Kuzaliwa Pamoja na Nafsi Isiyokufa au Ufufuo—Ni Jambo Gani?
Twakualika uchunguze kwa uangalifu mfululizo wa makala nne zinazoanza kwenye ukurasa huu. Zinaeleza maoni ya Biblia juu ya yale yanayoipata nafsi wakati wa kufa, ufufuo, siku ya hukumu ya Mungu na dhiki ya mwisho, na kuzihusianisha hizo na habari kuu ya Neno la Mungu, ule Ufalme.
KILA Machi au Aprili zaidi ya robo ya wakaaji wa dunia wanasherehekea Easter, ambayo inaitwa “sikukuu ya ufufuo wa Kristo.” Kwa hiyo jambo hilo linamaanisha kwamba mamilioni mengi wanaosherehekea kufufuliwa kwa Kristo siku ya Jumapili ya Easter kwa kweli wanaonyesha tumaini la wao kufufuliwa kutoka kwa wafu hatimaye. Hata hivyo, inashangaza kwamba wengi kati ya watu hao hawaamini kwamba uzima baada ya kufa unategemea ufufuo, bali kwamba ‘nafsi yao isiyokufa’ inaokoka.
Mamia ya mamilioni ya watu wengine, wasiosherehekea Easter, vilevile wanaamini kwamba tumaini lao la uzima baada ya kifo linategemea kuokoka kwa “nafsi” zao wala si ufufuo. Kwa wazi watu hao wote, ndani na nje ya Jumuiya ya Wakristo wanaona kwamba lazima pawepo jambo fulani baada ya muda wao mfupi wa maisha duniani. Wangeshuka moyo kufikiri kwamba wanadamu wanaishi na kufa kama wanyama tu. Tamaa yao ya kutaka uzima wa wakati ujao ni asili ya wanadamu kabisa. Pengine wewe una tamaa hiyo. Lakini inawezekanaje kuishi baada ya kufa?
Uzima Baada ya Kufa—Jinsi Gani?
“Vitabu vitakatifu” vya dini mbalimbali mara nyingi vinatoa majibu mawili kuhusu tatizo hilo. Baadhi ya vitabu hivyo vinaeleza kwamba “nafsi,” au “roho” ya mtu aliyekufa inaokoka tu. Kwa upande mwingine, Biblia inafundisha kwamba watu wanarudishwa kwenye uzima kupitia ufufuo.—Waebrania 11:17-19; Luka 20:37, 38; Yohana 5:28, 29; 11:24.
Haishangazi kwamba dini za nchi za Mashariki zinafundisha juu ya kuokoka kwa “nafsi,” au “roho,” kwa kuwa historia ya kutegemeka inaonyesha asili ya imani hiyo ni kutoka nchi za Mashariki. Wababiloni wa kale walikuwa wanaamini juu ya ulimwengu wa chini uliokuwa na nafsi za watu waliokufa wakiwa chini ya usimamizi wa mungu Nergali na mungu wa kike Eresh-kigali. Wamisri wa kale vilevile waliamini juu ya kutokufa kwa nafsi, na walikuwa na “ulimwengu wa chini” wao wenyewe. Wao walimwabudu Osirisi akiwa “mungu wa wafu.” Kama Wamisri, Waajemi wa kale waliamini juu ya “kupimwa kwa nafsi” baada ya kifo. Wanafalsafa wengi Wagiriki wa kale walilichukua wazo hilo la nchi za Mashariki la nafsi isiyokufa, ambalo lilifafanuliwa zaidi na Plato katika karne ya nne K.W.K.
Jambo la kushangaza ni kwamba dini ya Kiyahudi na dini za Jumuiya ya Wakristo zilichukua wazo la kwamba uzima wa wakati ujao unategemea kuwa na nafsi isiyokufa. Hilo Si fundisho la Biblia hata kidogo, kama inavyofunuliwa na kitabu The Concise Jewish Encyclopedia (1980): “Biblia haisemi juu ya fundisho la kutokufa kwa nafsi, wala hilo halionekani wazi katika vitabu vya marabi wa [Kiyahudi]. . . . Hatimaye imani hiyo ya kwamba sehemu fulani ya utu wa kibinadamu ni ya milele na haiwezi kuharibika ilipata kuwa sehemu ya imani ya kirabi na karibu ikawa imekubalika kabisa mahali pote katika dini ya Kiyahudi ya wakati wa baadaye.”
Wasomi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walifuata mfano wa marabi Wayahudi wakalichukua wazo la Kibabiloni, Kimisri, Kiajemi na Kigiriki la kwamba mwanadamu ana nafsi isiyokufa. Hata hivyo, kwa sababu makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanadai yanaikubali Biblia, yalitokeza hali mbili zenye kuwatatiza kwa kuchukua fundisho hilo lisilo la Kikristo. Hali hizo mbili zenye kutatiza ni hizi: Makanisa yanawezaje kufuata fundisho la Biblia la ufufuo na, wakati huo huo, yafundishe kwamba nafsi ya mtu inaokoka wakati wa kifo?
Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanaepaje utatizi huo? Kitabu Catholic Encyclopedia kinatuambia jinsi wanavyofanya, kwa kusema hivi: “Baraza la Mimbari ya Nne linafundisha kwamba watu wote, wawe ni wema au waovu, ‘watafufuliwa tena wakiwa na miili yao wenyewe ambayo sasa wanayo.’ Katika usemi imani za kidini na madai ya imani kurudi huko kwenye uzima kunaitwa ufufuo wa mwili.” (Sisi tumelaza maneno hayo) Ndiyo kusema, dai linafanywa kwamba ufufuo wa wafu ni kuvika tena nafsi isiyokufa mwili wa nyama. Lakini hivyo sivyo Biblia inavyofundisha.
Tumaini la Ufufuo la Kweli
Wasomi wengi wa Biblia wanakubali kwamba mafundisho ya kuzaliwa pamoja na nafsi isiyokufa na “ufufuo wa mwili” hayafundishwi katika Biblia. Georges Auzou, profesa wa Ukatoliki wa Ufaransa wa Maandiko Matakatifu, anaandika hivi; “Wazo la ‘nafsi,’ linalomaanisha kitu cha kiroho kabisa, kisicho na mwili, ambacho ni tofauti na ‘mwili,‘ . . . halipatikani ndani ya Biblia.” “Agano Jipya halizungumzi kamwe juu ya ‘ufufuo wa mwili,’ bali juu ya ‘ufufuo wa wafu.’”
Sawa na hayo, Profesa wa Uprotestanti wa Ufaransa Oscar Cullman, anasema hivi katika kitabu chake Immortality of the Soul or Resurrection of the Dead? (Kutokufa kwa Nafsi au Kufufuliwa kwa Wafu?): “Kuna tofauti kubwa kati ya tazamio la Kikristo la kufufuliwa kwa wafu na imani ya Kigiriki ya nafsi isiyokufa. . . . Ingawa baadaye Ukristo ulihusianisha tena imani hizo mbili, na leo Mkristo wa kawaida anavurugwa akili nazo kabisa, sioni sababu ya kuficha yale ambayo mimi na wasomi wengi wanaona kuwa ni kweli. . . . mkazo na wazo la Agano Jipya yanaongozwa kabisa na imani ya ufufuo. . . . mtu kamili, ambaye amekufa, anarudishwa kwenye uzima kwa tendo jipya la uumbaji la Mungu.”—(Kilitafsiriwa kutoka chapa ya kwanza ya Kifaransa.)
Ndiyo, tumaini la kweli la Biblia la uzima wa wakati ujao linategemea ufufuo, au “kufufuliwa tena kutoka kwa wafu,” si kuendelea kuishi kwa nafsi isiyokufa. Biblia inasema hivi kwa njia ya wazi kabisa: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Jinsi kuvurugika kwingi kwa kidini kulivyotokea baadaye itazungumzwa katika makala inayofuata.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Picha ya nafsi ikiruka juu ya mwili uliokufa inaonyesha kwamba Wamisri wa kale walisadiki kwamba nafsi haikufa