Tumia kwa Hekima Uhuru Wako wa Kikristo
“[Iweni] kama [watu] huru, ila wasioutumia uhuru huo kwa kusitiri ubaya, bali kama watumwa wa Mungu.”—1 PETRO 2:16.
1. Adamu alipoteza uhuru gani, na Yehova atarudisha ainabinadamu kwenye uhuru gani?
WAZAZI wetu wa kwanza walipotenda dhambi katika shamba la Edeni, waliwapotezea watoto wao urithi mtukufu—uhuru bila dhambi na uharibifu. Tokeo likawa kwamba, sisi sote tulizaliwa kuwa watumwa wa uharibifu na kifo. Lakini, kwa furaha, Yehova akusudia kurudisha wanadamu waaminifu kwenye uhuru mzuri ajabu. Leo, wale wenye mioyo inayofaa hungojea kwa hamu “kufunuliwa kwa wana wa Mungu,” tokeo la hilo likiwa kwamba ‘watawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata waingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.’—Warumi 8:19-21.
‘Kupakwa Mafuta Ili Kuhubiri’
2, 3. (a) “Wana wa Mungu” ni nani? (b) Wao huonea shangwe msimamo gani mzuri ajabu, huo ukileta daraka gani?
2 Hao “wana wa Mungu” ni akina nani? Wao ni ndugu wa Yesu wapakwa-mafuta kwa roho watakaotawala pamoja naye katika ule Ufalme wa kimbingu. Wa kwanza kati ya hao walitokea katika karne ya kwanza W.K. Walikubali ile kweli inayoweka huru ambayo Yesu alifundisha, na kutoka Pentekoste 33 W.K., walishiriki yale mapendeleo matukufu ambayo Petro alisema juu yayo alipowaandikia: “Ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu.”—1 Petro 2:9a; Yohana 8:32.
3 Kuwa watu wa pekee wa Mungu—hiyo ni baraka nzuri ajabu kweli kweli! Na mabaki wa ki-siku-hizi wa wale wana wa Mungu wapakwa-mafuta huonea shangwe msimamo huo huo wenye baraka pamoja na Mungu. Lakini pamoja na pendeleo hilo zuri ajabu kuna madaraka fulani. Petro alielekeza fikira kwa mojawapo madaraka hayo alipoendelea kusema hivi: “Mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu.”—1 Petro 2:9b.
4. Wakristo wapakwa-mafuta wametimizaje lile daraka linalotokana na uhuru wao wa Kikristo?
4 Je! Wakristo wapakwa-mafuta wametimiza daraka hilo la kutangaza kotekote utukufu za Mungu? Ndiyo. Akisema kiunabii juu ya wapakwa-mafuta tangu 1919, Isaya alisema hivi: “Roho ya Bwana MUNGU [Yehova, NW] i juu yangu; kwa sababu BWANA [Yehova, NW] amenitia mafuta, niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao. Kutangaza mwaka wa BWANA [Yehova, NW] uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu.” (Isaya 61:1, 2) Leo, mabaki wapakwa-mafuta, wakifuata mfano wa Yesu, ambaye andiko hilo hutumika kwake hasa, hutangazia wengine kwa bidii habari njema za uhuru.—Mathayo 4:23-25; Luka 4:14-21.
5, 6. (a) Tokeo la kuhubiri kwa bidii kwa Wakristo wapakwa-mafuta limekuwa nini? (b) Wale wa mkutano mkubwa huonea shangwe mapendeleo na madaraka gani?
5 Likiwa tokeo la kuhubiri kwao kwa uchangamfu, mkutano mkubwa wa kondoo wengine umetokea kwenye mandhari ya ulimwengu katika siku hizi za mwisho-mwisho. Wametoka kwa mataifa yote ili kujiunga na wapakwa-mafuta katika kumtumikia Yehova, na kweli imewaweka huru hao pia. (Zekaria 8:23; Yohana 10:16) Kama Abrahamu wao hutangazwa rasmi kuwa waadilifu kwa msingi wa imani nao wameingia katika uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu. Na kama Rahabu kutangazwa kwao rasmi kuwa waadilifu huwaweka katika mstari wa kupata wokovu—kwa habari yao, huo ni wokovu wa Har–Magedoni. (Yakobo 2:23-25; Ufunuo 16:14-16) Lakini mapendeleo hayo mazuri ajabu pia huleta lile daraka la kuambia wengine juu ya utukufu wa Mungu. Hiyo ndiyo sababu kwa nini Yohana aliwaona wakimsifu Yehova peupe, “wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 7:9, 10, 14.
6 Mwaka jana ule mkutano mkubwa, sasa wakihesabika kuwa zaidi ya milioni nne, pamoja na kile kikundi kidogo kinachobaki cha Wakristo wapakwa-mafuta, walitumia karibu saa bilioni moja wakitangaza kotekote utukufu wa Yehova. Hakika huo ulikuwa utumizi bora zaidi wa uhuru wao wa kiroho.
“Mpeni Heshima Mfalme”
7, 8. Uhuru wa Kikristo huleta daraka gani kuelekea mamlaka za kilimwengu, na kwa habari hiyo, ni lazima tuepuke mtazamo gani mbaya?
7 Uhuru wetu wa Kikristo huleta madaraka mengine. Petro alielekezea baadhi yayo alipoandika hivi: “Waheshimuni watu wote. Wapendeni ndugu. Mcheni Mungu. Mpeni heshima mfalme.” (1 Petro 2:17) Ni nini kinachodokezwa kwa yale maneno “mpeni heshima mfalme?”
8 “Mfalme” huwakilisha watawala wa kilimwengu. Leo, roho ya kutoheshimu mamlaka imeongezeka ulimwenguni, nayo yaweza kuathiri Wakristo kwa urahisi. Mkristo huenda akataka kujua kwa nini apaswa kumheshimu “mfalme,” kwa kuwa “dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Kwa sababu ya maneno hayo, huenda akahisi kuwa huru kutotii sheria ambazo hazimfai kushika na kutolipa kodi ikiwa angeweza kuepa. Lakini hilo lingekuwa kinyume cha ile kanuni ya mwongozo ya Yesu ya ‘kulipa Kaisari yaliyo ya Kaisari.’ Kwa kweli, hiyo ingekuwa ‘kutumia uhuru wake kwa kusitiri ubaya.’—Mathayo 22:21; 1 Petro 2:16.
9. Ni nini sababu mbili nzuri za kuwa watiifu kwa mamlaka za kilimwengu?
9 Wakristo wana wajibu wa kuheshimu mamlaka na kujitiisha kwayo—hata ikiwa hiyo ni kwa njia ya kadiri. (Matendo 5:29) Kwa nini? Kwenye 1 Petro 2:14, 15, Petro aonyesha sababu tatu anaposema kwamba magavana ‘wanatumwa na Mungu ili kwalipiza kisasi watenda mabaya na kuwasifu watenda mema.’ Kuogopa kuadhibiwa ni sababu ya kutosha ya kutii mamlaka. Ingekuwa aibu iliyoje kwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kutozwa faini au kufungwa gerezani kwa ajili ya kushambulia mtu, kuiba, au kwa tendo jingine la uhalifu! Wazia jinsi wengine wangefurahia kutangaza peupe jambo kama hilo! Kwa upande ule mwingine, tusitawishapo sifa bora sana kwa ajili ya utii wa sheria, tunapokea pongezi kutoka kwa watawala wenye haki. Huenda tukapewa uhuru mwingi zaidi kufanya kazi yetu ya kuhubiri habari njema. Zaidi ya hayo, ‘kwa kutenda mema tunaziba vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu.’ (1 Petro 2:15b) Hiyo ni sababu ya pili ya kutii mamlaka.—Warumi 13:3.
10. Ni nini sababu yenye nguvu zaidi ya kutii mamlaka za kilimwengu?
10 Lakini kuna sababu yenye nguvu zaidi. Wenye mamlaka wako kwa ruhusa ya Yehova. Kama Petro asemavyo, watawala wa kisiasa ‘wanatumwa na’ Yehova, na ni “mapenzi ya Mungu” kwamba Wakristo waendelee kujitiisha kwayo. (1 Petro 2:15a) Vivyo hivyo, mtume Paulo asema hivi: “[Mamlaka] ile iliyopo imeamriwa na Mungu.” Kwa hiyo, dhamiri yetu yenye kuzoezwa kwa Biblia hutusukuma kuwatii wenye mamlaka. Tukikataa kujitiisha kwao, ‘tumeshindana na agizo la Mungu.’ (Warumi 13:1, 2, 5) Ni nani miongoni mwetu ambaye angekuwa na nia ya kushindana na agizo la Mungu? Ungekuwa utumizi mbaya kama nini wa uhuru wa Kikristo!
‘Mwe na Upendo kwa Ajili ya Ndugu’
11, 12. (a) Ni daraka jipi kuelekea waamini wenzetu linalotokana na uhuru wetu wa Kikristo? (b) Ni nani hasa wanaostahili upendo wetu wenye ufikirio, na kwa nini?
11 Petro alisema pia kwamba Mkristo apaswa ‘aupende ushirika mzima wa ndugu.’ (1 Petro 2:17, NW) Hilo ni daraka jingine linaloletwa na uhuru wa Kikristo. Wengi wetu ni washiriki wa kundi. Kwa kweli, sisi sote ni sehemu ya ushirika, au tengenezo la kimataifa, la ndugu. Kuwaonyesha hao upendo ni utumizi wenye hekima wa uhuru wetu.—Yohana 15:12, 13.
12 Mtume Paulo alikazia kikundi kimoja cha Wakristo ambacho hasa hustahili upendo wetu. Alisema hivi: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.” (Waebrania 13:17) Wale wanaoongoza katika kundi ni wazee. Ni kweli, wanaume hao si wakamilifu. Ijapokuwa hivyo, wao huwekwa rasmi chini ya uangalizi wa Baraza Linaloongoza. Wao huongoza kwa mfano wao na kwa ufikirio, nao hupewa mgawo wa kukesha kwa ajili ya nafsi zetu. Huo ni mgawo mzito kama nini! (Waebrania 13:7) Kwa furaha, makundi yaliyo mengi yana roho nzuri, ya ushirikiano, na wazee huwa na shangwe kufanya kazi pamoja nayo. Inakuwa vigumu zaidi wakati watu mmoja mmoja hawataki kushirikiana. Bado mzee hufanya kazi yake, lakini kama alivyosema Paulo, yeye huifanya kwa “kuugua.” Kwa hakika, hatutaki kuwafanya wazee waugue! Twataka wapate shangwe katika kazi yao ili waweze kutujenga.
13. Ni baadhi ya njia zipi ambazo katika hizo twaweza kushirikiana na wazee?
13 Ni baadhi ya njia zipi ambazo katika hizo twaweza kushirikiana na wazee? Moja ni kwa kusaidia na utunzaji na usafishaji wa Jumba la Ufalme. Nyingine ni kwa kushirikiana katika kazi ya kutembelea wagonjwa na kuwasaidia wasiojiweza. Kuongezea hayo, twaweza kujitahidi kubaki tukiwa wenye nguvu kiroho, ili tusiwe mzigo. Eneo moja la maana la ushirikiano ni kwa kudumisha usafi wa kundi wa kiadili na wa kiroho, kwa mwenendo wetu na pia kwa kuripoti visa vya dhambi nzito ambavyo tumepata kujua.
14. Twapaswa kushirikianaje na hatua ya kinidhamu inayochukuliwa na wazee?
14 Nyakati nyingine, ili kudumisha kundi likiwa safi, wazee wanahitaji kutenga na ushirika mkosaji asiyetubu. (1 Wakorintho 5:1-5) Hilo hulinda kundi. Huenda pia likamsaidia mkosaji. Mara nyingi, nidhamu kama hiyo imesaidia kumrudisha mtenda dhambi kwenye fahamu zake. Lakini, iweje, ikiwa aliyetengwa ni rafiki wa karibu au mtu wa ukoo? Tuseme mtu huyo ni baba au mama yetu, au mwana au binti yetu. Je! bado tunaiheshimu hatua iliyochukuliwa na wazee? Ni kweli, hilo laweza kuwa jambo gumu. Lakini ungekuwa utumizi mbaya kama nini wa uhuru wetu kutilia shaka uamuzi wa wazee na kuendelea kuwa na ushirika wa kiroho pamoja na mtu ambaye amethibitika kuwa uvutano wenye kufisidi katika kundi! (2 Yohana 10, 11) Watu wa Yehova kwa ujumla wapaswa kupongezwa kwa sababu ya njia ambayo wao hushirikia-na katika mambo hayo. Tokeo ni kwamba, tengenezo la Yehova hutunzwa likiwa safi katika ulimwengu huu mchafu.—Yakobo 1:27.
15. Mtu akitenda dhambi nzito, yeye apaswa kufanya nini mara moja?
15 Namna gani ikiwa sisi twatenda dhambi nzito? Mfalme Daudi alieleza juu ya wale ambao Yehova hupendelea aliposema hivi: “Ni nani atakayepanda katika mlima wa BWANA [Yehova, NW]? Ni nani akayesimama katika patakatifu pake? Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili.” (Zaburi 24:3, 4) Ikiwa kwa sababu fulani sisi si ‘safi tena katika mikono au mioyo yetu,’ ni lazima tutende kwa haraka. Uhai wetu wa milele umo hatarini.
16, 17. Ni kwa nini mtu aliye na hatia ya dhambi nzito hapaswi kujaribu kusuluhisha jambo hilo peke yake?
16 Wengine wameshawishwa kuficha dhambi nzito, labda wakitoa sababu hii: ‘Nimeungama kwa Yehova na kutubu. Kwa hiyo kwa nini kuwahusisha wazee?’ Huenda mkosaji akawa na aibu au akaogopa lile ambalo wazee huenda wakafanya. Hata hivyo, apaswa kukumbuka kwamba ingawa Yehova peke yake ndiye aweza kutusafisha dhambi, Yeye amewapa wazee hasa daraka la usafi wa kundi. (Zaburi 51:2) Wako kwa ajili ya kuponya, kwa ajili ya “kuwarekebisha watakatifu.” (Waefeso 4:12, NW) Kutokuwaendea tunapohitaji msaada wa kiroho ni sawa na kutomwendea daktari tunapokuwa wagonjwa.
17 Wengine ambao hujaribu kushughulikia mambo peke yao hupata kwamba miezi au miaka kadhaa baadaye, dhamiri yao ingali ikiwasumbua sana. Kwa ubaya zaidi, wengine ambao huficha kosa zito hutumbukia katika dhambi kwa mara ya pili na hata ya tatu. Jambo hilo linapopata kujulikana na wazee, inakuwa kisa cha ukosaji wenye kurudiwa-rudiwa. Ni afadhali kama nini kufuata shauri la Yakobo! Aliandika hivi: “Je! kuna mtu yeyote mgonjwa miongoni mwenu? Mwacheni awaite wanaume wazee wa kundi waje kwake, na kuwaacha wamwombee, wampake mafuta kwa jina la Yehova.” (Yakobo 5:14, NW) Waendee wazee ungali wakati wa kuponya. Tukingojea muda mrefu mno, huenda tukawa wagumu katika mwendo wa dhambi.—Mhubiri 3:3; Isaya 32:1, 2.
Sura na Tafrija
18, 19. Ni kwa nini padri mmoja alisema juu ya Mashahidi wa Yehova kwa upendeleo?
18 Miaka mitano iliyopita, katika gazeti la parishi, padri Mkatoliki katika Italia alisema kwa uchangamfu juu ya Mashahidi wa Yehova.a Alisema hivi: “Mimi binafsi, nawapenda Mashahidi wa Yehova; nakiri hivyo kwa unyofu. . . . Wale ninaojua ni wenye adabu isiyoweza kushutumiwa, husema kwa wororo . . . [na] ni wenye kushawishi sana kwa maneno. Sisi tutaelewa lini kwamba ukweli wataka kutolewa kwa njia yenye kukubalika? Kwamba wale watangazao ukweli hawapaswi kuwa bila shauku, wenye kunuka vibaya, wasio nadhifu, wenye kuvalia ovyoovyo?
19 Kulingana na maneno hayo, padri huyo alikuwa amevutiwa, miongoni mwa mambo mengine, na ile njia ambayo Mashahidi huvalia na kujitokeza mbele ya watu. Ni wazi, wale alioonana nao walikuwa wamesikiliza lile shauri lililotolewa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” kwa miaka iliyopita. (Mathayo 24:45) Biblia husema kwamba mavazi ya wanawake yapaswa kuwa ‘ya kujisitiri na ya adabu nzuri.’ (1 Timotheo 2:9) Katika wakati huu wenye maadili yaliyoharibika, shauri hilo lawafaa wanaume pia. Je! si jambo lenye kupatana na akili kwamba wawakilishi wa Ufalme wa Mungu wapaswa wajitokeze mbele ya watu wa nje kwa adabu nzuri?
20. Ni kwa nini Mkristo apaswa kuwa mwangalifu juu ya mavazi yake nyakati zote?
20 Huenda wengine wakakubali kwamba kwenye mikutano na katika utumishi wa shambani, wapaswa kuwa waangalifu juu ya jinsi wanavyovaa, lakini huenda pia wakahisi kwamba kanuni za Biblia hazitumiki kwa nyakati nyinginezo. Lakini je, tunaacha kuwa wawakilishi wa Ufalme wa Mungu wakati wowote? Ni kweli, hali huwa tofauti. Ikiwa tunasaidia katika ujenzi wa Jumba la Ufalme, tutavalia tofauti na wakati tunapohudhuria mkutano katika Jumba la Ufalme hilo hilo. Katika wakati wetu wa starehe, huenda tukavalia mavazi ya ustarehe zaidi. Lakini mavazi yetu yapasa sikuzote yawe yenye kusitiri na ya adabu nzuri, wakati wowote tutazamwapo na wengine.
21, 22. Tumelindwaje dhidi ya tafrija zenye kudhuru, na twapaswa kuonaje shauri juu ya mambo kama hayo?
21 Eneo jingine ambalo limeelekezewa fikira ni lile jambo la tafrija. Binadamu—hasa vijana—huhitaji tafrija. Si dhambi wala si kupoteza wakati kuratibu tafrija kwa ajili ya familia. Hata Yesu alialika wanafunzi wake ‘wapumzike kidogo.’ (Marko 6:31) Lakini uwe mwangalifu kwamba tafrija haiupi nafasi uchafu wa kiroho. Tunaishi katika ulimwengu ambamo tafrija hukazia ukosefu wa adili kingono, jeuri mbaya sana, mambo yenye kuogofya, au uwasiliano na roho waovu. (2 Timotheo 3:3; Ufunuo 22:15) Mtumwa mwaminifu mwenye akili huwa chonjo kuona hatari za jinsi hiyo na hutuonya daima juu yayo. Je! wewe wahisi kwamba vikumbusha hivyo ni kuingilia uhuru wako? Au wewe washukuru kwamba tengenezo la Yehova linajali vya kutosha juu yako kuvuta fikira zako daima kwenye hatari hizo?—Zaburi 19:7; 119:95.
22 Usisahau kamwe kwamba ingawa uhuru wetu hutoka kwa Yehova, sisi tuna daraka juu ya jinsi tunavyoutumia. Tukipuuza shauri zuri na kufanya maamuzi mabaya, hatuwezi kumlaumu mtu mwingine. Mtume Paulo asema hivi: “Kila mtu . . . atatoa habari [hesabu, NW] zake mwenyewe mbele za Mungu.”—Warumi 14:12; Waebrania 4:13.
Tazamia kwa Hamu Uhuru wa Watoto wa Mungu
23. (a) Ni baraka zipi zinazohusika na uhuru tunazoonea shangwe sasa? (b) Sisi tunatazamia baraka zipi kwa hamu?
23 Kweli kweli sisi ni watu waliobarikiwa. Sisi tuko huru na dini bandia na ushirikina. Kwa sababu ya dhabihu ya fidia, twaweza kumkaribia Yehova tukiwa na dhamiri safi, tukiwa huru katika njia ya kiroho bila utumwa kwa dhambi na kifo. Na hivi karibuni kutakuja kule “kufunuliwa kwa wana wa Mungu.” Kwenye Har–Magedoni, ndugu wa Yesu katika utukufu wao wa kimbingu watafunuliwa kwa wanadamu kuwa waharabu wa adui za Yehova. (Warumi 8:19; 2 Wathesalonike 1:6-8; Ufunuo 2:26, 27) Baadaye, wana hao wa Mungu watafunuliwa kuwa mifereji ya baraka zinazotiririka kutoka kwa kiti cha ufalme cha Mungu hadi kwa ainabinadamu. (Ufunuo 22:1-5) Hatimaye, kufunuliwa huko kwa wana wa Mungu kutakuwa na tokeo la kubariki ainabinadamu jaminifu na uhuru mtukufu wa watoto wa Mungu. Je! wewe unatazamia wakati huo kwa hamu? Basi tumia uhuru wako wa Kikristo kwa hekima. Mtumikie Mungu sasa, nawe utaonea shangwe uhuru huo mzuri ajabu kwa umilele wote!
[Maelezo ya Chini]
a Baadaye padri huyo alitangua pongezi hiyo, yaelekea akiwa chini ya mbano.
Sanduku la Kurudia
◻ Wapakwa-mafuta na kondoo wengine wamemtukuzaje Yehova?
◻ Ni kwa nini Wakristo wapaswa kuheshimu mamlaka za kilimwengu?
◻ Mkristo aweza kushirikiana na wazee katika njia zipi?
◻ Kuhusu mavazi, ni kwa nini Mashahidi wa Yehova hutokeza kuwa tofauti na wengi ulimwenguni?
◻ Twapaswa kuepuka nini kwa habari ya tafrija?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Wazee hasa hustahili upendo na ushirikiano wetu
[Picha katika ukurasa wa 18]
Mavazi ya Mkristo yapasa kuwa yenye kusitiri, na ya adabu nzuri, na yenye kufaa hali