Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 9/1 kur. 11-14
  • Ufufuo, Siku ya Hukumu na Uasi-imani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufufuo, Siku ya Hukumu na Uasi-imani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ufufuo na Uasi-imani
  • Uasi-imani ‘Waenea kama Donda-ndugu’
  • Kushikamana na Kweli ya Biblia
  • Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Kuzaliwa Pamoja na Nafsi Isiyokufa au Ufufuo—Ni Jambo Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Ule Ufalme na lile Tumaini la Ufufuo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Nguvu za Tumaini la Ufufuo
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 9/1 kur. 11-14

Ufufuo, Siku ya Hukumu na Uasi-imani

MAKANISA ya Katoliki ya Roma, Orthodoksi na Protestanti yamezipa kisogo kweli za Biblia zilizo wazi zinazohusu hali ya wafu na tumaini la uzima baada ya kufa. Yanapendelea imani ya kale isiyo ya Kimaandiko ya nafsi isiyokufa. Kama tulivyokwisha kuona, imani hiyo asili yake ni Babilonia na ilirekebishwa na mwana-falsafa Mgiriki, Plato katika karne ya nne K.W.K.

Watheologia (wasomi wa elimu ya kidini) wanadai kwamba kila mwanamume, mwanamke na mtoto ambaye amepata kuishi ana nafsi inayotoka mwilini anapokufa. Ili fundisho hilo lifae, wamebuni mahali kama limbo (mahali pa kuwazia ambapo nafsi zilizozuiwa kwenda mbinguni zinakaa), purgatori (matohara) na moto wa mateso: Inasemekana huko ndiko zinakokwenda nafsi zilizotoka mwilini ambazo hazistahili “paradiso,” ambayo wanasema iko mbinguni.

Vilevile makanisa hayo yanasema kwamba wafu hawajakufa kabisa. Badala yake, wanadai nafsi zinaendelea kuishi. Kwa hiyo hayawezi kufundisha fundisho la kweli la Biblia la ufufuo, linalofafanuliwa kuwa ni “kurudi kwenye uzima.” Kwa hiyo watheologia wao walibuni ule unaoitwa ufufuo wa mwili, na kudai kwamba wakati wa Siku ya Hukumu miili ya wenye haki na ya waovu itaungana pamoja na nafsi zao ili washiriki katika raha ya mbinguni au laana ya moto wa mateso. Na kwa kuwa wanasadiki kwamba “nafsi” hizo hazipasi kungojea Siku ya Hukumu ili zipelekwe “mbinguni,” “moto wa mateso” au hizo ‘sehemu za kungojea’ kama “limbo” au “purgatori,” watheologia wa Jumuiya ya Wakristo walibuni pia fundisho la hukumu mbili. Ya kwanza kati ya hizo inaitwa Hukumu ya Mtu, ambayo ni wakati “nafsi” inaposemekana inatoka mwilini wakati wa kifo. Ya pili inaitwa Hukumu ya Wote, ambayo ni wakati miili ‘inafufuliwa’ na inaposemekana inaungana tena na “nafsi” wakati wa Siku ya Hukumu.

Ufufuo na Uasi-imani

Mabuni hayo yote ya kitheologia yaliyotangulia kutajwa yalitokezwa kwa sababu Kanisa la Katoliki ya Roma, lililoigwa kwa sehemu fulani za msingi na makanisa ya Orthodoksi na Protestanti, halikushikamana na mafundisho ya Biblia yaliyo wazi juu ya ufufuo na habari kama hizo juu ya kifo, nafsi ya kibinadamu na hukumu ya mwisho.

Kuhusiana na jambo hilo uasi-imani ulianza mapema katika historia ya Ukristo. Miaka inayozidi kidogo 20 tu baada ya kifo na kufufuliwa kwa Kristo, mtume Paulo aliandikia kundi changa la Kikristo huko Korintho, Ugiriki akiwa Efeso, akasema: Basi, ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu [Wakristo watiwa mafuta] husema kwamba hakuna [ufufuo wa] wafu?”​—1 Wakorintho 15:12.

Inaweza kuwa kwamba baadhi ya Wakristo ambao Paulo alikuwa akiandikia katika Korintho walikuwa wangali chini ya uongozi wa falsafa ya Kigiriki. Miaka michache kutangulia hapo, Paulo alikuwa ametangaza “habari [njema] za Yesu na ufufuo” kwa wanafalsafa Wagiriki katika Athene. Lakini “waliposikia habari za ufufuo wa wafu wengine walifanya dhihaka.” (Matendo 17:18, 32) Waepikureo na Wastoiko walikuwa na maoni yao wenyewe juu ya mambo yaliyoipata nafsi baada ya kifo. Wanafalsafa wengine Wagiriki, waliofuata baada ya Socrates na Plato, waliamini juu ya nafsi isiyokufa. Hakuna ye yote wao aliyeuamini ufufuo, kama unavyofundishwa katika Biblia.

Pia inaweza kuwa kwamba Wakristo fulani Wakorintho tayari walikuwa na maoni yaliyoasi imani juu ya ufufuo ambayo mtume Paulo alilaani miaka 10 baadaye, Kumbuka kwamba Paulo alipomwandikia Timotheo, ambaye inaelekea alikuwa katika Efeso wakati huo, yeye alionya hivi: “Epuka semi zisizo na maana zinazochafua yaliyo matakatifu; kwa maana watazidi kuwa wabaya hata wakose kuheshimu Mungu, na neno lao litaenea kama donda-ndugu. Himenayo na Fileto ni wa idadi hiyo. Wanaume hao hao wamepotoka wakaiacha kweli, wakisema kwamba ufufuo umekwisha kutokea; nao wanaipindua imani ya wengine.”​—2 Timotheo 2:16-18.NW

Kwa kusema kwamba “ufufuo umekwisha kutokea,” waasi-imani hao hawakuwa wakidai kwamba Wakristo waliokufa walikuwa wamekwisha kufufuliwa kutoka kwa wafu. Inaonekana waliamini kwamba Wakristo wanaoishi walikuwa wamekwisha kufufuliwa, ufufuo huo ukiwa ni wa aina ya mfano tu, wa kiroho tu. Walikana wakisema hakutakuwako ufufuo wo wote wa wafu wakati ujao. Mawazo hayo yalikuwa ‘yanapindua imani ya wengi,’ hata mtume Paulo akatoa onyo kali juu ya walimu hao waliokana imani.

Uasi-imani ‘Waenea kama Donda-ndugu’

Bila shaka Himenayo huyo ni yule yule anayetajwa na Paulo katika barua yake ya kwanza aliyomwandikia Timotheo. Mwanamume huyo alikuwa amekwisha kutengwa na ushirika wa kundi la Kikristo, pamoja na Aleksanda fulani, kwa sababu walikuwa ‘wameangamia kwa habari ya Imani yao.’ Paulo alimshauri Timotheo aendelee ‘kupiga vile vita vizuri’ juu ya waasi-imani hao.​—1 Timotheo 1:18-20.

Mitume walipokuwa wangali hai, waliweka mfano mzuri wa kupambana na uasi-imani. Lakini mara walipokuwa hawapo wawe ‘kizuizi,’ mambo aliyoogopa Paulo yalitokea, na lile “neno” la waasi-imani‘lilienea kama donda-ndugu.​—2 Wathesalonike 2:3-12; Matendo 20:29, 30.

Mawazo ya ufufuo wa mfano kabisa, kama yale waliyofundisha Himenayo na Fileto katika Efeso, yalisitawishwa baadaye na waginosi (wajuzi). Wakati wa karne ya pili na mapema karne ya tatu W.K., Waginosi (Kutoka neno la Kigiriki gnoʹsis , “maarifa”) waliunganisha Ukristo ulioasi imani pamoja na falsafa ya Kigiriki na mafumbo ya nchi za Mashariki. Walidai kwamba vitu vyote ni viovu na wakakazia kwamba wokovu ulikuja kupitia “maarifa” ya mafumbo (gnoʹsis) wala si kupitia imani kwa Kristo akiwa mkombozi.

Walakini Uginosi haukuwa namna pekee ya uasi-imani ‘ulioenea kama donda-ndugu.’ Kufikia karne ya nne Ukristo wa kweli uliofundishwa na Kristo na mitume na wanafunzi wake waaminifu ulikuwa umechafuliwa na watu wengine waliokuwa “wamepotoka wakaiacha imani.” Kitabu cha usomi New International Dictionary of New Testament Theology kinakubali kwamba wakati wa “historia iliyoendelea ya kanisa mawazo mengi yasiyo ya kibiblia, picha na mafikira yalitiwa ndani ya wazo la paradiso.” Kamusi hiyo ya Biblia inaendelea kusema juu ya “uhakika wa kwamba fundisho la kidini la kutokufa kwa nafsi lilikuja kuchukua nafasi ya somo la A[gano] J[ipya] la mambo ambayo yameandikwa yatawapata wanadamu na ulimwengu hatimaye pamoja na tumaini la ufufuo wa wafu.”

Kama tulivyokwisha kuona hapo juu na katika makala iliyotangulia, kukana ukweli wa kifo na kukubali wazo la kipagani la kuendelea kuishi kwa nafsi isiyokufa kulifanya makanisa ya Katoliki na Orthodoksi yatoke mbali zaidi na zaidi na mafundisho yaliyo wazi ya Biblia juu ya ufufuo na hukumu. Kulitokeza wazo lisilo na msingi linalomvunjia Mungu heshima la moto wa mateso na purgatori (matohara) na wazo la kipumbavu la miili yenye nyama kufufuliwa ielee huku na huku mbinguni au iteswe milele na milele katika moto wa mateso.

“Donda-ndugu” hilo halikukomea hapo. Katika karne za baadaye waleta mabadiliko ya kidini Waprotestanti waliongeza mawazo yao wenyewe yasiyo ya Kibiblia juu ya kifo, ufufuo na hukumu ya mwisho. Kwa sehemu kubwa, walifuata wazo lisilo na msingi la Katoliki juu ya kuzaliwa pamoja na nafsi isiyokufa, ambalo liliwataka pia wakubali fundisho la kidini la “ufufuo wa mwili.” Makanisa mengi ya Protestanti yanafundisha juu ya moto wa mateso pia. Walakini watheologia (wasomi wa elimu ya kidini) Waprotestanti wamethibitisha uwezo wao wa kuvumbua mambo pia kwa kujitungia mafundisho mengine ya kidini yasiyofundishwa ndani ya Biblia. Kwa mfano, makanisa mengine ya Wakalvini Yaliyofanya Mabadiliko ya Kidini, yanafundisha kwamba Mungu anatangulia kuandikia nafsi fulani wokovu na nyingine laana ya milele. Waprotestanti wengine wanaamini juu ya wokovu wa ulimwengu wote, yaani, kuokolewa hatimaye kwa nafsi zote, hata zile za waovu.

Kushikamana na Kweli ya Biblia

Baada ya kuonya juu ya uasi-imani wa Himenayo na Fileto, Paulo aliongeza hivi kuhusu ufufuo: “Kwa sababu hiyo, msingi imara wa Mungu unaendelea kusimama, ukiwa na muhuri huu: ‘Yehova anawajua wale walio wake.’”​—2 Timotheo 2:19 NW.

Ukiwa umerudia historia ya usitawi wa mawazo ya uasi-imani kuhusu nafsi, kifo, ufufuo na hukumu ya mwisho, na ukiwa umekwisha kuona mvurugo wa imani za siku hizi juu ya mambo hayo ya maana sana, utafanya nini? Mkristo mwenye moyo mweupe atakuwa na hakika zaidi ya wakati mwingine juu ya uhitaji wa kushikamana na “msingi imara wa Mungu” juu ya mambo hayo, kama ilivyoandikwa katika Neno Lake, Biblia.

Hata hivyo, ingawa wanakubali fundisho lililo wazi la Biblia juu ya nafsi ya kibinadamu, kifo na ufufuo, kwa sababu ya maono ya kimoyoni huenda Wakristo fulani wakawa na mawazo juu ya hukumu ya mwisho ambayo yanaonekana yanatukuza fadhili za upendo za Yehova lakini ambayo, kwa kweli, yanatia mashaka juu ya haki yake ya hukumu na haki yake ya kuwaharibu waovu. Kwa kusudi la kujibu maulizo hayo, makala zinazofuata zitachunguza yale ambayo Biblia inasema juu ya tumaini la kweli juu ya ufufuo kama linavyohusiana na ufalme wa Mungu na siku ya hukumu ya Mungu. Tunakualika uendelee kusoma.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Yale Ambayo Biblia Inasema Juu ya Nafsi, Kifo, Ufufuo na Hukumu ya Mwisho

Mwanadamu hana nafsi; yeye NI nafsi.​—1 Wakorintho 15:45.

Nafsi, au mtu mzima, anakufa.​—Ezekieli 18:4, NW; ZSB.

Kifo ni adui, wala si rafiki.​—1 Wakorintho 15:26.

Uzima baada ya kifo unaweza kuja tu kupitia ufufuo.​—Yohana 5:28, 29.

Thawabu ya uaminifu ni uzima wa milele.​—Yohana 10:27, 28.

Hukumu ya dhambi ya kukusudia ni kifo cha milele, wala si mateso ya milele.​—Warumi 6:23.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

Fundisho Rasmi la Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo

Imani ya Athanasia, inayokubaliwa rasmi na Katoliki ya Roma, Anglikana na makanisa mengine ya protestanti, inasema hivi: “Yeye [Yesu] alipaa kwenda mbinguni, yeye anaketi kwenye mkono wa kuume wa Baba, Mungu Mwenyezi. Kutoka hapo yeye atakuja kuwahukumu walio hai na wafu. Katika kuja kwake watu wote watafufuka tena pamoja na miili yao, na watatoa jibu kwa ajili ya kazi zao wenyewe. Nao ambao wamefanya mema watakwenda kwenye uzima wa milele, nao ambao wamefanya maovu kwenye moto wa milele.”

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

Maoni ya Kanisa Juu ya Ufufuo

“Hakuna sababu zinazoweza kuthibitisha kufufuliwa kwa watu wote, ingawa tunaweza kuonyesha namna kunavyofaa. (a) Kwa sababu kiasili nafsi inapatana na mwili, kutenganishwa kwayo milele kutoka kwa mwili kunaonekana si jambo la asili. (b) Kwa kuwa mwili unashiriki uhalifu wa nafsi, na ni mwenzi katika maadili yake, haki ya hukumu ya Mungu inaonekana kuwa inautaka mwili uwe mshiriki wa adhabu na thawabu ya nafsi. (c) Kwa sababu kiasili nafsi ikitenganishwa na mwili inakuwa haijakamilika, kukamilika kwa furaha yake, ijawe kila wema, kunaonekana kuwa kunautaka mwili ufufuliwe.”​—Catholic Encyelopedia (Sisi tumetia mkazo).

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki