ilisaidia hapa pia. Ilikataza ndoa pamoja na Wakanaani, watu waliojulikana sana kwa mazoea na vitendo vya ibada vyenye kukosa maadili, kama vile ile desturi ya kuchoma watoto wakiwa hai. (Mambo ya Walawi 18:6-24; 20:2, 3; Kumbukumbu la Torati 12:29-31; 18:9-12) Mungu aliagiza kwamba wao na mazoea yao yalipasa yaangamizwe. Jambo hilo lingekuwa kwa faida ya muda mrefu ya wote, kutia na mkazi mgeni, kwa kuwa lingetumika kulinda nasaba ya Mbegu ili isifisidiwe.—Mambo ya Walawi 18:24-28; Kumbukumbu la Torati 7:1-5; 9:5; 20:15-18.
7. Kulikuwako wonyesho gani wa mapema kwamba Mungu aliwakaribisha wageni?
7 Hata wakati Sheria ilipokuwa ikitenda na Mungu aliona Israeli kuwa taifa la pekee, alionyesha huruma kwa wasio Waisraeli. Nia yake ya kufanya hivyo ilikuwa imeonyeshwa wakati Israeli walipoondoka katika utumwa wa Kimisri kuelekea bara lao wenyewe. “Kundi kubwa la watu waliochangamana nao wakakwea pamoja nao.” (Kutoka 12:38) Profesa C. F. Keil hutambulisha hao kuwa “Kundi la wageni . . . mchanganyiko, au umati wa watu wa mataifa tofauti.” (Mambo ya Walawi 24:10; Hesabu 11:4) Yaelekea kwamba wengi walikuwa Wamisri waliomkubali Mungu wa kweli.
Ukaribishaji kwa Wageni
8. Wagibeoni walipataje mahali miongoni mwa watu wa Mungu?
8 Israeli walipotekeleza amri ya Mungu ya kuondolea mbali mataifa mapotovu kutoka kwa Bara Lililoahidiwa, alilinda kikundi kimoja cha wageni, Wagibeoni, walioishi kaskazini mwa Yerusalemu. Walituma kwa Yoshua mabalozi waliofanya hila waende, wakiomba na kupata amani. Hila yao ilipogunduliwa, Yoshua aliamuru kwamba Wagibeoni wangetumikia wakiwa “wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya mkutano, na kwa ajili ya madhabahu ya BWANA [Yehova, NW].” (Yoshua 9:3-27) Leo wahamiaji wengi pia hukubali vyeo vya utumishi vya chini ili kuwa sehemu ya watu wapya.
9. Mfano wa Rahabu na familia yake unatiaje moyo kwa habari ya wageni katika Israeli?
9 Huenda ikakutia moyo kujua kwamba ukaribishaji wa Mungu haukuwa kwa vikundi vya wageni tu wakati huo wa nyuma; watu mmoja mmoja walikaribishwa pia. Leo baadhi ya mataifa hukaribisha wale wahamiaji tu walio na cheo cha juu, mali ya kufanyia biashara, au elimu ya juu. Sivyo na Yehova, kama tunavyoona kutokana na tukio la kabla tu ya kile kisa cha Wagibeoni. Hilo lilihusisha Mkanaani ambaye kwa hakika hakuwa na cheo cha juu. Biblia humwita “Rahabu, yule kahaba.” Kwa sababu ya imani yake katika Mungu wa kweli, yeye na familia yake walikombolewa wakati Yeriko uliposhindwa. Ingawa Rahabu alikuwa mgeni (asiye mzalia), Waisraeli walimkubali. Yeye alikuwa kiolezo cha imani kinachostahili kuigwa na sisi. (Waebrania 11:30, 31, 39, 40; Yoshua 2:1-21; 6:1-25) Yeye hata alipata kuwa nyanya wa kale wa Mesiya.—Mathayo 1:5, 16.
10. Kukubaliwa kwa wageni katika Israeli kulitegemea nini?
10 Wasio Waisraeli walikubaliwa katika Bara Lililoahidiwa kwa kupatana na jitihada yao ya kumpendeza Mungu wa kweli. Waisraeli waliambiwa wasishirikiane, hasa kidini, pamoja na wale ambao hawakumtumikia Yehova. (Yoshua 23:6, 7, 12, 13; 1 Wafalme 11:1-8; Mithali 6:23-28) Bado, masetla wengi wasio Waisraeli walitii sheria za msingi. Wengine hata walipata kuwa waongofu waliotahiriwa, na Yehova aliwakaribisha kikamili kuwa washiriki wa kundi lake.—Mambo ya Walawi 20:2; 24:22; Hesabu 15: 14-16; Matendo 8:27.a
11, 12. (a) Waisraeli walitakiwa watendeeje waabudu wageni? (b) Kwa nini huenda tukahitaji kufanya maendeleo katika kufuata mfano wa Yehova?
11 Mungu aliwaamuru Waisraeli wauige mtazamo wake kuelekea waabudu wageni: “Na mgeni [mkazi mgeni, NW] akikaa pamoja nawe katika nchi yako, usimdhulumu. Mgeni akaaye pamoja nawe atakuwa kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako; kwa maana ninyi mlikuwa wageni [wakazi wageni, NW] katika nchi ya Misri.” (Mambo ya Walawi 19:33, 34; Kumbukumbu la Torati 1:16; 10:12-19) Hilo huandaa somo kwetu, hata ingawa hatuko chini ya Sheria. Ni rahisi kunaswa katika mtego wa kuwa na chuki zisizo na msingi na uadui kuelekea wale wa jamii, taifa, au desturi nyingine. Kwa hiyo twafanya vema kuuliza: ‘Je! ninajaribu kujiondolea mbali chuki kama hizo zisizo na msingi, kwa kufuata mfano wa Yehova?’
12 Waisraeli walikuwa na uthibitisho wenye kuonekana wa ukaribishaji wa Mungu. Mfalme Sulemani alisali hivi: “Mgeni [asiye mazalia, NW] naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana kwa ajili ya jina lako . . . atakapokuja na kuomba kuielekea nyumba hii; basi, usikie huko mbinguni . . . ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukucha wewe.”—1 Wafalme 8:41-43; 2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33.
13. Ni kwa nini Mungu alitoa uwezekano wa kubadili kushughulika kwake na Israeli?
13 Yehova alipokuwa angali akilitumia taifa la Israeli kuwa watu wake na hivyo akiilinda nasaba ya Mesiya, Mungu alitabiri mabadiliko ya maana. Mapema zaidi, Israeli walipokubali kuwa katika agano la Sheria, Mungu aliwatolea uwezekano wa kuwa chanzo cha “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6) Lakini Israeli hawakuonyesha uaminifu kwa muda wa karne nyingi. Kwa hiyo Yehova alitabiri kwamba yeye angefanya agano jipya ambalo chini yalo wale waliofanyiza “nyumba ya Israeli” wangesamehewa makosa na dhambi zao. (Yeremia 31:33, 34) Lile agano jipya lilimngojea Mesiya, ambaye dhabihu yake kwa kweli ingesafisha wengi dhambi.—Isaya 53:5-7, 10-12.
Waisraeli Mbinguni
14. Yehova alikubali “Israeli” gani mpya, na kwa jinsi gani?
14 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hutusaidia tuelewe jinsi hayo yote yalivyotimizwa. Yesu ndiye aliyekuwa Mesiya, ambaye kifo chake kilitimiza ile Sheria na kuwekea msingi msamaha kamili wa dhambi. Kupata faida hiyo, mtu hakuhitaji kuwa Myahudi aliyetahiriwa katika mnofu. La. Mtume Paulo aliandika kwamba katika agano jipya, “yeye ni Myahudi aliye Myahudi kwa ndani; na tohara ni ya moyo, katika roho, si katika andiko.” (Warumi 2:28, 29; 7:6) Wale walioweka imani katika dhabihu ya Yesu walipata msamaha, na Mungu aliwakubali kuwa ‘Wayahudi katika roho,’ waliojumuika kuwa taifa la kiroho liitwalo “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16.
15. Ni kwa nini utaifa wa kimnofu si jambo la maana katika kuwa sehemu ya Israeli wa kiroho?
15 Naam, kukubaliwa katika Israeli wa kiroho hakukutegemea malezi fulani ya kitaifa au ya kikabila. Wengine, kama vile mitume wa Yesu walikuwa Wayahudi wa asili. Wengine, kama vile yule ofisa wa jeshi Mroma Kornelio, walikuwa Wasio-Wayahudi wasiotahiriwa. (Matendo 10:34, 35, 44-48) Paulo alisema kwa usahihi kuhusu Israeli wa kiroho: “Hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru.” (Wakolosai 3:11, HNWW) Wale waliopakwa mafuta kwa roho ya Mungu walipata kuwa “mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu.”—1 Petro 2:9; linganisha Kutoka 19:5, 6.
16, 17. (a) Waisraeli wa kiroho wana daraka gani katika kusudi la Mungu? (b) Ni kwa nini inafaa kufikiria wale wasio wa Israeli wa Mungu?
16 Waisraeli wa kiroho wana wakati ujao gani katika kusudi la Mungu? Yesu alijibu hivi: “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.” (Luka 12:32) Wale wapakwa-mafuta, ambao ‘wenyeji wao uko mbinguni,’ watakuwa warithi-wenzi pamoja na Mwana-Kondoo katika utawala wake wa Ufalme. (Wafilipi 3:20; Yohana 14:2, 3; Ufunuo 5:9, 10) Biblia huonyesha kwamba hao ‘wanatiwa muhuri katika kila kabila ya Waisraeli’ na ‘kununuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.’ Idadi yao ni 144,000. Hata hivyo, baada ya kusimulia juu ya kukamilishwa kwa idadi hiyo, Yohana ajulisha kikundi tofauti—“mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.”—Ufunuo 7:4, 9; 14:1-4.
17 Wengine huenda wakataka kujua: ‘Vipi wale mamilioni ambao si sehemu ya Israeli wa kiroho, kama vile wale ambao huenda wakapitia dhiki kubwa wakiwa huo umati mkubwa? Wao wana daraka gani leo kuhusiana na wale wachache waliobaki wa Israeli wa kiroho?’b
Wageni Katika Unabii
18. Ni nini kilichoongoza kwenye kurudi kwa Israeli kutoka uhamisho wa Kibabuloni?
18 Tukirudi nyuma hadi wakati Israeli walipokuwa chini ya agano la Sheria lakini wakiwa wasio waaminifu kwalo, twapata kwamba Mungu aliazimia kuruhusu Wababuloni wafanye Israeli ukiwa. Katika 607 K.W.K., Israeli walipelekwa utumwani kwa muda wa miaka 70. Kisha Mungu akalinunua taifa hilo tena. Chini ya utawala wa Gavana Zerubabeli, mabaki ya Israeli wa asili walirudi bara lao. Watawala wa Wamedi na Waajemi, waliokuwa wamepindua Babuloni, hata waliwasaidia wale wahamishwa waliokuwa wakirudi kwa kuwapa maandalizi. Kitabu cha Isaya kilitabiri matukio hayo. (Isaya 1:1-9; 3:1-26; 14:1-5; 44:21-28; 47:1-4) Na Ezra anatupa sisi maelezo mengi hata yale madogomadogo ya kihistoria juu ya kurudi huko.—Ezra 1:1-11; 2:1, 2.
19. Kuhusiana na kurudi kwa Israeli, ni wonyesho gani wa kiunabii uliokuwako kwamba wageni wangehusika?
19 Bado, katika kutabiri kununuliwa tena na kurudi kwa watu wa Mungu, Isaya alitoa unabii huu wenye kushtusha: “Mataifa wataijilia nuru yako, na wafalme kuujia mwanga wa kuzuka kwako.” (Isaya 59:20; 60:3) Hilo lamaanisha zaidi ya kwamba wageni mmoja mmoja walikaribishwa, kwa kupatana na sala ya Sulemani. Isaya alikuwa akielekeza kwenye badiliko lisilo la kawaida katika cheo. “Mataifa” yangetumikia pamoja na wana wa Israeli: “Wageni [wasio wazalia, NW] watajenga kuta zako, na wafalme wao watakuhudumu; maana katika ghadhabu yangu nalikupiga, lakini katika upendeleo wangu nimekurehemu.”—Isaya 60:10.
20, 21. (a) Katika nyakati za ki-siku-hizi twapata ulinganisho gani wa kurudi kwa Israeli kutoka utumwani? (b) ‘Wana na binti’ waliongezwaje baadaye kwa Israeli wa kiroho?
20 Katika njia nyingi, kwenda kwa Israeli uhamishoni na kurudi kutoka huko kumepata ulinganisho katika nyakati za ki-siku-hizi katika Israeli wa kiroho. Kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, mabaki ya Wakristo wapakwa-mafuta hawakupatana kikamili na mapenzi ya Mungu; walishikilia maoni na mazoea fulani yaliyotoka makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Halafu, wakati wa msisimuko wa vita na kwa sehemu fulani kwa sababu ya kichocheo cha makasisi, wale wenye kuongoza miongoni mwa mabaki ya Israeli wa kiroho walifungwa gerezani isivyo haki. Baada ya vita, katika 1919 W.K., wale wapakwa-mafuta waliokuwa katika gereza halisi waliwekwa huru na kuondolewa hatiani. Hilo lilitoa ushuhuda kwamba watu wa Mungu walikuwa wamewekwa huru na utumwa wa Babuloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini bandia. Watu wake wakasonga mbele kujenga na kukalia paradiso ya kiroho.—Isaya 35:1-7; 65:13, 14.
21 Hilo lilionyeshwa katika ufafanuzi wa Isaya: “Wote wanakusanyana; wanakujia wewe; wana wako watakuja kutoka mbali; na binti zako watabebwa nyongani. Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, utajiri wa mataifa utakuwasilia.” (Isaya 60:4, 5) Katika miongo iliyofuata, ‘wana na binti’ waliendelea kuja, wakipakwa mafuta kwa roho kupajaza mahali pa mwisho katika Israeli wa kiroho.
22. “Wageni” wamekujaje kufanya kazi pamoja na Waisraeli wa kiroho?
22 Vipi juu ya ‘wageni watakaojenga kuta zako’? Hilo pia limetukia katika wakati wetu. Mwito wa wale 144,000 ulipokuwa karibu kukamilika, umati mkubwa kutoka mataifa yote ulianza kumiminika kuabudu pamoja na Israeli wa kiroho. Hawa wapya zaidi wana lile tazamio lenye msingi wa Biblia la uhai wa milele kwenye paradiso ya kidunia. Ingawa mahali ambapo hatimaye watafanya utumishi wao mwaminifu pangekuwa tofauti, walifurahia kusaidia mabaki ya wapakwa-mafuta katika kuhubiri habari njema za Ufalme.—Mathayo 24:14.
23. “Wageni” wamesaidia wapakwa-mafuta kwa kadiri gani?
23 Leo, zaidi ya 4,000,000 ambao ni “wageni,” pamoja na wale mabaki ya wale ‘wenyeji wa mbinguni,’ wanathibitisha ujitoaji wao mbidiifu kwa Yehova. Wengi wao, wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee, wanatumikia katika huduma ya wakati wote wakiwa mapainia. Katika mengi ya yale makundi zaidi ya 66,000, wageni kama hao wanachukua madaraka wakiwa wazee na watumishi wa huduma. Mabaki hushangilia hilo, wakiona utimizo wa maneno ya Isaya: “Wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu.”—Isaya 61:5.
24. Ni kwa nini twaweza kutiwa moyo na jinsi Mungu alivyoshughulika na Israeli na wengine katika wakati uliopita?
24 Kwa hiyo haidhuru wewe ni mwenyeji, mhamiaji, au mkimbizi katika nchi gani ya dunia, una ile fursa tukufu la kuwa mgeni wa kiroho ambaye akaribishwa kwa uchangamfu na Mweza Yote. Ukaribishaji wake hutia ndani uwezekano wa kuonea shangwe mapendeleo katika utumishi wake sasa na hata wakati ujao wa milele.
[Maelezo ya Chini]
a Kuhusu tofauti kati ya “alien resident” (mkazi mgeni), “settler” (setla), “stranger” (mtu asiyejulikana), na “foreigner” (mgeni), ona Insight on the Scriptures, Buku 1, kurasa 72-5, 849-51, lililotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Zaidi ya 10,600,000 walihudhuria ule ukumbusho wa kila mwaka wa Chakula cha Jioni cha Bwana uliofanywa na Mashahidi wa Yehova katika 1991, lakini ni 8,850 peke yao waliodai kuwa mabaki ya Israeli wa kiroho.
Je! Uliona Jambo Hili?
◻ Mungu alitoaje tumaini kwamba watu wa mataifa yote wangekubaliwa na Yeye?
◻ Ni nini kinachoonyesha kwamba watu wengine kuliko watu wa Mungu wa pekee, Israeli, wangeweza kumkaribia Yeye?
◻ Katika unabii, Mungu alionyeshaje kwamba wageni wangejiunga na Israeli?
◻ Ni nini ambalo limelingana na kurudi kwa Israeli kutoka uhamisho katika Babuloni, na “wageni” wamehusikaje?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mfalme Sulemani alisali kuhusu wageni ambao wangekuja kumwabudu Yehova