Jizoeze Imani Ili Upate Uhai wa Milele
”Uwe na imani ya kuhifadhi hai nafsi.’—WAEBRANIA 10:39, NW.
1. Ensaiklopedia moja ya Kikatoliki hukiri nini juu ya utumizi wa Biblia wa neno “nafsi”?
HAKUNA mahali ambapo Biblia husema kwamba wanadamu wana nafsi isiyokufa ambayo hubaki hai mwili ufapo na kuendelea kuishi katika makao ya roho. Hata New Catholic Encyclopedia hukiri hivi: “Wazo la nafsi ikiendelea kuwa hai baada ya kifo halionekani vyepesi katika Biblia. . . . Nafsi katika A[gano la] K[ale] haimaanishi sehemu ya mwanadamu, bali mwanadamu mzima—mwanadamu akiwa mtu aliye hai. Vivyo hivyo, katika A[gano] J[ipya] humaanisha uhai wa kibinadamu: uhai wa mtu akiwa mmoja.” Kwa hiyo si kwamba wanadamu wanazo nafsi, wao ni nafsi.
2. (a) Asili ya imani ya nafsi isiyokufa ilikuwa wapi? (b) Ni nini ukweli juu ya hali ya mwanadamu baada ya kifo?
2 Kama vile makala iliyotangulia ilivyoonyesha wazi, imani ya nafsi isiyokufa ni wazo la kipagani ambalo laweza kufuatiliwa nyuma hadi kwenye nyakati za mapema katika historia. Mtungaji walo ni yule mmoja aliyepinganisha ujulisho rasmi wa Mungu kwamba mwanadamu ‘angekufa hakika’ kwa kutotii. (Mwanzo 2:17) Mpinzani, Shetani Ibilisi, ndiye aliyesema hivi: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4) Na huo ulikuwa uwongo. (Yohana 8:44) Baadaye, Shetani alichochea fundisho la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu. Lakini ukweli juu ya hali ya mwanadamu baada ya kifo ni kama vile ulivyoandikwa katika Neno la Mungu lenye uvuvio kwenye Mhubiri 9:5: “Wafu . . . hawajui neno lo lote.”—Ona pia Warumi 5:12.
Tumaini la Uhai wa Milele
3. Biblia ina mengi ya kusema juu ya tumaini gani?
3 Ingawa Biblia huonyesha wazi kwamba hakuna kitu kama nafsi isiyokufa, hiyo husema mengi juu ya uhai wa milele. Tumaini la uhai (uzima) wa milele lilikuwa fundisho la Yesu la msingi. Alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Kuhusu wale ambao hujizoeza imani katika Mungu na Kristo, Yesu alitaarifu hivi: “Nami nawapa uzima wa milele.” (Yohana 10:28) Akiwa na uhakika kamili, yeye alisema hivi: “Yeye aaminiye yuna uzima wa milele. . . . Ataishi milele.” (Yohana 6:47, 51) Na pia alijulisha wazi hivi: “Jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
4. Yesu alisema nini juu ya tumaini la wakati ujao?
4 Kwa kuwa hakuna nafsi isiyokufa ambayo huendelea kuishi baada ya kifo, ahadi ya Biblia ya uhai wa milele itatimizwaje? Yesu alitoa habari zaidi juu ya hilo alipozuru Martha na Mariamu baada ya Lazaro ndugu yao kuwa amekufa. Alisema hivi kwa Martha: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi.” Akamwuliza Martha: “Je! unayasadiki hayo?” Naye akajibu: “Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu.”—Yohana 11:25-27.
5, 6. Kitendo cha Yesu cha kumwinua Lazaro arudie uhai kilionyesha nini?
5 Kuonyesha kwamba yeye, akiwa Mwana wa Mungu, alipewa nguvu za kuinua wafu warudie uhai, Yesu alienda kwenye ziara (kaburi) la Lazaro. Lazaro alikuwa amekuwa mfu siku nne, na mwili wake ulikuwa umeanza kuoza. Hata hivyo, “[Yesu] akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.” (Yohana 11:43, 44) Lazaro mfu alikuwa amerudishwa kwenye uhai!
6 Lazaro hakurudishwa kutoka mbinguni au mahali pengine popote katika makao ya roho. Hakuwa ameenda kwenye makao ya kiroho alipokufa bali alikuwa amekuwa bila fahamu kaburini, walimo wafu wote. (Zaburi 146:4; Yohana 3:13; Matendo 2:34) Halingekuwa jambo la akili kufikiri kwamba nafsi isiyokufa ya Lazaro ilikuwa ikiona shangwe ya uraha-mustarehe wa kimbingu halafu nafsi hiyo ikanyakuliwa kutoka mbinguni ili iungamanishwe upya na mwili wake usiokamilika duniani ili iishi tena katika ulimwengu wenye kujaa mateso, magonjwa, na kifo. Lakini kwa sababu hakuwa mbinguni, kurudishwa kwake aishi tena kulifurahiwa, kwa maana kulimaanisha angekuwako kwa miaka ya ziada na kuungamana upya pamoja na wapendwa wake. Baadaye, angekufa tena.
7, 8. (a) Ni katika pindi gani nyinginezo Yesu aliinua wafu? (b) Kwa nini Yesu alifanya miujiza ya kurudisha watu kwenye uhai?
7 Yesu alipoinua msichana mchanga aliyekuwa amekuwa mfu, wazazi wake “wakashangaa mshangao mkuu.” (Marko 5:42) Hata hivyo, msichana huyo pia alikufa tena hati-maye. Yesu alipoinua mwana mfu wa mjane wa Naini, “hofu ikawashika wote, wakamtukuza Mungu.” (Luka 7:16) Lakini mwanamume huyo pia alikufa hatimaye. Kuhusu miujiza hii, The New International Dictionary of New Testament Theology huhakikishia hivi: “Wale walioinuliwa na Kristo katika huduma yake ya kidunia walilazimika kufa, kwa kuwa miinuo hii haikuwapa kutokufa.”
8 Kwa nini Yesu akawainua kutoka kwa wafu? Si ili awape uhai wa milele wakati huo, bali ili aonyeshe kwamba ndiye aliyekuwa Mesiya na ili aonyeshe mambo ambayo Mungu alikuwa amempa nguvu za kufanya. Hiyo ilijenga imani katika tumaini la ufufuo na uhai wa milele chini ya utawala wa wakati ujao wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu mikononi mwa Kristo.—Mathayo 6:9, 10; Yohana 11:41, 42.
9. Martha na Paulo walielewaje fundisho la Yesu kwa usahihi juu ya tumaini la ufufuo?
9 Martha alijua juu ya tumaini hilo kwa kushirikiana na Yesu, kwa maana hapo kwanza yeye Martha alikuwa amesema kwake hivi kuhusu Lazaro: “Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:24) Alijua kwamba ufufuo haungekuwa katika siku yake (Lazaro) ya mwisho, bali wakati ujao katika “siku ya mwisho”—Siku ya Hukumu, ambapo wafu wangeinuliwa wakiwa chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Mtume Paulo alijua hilo pia, kwa maana alisema: “[Mungu] ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki [uadilifu, NW].” (Matendo 17:31) Pia Paulo alisema: “kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Hakusema kwamba ufufuo ulikuwa tayari unatukia bali kwamba ‘ungekuwako’ wakati ujao—chini ya utawala wa Ufalme.
10. Profesa Mfaransa atoa elezo gani juu ya imani za Jumuiya ya Wakristo juu ya ufufuo kwa kulinganishwa na fundisho wazi la Biblia?
10 Katika kitabu Immortality of the Soul or Resurrection of the Dead? Profesa Mfaransa wa Kiprotestanti Oscar Cullmann aandika hivi: “Kuna tofauti kubwa kati ya tarajio la Kikristo la ufufuo wa wafu na imani ya Kigiriki katika kutokufa kwa nafsi. . . . Ingawa baadaye Ukristo uliweka kiunzi kati ya imani mbili hizi, na leo Mkristo wa wastani huzivuruga kabisa, mimi sioni sababu ya kuficha mambo ambayo mimi na wengi wa wanachuo hufikiria kuwa ukweli. . . . Simulizi na wazo la Agano Jipya limejaa kabisa imani katika ufufuo . . . . Mwanadamu mzima, ambaye ni mfu kikweli, hurudishwa kwenye uhai na kitendo kipya cha uumbaji wa Mungu.”
Ufufuo—Kwenda Wapi?
11, 12. (a) Ni nini kusudi la Mungu kwa wanadamu na dunia hii? (b) Yesu alionyeshaje kwamba kusudi la Mungu kwa dunia halijabadilika?
11 Mungu alipoumba wanadamu, aliwapa dunia iwe kao lao la milele na akakusudia kujaza sayari hii jamii ya watu waadilifu. (Mwanzo 1:26-28; Zaburi 115:16) Biblia hunena juu ya Yehova kuwa “aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.
12 Kujapokuwa na maelfu ya miaka ya kutokamilika na kifo tangu uasi wa mwanadamu, bado ni kusudi la Mungu kwamba dunia iwe kao la milele la mwanadamu: “Wenye haki watairithi nchi [dunia, NW], nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) “Wenye furaha ni wale wapole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:5, NW) Hivyo, Yesu aliporudisha wafu kwenye uhai, aliwainua papa hapa duniani, nao walitambuliwa mara iyo hiyo na wengine kuwa ndio watu wale waliokuwa wamekufa. Hiyo ilihakikishia kwamba chini ya utawala wa Ufalme walio wafu watarudishwa kwenye uhai duniani wawe na fursa ya kuishi milele humo. (Ufunuo 20:12, 13) Hiyo itatimiza kusudi la Mungu kwa wanadamu na kwa dunia.—Isaya 46:9-11; 55:11; Tito 1:1, 2.
13. Ni tatizo gani lenye kubana pande zote linalokabili makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, nao hujaribu kulitatuaje?
13 Hata hivyo, kwa kuwa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo huamini katika kutokufa kwa nafsi, hiyo huwatokezea tatizo lenye kuwabana pande zote: Watapatanishaje ufufuo wa “mwanadamu mzima,” kama ulivyoonyeshwa na Yesu, pamoja na imani yao katika nafsi isiyokufa ambayo tayari inaishi katika mbingu au katika helo? The Catholic Encyclopedia hukazania hivi: “Baraza la Nne la Kilateri hufundisha kwamba wanadamu wote, wawe ni wateule au walioandikiwa kupata laana, ‘watainuka tena pamoja na miili yao wenyewe ambayo sasa wanachukuana nayo huku na huku.’” Huongezea hivi: “Kwa kuwa mwili ni mshiriki wa vitendo vya uhalifu wa nafsi, na mwandamani wa mema yayo, yaonekana kuwa haki ya Mungu hudai kwamba mwili uwe mshiriki katika adhabu na thawabu ya nafsi.” Kulingana na imani hii, mwili utaungamanishwa upya na nafsi katika mbingu au katika helo. Kwa muda gani? “Miili iliyoinuka ya watakatifu na watenda dhambi itavikwa kutokufa,” chadai chanzo hicho.
14. Mwandikaji mmoja Myeswiti hujaribuje kuelewesha wazi maoni ya Jumuiya ya Wakristo juu ya ufufuo wa mwili?
14 Katika kitabu The Future Life, kilichotungwa na Myeswiti J. C. Sasia, twasoma hivi: “Kwa hiyo uhai wa mbinguni utakuwa wa mambo ya raha pia kupitia milango ya fahamu zilizotukuzwa [za mwili ulioungamanishwa upya pamoja na nafsi].” Kuhusu miili iliyoungamanishwa pamoja na nafsi zayo katika helo, chanzo hicho chadai hivi: “Katika helo, baada ya ufufuo [wa mwili], kila hisia ya mwili wa kibinadamu itakuwa na adhabu ya aina yayo yenyewe . . . Mlango wa fahamu ya kuhisi au kugusa utateswa kwa njia ya pekee, kwa sababu wale walioandikiwa kupata laana wamemkosea Mungu kupitia dhambi za mnofu hasa. . . . Ushirika wao pamoja na miili yao utawasababishia mateso na mashaka zaidi.”
15. Kwa nini ni kufuru kufundisha kwamba Mungu hutesa watu milele katika helo?
15 Hivyo, kukubali wazo la kipagani la kutokufa kwa nafsi kuliandaa njia ya Jumuiya ya Wakristo kukubali pia wazo la kipagani la kuteswa vikali sana kwa nafsi—na hata miili—katika helo milele. Hata hivyo, kuhusu lile zoea la kale la kuchoma watoto kuwa dhabihu kwa miungu bandia, Yehova alitaarifu hivi: “Nao . . . [wawachoma] moto wana wao, wawe sadaka za kuteketezwa kwa Baali; tendo nisiloliamuru mimi, wala kulinena, wala halikuingia moyoni mwangu.” (Yeremia 19:5) Kwa hiyo ni kufuru kufundisha kwamba Mungu hutesa watu kwa umilele, hali Neno lake mwenyewe huonyesha wazi kwamba wakosaji wasiotubu wataharibiwa, watokomezwe. “Nafsi yoyote ambayo haitasikiliza Nabii huyo [Yesu] itaharibiwa kabisa.”—Matendo 3:23, NW; ona pia Mathayo 10:28; Luka 17:27; Yohana 3:16; 2 Petro 2:12; Yuda 5.
Kutokufa
16. Biblia hufundisha nini juu ya kutokufa?
16 Hata hivyo, je! Biblia haifundishi kwamba wanadamu wangepelekwa mbinguni wakaishi huko wakiwa na uhai usiokufa? Ndiyo. Lakini hilo halina uhusiano wowote na nafsi za kibinadamu zisizokufa. Kutokufa hutokana na kufufuliwa kwa mtu akiwa uumbaji-roho (kama ilivyokuwa kwa Yesu) wala si kutokana na kuwa kwake na nafsi isiyokufa ambayo imebaki hai baada ya kufa. Thawabu ya wakati ujao ya kutokufa ilinyooshwa kwa wanadamu fulani waaminifu walio kama Kristo, nayo ingepatikana wakati tu Kristo angekuja katika mamlaka ya Ufalme mbinguni, si mara baada ya kupaa kwa Kristo mbinguni katika karne ya kwanza.—Zaburi 110:1; 1 Wakorintho 15:53, 54.
17. Ni wangapi watafikia kutokufa, nao hushiriki sehemu gani katika kusudi la Mungu kwa dunia?
17 Zaidi ya hilo, tumaini hilo lilinyooshwa kwa watu wa jamaa ya kibinadamu ambao ni wachache kwa kulinganishwa. Yesu aliwaita “kundi dogo.” (Luka 12:32) Kikundi hiki, hesabu yacho ikiwa ni 144,000, hufufuliwa kwenye uhai wa kimbingu kuwa viumbe-roho wasiokufa ili kutawala juu ya dunia pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa kimbingu. (2 Petro 3:13; Ufunuo 7:4; 14:1, 4; 20:4) Baada ya muda fulani, dunia ambayo wataitawala wakiwa juu itakuwa yakaliwa na wanadamu wakamilifu, bila shaka maelfu kwa mamilioni. Wengi wa wanadamu hao watakuwa wale wenye kurudi duniani katika “ufufuo wa wafu, wenye haki [waadilifu, NW] na wasio haki [wasio waadilifu, NW] pia.” (Matendo 24:15) Hata hivyo, kutakuwako wengine ambao watapata uhai katika ulimwengu mpya kando na wale wenye kufufuliwa kutoka kwa wafu. Wengine hawa ni akina nani?
“Hatakufa Kamwe”
18. Zaidi ya tumaini la ufufuo kwa watu wafu, Yesu alitabiri jambo gani la kustaajabisha?
18 Ingawa tumaini hakika kwa watu wafu ni ufufuo, kuna tumaini jingine zuri ajabu katika wakati wetu. Lahusiana na yale ambayo Yesu aliendelea kumwambia Martha. Baada ya kusema: “Anayeniamini mimi [ajizoezaye imani katika mimi, NW] hata kama anakufa ataishi [katika ule ufufuo, NW],” Yesu akaongezea, “na kila anayeishi na kuniamini hatakufa kamwe.” (Yohana 11:25, 26, HNWW) Katika taarifa hii ya pili, Yesu alitabiri jambo la kustaajabisha: Wakati ungekuja ambapo watu wanaoishi hawangehitaji tena kufa! Lakini ingekuwa hivyo wakati gani?
19. (a) Tumaini la kutokufa kamwe lingetimizwa katika kipindi gani? (b) Biblia huelezaje juu ya wale walio na tumaini la kutokufa kamwe?
19 Sasa—wakati wetu—ndio wakati wa ahadi hiyo kutimizwa! Ithibati yote yaonyesha kwamba tuko karibu sana na mwisho wa ulimwengu huu mwovu. (Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5, 13) Hivyo, watu ambao leo hujizoeza imani katika Mungu na katika Mwana wake wana tumaini lenye kusisimua juu ya kubaki hai wakati wa mwisho wa mfumo huu na kuendelea kuishi waingie ulimwengu mpya wa Mungu—wasife kamwe kamwe! Hawa hunenwa kwenye Ufunuo 7:9-14, NW, kuwa “umati mkubwa, ambao hakuna binadamu aliyeweza kuhesabu kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na ndimi . . . ambao huja kutoka dhiki kubwa,” wakihifadhiwa na Mungu kwa sababu ya kujizoeza kwao imani. Yesu aliunena mfumuo unaokuja wa mfumo huu mwovu uliopo kuwa “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.”—Mathayo 24:21; ona pia Mithali 2:21, 22; Zaburi 37:10, 11, 34.
20, 21. Leo mamilioni wanajizoezaje imani katika Mungu na Kristo, na wengi wao hawatahitaji nini?
20 Katika sehemu zote za ulimwengu, mamilioni ya umati mkubwa watakao kuishi milele duniani wanajizoeza imani tayari katika ahadi za Mungu na katika yule mmoja ambaye yeye amempa mamlaka ya kuwa ndiye ‘ufufuo na uzima,’ Yesu Kristo. Nao wamejiweka wakfu kwa Mungu, wakiufananisha kwa ubatizo wa maji. (Mathayo 28:19, 20) Wao hukiri kwamba deni lote la wokovu walilo nalo ni kwa ‘Mungu, ambaye ameketi juu ya kiti cha ufalme, na kwa Mwana-Kondoo,’ Yesu Kristo.—Ufunuo 7:10, NW.
21 Wale wa umati mkubwa watakaookoka mwisho wa ulimwengu huu hawatahitaji ufufuo kutoka kwa wafu kwa sababu ‘hawatakufa kamwe’! Je! wewe unachukua hatua za kuwa mmoja wa kikundi hiki? Ikiwa ndivyo, umeachiwa wazi pendeleo la kustaajabisha tena lisilo na kifani—lile la kubaki hai mwishoni mwa mfumo mwovu wa Shetani na kuingizwa upesi katika enzi mpya ya uadilifu itakayokuletea afya kamilifu na uhai wa milele katika dunia-paradiso! (Luka 23:43; Ufunuo 21:4, 5) Kwa kujifunza mapenzi ya Mungu ni nini na kudumu katika kuyafanya, waweza kuonyesha kwamba wewe ‘si aina ya warudio nyuma kwenye uharibifu.’ Wewe pia waweza kuwa na “imani ya kuhifadhi hai nafsi.”—Waebrania 10:39, NW; 1 Yohana 2:15-17; Ufunuo 7:15.
Maswali kwa Kupitia
◻ Ni nini tumaini la kweli kwa wafu?
◻ Kwa nini imani ya Jumuiya ya Wakristo katika ufufuo wa mwili ni la kuvunjia Mungu heshima?
◻ Biblia hufundisha nini juu ya kutokufa?
◻ Ni tumaini gani la kustaajabisha ambalo watu waweza kuwa nalo leo?