Paulo kwa Kulinganishwa na Plato Juu ya Ufufuo
MTUME Paulo aliandika juu ya ufufuo kwenye 1 Wakorintho 15:35-58 na 2 Wakorintho 5:1-10. Katika kufanya hivyo, je, alifuata mawazo ya Plato na wanafalsafa Wagiriki kuhusu kutoweza kufa kwa nafsi, au alipatana na mafundisho ya Yesu na ya Maandiko yale mengine?
Kijitabu Immortality of the Soul or Resurrection of the Individual: St. Paul’s View With Special Reference to Plato, kilichoandikwa katika 1974 na kuungwa mkono na askofu mkuu wa Kanisa Orthodoksi ya Kigiriki ya Amerika Kaskazini na Kusini, chatoa jibu lenye kufunua mambo. Baada ya kuzungumzia asili ya ufufuo katika maandiko yaliyotajwa juu na uvutano wa Kigiriki wa wakati huo, mwandikaji afikia mkataa huu:
“Plato hufundisha kwamba nafsi huendelea kuwako milele bila mwisho, mbali na mwili. Kwa Plato nafsi ni yenye kutoweza kufa kiasili na kindani . . . Mt. Paulo hafundishi maoni kama hayo wala hadai kwa njia yoyote kufanya hivyo . . .
“Mtume Paulo hashughuliki na kutoweza kufa kwa nafsi au roho zikiwa sehemu tofauti zilizotengwa bali ashughulika na ufufuo wa mwili wote wa mwanadamu wenye roho na nafsi likiwa tokeo la ufufuo wa Kristo. Wazo la Paulo la ufufuo halihusu kwa vyovyote kuhuishwa kwa miili mifu kutoka kaburini.
“Wazo lake la ufufuo wa mwili laweza kuelezwa vizuri zaidi kuwa ugeuzi, kuumbwa upya, na kurudishiwa umbo la zamani, kwa mwili wote wa mwanadamu, kwa mtu yule yule, kwa utu, kwa mielekeo ya kiakili na kihisia-moyo, kwa mtu pamoja na sifa zake za kiakili na kimwili, kwa uwezo wa Mungu. Ufufuo wetu wa wakati ujao utatukia si ukiwa mali yetu ya kiasili, bali ukiwa zawadi ya kifalme kutoka kwa Mungu.”
Naam, kutoweza kufa si mali ya kiasili ya mwanadamu yeyote. Bali, ni zawadi yenye thamani kubwa na yenye neema kutoka kwa Yehova kupitia Bwana wetu Yesu Kristo kwa wote wanaojumuika kuwa kundi la Kikristo la wapakwa-mafuta.—1 Wakorintho 15:20, 57; Wafilipi 3:14.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mwanafalsafa Mgiriki Plato
[Hisani]
Vatican Museum photograph