Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 7/15 kur. 21-23
  • Yoeli Atoa Unabii juu ya Kisasi cha Yehova na Upendo Wake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yoeli Atoa Unabii juu ya Kisasi cha Yehova na Upendo Wake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • PIGO KUBWA NA NJAA KALI
  • KUTUBU NA KURUDISHWA
  • KUFIKILIZA HUKUMU
  • Kitabu Cha Biblia Namba 29—Yoeli
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Shambulizi Kutoka Kaskazini!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Karibisha Akilini Siku ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Siku ya Yehova Iko Karibu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 7/15 kur. 21-23

Yoeli Atoa Unabii juu ya Kisasi cha Yehova na Upendo Wake

“HATA itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono; tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho yangu.”​—Yoeli 2:28, 29.

Kwa uhakika kabisa, mistari miwili hiyo ndiyo sehemu ya unabii wa Yoeli inayojulikana vizuri zaidi, sababu ikiwa kwamba Petro aliyataja maneno yaliyomo siku ya Pentekoste. (Matendo 2:14-18) Lakini kitabu cha Biblia cha Yoeli kina habari nyingine nyingi, ingawa unabii wake una sura tatu tu, na jumla ya mistari 73. Kitabu hicho kinaeleza pia habari za pigo la nzige wenye kuharibu vitu mpaka inapokuja kutokea njaa kali, na kueleza wakati wa kutubu kwa watu na kurudishwa kwao katika hali nzuri na pia habari za kutekeleza kisasi kwa Yehova juu ya mataifa. Katika Biblia yetu, Yoeli anaonyeshwa kuwa ndiye wa pili wa wale waitwao Manabii Wadogo​—wadogo kwa habari ya urefu wa kila kitabu kimojachapo, lakini si kwa habari ya ubora wa kitabu chenyewe.

Kanuni ya Biblia inayoonekana wazi tunapoangalia unabii wa Yoeli ni kwamba ujumbe uliomo ndio wa maana, wala si mtu aliyetumiwa kuutoa. Basi habari za pekee tulizo nazo juu ya mwandikaji, Yoeli, ni kwamba yeye ndiye mwana wa Pethueli. Mara nyingi majina ya watu wa Biblia huwa na maana kubwa, na ndivyo ilivyo kwa habari ya Yoeli na baba yake. “Pethueli” maana yake ni “Mungu hukomboa,” na “Yoeli” maana yake ni “Yehova ni Mungu.”

Ushuhuda wa ndani ya kitabu hicho unafanya ielekee sana kuwa kwamba Yoeli alikuwa wa ufalme wa Yuda wenye makabila mawili. Jambo linaloonyesha hivyo ni namna unabii wake unavyotia mkazo juu ya Yuda na Yerusalemu na utumishi wa hekaluni huko Yerusalemu.

Unabii huo uliandikwa wakati gani? Hatuwezi kutoa maoni ya kibinafsi. Wanachuo mbalimbali husema ni mapema kwenye karne ya 10 K.W.K. na wengine wao karne ya pili. Uzito wa ushuhuda uliopo unaelekea zaidi kuthibitisha unabii huo uliandikwa karibu na mwaka wa 820 K.W.K. Tarehe hiyo inaelekea kuhakikishwa na uhakika wa kwamba adui wa zamani wa Israeli wanatajwa​—Tiro, Sidoni, Filistia, Edomu na Misri​—badala ya kutaja adui wa baadaye kama Ashuru na Babeli. Jambo hilo linaonyeshwa pia na mahali ambapo kitabu hicho kimepangwa katika maandiko yanayokubalika ya Kiebrania.

Namna iliyotumiwa kukiandika inaongeza uzito wenye kuonyesha kitabu hicho kiliandikwa wakati wa zile tarehe za mapema. Watu wengi wanaona Yoeli aliandika kitabu chake kwa usanifu mwingi unaofanya unabii wake uelekee kulinganishwa na almasi iliyosuguliwa sana ikasafika vizuri. Kwa kweli, kimeandikwa kwa ustadi mwingi sana hivi kwamba wana-chuo wengine wanatanguliza unabii wa Yoeli mbele ya manabii wengine wote waliomfuata. Namna yake ya kuandika ni ya kimashairi sana na ina semi zenye kurudiwa-rudiwa kwa ufanani wa kupendeza. Anaonyesha pia alipenda sana kutumia mifano ya viumbe ili akazie maana na kutumia pia mafumbo ya mithali.

Unyofu wa unabii wa Yoeli haujatiliwa mashaka kamwe na Waisraeli wenyewe; wanaupanga mwanzoni-mwanzoni na kuupa mahali penye kuheshimika katika maandiko yao yanayokubalika. Unyofu wa unabii huo unaendelea kuonekana wakati mitume Petro na Paulo wanapotumia maneno yake. Unyofu wa unabii huo unahakikishwa pia na utimizo wa unabii mbalimbali wa kitabu hicho kuhusu Tiro, Filistia na Edomu.​—Matendo 2:14-18; Warumi 10:13.

PIGO KUBWA NA NJAA KALI

Unabii wa Yoeli unaweza kusemwa kuwa una sehemu tatu. Sehemu ya kwanza (1:1 mpaka 2:11) inatoa maelezo yenye mafungu mawili ya pigo kubwa la kutumia nzige. Maelezo ya kwanza yanalionyesha kuwa pigo kubwa la nzige walio na magego (meno) na mataya ya simba. Kuhusu maelezo aliyotoa Yoeli juu ya kisa hicho, tunaambiwa hivi: “Ule uharibifu mkubwa sana unaoletwa na pigo la nzige juu ya maisha ya watu ya ukulima, ya uchumi na ya kidini unaelezwa kwa usahihi unaokaribia sana kuwa wa kisayansi, kulingana na maoni ya watu wengi ambao wamekwisha kuona nzige wakiharibu vitu.”

Kama anavyotuambia Yoeli, kila kitu kinaliwa, nchi inaachwa ukiwa, wakulima wanadhikika na watunzaji wa mizabibu wanapiga yowe. Hata wanyama wa kufugwa wanaugua na makundi ya ng’ombe yamefadhaika. Si ajabu basi kwamba makuhani na wahudumu walio kwenye nyumba ya Yehova wanaambiwa wapige yowe, walale usiku kucha katika magunia, watakase wakati wa kufunga kula na ‘kumlilia Yehova awasaidie’!​—Yoeli 1:14.

Maelezo yale ya pili juu ya pigo kubwa la nzige yanaanza kwa amri inayoagiza mbiyu ipigwe kuamsha watu: “Pigeni tarumbeta katika Sayuni, pigeni na kelele katika mlima wangu mtakatifu.” Ndipo yanapofuata maelezo haya: “Hupiga mbio kama mashujaa; huupanda ukuta kama watu wa vita; . . . Wala hapana mmoja amsukumaye mwenzake; huendelea mbele kila mmoja katika njia yake; hujifanyizia njia kwa nguvu kati ya silaha, wala hawaachi kuifuata njia yao. Huurukia mji; hupiga mbio juu ya ukuta; hupanda na kuingia ndani ya nyumba; huingia madirishani kama aingiavyo mwivi.”​—Yoeli 2:1, 7-9.

Kwa sababu ya usemi wenye mifano mingi wa Yoeli, inaonekana kwamba yatupasa tuyaone maneno yake kuwa unabii badala ya kuyaona kuwa habari zenye kueleza matukio yaliyokwisha kutendeka zamani. Unabii huo unahusu kitu gani? Mambo ya hakika yanaelekea kuonyesha kwamba unahusu kazi ya kisasa inayofanywa na Mashahidi wa Yehova kwa kujikaza sana kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba tangu miaka ya mwanzo-mwanzo wa 1920. Hakika wao wamekuwa pigo kubwa kwa Jumuiya ya Wakristo ya kisasa na wakasonga mbele kama jeshi lenye nidhamu (adabu) nyingi.a

KUTUBU NA KURUDISHWA

Ile sehemu ya pili ya unabii wa Yoeli inahusu kutubu na hatua ya kurudishwa iliyofuata. Tunasoma hivi kwenye Yoeli 2:12-14: “Nirudieni, mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga na kwa kulia, na kwa kuombolea; rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie [Yehova], Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema. . . . N’nani ajuaye kwamba hatarudi na kugeuka, na kutuachia baraka nyuma yake, naam, sadaka ya unga, na sadaka ya kinywaji, kwa [Yehova], Mungu wenu?”

Sehemu hii ya unabii inaonekana pia kuwa ilitimizwa kwa njia ya pekee katika nyakati wa kisasa, sana sana wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza watu wa Mungu walipokuwa na midomo michafu na Yehova akawa amewakasirikia. Hapo ndipo watu wa Yehova walipomsihi sana Mungu kwa kutubu, kama unavyosemwa kwenye Yoeli 2:17: “Uwaachilie watu wako, Ee [Yehova], wala usiutoe urithi wako upate aibu, hata mataifa watawale juu yao; kwani waseme kati ya watu, Yuko wapi Mungu wao?”​—Linganisha Isaya 12:1; 6:5.

Unabii wa Yoeli kwenye 2:​21-27 na 3:​18-21 unaonyesha matunda ya toba hiyo, yaani, ahadi ya kurudishwa kwenye hali inayofaa. Kwa kweli, baada ya matatizo yenye kuwaumiza moyo yaliyowapata miaka hiyo ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, watu wa Yehova wamerudishwa kwenye hali ya paradiso ya kiroho.​—Angalia Isaya sura ya 35.

Kwa kulingana na maneno ya mtume Petro (Matendo 2:14-18), hakuwezi kuwa na shaka kwamba Yoeli 2:28, 29 ilitimizwa siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Lakini inaonekana ilikuwa na utimizo mwingine wakati wa “siku za mwisho” za taratibu nzima ya mambo ya Shetani. (2 Timotheo 3:1) Sana sana katika miaka ya 1919 na 1922 ndipo ilipotokea mimimino ya kisasa ya roho ya Yehova, hasa kuhusiana na makusanyiko mawili ya watu wa Yehova waliokuwa wakf huko Cedar Point, Ohio.

KUFIKILIZA HUKUMU

Sasa tunakuja kwenye sehemu ya tatu, inayohusu hukumu na kuuawa. (Yoeli 3:2-16, 19) Inatueleza kwa nini Yehova ameyakasirikia mataifa​—kwa sababu ya namna yalivyowatenda watumishi wake. Yaliwatawanya kati ya mataifa, yakawafanya watumwa wao. Pia, yalinyang’anya hekalu la Yehova dhahabu, fedha na vitu vingine vizuri, yakavileta na kuviingiza katika mahekalu yao wenyewe. Yaliwatenda jeuri wana wa Yuda yakamwaga damu isiyo na hatia. Angalia kwamba hapa Yehova Mungu anasema kwamba yeye ndiye aliyetendwa ubaya huo, sawa na vile Yesu alivyomwambia Sauli wa Tarso kwamba alikuwa akimtesa Yeye alipokuwa akitesa wafuasi wa Yesu.​—Matendo 9:5.

Baada ya kuyahesabia mataifa hayo mabaya yao, Yehova anawaamuru watu wake watangaze siku yake ya kisasi, watamke hivi kati ya mataifa hayo: “Takaseni vita; waamsheni mashujaa.” Ndipo tunaposikia maneno yanayotofautiana na ya Isaya 2:2-4 na Mika 4:1-3, yaani: “Yafueni majembe yenu yawe panga, na miundu yenu iwe mikuki; aliye dhaifu na aseme, Mimi ni hodari.” Wanaagizwa waende kwenye bonde la Yehoshafati, jina linalomaanisha “Yehova ni Hakimu.”​—Yoeli 3:9-12.

Kisha tunapata maelezo ya kisasi cha Yehova juu ya mataifa. Mwundu unatupwa kuvuna mataifa maovu yatakayopaswa kutupwa ndani ya shinikizo (mahali pa kutwangia zabibu za divai), napo panafurika. Basi kwa kufaa sehemu hii ya unabii inafikia mwisho kwa kutoa sababu hii ya maana sana inayoeleza kwa nini tendo hilo linafanywa: “Hivyo ndivyo mtakavyojua ya kuwa mimi ndimi [Yehova], Mungu wenu, nikaaye Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” (Yoeli 3:17) Unabii huu unalingana sana na yale tunayoambiwa juu ya Har–​Magedoni na kitabu cha Ufunuo.​—Ufunuo 16:14-16; 19:15-21.

Kitabu cha Yoeli kinatukuza enzi kuu ya Yehova Mungu. Tunaona hivyo anapolipeleka pigo la nzige juu ya ‘walevi wa Yuda’ (Jumuiya ya Wakristo), anapoyaambia mataifa yajitokeze yapigane naye na anapowaua katika “bonde la Yehoshafati.” Unabii huu unakazia pia rehema kubwa ya Yehova, kama tunavyosoma kwenye Yoeli 2:13: “Mkamrudie [Yehova], Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya.” Kuongezea hilo, katika kitabu hicho watu wa Yehova wanaamriwa watangaze onyo la siku yake inayokuja ya kisasi wakisema kati ya mataifa, “Takaseni vita.” Linalotufurahisha ni kwamba sasa tumeifikia siku hiyo ambapo Yehova ameketi ‘awahukumu mataifa yote yaliyo pande zote’!​—Yoeli 3:9-12.

[Maelezo ya Chini]

a Ili upate maelezo mengi angalia Mnara wa Mlinzi, Desemba 15, 1979, kurasa 16-18.

[Picha katika ukurasa wa 22]

“Huupanda ukuta kama watu wa vita . . . Hupanda na kuingia ndani ya nyumba.” Maneno hayo yanahusu nini?

Nzige

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki