Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Watoto wa Shule wa Naijeria Wabarikiwa kwa Ajili ya Uaminifu
Mtume Paulo aliandika hivi: “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.” (Warumi 12:18) Watoto wa shule wa Mashahidi wa Yehova katika Naijeria hutumia shauri hilo, hata wanaponyanyaswa. Tokeo ni, Yehova huwabariki.
◻ Mwalimu mmoja aliwachukia Mashahidi wa Yehova sana. Katika kusanyiko moja la asubuhi, aliwaita Mashahidi wote mbele na kuwaamuru waimbe wimbo wa taifa. Walikataa, wakitaarifu kwamba walitaka kumtolea Mungu ibada ya pekee. Kisha mwalimu akawatoa wote nje na kuwaambia wakate nyasi. Wakati ule ule, wanafunzi wale wengine waliendelea na masomo yao.
Shahidi mmoja mwenye umri mkubwa alimpelekea mwalimu huyo ile broshua Shule na Mashahidi wa Yehova, akieleza msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutokuwamo. Hata hivyo, mwalimu huyo alikataa kuzungumza juu ya jambo hilo wala kukubali broshua hiyo. Kwa kweli, aliizidisha adhabu ya watoto hao mara hiyo hiyo.
Mashahidi hao wachanga waliendelea kuvumilia adhabu hiyo na kuendelea kukata nyasi hata wakati mwalimu huyo hakuwako. Siku moja mwalimu huyo alijificha na kuwachungulia bila kuonekana walipokuwa wakiendelea kufanya kazi na kuimba nyimbo za Ufalme. Alivutiwa sana hivi kwamba aliwarudisha darasani, akionyesha mshangao juu ya mwelekeo wao. Tokeo likawa nini? Sasa mwalimu huyo anajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova!
Kwa wazi watoto hao wa shule walibarikiwa kwa ajili ya uaminifu wao kwa Yehova na kanuni zake.—Mithali 10:22.
◻ Ruth na marafiki wake walibarikiwa pia kwa ajili ya uaminifu wao kwa lile takwa la Yehova la ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 17:16, NW) Ruth, aliye na miaka 18, alianza kupainia alipokuwa na umri wa miaka 12. Yeye na Mashahidi wengine walipata upinzani kutoka kwa baadhi ya walimu wa shule kwa sababu ya kukataa kuimba wimbo wa taifa. Mwalimu mmoja aliomba kuwaona wazazi wa wasichana hao. Baada ya wao kutoa elezo, kwa kutumia ile broshua Shule, mwalimu huyo alitosheka na akaacha kuwasumbua wanafunzi hao.
Hata hivyo, siku moja, mwalimu mmoja kutoka India alimtukana na kumwadhibu mmoja wa wasichana hao mbele ya darasa alipokataa kuimba wimbo wa taifa. Msichana huyo alitetea imani yake kwa ujasiri na mwalimu huyo akampeleka ili amwone mwalimu mkuu wa shule. Walipofika kwake, Shahidi huyo mchanga alipata kwamba makamu wa mwalimu mkuu alikuwapo pia. Kwa mshangao wake, mwalimu mkuu na makamu wake walianza kucheka. Akimgeukia mwalimu huyo, mwalimu mkuu akasema hivi: “Bibi, usijihangaishe juu ya wasichana hawa. Hata ukiwaua, wangependelea kufa kuliko kuimba wimbo wa taifa. Je! hujapata kusikia juu yao?” Kisha yeye na makamu wake wakasema juu ya imani na moyo mkuu wa Mashahidi wa Yehova. Akisema na msichana huyo, mwalimu mkuu alisema kwamba alisikitika kwa ajili ya aibu ambayo msichana huyo alipata. Halafu akaongeza hivi: “Endelea na vitendo vyako vya imani. Ninavutiwa na dini yenu na msimamo wenu wenye ujasiri mkiwa nje na ndani ya shule pia.” Baadaye, yule mwalimu aliyekuwa amepinga alimwomba Shahidi huyo radhi, akisema kwamba sasa anaelewa ule msimamo wa kutokuwamo unaochukuliwa na Mashahidi.
Watoto hao walifuata mfano wa wale Waebrania watatu ambao wasingeweza kuvunja uaminifu wao wa kimaadili kwa Mungu kwa kuinamia mfano, na wa Danieli pia, aliyekataa kuacha kusali kwa Yehova. Wanaume hao walibarikiwa na Yehova kwa sababu walikuwa waaminifu kwa sheria za Mungu zenye uadilifu.—Danieli, sura ya 3 na ya 6.