Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 8/1 kur. 4-7
  • Je! Wafu Wako Hai? Yanayosemwa na Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wafu Wako Hai? Yanayosemwa na Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Udanganyifu wa Duniani Pote
  • Je! Nafsi Yako Haiwezi Kufa?
  • Je! Wataamshwa?
  • Huenda Wengine Wakauliza . . .
  • Imekupasa Wewe Ufanye nini?
  • Jizoeze Imani Ili Upate Uhai wa Milele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Inakuwaje Tunapokufa?
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
  • Inakuwaje Wakati wa Kufa?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Kuna Sababu ya Kuwaogopa Wafu?
    Amkeni!—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 8/1 kur. 4-7

Je! Wafu Wako Hai? Yanayosemwa na Mungu

NDEGE nyepesi iliruka kutoka jiji moja katika Afrika ya Kusini ikielekea kwenye mji uliokuwa umbali wa kilometa 400. Ndani alikuwamo rubani na binti yake mdogo mwenye umri wa miaka 12. Lakini walipojaribu kutusha ndege chini kwa dharura, ndege ile ilianguka, ikawaua wote wawili.

“Yehova Mungu peke yake ndiye aliyejua maumivu na hasara iliyonipata, na pia jinsi nilivyolazimika kupambana na hali hiyo,” anakumbuka Betty, mke wa rubani na mama ya binti huyo. Aliwezaje kushinda hali hiyo? “Mimi nilisali daima na kila wakati ili nipate ushujaa na nguvu za kujiweza mwenyewe ili niweze kusaidia wengine washindane na hali zao kama mimi.” Betty alipata pia faraja kutokana na yale yanayosemwa na Mungu juu ya hali ya wafu na tumaini la ufufuo.

Mungu anasema nini juu ya wafu? Biblia inajibu: “Wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Kwa hiyo wafu hawana fahamu. Ni hivyo tu. Basi mbona watu walio wengi wanaamini jambo tofauti? Ni kwa sababu wamedanganywa na udanganyifu mkubwa mno wa kale wa duniani pote!

Udanganyifu wa Duniani Pote

Mambo yote yalianza na ule uliokuwa ndio uwongo wa kwanza kusemwa. Usimulizi wa kihistoria ulio katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo unatoa maelezo kwa urefu. Unasema: “Walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Huyo alikuwa ni Yehova Mungu akisema na yule mtu wa kwanza, Adamu. Sasa, linganisha maneno hayo na Mwanzo 3:1-4, ambapo Shetani, akisema kupitia nyoka, alishawishi Hawa asimtii Mungu, akisema: “Hakika hamtakufa.” Kwa hiyo Shetani alipinganisha maneno yaliyokuwa yamesemwa na Mungu. Kwa njia hiyo alisema uwongo wa kwanza, akawa ndiye ‘baba wa uwongo.’—Yohana 8:44; Ufunuo 12:9.

Lakini Adamu na Hawa walikufa, ndivyo na mamilioni yasiyohesabika ya watu wengine. Shetani alifunikaje uwongo wake ilipotukia hivyo? Ni kwa kuimarisha baadaye wazo la kwamba, ingawa mwili unakufa, kitu fulani kinaendelea kuishi. Basi hilo likawa fundisho la dini za kale ambalo liliingizwa katika falsafa ya Kigiriki. Kwa sababu hiyo, imani ya kwamba nafsi haiwezi kufa iko karibu kila mahali ulimwenguni. Na watu wengi, wanaoamini kwamba wapendwa wao waliokufa wako hai mahali fulani, labda hilo ni wazo lenye kufariji. Lakini, ulizo lililo la maana ni hili: Je! hiyo ni kweli?

Je! Nafsi Yako Haiwezi Kufa?

Neno “kutokufa” linaonekana mara tatu katika Biblia, na mahali hapo pote ambapo linaonekana ni katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Uchunguzi wa matumizi yalo unaonyesha wazi jambo moja: Mwanadamu hakuumbwa akiwa na kutokufa.

Mfano, fikiria maneno ya mtume Paulo kwenye 1 Timotheo 6:15, 16, NW ambapo anaeleza kwamba Yesu Kristo ni “Mfalme wa wale wanaotawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale wanaotawala wakiwa mabwana, yeye peke yake aliye na kutokufa.” Kwa hiyo ni kwa njia gani Yesu yuko tofauti kabisa na “wafalme” na “mabwana” wengine wote? Yeye ana kutokufa; wao hawana.

Ni kweli kwamba wale wafuasi wa Kristo wanaoitwa wakatawale pamoja naye katika mbingu, wameahidiwa kutokufa. (1 Petro 1:3, 4, NW ) Hivyo, kwenye 1 Wakorintho 15:53, 54 tunasoma: “Sharti huu . . . wa kufa uvae kutokufa. Basi huu . . . wa kufa utakapovaa kutokufa, hapo ndipo litakapokuwa lile neno lililoandikwa, Mauti imemezwa milele.” Lakini angalia hapo kwamba kutokufa ‘kunavaliwa.’ Ni thawabu kwa Wakristo waaminifu, waliochaguliwa. Si jambo ambalo wanadamu wote wanarithi.

Tena, Biblia haisemi kwamba mwanadamu anayo au alipewa nafsi. Bali, inasema: “[Yehova] Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7; linganisha 1 Wakorintho 15:45.) Kuwa jambo fulani ni tofauti kabisa na kuwa na kitu fulani. Hakuna mtu atakayeshindana na uhakika wa kwamba kuwa mbwa ni tofauti na kuwa na mbwa! Vivyo hivyo, kuwa nafsi si sawa na kuwa na nafsi.

Kwamba si wanadamu wote wanaopokea zawadi ya kutokufa ni wazi kutokana na marejezo mengi yalio katika Biblia yanayosema nafsi inakufa. Kwa mfano: “Nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe ndiyo itakayokufa.” (Ezekieli 18:4, 20, NW ) “Kweli, nafsi yo yote isiyomsikiliza yule Nabii itaangamizwa kabisa kutoka miongoni mwa watu.”—Matendo 3:23, NW.

Kwa kuwa sisi hatuna nafsi zisizoweza kufa, ni jambo gani linalotukia tunapokufa? ‘Tunalala,’ kwa vile kwa sababu ya dhabihu ya ukombozi ya Kristo lipo tumaini la ufufuo. (1 Wakorintho 15:22) Lazaro alipokufa Yesu alisema: “Ninakwenda nipate kumwamsha [katika usingizi].” Halafu akaeleza: “Lazaro amekufa.” (Yohana 11:11-14) Paulo pia alinena juu ya wale “waliolala [katika] mauti.” (1 Wathesalonike 4:13, 14; 1 Wakorintho 15: 20) Basi, ikiwa wafu wanalala . . .

Je! Wataamshwa?

Fikiria tamasha hii ya kustaajabisha: kundi la watu limekusanyika mbele ya pango kule Bethania, karibu na Yerusalemu. Yesu yupo pamoja na Mariamu na Martha, dada za Lazaro, ambaye juzijuzi amekufa na maiti yake inalala katika pango lililofungwa kwa jiwe. “Liondoeni jiwe,” Yesu anaagiza. Martha anakataa: “Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne.” Lakini baada ya sala fupi Yesu anapaaza sauti: “Lazaro, njoo huku nje”! Na yule mwanamume Lazaro anatoka nje! (Yohana 11:38-44) Je! unaweza kuwazia mshangao na furaha ya lile kundi la watu—hasa Mariamu na Martha?

Kama Lazaro angalikuwa hai wakati wa siku nne hizo, je! asingalifunulia kila mtu jambo hilo? Lakini hakuna maandishi ya kuonyesha kwamba yeye alinena juu ya jambo lo lote lililompata alipokuwa mfu, na hiyo inaendelea kuthibitisha, vile Biblia inavyosema kwamba “Wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5.

Kisa cha Lazaro hakikuwa tofauti na vile vya watu wengine. Katika mahali penye kuitwa Naini, Yesu alikutana na andamano la maziko ya kijana mwanamume aliyekuwa karibu kuzikwa. Yesu akasema: “Kijana, nakuambia, Inuka.” Halafu ikawaje? “Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema.” (Luka 7: 11-17) Lakini, hapa tena, je! yule kijana mwanamume alisema lo lote juu ya mahali ambapo watu wanaenda wakifa? Hapana, kwa maana ni wazi yeye alikuwa amekufa fo fo fo.

Yesu, Paulo, Petro, Eliya, na Elisha wote walifufua wafu. Hakuna ye yote wa wale waliokuwa wamekufa wakati mmoja aliyesema neno lo lote juu ya kuwako kwa uhai baada ya kufa.

Miujiza hiyo ya ajabu ni mfano wa kuutangulia kuonyesha njia moja tu ambayo wafu walio wengi sana wanaweza kuishi tena—kwa kufufuliwa warudie uhai duniani chini ya Ufalme wa Mungu. Akasema Yesu: “Msione hili kuwa ajabu, kwa sababu ile saa inakuja ambayo katika hiyo wale wote walio katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti [yangu] watoke.” (Yohana 5:28, 29, NW ) Hilo litakuwa tukio la kusisimua sana kwa wale watakaopendelewa kuishi chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo wa miaka elfu moja, ambao sasa u karibu. (Ufunuo 20:4, 6) Lile tumaini lenyewe tu la ufufuo linathibitisha kwamba wafu hawawezi kuwa wako hai. Ikiwa watu watafufuliwa, basi ni lazima kwanza wawe hawana uhai.

Huenda Wengine Wakauliza . . .

Lakini namna gani madai yanayofanywa na vyombo vya kuwasiliana na ulimwengu wa roho, na pia watu wengine ya kwamba wao wanapokea ujumbe kutoka kwa waliokufa? Je! jambo hilo halithibitishi kwamba wafu wako hai? Hapana. Shetani ni mwerevu sana, mdanganyifu mkuu ambaye mara nyingi “anavaa kinyago aonekane kama malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14, The New English Bible) Yeye na mashetani wake wanaweza kuvaa kinyago wawe kama ndio roho za watu ambao wamekufa, na mara nyingi wanafanya hivyo! Kwa hiyo, Sheria ya Yehova kwa Israeli ilisema waziwazi hivi: “Mtu ye yote anayeenda kuomba mashauri kwa chombo cha kuwasiliana na ulimwengu wa roho . . . au mtu ye yote anayeuliza juu ya wafu . . . ni kitu cha kuchukiza sana kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12, NW ) Yehova anasema pia kwamba wale Wanaozoea mawasiliano na ulimwengu wa roho “hawataurithi ufalme wa Mungu” bali wataharibiwa.—Wagalatia 5: 19-21; Ufunuo 21:8.a

Namna gani wale wanaodai kwamba walipatwa na vituko vya kukaribia kufa? Je! hiyo haithibitishi kwamba roho au nafsi inauacha mwili wakati mtu anapokufa? George Gallup Mdogo, aliye mwanzilishi wa kura ya kuchunguza maoni ya watu wengi katika United States, alichunguza habari hiyo na kutangaza matokeo katika kichapo Adventures in Immortality. Madaktari na wanasayansi waliohojiwa walikuwa na mashaka-mashaka juu ya ukweli wa masimulizi yanayohusu vituko vya kukaribia kufa. Alisema hivi mtaalamu mmoja wa elimu ya viumbe na ya fizikia katika Maryland: “Hivyo ni vituko vya akili ikiwa katika hali ya kutokufanya kazi vizuri . . . Ubongo ni kiungo chenye mambo mengi magumu kufahamika nao unaweza kukudanganya sana ukiutenda vibaya—tazama vituko vinavyopata watu wanaotumia dawa zenye kuwafanya waone ndoto.” Daktari mmoja anayeshughulika na magonjwa ya akilini katika Ohio alisema hivi: “Ripoti hizo ni mambo ya kuwaziwa-waziwa tu au vituko vya kuona ndoto tu.” Mwanasayansi wa Michigan alisema: “Hayo ni mawazo-mawazo ya msisimuko tu yanayosababishwa na hitilafu fulani za akili na mwili.”

Gallup alikata shauri kwamba masimulizi yanayohusu vituko vya kukaribia kufa ‘hayawi kwa vyo vyote kile kinachoweza kufikiriwa kuwa ni uthibitisho wa kwamba kuna hali ya kutokufa au maisha baada ya kifo.’ Anaongeza hivi: “Hizo zinaweza kuwa ni mfululizo wa tamasha za akilini tu zinazoonekana kama kwamba ziko nje kulingana na akili za wale wanaopatwa na maumizo ya mwili.” Yeye anadokeza pia kwamba wanadini fulani wenye kufikiri wangeeleza vituko hivyo kuwa ni “sehemu ya maarifa ya kishetani ya kudanganya wanadamu.” Maneno aliyosema Yehova Mungu zamani yangali ni ya kweli: “Wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5.

Imekupasa Wewe Ufanye nini?

Jihadhari na mawazo au mafundisho yanayotegemea uwongo wa kwanza wa Shetani —“hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:1-5) Kubali yanayofundishwa na Neno la Mungu, kwamba wakati mtu anapokufa “mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:4) Kubali, pia, kwamba wafu wanaolala wataamka wakati wa utawala mtukufu wa Ufalme wa Mungu, ambao wengi wanaomba, wakati ambao “kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”—Matendo 24:15; Mathayo 6:9, 10.

Yule mwanamke mgonjwa-mgonjwa aliyetajwa katika makala yetu ya kwanza alifurahi sana alipoambiwa mambo ambayo Mungu anasema juu ya wafu na juu ya roho za kishetani zenye udanganyifu. Yeye aliharibu hirizi zake na vitu vingine vya kutumia kuwasiliana na ulimwengu wa roho, na katika muda wa siku chache akajisikia vizuri zaidi. Sasa yeye anasaidia wengine wajiondoe katika ibada ya mashetani.

Yule mjane aliyepoteza wapendwa wake katika lile anguko la ndege alifarijiwa na wazo hili: Kwa kuwa wafu hawajui lo lote, kwao wakati si kitu. Kwa hiyo kulingana na vile hali yao ilivyo, wao wataamka dakika ile nyingine katika paradiso ya kidunia chini ya Ufalme wa Mungu! Mwanamke huyo anafurahia sana kusaidia wengine wajue kwamba karibuni “[Yehova] atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8) Yeye anaitazamia siku ambayo wapendwa wake waliokufa watakuwa hai kupitia ufufuo.

[Maelezo ya Chini]

a Ona pia kijitabu Roho Zisizoonekana—Je! Zinatusaidia? au Zinatuumiza? Kiiichochapishwa na Sosaiti yetu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki