Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 5/1 kur. 8-13
  • Karibisha Akilini Siku ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Karibisha Akilini Siku ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Raia Wenye Kutii Sheria
  • Kutekeleza Uamuzi Wake
  • Kikosi cha Nzige
  • “Watu Wengi na Wenye Nguvu”
  • ‘Jazwa Roho Takatifu’
  • Siku ya Yehova Iko Karibu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Kitabu Cha Biblia Namba 29—Yoeli
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Yoeli Atoa Unabii juu ya Kisasi cha Yehova na Upendo Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Shambulizi Kutoka Kaskazini!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 5/1 kur. 8-13

Karibisha Akilini Siku ya Yehova

“Siku ya BWANA [Yehova, “NW”] i karibu, katika bonde la kukata maneno.”—YOELI 3:14.

1. Ni kwa nini ile vita takatifu inayokuja ambayo hutangazwa na Yehova itakuwa tofauti na vile vita ‘vitakatifu’ vya ainabinadamu?

“TANGAZENI haya kati ya mataifa; takaseni vita”! (Yoeli 3:9) Je! hilo lamaanisha vita takatifu? Tukitazama nyuma kwenye zile Krusedi, vita vya kidini, na vita vya ulimwengu viwili—ambavyo katika hivyo Jumuiya ya Wakristo ilishiriki sehemu kuu—huenda tukatetemeka kwa hofu kuwa na wazo tu la vita iitwayo eti “takatifu.” Hata hivyo, vita takatifu ya unabii wa Yoeli si vita miongoni mwa mataifa. Si kule kushindania kwa chuki juu ya eneo au mali, kwa kutumia dini kuwa udhuru. Hiyo ni vita yenye uadilifu. Ni vita ya Mungu ya kuondolea mbali pupa, ugomvi, ufisadi, na uonevu kutoka dunia. Itatetea enzi kuu iliyo haki ya Yehova juu ya milki yote ya uumbaji wake. Vita hiyo itafungulia njia Ufalme wa Kristo kuiingiza ainabinadamu ndani ya Mileani ya amani, ufanisi, na furaha ya ulimwengu wote mzima iliyotabiriwa na manabii wa Mungu.—Zaburi 37:9-11; Isaya 65:17, 18; Ufunuo 20:6.

2, 3. (a) “Siku ya BWANA [Yehova, NW]” iliyotolewa unabii kwenye Yoeli 3:14 ni nini? (b) Kwa nini mataifa hustahili lile watakalokabili kwa lazima katika siku hiyo?

2 Ni nini basi hiyo “siku ya BWANA [Yehova, NW]” iliyotabiriwa kwenye Yoeli 3:14? “Ole wake siku hii,” Yehova mwenyewe apaaza sauti, “kwa maana siku ya BWANA [Yehova, NW], inakaribia, nayo itakuja kama uangamivu utokao kwake aliye Mwenyezi”! Ni uangamivu jinsi gani? Nabii huyo aeleza baadaye: “Makutano makubwa, makutano makubwa, wamo katika bonde la kukata maneno! kwa maana siku ya BWANA [Yehova, NW] i karibu, katika bonde la kukata maneno.” (Yoeli 1:15; 3:14) Hiyo ndiyo siku ambayo katika hiyo Yehova atekeleza uamuzi wake wa kihukumu juu ya makutano ya kibinadamu yasiyomhofu Mungu ambayo huikataa enzi kuu iliyo haki yake juu ya mbingu na dunia. Ni uamuzi wa Yehova kuuangamiza mfumo wa mambo wa kishetani ambao kwa muda mrefu umekumbatia ainabinadamu katika mikono yao.—Yeremia 17:5-7; 25:31-33.

3 Ni lazima mfumo wa mambo wenye ufisadi ulio juu ya dunia ukabili uamuzi huo. Lakini je, mfumo wa ulimwengu ni mbaya sana hivyo? Kuchunguza kumbukumbu lao mara moja kwatosha! Yesu alitaarifu kanuni moja kwenye Mathayo 7:16: “Mtawatambua kwa matunda yao.” Je! majiji makubwa ya ulimwengu huu hayajawa madimbwi machafu ya dawa za kulevya, uhalifu, mao-gofyo makuu, utovu wa maadili, na uchafuzi? Katika nchi nyingi uhuru uliopatikana hivi karibuni unanyamazishwa na mvurugo wa kisiasa, upungufu wa chakula, na umaskini. Watu zaidi ya milioni elfu moja wanaishi kwa kutegemea riziki ya vipimo vya chakula wanachopewa wenye njaa. Zaidi ya hayo, ambukizo kubwa la UKIMWI, likichochewa na dawa za kulevya na mitindo ya maisha ya utovu wa maadili, linatisha sehemu kubwa ya dunia. Hasa tangu Vita ya Ulimwengu 1 ilipofyatuka katika 1914, kumekuwa mzoroto wa ulimenguni pote katika kila upande wa maisha.—Linganisha 2 Timotheo 3:1-5.

4. Yehova huwatolea mataifa mwito gani wa ushindani?

4 Hata hivyo, Yehova amekuwa akikusanya kutoka mataifa yote kikundi cha watu ambao hupokea kwa furaha maagizo juu ya njia zake na kutembea katika vijia vyake. Watu hao wa ulimwenguni pote wamefua panga zikawa majembe, wakiacha njia zenye jeuri za ulimwengu. (Isaya 2:2-4) Naam, panga kuwa majembe! Lakini je, hilo si kinyume cha wito ambao Yehova hufanya upigwe mbiu kwenye Yoeli 3:9, 10? Hapo twasoma hivi: “Tangazeni haya kati ya mataifa; takaseni vita; waamsheni mashujaa; watu wa vita na wakaribie; na wapande juu. Yafueni majembe yenu yawe panga, na miundu yenu iwe mikuki.” Lo, hapa Yehova anatolea watawala wa ulimwengu mwito wa ushindani walete nguvu yao ya kijeshi iliyounganishwa dhidi yake kwenye Har–Magedoni. Lakini hawawezi kufaulu! Ni lazima washindwe kabisa!—Ufunuo 16:16.

5. Tokeo litakuwa nini wakati Yesu anapovuna “mzabibu wa nchi”?

5 Watawala wenye nguvu wameunda zana za vita zenye kuogopesha, katika kukaidi Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova—lakini ni bure tu! Yehova atoa amri hii kwenye Yoeli 3:13: “Utieni mundu, maana mavuno yameiva; njoni, kanyageni; kwa maana shinikizo limejaa, mapipa nayo yanafurika; kwani uovu wao ni mwingi sana.” Maneno hayo yalingana na Ufunuo 14:18-20 ambapo yule Mfalme wa Kimesiya aliyevikwa taji, Yesu, aamuriwa ‘achume vichala vya mzabibu wa nchi, maana zabibu zake zimeiva sana.’ Mfalme huyo atia mundu mkali na kuyavurumisha mataifa hayo yenye ukaidi “katika shinikizo hilo kubwa la ghadhabu ya Mungu.” Kwa ufananisho, damu inatoka katika shinikizo hilo kufikia urefu wa hatamu za farasi, kwa mwendo wa farlong’i 1,600—karibu kilometa 300! Ni taraja lenye kuogofya kama nini kwa mataifa hayo ambayo humvunjia Yehova heshima!

Raia Wenye Kutii Sheria

6. Mashahidi wa Yehova huonaje mataifa na watawala wao?

6 Je! hilo lamaanisha kwamba Mashahidi wa Yehova hawastahi mataifa na watawala wayo? Sivyo hata kidogo! Wao hulaani tu ufisadi ambao wote waweza kuona waziwazi, nao hutoa onyo juu ya siku ya Yehova inayokaribia kwa kasi sana ya kutekeleza uamuzi wake. Wakati ule ule, wao hutii kwa unyenyekevu shauri la mtume Paulo kwenye Warumi 13:1: “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu.” Wanawapa watawala hao wa kibinadamu heshima wanaostahili lakini si ibada. Wakiwa raia wenye kutii sheria, wao hufuata viwango vya Biblia vya ufuatiaji haki, ukweli, na usafi nao hujenga maadili mazuri katika familia zao wenyewe. Wao husaidia wengine wajifunze jinsi wao pia wawezavyo kufanya hivyo. Wao huishi kwa amani na watu wote, hawajihusishi na maandamano ya kuteta au mapinduzi ya kisiasa. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuwa vielelezo vyema katika kutii sheria za mamlaka zilizo kuu za kibinadamu, huku wakingojea Mwenye Mamlaka Kuu Zaidi, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, arudishe amani kamilifu na serikali yenye uadilifu katika dunia hii.

Kutekeleza Uamuzi Wake

7, 8. (a) Mataifa yatatetemeshwa kwa njia gani na giza litakujaje juu yao? (b) Yoeli hufananisha nani leo, na tofauti na ulimwengu kwa ujumla, hao hubarikiwaje?

7 Katika lugha dhahiri ya ufananisho, Yehova atoa ufafanuzi huu wa ziada juu ya kutekeleza kwake uamuzi wake: “Jua na mwezi vimetiwa giza, na nyota zimeacha kuangaza. Naye BWANA [Yehova, NW] atanguruma toka Sayuni, atatoa sauti yake toka Yerusalemu; na mbingu na nchi zitatetemeka; lakini BWANA [Yehova, NW] atakuwa kimbilio la watu wake, na ngome ya wana wa Israeli.” (Yoeli 3:15, 16) Hali ya ainabinadamu ionekanayo kuwa nyangavu, yenye ufanisi ita-geuka kuwa giza, yenye kuonyesha hali mbaya, na mfumo huu wa ulimwengu wenye kugawanyika utatetemeshwa usiwepo tena, ukiwa ni kama umekumbwa na tetemeko la dunia lenye nguvu nyingi!—Hagai 2:20-22.

8 Ona ule uhakikisho wenye furaha kwamba Yehova atakuwa kimbilio na ngome kwa watu wake! Kwa nini? Kwa sababu wao ndio watu peke yao—watu wa kimataifa—ambao wameitikia maneno ya Yehova: “Hivyo ndivyo mtakavyojua ya kuwa mimi ndimi BWANA [Yehova, NW], Mungu wenu.” (Yoeli 3:17) Kwa kuwa jina la Yoeli humaanisha “Yehova ndiye Mungu,” yeye kwa kufaa hufananisha Mashahidi wapakwa-mafuta wa Yehova wa ki-siku-hizi, wanaotumikia kwa ujasiri katika kupiga mbiu enzi kuu ya Yehova. (Linganisha Malaki 1:11.) Tukigeukia maneno ya kufungua ya unabii wa Yoeli, tutapata jinsi anavyotabiri kwa dhahiri utendaji wa watu wa Mungu leo.

Kikosi cha Nzige

9, 10. (a) Ni pigo gani linalotabiriwa na Yoeli? (b) Ufunuo hurudiaje unabii wa Yoeli wa pigo, na pigo hilo lina tokeo gani kwa Jumuiya ya Wakristo?

9 Sikiliza sasa “Neno la BWANA [Yehova, NW] lililomjia Yoeli”: “Sikieni haya, enyi wazee; sikilizeni, enyi wenyeji wote wa nchi. Je! mambo haya yamekuwako katika siku zenu, au katika siku za baba zenu? Waarifuni watoto wenu habari yake, watoto wenu waambie watoto wao, na watoto wao wakakiambie kizazi kingine. Yaliyosazwa na tunutu yameliwa na nzige; na yaliyosazwa na nzige yameliwa na parare; na yaliyosazwa na parare yameliwa na madumadu.”—Yoeli 1:1-4.

10 Hiyo ni kampeni isiyo ya kawaida, moja itakayokumbukwa kwa wakati wote. Mfululizo wa mawimbi ya wadudu, na hasa nzige, waiharibu nchi. Hilo lamaanisha nini? Ufunuo 9:1-12, NW, husema pia juu ya pigo la nzige, waliotumwa na Yehova chini ya “mfalme . . . malaika wa abiso,” ambaye siye mwingine ila Kristo Yesu. Majina yake ni Abadoni (Kiebrania) na Apolioni (Kigiriki) yanayomaanisha “Uharibifu” na “Mharabu.” Nzige hao hufananisha mabaki wapakwa-mafuta wa Wakristo ambao, sasa katika siku ya Bwana, husonga mbele kuharibu malisho ya Jumuiya ya Wakristo kwa kufichua kabisa dini bandia na kupiga mbiu kisasi cha Mungu juu yayo.

11. Nzige wa ki-siku-hizi huimarishwaje, na ni nani hasa walio shabaha ya mashambulio yao?

11 Kama ilivyoonyeshwa na Ufunuo 9:13-21, pigo la nzige linafuatwa na pigo kubwa la jeshi la wapanda-farasi. Hilo ni kweli kama nini leo, wakati wale maelfu machache wanaobaki wa wapakwa-mafuta Wakristo wanapoimarishwa na zaidi ya milioni nne ya “kondoo wengine” wote wakijumuika kuwa jeshi la wapanda-farasi lisiloweza kuzuiwa! (Yohana 10:16) Wao hujiunga pamoja katika kupiga mbiu hukumu za Yehova zenye kuchoma juu ya waabudu wa sanamu wa Jumuiya ya Wakristo na juu ya wale ambao ‘hawautubii uuaji wao, wala uchawi wao, wala uasherati wao wala wivi wao.’ Makasisi—Wakatoliki na Waprotestanti pia—ambao wameunga mkono kwa bidii vita vya uuaji wa kimakusudi vya karne hii, pamoja na mapadri wenye kuvutiwa kwa watoto kingono na waevanjeli wa televisheni waliopotoka, wamo miongoni mwa hao ambao huelekezewa ujumbe huo mbalimbali wa hukumu.

12. Ni kwa nini viongozi wa Jumuiya ya Wakristo hustahili kupokea ujumbe mbalimbali wa hukumu, na ni jambo gani litakalowapata wao, pamoja na washiriki wote wa Babuloni Mkubwa hivi karibuni?

12 Kwa makasisi hao waliopotoka waonwao kuwa “waungwana,” mwito huu wa Yehova huvuma: “Levukeni, enyi walevi, mkalie; pigeni yowe, ninyi nyote mnywao divai; kwa sababu ya divai mpya; maana umekatiliwa mbali na vinywa vyenu.” (Yoeli 1:5) Katika karne hii ya 20, dini ya Jumuiya ya Wakristo imeweka uendekevu wa ulimwengu huu mahali pa kanuni safi za kimaadili za Neno la Mungu. Limeonekana kuwa jambo lililo tamu kwa dini bandia na wafuasi wayo kufuata njia za ulimwengu, lakini wamevuna mavuno yaliyoje ya magonjwa ya kiroho na ya kimwili! Karibuni, kama ielezwavyo kwenye Ufunuo 17:16, 17, “shauri” la Mungu litakuwa kwamba serikali za kisiasa ziishambulie kwa ghafula milki ya ulimwengu wote ya dini bandia, Babuloni Mkubwa, na kuiharibu. Wakati tu ionapo uamuzi wa Yehova ukitekelezwa dhidi yayo, ndiyo ‘itakapolevuka’ kutoka kupumbaa-pombe kwayo.

“Watu Wengi na Wenye Nguvu”

13. Kundi la nzige huonekana kwa Jumuiya ya Wakristo kuwa “wengi na wenye nguvu” katika njia gani?

13 Nabii wa Yehova aendelea kueleza juu ya kundi hilo la nzige kuwa “watu wengi na wenye nguvu,” na ndivyo lionekanavyo kwa Babuloni Mkubwa. (Yoeli 2:2, NW) Kwa mfano, makasisi wayo huomboleza kwamba dini za Jumuiya ya Wakristo zimeshindwa kufanya waongofu katika Japani ya Kibuddha. Hata hivyo, leo, Mashahidi wa Yehova Wajapani zaidi ya 160,000 huenea kotekote katika nchi hiyo na huongoza mafunzo ya Biblia ya kibinafsi katika nyumba za watu zaidi ya 200,000. Katika Italia wale Mashahidi wa Yehova 180,000 hutambuliwa sasa kuwa wa pili tu kwa idadi kutoka kwa Wakatoliki. Padri wa cheo cha juu Mroma Katoliki katika Italia aliomboleza bila kufanikiwa kwamba Mashahidi wa Yehova wanatwaa kutoka kanisa hilo ‘Wakatoliki waaminifu angalau 10,000’ kila mwaka.a Mashahidi hufurahia kuwakaribisha watu kama hao.—Isaya 60:8, 22.

14, 15. Yoeli aelezaje juu ya kundi la nzige, na hilo limetimizwaje leo?

14 Ikieleza juu ya kundi hilo la nzige la Mashahidi wapakwa-mafuta, Yoeli 2:7-9 hutaarifu hivi: “Hupiga mbio kama mashujaa; huupanda ukuta kama watu wa vita; nao huendelea mbele kila mmoja katika njia zake, wala hawapotoshi safu zao. Wala hapana mmoja amsukumaye mwenzake; huendelea mbele kila mmoja katika njia yake; hujifanyizia njia kwa nguvu kati ya silaha [na iwapo wengine waanguka hata kati ya makombora, NW], wala hawaachi kuifuata njia yao. Huurukia mji; hupiga mbio juu ya ukuta; hupanda na kuingia ndani ya nyumba; huingia madirishani kama aingiavyo mwivi.”

15 Kwa kweli, huo ni wonyesho dhahiri wa jeshi la “nzige” wapakwa-mafuta, sasa wakiwa na waandamani zaidi ya milioni nne ambao wamejiunga nao, wale kondoo wengine! Hakuna “ukuta” wowote wa uadui wa kidini uwezao kuwazuia. Kwa ujasiri, wao ‘huendelea kutembea kwa utaratibu katika kawaida ile ile’ ya kutoa ushahidi wa peupe na kufanya utendaji mwingine mbalimbali wa Kikristo. (Linganisha Wafilipi 3:16, NW.) Badala ya kuridhiana, wamekuwa na nia ya kukabili kifo, sawa na wale maelfu ya Mashahidi ‘walioanguka kati ya makombora’ kwa sababu walikataa kumwita Hitla aliyekuwa Mkatoliki wa Ujerumani wa Nazi, mwokozi wao. Kundi hilo la nzige limetoa ushahidi kamili katika “mji” wa Jumuiya ya Wakristo, wakipanda vizuizi vyote, na kuingia, kana kwamba mwivi katika nyumba wanapogawanya maelfu ya mamilioni ya vichapo vya Biblia kupitia utendaji wao wa nyumba kwa nyumba. Ni mapenzi wa Yehova kwamba ushahidi huo utolewe, na haku-na nguvu yoyote mbinguni wala duniani iwezayo kuuzuia.—Isaya 55:11.

‘Jazwa Roho Takatifu’

16, 17. (a) Maneno ya Yoeli 2:28, 29 yalikuwa na utimizo wenye kutokeza wakati gani? (b) Ni maneno gani ya Yoeli ya kiunabii yasiyotimizwa kikamili katika karne ya kwanza?

16 Yehova huwaambia Mashahidi wake hivi: “Nanyi mtajua ya kuwa mimi ni katikati ya Israeli, na ya kuwa mimi ndimi BWANA [Yehova, NW], Mungu wenu, wala hakuna mwingine.” (Yoeli 2:27) Watu wake walipata utambuzi huo wa thamani kubwa wakati Yehova alipoanza kutimiza maneno yake kwenye Yoeli 2:28, 29: “Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri.” Hilo lilitukia Pentekoste ya 33 W.K., wakati wanafunzi wa Yesu waliokuwa wamekusanyika walipopakwa mafuta na “wote wakajazwa Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].” Kwa nguvu ya roho takatifu walihubiri, na kwa siku hiyo moja, “wakaongezeka watu wapata elfu tatu.”—Matendo 2:4, 16, 17, 41.

17 Katika pindi hiyo yenye furaha, Petro alinukuu pia Yoeli 2:30-32: “Nami nitaonyesha mambo ya ajabu katika mbingu na katika dunia, damu, na moto, na minara ya moshi. Jua litageuzwa kuwa giza, na mwezi kuwa damu, kabla haijaja hiyo siku ya BWANA [Yehova, NW] iliyo kuu na itishayo. Na itakuwa ya kwamba mtu awaye yote atakayeliitia jina la BWANA [Yehova, NW] ataponywa.” Maneno hayo yalitimizwa kwa sehemu wakati Yerusalemu ulipoharibiwa katika 70 W.K.

18. Utimizo mkubwa zaidi wa Yoeli 2:28, 29 ulianza kutukia wakati gani?

18 Hata hivyo, kungekuwako utumizi zaidi wa Yoeli 2:28-32. Kwa kweli, unabii huo umekuwa na utimizo wenye kutokeza tangu Septemba 1919. Wakati huo mkusanyiko wa watu wa Yehova wenye kukumbukwa ulifanywa katika Cedar Point, Ohio, U.S.A. Roho ya Mungu ilidhihirika kwa wazi, na watumishi wake wapakwa-mafuta walichochewa waanze kampeni ya kutoa ushahidi duniani pote inayoenea hadi siku ya leo. Ni upanuzi ulioje ambao umetokea! Wale zaidi ya 7,000 waliohudhuria mkusanyiko huo katika Cedar Point wameongezeka wakawa jumla ya 10,650,158 waliohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu katika Machi 30, 1991. Kati ya hao, ni 8,850 tu waliodai kuwa Wakristo wapakwa-mafuta. Shangwe ya hao wote ni nyingi kama nini wanapoona matunda ya duniani pote yakitokezwa kwa roho ya Yehova yenye nguvu ya kuendesha!—Isaya 40:29, 31.

19. Kwa sababu ya ukaribu wa siku ya Yehova, mtazamo wa kila mmoja wetu wapasa kuwa nini?

19 Mbele tu yaja “hiyo siku ya BWANA [Yehova, NW] iliyo kuu na itishayo” itakayoharibu mfumo wa mambo wa Shetani. (Yoeli 2:31) Kwa furaha, “kila atakayeliitia jina la Bwana [Yehova, NW] ataokolewa.” (Matendo 2:21) Jinsi gani? Mtume Petro atuambia kwamba “siku ya Bwana [Yehova, NW] itakuja kama mwivi” na huongeza: “Kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa nyingi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa [ujitoaji kimungu, NW], mkitazamia hata ije [mkikaribisha akilini, NW] siku ile ya Mungu [Yehova, NW].” Tukikumbuka kwamba siku ya Yehova i karibu, tutashangilia pia kuona utimizo wa ahadi ya Yehova ya “mbingu mpya na nchi [dunia, Habari Njema Kwa Watu Wote] mpya” yenye uadilifu.—2 Petro 3:10-13.

[Maelezo ya Chini]

a La Repubblica, Roma, Italia, Novemba 12, 1985, na La rivista del clero italiano, Mei, 1985.

Je! Waweza Kueleza?

◻ “Siku ya BWANA [Yehova, NW]” ni nini?

◻ Yesu atavunaje ‘mzabibu wa nchi,’ na kwa nini?

◻ Pigo la nzige limetesa Jumuiya ya Wakristo kwa njia gani tangu 1919?

◻ Roho ya Yehova ilimiminwaje juu ya watu wake katika 33 W.K., na tena katika 1919?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki