Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 5/1 kur. 14-19
  • Nani Atakayeponyoka Ule “Wakati wa Taabu”?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nani Atakayeponyoka Ule “Wakati wa Taabu”?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi “Vitu Vinavyotamaniwa” Vinavyokuja
  • ‘Tafuteni, Tafuteni, Tafuteni’
  • Mikaeli Atenda!
  • Kufichwa Katika Siku ya Hasira ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Mtafuteni Yehova Kabla ya Siku Yake ya Hasira
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Fanya Tangazo la Hadharani kwa Ajili ya Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Siku ya Hukumu ya Yehova I Karibu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 5/1 kur. 14-19

Nani Atakayeponyoka Ule “Wakati wa Taabu”?

“Mtu awaye yote atakayeliitia jina la BWANA [Yehova, “NW”] ataponywa.”—YOELI 2:32.

1. Kulingana na Danieli na Malaki, ni nini kinachotambulisha wale walio katika mstari wa kupata wokovu katika “wakati wa taabu” unaokuja?

AKITAZAMA mbele kwa wakati wetu, nabii Danieli aliandika hivi: “Kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile.” (Danieli 12:1) Hayo kwa kweli ni maneno yenye kutia moyo! Watu wa Yehova wenye kukubaliwa watakumbukwa na yeye, jinsi Malaki 3:16 itangazavyo rasmi pia: “Ndipo wale waliomcha BWANA [Yehova, NW] waliposemezana wao kwa wao. Naye BWANA [Yehova, NW] akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha Bwana na kulitafakari jina lake.”

2. Ni nini tokeo la kulitafakari jina la Yehova?

2 Kulitafakari jina la Yehova huongoza kwenye kupata maarifa sahihi kuhusu yeye, Kristo wake, na makusudi matukufu yake yote ya ufalme. Hivyo, watu wake hujifunza jinsi ya kumwona kwa kicho, jinsi ya kuingia katika uhusiano wa karibu wenye wakfu pamoja na yeye, na jinsi ya kumpenda ‘kwa moyo wao wote na kwa ufahamu wao wote na kwa nguvu zao zote.’ (Marko 12:33; Ufunuo 4:11) Yehova amefanya ule uandalizi wenye neema, kupitia dhabihu ya Yesu Kristo, ili wasikivu wa dunia wapate uhai wa milele. Kwa hiyo, hao waweza kurudia kwa uhakika yale maneno ya lile jeshi la kimbingu lililomsifu Mungu wakati wa kuzaliwa kwa Yesu, wakisema: “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.”—Luka 2:14.

3. Kabla ya amani kuweza kuja kwenye dunia hii, ni lazima tendo gani la Yehova litukie?

3 Amani hiyo iko karibu zaidi ya jinsi wengi wafikiriavyo. Lakini ni lazima hukumu ya Yehova itekelezwe kwanza juu ya ulimwengu huu wenye ufisadi. Nabii wake Sefania atangaza rasmi hivi: “Hiyo siku ya BWANA [Yehova, NW] iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana.” Hiyo ni siku ya aina gani? unabii waendelea hivi: “Sauti ya siku ya BWANA [Yehova, NW]; shujaa hulia kwa uchungu mwingi huko! Siku ile ni siku ya ghadhabu, siku ya fadhaa na dhiki, siku ya uharibifu na ukiwa, siku ya giza na utusitusi, siku ya mawingu na giza kuu, siku ya tarumbeta na ya kamsa, juu ya miji yenye maboma, juu ya buruji zilizo ndefu sana. Nami nitawaletea wanadamu dhiki, hata watakwenda kama vipofu, kwa sababu wamemtenda BWANA [Yehova, NW] dhambi.”—Sefania 1:14-17; ona pia Habakuki 2:3; 3:1-6, 16-19.

4. Ni nani leo wanaoitikia ule mwaliko wa kumjua na kumtumikia Mungu?

4 Kwa furaha, mamilioni leo wanaitikia mwaliko huo wa kumjua na kumtumikia Mungu. Kuhusu Wakristo wapakwa-mafuta, wanaoingizwa katika agano jipya, unabii huu ulitolewa: “Watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema BWANA [Yehova, NW].” (Yeremia 31:34) Hao wameitanguliza kazi ya kutoa ushahidi ya ki-siku-hizi. Na sasa wakati mabaki wa wapakwa-mafuta zaidi na zaidi wanapomaliza mwendo wao wa kidunia, ule “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wamekuja ‘kumtumikia Mungu mchana na usiku’ katika mpango wake ulio kama hekalu.’ (Ufunuo 7:9, 15; Yohana 10:16) Je! wewe ni mmoja anayeonea shangwe pendeleo hilo lisilokadirika?

Jinsi “Vitu Vinavyotamaniwa” Vinavyokuja

5, 6. Kabla ya mataifa yote kutikiswa hadi uharibifu, ni kazi gani ya kuokoa inayotukia?

5 Sasa acheni tugeukie Hagai 2:7, ambapo Yehova hutoa unabii kuhusu nyumba yake ya kiroho ya ibada. Yeye asema hivi: “Nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.” Unabii mbalimbali wa Biblia huonyesha kwamba ‘kutikisa mataifa’ huko hurejezea kule kutekeleza hukumu kwa Yehova juu ya mataifa. (Nahumu 1:5, 6; Ufunuo 6:12-17) Kwa hiyo, tendo la Yehova lililotolewa unabii kwenye Hagai 2:7 litakuwa na upeo walo katika kutikiswa kwa mataifa yasiwepo tena—yakiwa yameangamizwa. Lakini namna gani “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote”? Je! ni lazima vingojee kule kutikiswa kwa mwisho kwenye uharibifu ili vije? Sivyo.

6 Yoeli 2:32 husema kwamba “mtu awaye yote atakayeliitia jina la BWANA [Yehova, “NW”] ataponywa; kwa kuwa katika mlima Sayuni na katika Yerusalemu watakuwako watu watakaookoka, kama BWANA [Yehova, NW] alivyosema; na katika mabaki hao awaitao BWANA [Yehova, “NW”].” Yehova huwaita watoke, na wao huliitia jina lake wakiwa na imani katika dhabihu ya Yesu kabla ya kule kutikiswa kwa dhiki kubwa kutakakofanyiza upeo. (Linganisha Yohana 6:44; Matendo 2:38, 39.) Kwa furaha, ule mkutano mkubwa wenye thamani kubwa, ambao sasa hesabu yao ni zaidi ya milioni nne, ‘huja’ ndani ya nyumba ya Yehova ya ibada ukitazamia kule ‘kutikisa kwake mataifa yote’ kwenye Har–Magedoni.—Ufunuo 7:9, 10, 14.

7. ‘Kuliitia jina la Yehova’ kunahusisha nini?

7 Waokokaji hao wanaliitiaje jina la Yehova? Yakobo 4:8 hutuonyesha, ikitaarifu hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili.” Sawa na wale mabaki wapakwa-mafuta walioongoza njia, ni lazima wale watumainio kuwa sehemu ya mkutano mkubwa wa waokokaji wa Har–Magedoni watende kwa njia ya kukata maneno. Ikiwa wewe watumaini kuokoka, ni lazima unywe sana kutokana na Neno la Yehova lenye kutakasa na kutumia viwango vyake vya uadilifu katika maisha yako. Ni lazima utende kwa kukata maneno katika kuweka maisha yako wakfu kwa Yehova, ukionyesha hivyo kwa ubatizo wa maji. Kuliitia kwako jina la Yehova kwa imani kwatia ndani pia kutoa ushahidi kwa ajili yake. Hivyo, kwenye Warumi sura ya 10, mstari wa 9 na wa 10, Paulo aandika hivi: “Ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.” Kisha, katika mstari wa 13, mtume huyu anukuu unabii wa Yoeli, akikazia kwamba “kila atakayeliitia Jina la Bwana [Yehova, NW] ataokoka.”

‘Tafuteni, Tafuteni, Tafuteni’

8. (a) Kulingana na nabii Sefania, Yehova ataka nini ili wokovu upatikane? (b) Neno “huenda” kwenye Sefania 2:3 latutolea onyo gani?

8 Tukigeukia kitabu cha Biblia cha Sefania, sura ya 2, mstari wa 2 na wa 3, twasoma matakwa ya Yehova ili kuokoka: “Kabla haijawajilia hasira kali ya BWANA [Yehova NW], kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW]. Mtafuteni BWANA [Yehova, NW] enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki [uadilifu, NW], utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW].” Angalia neno hilo “huenda.” Haiwi kwamba ukiisha okolewa, umeokolewa daima. Kufichwa kwetu katika siku hiyo kwategemea kuendelea kwetu kufanya mambo hayo matatu. Lazima tumtafute Yehova, tuutafute uadilifu, na tuutafute unyenyekevu.

9. Wale wanaotafuta unyenyekevu huthawabishwaje?

9 Kwa kweli, thawabu ya kuutafuta unyenyekevu ni nzuri ajabu! Kwenye Zaburi 37, mstari wa 9 hadi wa 11, twasoma hivi: “Wamngojeao BWANA [Yehova, NW] ndio wakaoirithi nchi. . . . Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole [wanyenyekevu, NW] watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” Na namna gani kuutafuta uadilifu? Mstari wa 29 hutaarifu: “Wenye haki [wadilifu, NW] watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Kwa habari ya kumtafuta Yehova, mstari wa 39 na wa 40 hutuambia: “Na wokovu wa wenye haki [waadilifu, NW] una BWANA [Yehova, NW]; yeye ni ngome yao wakati wa taabu. Naye BWANA [Yehova, NW] huwasaidia na kuwaopoa; huwaopoa na wasio haki na kuwaokoa; kwa kuwa wamemtumaini Yeye.”

10. Ni nani wametokeza katika katao lao la kumtafuta Yehova na kutafuta unyenyekevu?

10 Madhehebu ya Jumuiya ya Wakristo yameshindwa kumtafuta Yehova. Makasisi wayo hata hukataa katakata jina lake lenye thamani kubwa, wakiliondoa kimbelembele kutoka kwa tafsiri zao za Biblia. Wao hupendelea kuabudu Bwana au Mungu asiye na jina na kutolea kicho Utatu wa kipagani. Isitoshe, Jumuiya ya Wakristo haitafuti uadilifu. Wafuasi wayo wengi hufuata au kudhamini mitindo ya maisha yenye uendekevu. Badala ya kutafuta unyenyekevu kama Yesu alivyofanya, wao hufanya wonyesho wa fahari, kwa mfano katika televisheni, wa maisha ya anasa na mara nyingi yenye ukosefu wa adili. Makasisi hujinenepesha kwa gharama ya makundi yao. Katika maneno ya Yakobo 5:5, wao ‘hufanya anasa katika dunia, na kujifurahisha kwa tamaa.’ Siku ya Yehova ikaribiapo, kwa hakika watapata kwamba maneno haya yenye kupuliziwa roho hutumika kwao: “Mali hazifaidi kitu siku ya ghadhabu.”—Mithali 11:4.

11. Yule mtu wa kuasi ni nani, naye amerundikaje hatia kubwa sana ya damu?

11 Katika karne ya kwanza W.K., kama mtume Paulo asimuliavyo katika barua yake ya pili kwa Wathesalonike, Wakristo wengine walisisimuka, wakifikiri kwamba siku ya Yehova ilikuwa imewajia wakati huo. Lakini Paulo alionya kwamba ilikuwa lazima uasi-imani mkubwa uje kwanza, na “mtu wa kuasi” alihitaji afunuliwe. (2 Wathesalonike 2:1-3) Sasa, katika karne ya 20, twaweza kuthamini mweneo mkubwa wa uasi-imani huo na jinsi makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walivyowaasi wa sheria machoni pa Mungu. Katika siku hizi za mwisho tangu 1914, makasisi wamerundika hatia kubwa sana ya damu kwa kuunga mkono kule ‘kufua majembe yawe panga.’ (Yoeli 3:10) Wameendelea pia kufundisha mafundisho bandia, kama vile kutokufa kwa asili kwa nafsi ya kibinadamu, purgatori, moto wa helo wa mateso, ubatizo wa watoto, Utatu, na kadhalika. Watasimama wapi wakati Yehova anapotekeleza uamuzi wake wa kihukumu? Mithali 19:5 hutaarifu hivi: “Shahidi wa uongo hakosi ataadhibiwa.”

12. (a) Ni nini zile “mbingu” na “nchi” za kibinadamu zitakazoharibiwa hivi karibuni? (b) Tunajifunza nini kutokana na uharibifu unaokuja wa ulimwengu huu mbovu?

12 Kwenye 2 Petro 3:10, twasoma hivi: “Lakini siku ya Bwana [Yehova, NW] itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.” Tawala zenye ufisadi ambazo zimefunika ainabinadamu kama mbingu, pamoja na viumbe vya asili vyote vinavyofanyiza jamii ya kibinadamu ya leo iliyoharibika, vitafutiliwa mbali kutoka kwa dunia ya Mungu. Waundaji na wauzaji wa silaha za vita ziwezazo kuiharibu dunia, wadanganyi, wanadini wanafiki na makasisi wao, waenezaji upotovu, jeuri, na uhalifu—wote hao watatoweka. Watayeyushiwa mbali na ghadhabu ya Ye-hova. Lakini katika mistari 11 na 12, Petro aongeza hadhari hii kwa Wakristo: “Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa [ujitoaji kimungu, NW], mkitazama hata ije [mkikaribisha akilini, NW] siku ile ya Mungu [Yehova, NW].”

Mikaeli Atenda!

13, 14. Ni nani aliye Mteteaji mkuu wa utawala wa Yehova, naye amekuwaje mwenye kutenda tangu 1914?

13 Mtu yeyote ataweza kuponyokaje katika huo “wakati wa taabu” wa Yehova? Wakili wa Yehova wa kuandaa uponyokaji ni Mikaeli yule malaika mkuu, ambaye jina lake lamaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?” Kwa kufaa basi, yeye ndiye Yule ateteaye utawala wa Yehova, akishindania Yehova kuwa yule Mungu wa kweli peke yake na ambaye ana haki ya kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima.

14 Ni matukio yenye kutokeza kama nini yanayoelezwa na Ufunuo sura ya 12, mstari wa 7 hadi wa 17, kuhusu “siku ya Bwana” tangu 1914! (Ufunuo 1:10) Mikaeli yule malaika mkuu avurumisha mhaini Shetani hapa chini duniani kutoka mbinguni. Baadaye, kama ielezwavyo kwenye Ufunuo sura ya 19 mistari ya 11 hadi 16, mmoja aitwaye “Mwaminifu na Wa-kweli” “anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi.” Shujaa wa vita huyo wa kimbingu mwenye nguvu aitwa ‘Mfalme wa wafalme, na Bwana wa mabwana.’ Hatimaye, Ufunuo sura ya 20, mstari wa 1 na wa 2, husimulia juu ya malaika mkuu anayevurumisha Shetani ndani ya abiso na kumzuilia humo kwa miaka elfu. Kwa wazi, maandiko hayo yote huelekeza kwa yeye ambaye ndiye Mteteaji wa enzi kuu ya Yehova, Bwana Yesu Kristo, ambaye Yehova alimweka kwenye kiti chake cha ufalme chenye utukufu cha kimbingu katika 1914.

15. Mikaeli ‘atasimama’ katika njia gani ya pekee hivi karibuni?

15 Mikaeli amekuwa ‘akisimama’ kama ilivyotaarifiwa kwenye Danieli 12:1, kwa ajili ya watu wa Yehova tangu alipotawazwa kuwa Mfalme katika 1914. Lakini karibuni Mikaeli ‘atasimama’ kwa maana ya pekee sana—akiwa Wakili wa Yehova katika kuondoa uovu wote duniani na akiwa Mkombozi wa jamii ya duniani pote ya watu wa Mungu. Kadiri ya huo “wakati wa taabu” inaonyeshwa na maneno ya Yesu kwenye Mathayo 24:21, 22: “Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.”

16. Ni watu gani watakaookoka katika dhiki kubwa?

16 Jinsi tuwezavyo kuwa na furaha kwamba baadhi ya watu wataokolewa wakati huo! La, si kama wale Wayahudi waasi walionaswa katika Yerusalemu katika 70 W.K., ambao baadhi yao walichukuliwa Roma wakiwa watumwa. Badala ya hivyo, wale watakaoponyoka katika “wakati wa mwisho” watakuwa kama lile kundi la Kikristo lililokuwa tayari limekimbia kutoka Yerusalmu wakati kuzingirwa kwa mwisho kulipoanza. Watakuwa watu wa Mungu mwenyewe, mamilioni ya mkutano mkubwa pamoja na mabaki wapakwa-mafuta wowote ambao huenda wakabaki duniani bado. (Danieli 12:4) Mkutano mkubwa “ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu.” Kwa nini? Kwa sababu “wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Wanazoea imani katika uwezo wa kufidi wa damu ya Yesu iliyomwagwa na kuonyesha imani hiyo kwa kumtumikia Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu. Hata sasa, Yehova, “yeye aketiye katika kiti cha enzi,” atanda hema lake la ulinzi juu yao, naye Mwana-Kondoo, Kristo Yesu, awachunga na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai.—Ufunuo 7:14, 15.

17. Mkutano mkubwa hasa wanatiwaje moyo watende ili kufichwa katika ile siku ya taabu inayokuja?

17 Katika kutafuta Yehova, uadilifu, na unyenyekevu, ni lazima wale mamilioni ya mkutano mkubwa wasiruhusu kamwe upendo wao wa kwanza wa kweli upoe. Ikiwa wewe ni mmoja wa watu hao wa mfano wa kondoo, ni lazima ufanye nini? Kama ilivyotaarifiwa kwenye Wakolosai sura ya 3, mstari wa 5 hadi wa 14, NW, ni lazima wewe ‘uvue kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake.’ Ukitafuta msaada wa kimungu, jitahidi ‘kujivika utu mpya, unaotegemea maarifa sahihi.’ Kwa unyenyekevu, jenga na kudumisha bidii katika kusifu Yehova na katika kujulisha wengine makusudi yake matukufu. Hivyo huenda ukafichwa katika ule “wakati wa taabu,” ile siku ya ‘hasira kali ya Yehova.’

18, 19. Uvumilivu umekuwa wa muhimu kwa wokovu katika njia gani?

18 Siku hiyo i karibu! Inatujia haraka. Kukusanywa kwa watu mmoja mmoja wa ule mkutano mkubwa kumekuwa kukiendelea sasa kwa miaka 57 hivi. Hesabu fulani ya hao wamekufa na wao wanangojea ufufuo wao. Lakini sisi twahakikishiwa na unabii wa Ufunuo kwamba, wakiwa kikundi, mkutano mkubwa watatoka katika dhiki ile iliyo kuu wakawe kiini cha jamii ya “dunia mpya.” (Ufunuo 21:1, HNWW) Je! wewe utakuwako? Hiyo yawezekana, kwa kuwa Yesu alisema hivi kwenye Mathayo 24:13: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.”

19 Mikazo ambayo watu wa Yehova hupatwa nayo katika mfumo huu wa kale huenda ikaendelea kuongezeka. Na wakati dhiki kubwa yenye kutaabisha ifyatukapo, huenda ukapatwa na magumu. Lakini kaa karibu na Yehova na tengenezo lake. Baki ukikesha! “Ningojeni, asema BWANA [Yehova, NW], hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.”—Sefania 3:8.

20. “Wakati wa taabu” utakaofanyiza upeo ukaribiapo zaidi, ni lazima tufanye nini?

20 Kwa ajili ya ulinzi na kitia moyo chetu, Yehova ameandalia watu wake kwa neema “lugha iliyo safi,” inayotia ndani ule ujumbe mtukufu wa Ufalme wake unaokuja, “wapate kuliitia jina la BWANA [Yehova, NW], wamtumikie kwa nia moja.” (Sefania 3:9) Ule “wakati wa taabu” utakaofanyiza upeo ukaribiapo zaidi kwa kasi, na tutumikie kwa bidii, tukisaidia wanyenyekevu wengine ‘waliitie jina la Yehova’ wapate kuokoka.

Je! Unakumbuka?

◻ Ni tendo gani la Yehova litakalotangulia kuletwa kwa amani duniani?

◻ Kulingana na Yoeli, ni lazima mtu afanye nini ili aokoke?

◻ Kulingana na Sefania, wanyenyekevu waweza kupataje ulinzi kutoka kwa hasira kali ya Yehova?

◻ Ni nani yule “mtu wa kuasi,” naye amerundikaje hatia ya damu?

◻ Uvumilivu ni wenye maana jinsi gani kwa habari ya wokovu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki