Nilijinyenyekeza Mwenyewe Nikapata Furaha
KATIKA 1970, nilikuwa na miaka 23 nami nilitamani makuu. Mahali nilipoajiriwa kazi kwenye kilabu ya magari katika Ivrae, Italia, nilifanywa karani mkuu. Nilipiga moyo konde kuwa mtu mashuhuri. Na hata hivyo nilishuka moyo sana nikawa mwenye huzuni. Kwa nini?
Mume wangu alitumia wakati wake mwingi katika mabaa akicheza karata pamoja na marafiki wake, naye aliniacha mimi nishughulikie madaraka mengi ya familia. Uhusiano wetu ulidhoofika. Tuligombana juu ya mambo madogo-madogo sana. Tokeo likawa kwamba, akili yangu ilijawa na fikira hasi (mbaya).
‘Hakuna mtu apendezwaye na wewe kwa kweli,’ nilikuwa nikisema. ‘Wanataka tu kujifaidi wenyewe kwa cheo chako.’ Nilikuwa nikijiambia mwenyewe: ‘Mungu hawezi kuwako kwa sababu ikiwa angekuwako, asingeruhusu kuteseka na uovu mwingi kadiri hii. Uhai si kitu ila shindano la mbio kuelekea kifo.’ Sikuweza kuelewa kwa nini ilikuwa hivyo.
Mwanzo wa Badiliko
Siku moja katika 1977, Mashahidi wa Yehova wawili walibisha mlangoni petu. Mume wangu, Giancarlo, aliwaalika ndani, wakaingia sebuleni ili kuongea. Kusudi lake lilikuwa kuwafanya wawe waamini wa mageuzi kama yeye, lakini ni wao waliobadili kufikiri kwake.
Upesi Giancarlo akaanza pia kufanya mabadiliko maishani mwake. Akawa mwenye saburi zaidi, akinitolea mimi na binti yetu wakati na uangalifu mwingi zaidi. Alijaribu kuniambia juu ya mambo aliyokuwa akijifunza, lakini nilikuwa nikimaliza mazungumzo hayo kwa maneno makali.
Halafu siku moja Mashahidi hao walipotembelea, niliketi nikasikiliza kweli kweli. Walisema juu ya mwisho wa mfumo huu wa mambo na juu ya Ufalme wa Mungu, dunia-Paradiso, na ufufuo wa wafu. Nilipumbaa! Sikulala usingizi kwa masiku matatu yaliyofuata! Nilitaka kujua zaidi, lakini kiburi kilinizuia nisimwulize mume wangu maswali. Kisha, siku moja aliniambia hivi kwa ukali: “Leo utasikiliza. Mimi nina majibu kwa maswali yako yote.” Kisha akanitolea kweli nyingi za Biblia.
Giancarlo aliniambia kwamba Yehova ndilo jina la Muumba, kwamba sifa yake kuu ni upendo, kwamba Yeye alimtuma Mwana Wake kuwa fidia ili tuweze kuwa na uhai wa milele, na kwamba baada ya uharibifu wa waovu kwenye Har–Magedoni, Yesu Kristo atawafufua wafu wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu. Alisema kwamba wale waliofufuliwa wangekua kufikia ukamilifu wa kiakili na wa kimwili na kwamba wangekuwa na nafasi ya kuishi milele duniani katika Paradiso.
Siku iliyofuata, niliandamana pamoja na mume wangu kwenye Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza. Baadaye nilimwambia hivi: “Watu hawa wanapendana. Ninataka kuendelea kuja hapa kwa sababu wana furaha kweli kweli.” Nilianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, na funzo la Biblia likaanza kuongozwa pamoja na mimi. Nilifikiria sana niliyokuwa nikijifunza na upesi nikasadiki kwamba nilikuwa nimewapata watu wa Mungu wa kweli. Katika 1979 mume wangu na mimi tulionyesha wakfu wetu kwa Yehova kwa kubatizwa.
Utumishi wa Wakati Wote
Kwenye kusanyiko la mzunguko baadaye mwaka huo, hotuba ilitolewa iliyotia moyo utendaji wa kuhubiri wa wakati wote. Nilihisi nimechochewa kuianza utumishi huo, nami nikamwendea Yehova katika sala kuhusu jambo hilo. Lakini nikawa mja mzito, na mipango yangu yakakatizwa. Katika miaka minne iliyofuata, nilipata watoto watatu. Wawili kati yao, katika pindi tofauti, walipata kasoro fulani za kimwili zenye kutisha uhai. Kwa furaha, katika kila kisa, walipona kikamili.
Sasa nilihisi kwamba nsingeweza kuahirisha kwa muda mrefu zaidi mipango yangu kwa ajili ya utumishi wa wakati wote. Niliacha kazi yangu ya kimwili ili nikazie fikira vema zaidi kwenye madaraka yangu nikiwa mke na mama. Mume wangu na mimi tulifanya mipango kuishi kwa kutumia mshahara mmoja, lililomaanisha kuacha mambo yote yasiyohitajiwa. Hata hivyo, Yehova alitubariki sana, asituacha kamwe tuwe masikini au wenye uhitaji.
Katika 1984 binti yangu, aliyekuwa mwenye miaka 15 wakati huo na ambaye alikuwa amebatizwa karibuni, alianza utumishi wa wakati wote akiwa painia. Wakati huo huo, mume wangu akawekwa rasmi kuwa mzee. Na mimi? Nikihisi siwezi kuwa painia bado, niliweka mradi wa saa 30 kwa mwezi katika kazi ya kuhubiri. Niliutimiza mradi huo nikajiambia mwenyewe: ‘Vema!’ Unafanya mengi.’
Lakini mara nyingine tena, kiburi kikawa tatizo langu. (Mithali 16:18) Niliendelea kufikiria jinsi ninavyofanya vema na kwamba sikuhitaji kufanya maendeleo zaidi ya kiroho. Hali yangu ya kiroho ikaanza kufifia, na nikaanza hata kupoteza sifa njema nilizokuwa nimepata. Kisha nikapokea nidhamu niliyohitaji.
Katika 1985 waangalizi wasafirio wawili na wake zao walikuwa wageni nyumbani mwetu walipofanya ziara yao ya kawaida kwenye kundi letu. Kuwatazama Wakristo hawa wanyenyekevu, wenye kujidhabihu wenyewe kulinisababisha kwa kweli nitafakari juu ya mambo. Nilifanya utafiti juu ya habari kuhusu unyenyekevu, nikitumia vichapo vya Watch Tower Society. Nilifikiria juu ya ule unyenyekevu mkuu ambao Yehova huonyesha katika shughuli zake pamoja na sisi wanadamu wenye dhambi. (Zaburi 18:35) Nilijua kwamba nilazima nibadili kufikiri kwangu.
Nilimsihi Yehova anisaidie nisitawishe unyenyekevu ili nimtumikie kwa njia ambayo alinitaka nimtumikie na aniongoze katika kuzitumia zile zawadi nilizokuwa nazo kwa utukufu wake. Nilijaza ombi la utumishi wa painia, nikaanza kumtumikia katika utumishi wa wakati wote katika Machi 1989.
Naweza kusema sasa kwamba nina furaha kweli kweli na kwamba kujinyenyekeza mwenyewe ni jambo ambalo limechangia furaha yangu. Nimepata sababu ya kweli ya kuishi—ile ya kuwasaidia wale wenye uhitaji wapate kujua kwamba Yehova, Mungu wa kweli, hayuko mbali na wale wamtafutao.—Kama ilivyosimuliwa na Vera Brandolini.