Vitumbuizo vya Kijamii —Furahia Manufaa, Epuka Mitego
“Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha roho [nafsi, “NW”] yake kwa mema katika kazi yake.”—MHUBIRI 2:24.
1. Mwongozo wa Mungu husaidia watu wake katika njia zipi kwa habari ya vitumbuizo?
MWONGOZO wa Yehova huwaletea watumishi wake manufaa mengi. Twaweza kuona hilo kwa habari ya vitumbuizo. Mwelekezo wake husaidia Wakristo waepuke kupita kiasi kwa njia yoyote. Wanadini wengine, wanaosisitiza namna fulani tu ya nguo na mwenendo, huona kujifurahisha kokote kuwa dhambi. Kwa upande ule mwingine, watu walio wengi hufuatia mambo yenye kufurahisha hata ikiwa mambo hayo hupingana na sheria na kanuni za Yehova.—Warumi 1:24-27; 13:13, 14; Waefeso 4:17-19.
2. Ni nini kilichoonyesha mapema maoni ya Mungu juu ya vitumbuizo?
2 Lakini, namna gani watu wa Mungu? Wengi wanaoanza kujifunza Biblia hushangaa kujifunza kwamba Mungu kwa kweli aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuonea shangwe uhai. Aliwapa wazazi wetu wa kwanza kazi ya kufanya—lakini si ile kazi ngumu yenye kuchosha inayoshusha moyo ambayo huonekana katika maisha ya wanadamu wengi wasio wakamilifu. (Mwanzo 1:28-30) Ebu fikiria zile njia nyingi zifaazo ambazo kwazo wote wanaoishi kwenye dunia paradiso wanaweza kujifurahisha. Ebu wazia shangwe yao kwa kutazama wanyama wa porini ambao wasingeleta tisho lolote na wengine mbalimbali wa nyumbani ambao wangekuwa sehemu ya maisha ya kila siku! Na wangekuwa na milo mizuri kama nini kutokana na “kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa”!—Mwanzo 2:9; Mhubiri 2:24.
3-5. (a) Vitumbuizo vyapaswa kuwa na kusudi gani? (b) Ni kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu hakuwakataza Waisraeli wasijifurahishe?
3 Utendaji huo waweza, kwa kweli, kuonwa kuwa vitumbuizo, kusudi lavyo katika Paradiso lingekuwa sawa na la sasa: ili kuburudisha na kurudisha nguvu ya mtu ili aweze kufanya utendaji (kazi) mwingine zaidi wenye matokeo. Vitumbuizo vinapotimiza hilo, vina manufaa. Je! hilo lamaanisha kwamba waabudu wa kweli waweza kuweka kando wakati maishani mwao kwa ajili ya vitumbuizo hata ingawa bado hawaishi katika Paradiso? Ndiyo. Insight on the Scriptures husema hivi kuhusu vitumbuizo miongoni mwa watu wa Yehova wa kale:
4 “Mambo ya kufurahisha na tafrija za Waisraeli hazionyeshwi waziwazi katika rekodi ya Biblia. Hata hivyo, inaonyesha kwamba zilionwa kuwa zenye kufaa na kutamaniwa zilipopatana na kanuni za kidini za taifa hilo. Namna kuu za tafrija zilikuwa kucheza ala za muziki, kuimba, kucheza dansi, mazungumzo, pamoja na michezo mingineo. utoaji wa vitendawili na maswali magumu ulithaminiwa sana.—Amu 14:12.”—Buku 1, ukurasa 102.
5 Daudi aliporudi baada ya ushindi, wanawake Waebrania walitumia zeze na vigoma walipokuwa wakisherehekea (Kiebrania, sa·chaqʹ). (1 Samweli 18:6, 7) Na neno la Kiebrania humaanisha kwa msingi “-cheka,” na fasiri nyinginezo husema juu ya “wanawake wanaojifurahisha.” (Byington, Rotherham, The New English Bible) Sanduku la Agano lilipokuwa likihamishwa, “Daudi na nyumba yote ya Israeli walikuwa wakisherehekea mbele za Yehova kwa aina zote za ala.” Mikali, mke wa Daudi, alikuwa na maoni yasiyosawazika, kwani alipinga kushiriki kwa Daudi katika utendaji huo wa kutumbuiza. (2 Samweli 6:5, 14-20, NW) Mungu alitabiri kwamba wahamishwa waliokuwa wakirudi kutoka Babuloni wangeshiriki katika utendaji kama huo wenye shangwe.—Yeremia 30:18, 19; 31:4; linganisha Zaburi 126:2.
6. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatusaidiaje katika maoni yetu juu ya vitumbuizo?
6 Twapaswa pia kujaribu kuwa wenye usawaziko kuhusu vitumbuizo. Kwa mfano, je, tunathamini kwamba Yesu hakuwa mtu mwenye kujinyima furaha? Alichukua wakati kwa ajili ya milo yenye kuburudisha, kama vile ile “karamu kubwa” ambayo Lawi alimfanyia. Na wakati wale waliojiona kuwa waadilifu walipomchambua kwa ajili ya kula na kunywa, Yesu alikatalia mbali maoni na njia zao. (Luka 5:29-31; 7:33-36) Kumbuka pia, kwamba yeye alihudhuria arusi na pia kuchangia karamu hiyo. (Yohana 2:1-10) Yuda ndugu-nusu ya Yesu ataja kwamba Wakristo walikuwa na ‘karamu za upendo,’ yaonekana zilikuwa milo ambayo wenye uhitaji wangeweza kufurahia chakula na ushirika mzuri, wenye kuburudisha.—Yuda 12.
Vitumbuizo vya Kijamii Katika Wakati Wavyo na Mahali Pavyo
7. Neno la Mungu hutiaje moyo kuwe na usawaziko kuhusu vitumbuizo?
7 Mhubiri 10:19 husema kwa upendeleo juu ya ‘karamu inayofanywa kwa ajili ya kicheko, na divai inayofurahisha maisha.’ Je! hilo husikika kana kwamba vitumbuizo ni jambo lisilofaa au lililo baya? Hata hivyo, kitabu icho hicho husema hivi: “Kwa kila jambo kuna majira yake, . . . wakati wa kulia, na wakati wa kucheka; wakati wa kuomboleza, na wakati wa kucheza.” (Mhubiri 3:1, 4) Naam, ingawa Biblia haishutumu vitumbuizo vinavyofaa, inatupa sisi maonyo. Hayo hutia ndani kuweka vitumbuizo vya kijamii katika mahali pavyo kwa habari ya wakati na kiasi. Inatuonya pia juu ya mitego ambayo imekuwa ya kawaida sana katika vikusanyiko vikubwa vya kijamii.—2 Timotheo 3:4.
8, 9. Ni kwa nini ule wakati tunamoishi na mgawo wetu wa kupewa na Mungu vyapaswa kuathiri vitumbuizo?
8 Tuliona kwamba Wayahudi waliokuwa wakirudi kutoka Babuloni—waliokuwa na kazi nyingi ngumu kufanya—wangeshiriki katika burudisho lenye shangwe. Hata hivyo, mapema zaidi, Yeremia alisema kwamba yeye ‘asingeketi katika mkutano wao wanaojifurahisha, wala asingefurahi.’ (Yeremia 15:17) Alipewa mgawo kimungu kupeleka ujumbe kuhusu adhabu ambayo ingekuja, kwa hiyo huo haukuwa wakati ufaao kwake kujifurahisha.
9 Wakristo leo wamepewa mgawo wa kupiga mbiu ujumbe wa Mungu wenye tumaini pamoja na kutamka hukumu zake dhidi ya mfumo mbovu wa Shetani. (Isaya 61:1-3; Matendo 17:30, 31) Hivyo yapaswa iwe wazi kwamba hatupaswi kuruhusu vitumbuizo viwe mashuhuri maishani mwetu. Twaweza kuonyesha jambo hilo kwa kutumia chumvi kidogo au kiungo cha pekee kinachoongezea ladha ya chakula. Je! wewe ungemimina kiungo hicho kwa wingi hivi kwamba kinapita kiasi cha chakula? Bila shaka la. Kulingana na maneno ya Yesu kwenye Yohana 4:34 na Mathayo 6:33, hangaiko letu kuu—chakula chetu chenyewe—lapasa kuwa kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo tafrija yawa kama kiungo. Yapaswa ituburudishe na kuongezea furaha, wala si kuchosha au kupita kiasi.
10. Ni kwa nini sisi sote twapaswa tujichunguze tena kwa habari ya kiasi cha wakati tunaotumia kwa ajili ya vitumbuizo?
10 Lakini, tua ukafikiri: Je! watu wengi wasingesema kwamba wakati na uangalifu wanaotolea vitumbuizo ni wa kiasi? Kama wangalihisi tofauti, wangalirekebisha mambo. Je! hilo halidokezi kwamba kila mmoja wetu apaswa atue na kwa uzito, achanganue kwa unyoofu, mahali vitumbuizo vilivyopo hasa maishani mwake? Je! yawezekana kwamba vimekuwa jambo kuu kisiri? Kwa mfano, je, sisi huwasha televisheni bila kufikiria, wakati wowote tunaporudi nyumbani? Je! tumefanyiza kawaida ya kuweka kando sehemu kubwa ya wakati kwa ajili ya vitumbuizo kila juma, kama vile kila Ijumaa usiku au kila Jumamosi usiku? Je! tungetamauka ikiwa wakati huo ungefika na tungekuwa nyumbani bila mpango wowote wa tafrija? Maswali mawili ya ziada: Siku baada ya kikusanyiko, je, tunapata kwamba tulirudi tumechelewa mno au tulisafiri mbali sana hivi kwamba tumechoka, labda tukiwa tumeishiwa nguvu mno kushiriki katika huduma ya Kikristo au kumpa mwajiri wetu siku nzima ya kazi? Ikiwa vitumbuizo vyetu vina tokeo hilo mara kwa mara, au mara nyingi, je, kwa kweli vinafaa na ni furaha yenye usawaziko?—Linganisha Mithali 26:17-19.
11. Ni kwa nini kupitia namna ya vitumbuizo vyetu kwafaa?
11 Huenda likawa jambo zuri kwetu kupitia, pia, namna ya vitumbuizo vyetu. Kuwa kwetu watumishi wa Mungu si uthibitisho kwamba vitumbuizo vyetu vinafaa. Chunguza lile ambalo mtume Petro aliwaandikia Wakristo wapakwa-mafuta: “Wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali.” (1 Petro 4:3) Hakuwa kana kwamba, anawapungia kidole ndugu zake, akiwashtaki juu ya kuiga lile ambalo wale waliomo ulimwenguni walikuwa wakifanya. Hata hivyo, kuwa macho ni muhimu kwa Wakristo (wakati huo na sasa) kwa sababu mtu aweza kwa urahisi kunaswa na vitumbuizo vyenye kudhuru.—1 Petro 1:2; 2:1; 4:7; 2 Petro 2:13.
Uwe Macho Kuona Mitego
12. Petro ya kwanza 4:3 hukazia mtego wa aina gani?
12 Twapaswa tuwe macho tuone mtego wa aina gani? Petro alitaja “ulevi, na karamu za ulafi, na vileo.” Mfafanuzi Mjerumani alieleza kwamba maneno ya Kigiriki yaliyotumiwa “yalitumika hasa kuhusu unywaji wa kijamii kwenye karamu.” Profesa mmoja Mswisi aliandika kwamba mazoea ya jinsi hiyo yalipendwa na wengi wakati huo wa nyuma: “Ni lazima ufafanuzi huo uhusu vikusanyiko vilivyopangwa au hata vilabu vya kawaida ambavyo katika hivyo utendaji wa aibu ulioelezwa ulifanywa.”
13. Utumizi wa vileo kwenye vikusanyiko umekuwaje mtego? (Isaya 5:11, 12)
13 Kuwa na vileo kwenye vikusanyiko vikubwa vya kijamii kumenasa wengi. Si kana kwamba Biblia hukataza utumizi wa kiasi wa vinywaji hivyo, kwani haikatazi. Kama ushuhuda wa hilo, Yesu alitengeneza divai kwenye karamu ya arusi katika Kana. Ni lazima iwe kwamba hakukuwako unywaji wa kupindukia, kwani Yesu angetii shauri la Mungu na kuepuka kuwa miongoni mwa walevi. (Mithali 23:20, 21) Lakini fikiria jambo hili: Mwelekezi wa karamu hiyo alisema kwamba kwenye karamu nyinginezo divai iliyo njema hutolewa kwanza ‘na watu wakiisha kunywa sana ndipo divai iliyo dhaifu’ huletwa. (Yohana 2:10) Kwa hiyo lilikuwa jambo la kawaida kwa Wayahudi kulewa kwenye arusi ambapo divai ilipatikana kwa wingi kwa wote.
14. Wakaribishaji Wakristo wanaweza katika njia zipi kukabiliana na ule mtego unaotolewa na vileo?
14 Kulingana na hilo, wakaribishaji wengine Wakristo wameamua kuandaa divai, bia, na vileo vingine ikiwa tu wao binafsi waweza kutolea uangalizi kile ambacho wageni wao wanatolewa au wanakunywa. Ikiwa kikundi ni kikubwa kuliko kile ambacho mkaribishaji aweza kutolea uangalizi moja kwa moja, kama vile ile arusi ya Kiyahudi iliyotajwa, kileo kingi chaweza kuwa mtego wenye hatari. Huenda ikawa kwamba mtu yupo ambaye alikuwa amepigana na kushinda tatizo la kunywa. Waweza kuthamini kwamba kupatikana kwa kileo kwa wingi bila kizuizi kwaweza kumshawishi anywe kupita kiasi na kuwaharibia wote sherehe hiyo. Mwangalizi ambaye ni baba ya watoto katika Ujerumani alieleza kwamba familia yake hunufaika kutokana na ushirika mzuri pamoja na waamini wenzao kwenye vikusanyiko vya kijamii. Lakini, aliongeza kwamba uwezekano wa kuwa na matatizo ulikuwa bila shaka mkubwa zaidi wakati bia ilipopatikana kwa urahisi.
15. Mwongozo ufaao wa vikusanyiko vya kijamii waweza kutimizwaje?
15 Ile arusi katika Kana ilikuwa na “mwelekezi wa karamu.” (Yohana 2:8, NW) Hiyo haimaanishi kwamba familia inayoalika kikundi cha watu nyumbani mwayo kwa ajili ya mlo au kipindi cha ushirika yapaswa iweke rasmi mwelekezi. Mume ndiye angekuwa na daraka la kutolea uangalizi kikusanyiko hicho. Lakini iwe kikundi ni chenye familia mbili tu au kikubwa kidogo kuliko hicho, yapaswa iwe wazi kwamba mtu fulani ana daraka juu ya yale yanayotukia. Wazazi wengi huchunguza hilo wakati mwana au binti yao anapoalikwa kwenye kikusanyiko cha kijamii. Wanawasiliana na mkaribishaji ili kumwuliza ni nani atakayetolea uangalizi sherehe hiyo nzima, kutia na kuwapo hadi mwisho wayo. Wazazi Wakristo hata wamerekebisha ratiba yao wenyewe ili wawepo ili kwamba watu wenye umri mkubwa zaidi na wachanga waweze kuonea shangwe ushirika wa wao kwa wao.
16. Ni nini maoni yanayofaa kuhusu ukubwa wa vikusanyiko?
16 Tawi la Kanada la Watch Tower Society laandika hivi: “Shauri linalohusu kuzuia ukubwa wa vikusanyiko vya kijamii limeeleweka na wazee wachache kumaanisha kwamba vikusanyiko vikubwa kwenye mapokezi ya arusi vinakosa kutii shauri hilo. Wamekata maneno kwamba tukishauriwa kudumisha vikusanyiko vyetu vikiwa vyenye ukubwa mdogo, uwezao kutolewa uangalizi, ingekuwa kosa kuwa na watu 200 au 300 kwenye mapokezi ya arusi.”a Badala ya kukazia sana mno ukubwa ulioamuliwa kibinafsi, uangalifu wapaswa ukaziwe hasa kwenye uangalizi ufaao, haidhuru ni watu wangapi waliopo. Kiasi cha divai ambacho Yesu aliandaa huonyesha kwamba ni kikundi kikubwa kilichohudhuria ile arusi katika Kana, lakini kwa wazi kilitolewa uangalizi ifaavyo. Karamu nyinginezo wakati huo wa nyuma hazikutolewa uangalizi ifaavyo; ukubwa wao huenda ikawa ulikuwa kisababishi cha kutokutolewa uangalizi vya kutosha. Kadiri kikusanyiko kinavyokuwa kikubwa, ndivyo tatizo linavyokuwa kubwa, kwa sababu ni rahisi zaidi kwa wale walio dhaifu, walio na mwelekeo wa kufanya mambo kupita kiasi, wajitokeze wenyewe. Kwenye vikusanyiko visivyosimamiwa huenda wakachochea utendaji wenye kutiliwa shaka.—1 Wakorintho 10:6-8.
17. Usawaziko wa Kikristo waweza kuonyeshwaje wakati kikusanyiko kinapopangwa?
17 Uangalizi mzuri wa kikusanyiko cha kijamii unatia ndani mipango na maandalio yacho. Hilo halihitaji kubuni jambo kubwa lenye kutokeza ili kiwe cha kipekee au chenye kukumbukwa lakini ambacho kingeiga karamu za kilimwengu, kama vile karamu kubwa ya kucheza dansi ambamo watu huvaa mavazi ya kiajabu au karamu ambamo watu huvaa vinyago. Je! waweza kuwazia Waisraeli waaminifu katika Bara Lililoahidiwa wakipanga karamu ambamo wote walipaswa wajivike kama wapagani katika Misri au nchi nyingineo? Je! wangepanga kucheza dansi za kiashiki au kuwa na muziki wenye makelele ambao huenda ukapendwa sana na wapagani? Huko kwenye Mlima wa Sinai, walinaswa na muziki na dansi za jinsi hiyo ambazo huenda ikawa zilienea wakati huo na kupendwa sana katika Misri. Twajua jinsi Mungu na mtumishi wake mkomavu Musa walivyoona vitumbuizo hivyo. (Kutoka 32:5, 6, 17-19) Kwa hiyo, mkaribishaji au mwangalizi wa kikusanyiko cha kijamii apaswa achunguze kama kutakuwako kuimba au kucheza dansi kokote; ikiwa ndivyo, apaswa awe na uhakika kwamba kunapatana na kanuni za Kikristo.—2 Wakorintho 6:3.
18, 19. Twaweza kupata mwono-ndani upi kutokana na kualikwa kwa Yesu kwenye arusi, na twaweza kutumiaje huo?
18 Hatimaye, twakumbuka kwamba ‘Yesu alikuwa amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake.’ (Yohana 2:2) Ni kweli, Mkristo mmoja mmoja au familia yaweza kuwatembelea wengine ili wawe na ushirika mzuri, wenye kujenga. Lakini kwa habari ya vikusanyiko vya kijamii vilivyopangwa, imeonwa kwamba kuamua kimbele ni nani watakaokuwako husaidia kuzuia matatizo. Umaana wa hilo ulikaziwa na mzee mmoja katika Tennessee, U.S.A., ambaye alikuwa amewalea wana na binti waliomo katika huduma ya wakati wote. Kabla ya yeye na mke kukubali mwaliko, au kuwapa watoto wao ruhusa ya kuhudhuria, aliwasiliana na mkaribishaji ili awe na uhakika kwamba wale ambao wangehudhuria walijulikana kimbele. Familia yake ililindwa na mitego ambayo ilikuwa imewanasa wengine kwenye vikusanyiko ambavyo watu wowote wangeweza kuhudhuria, iwe kwa ajili ya mlo, mandari, au mazoezi, kama vile kucheza mpira.
19 Yesu alikataza kualika tu watu wa ukoo, marafiki wa zamani, au wale wenye umri au hali ya kiuchumi iliyo sawa na yetu kwenye kikusanyiko. (Luka 14:12-14; linganisha Ayubu 31:16-19; Matendo 20:7-9.) Ukichagua kwa uangalifu wale wa kualika, ni rahisi zaidi kutia ndani Wakristo wenye umri na hali mbalimbali. (Warumi 12:13; Waebrania 13:2) Wachache kati yao huenda wakawa dhaifu kiroho au wapya ambao waweza kunufaika kutokana na ushirika pamoja na Wakristo wakomavu.—Mithali 27:17.
Vitumbuizo Mahali Pavyo
20, 21. Kwa nini vitumbuizo vyaweza kuwa na mahali pafaapo maishani mwetu?
20 Inafaa kwetu tukiwa watu wanaomcha Mungu kupendezwa na vitumbuizo vyetu na kuhangaikia kwamba vinafaa na kwamba tuna usawaziko katika kiasi cha wakati tunaotumia kwa ajili yavyo. (Waefeso 2:1-4; 5:15-20) Mwandikaji wa Mhubiri aliyepuliziwa roho alihisi jinsi hiyo: “Kisha nikaisifu furaha, kwa sababu mwanadamu hana neno lo lote lililo jema chini ya jua, kuliko, kula, na kunywa, na kucheka, na ya kuwa hilo likae naye katika amali yake, siku zote za maisha yake alizompa Mungu chini ya jua.” (Mhubiri 8:15) Mambo hayo ya kufurahisha yenye usawaziko yaweza kuburudisha mwili na kusaidia kusawazisha matatizo na mafadhaiko ambayo ni ya kawaida katika mfumo huu uliopo.
21 Kuonyesha hilo, painia mmoja kutoka Austria alimwandikia rafiki wa zamani hivi: “Tulikuwa na matembezi mazuri juzi. Sisi karibu watu 50 tulitembelea kiziwa kidogo karibu na mji wa Ferlak. Ndugu B—— aliongoza msafara huo katika gari lake, akibeba majiko matatu, viti vya kukunjwa, meza, na hata meza ya kuchezea tenisi. Tulifurahia sana matembezi hayo. Dada mmoja alikuwa na kinanda cha mkono, kwa hiyo kulikuwako nyimbo nyingi za Ufalme. Akina ndugu, vijana kwa wazee, walionea shangwe ushirika huo.” Alikuwa na kumbukumbu zenye kupendeza juu ya tafrija iliyosimamiwa vizuri ambayo haikuwa na mitego kama vile unywaji wa kupindukia au mwenendo mbaya.—Yakobo 3:17, 18.
22. Tunapoonea shangwe vitumbuizo vya kijamii, kila mmoja wetu apaswa kuzingatia akilini onyo jipi?
22 Paulo alitusihi tuwe waangalifu tusifuate tamaa za mnofu usio mkamilifu, hata kutofanya mipango inayotufunua tupate vishawishi. (Warumi 13:11-14) Hiyo yatia ndani mipango ya vitumbuizo vya kijamii. Tunapotumia shauri lake katika mambo hayo, tutaweza kuepuka hali ambazo zimeongoza wengine kwenye uharibifu wa kiroho. (Luka 21:34-36; 1 Timotheo 1:19) Badala ya hiyo, tutachagua kwa hekima tafrija ifaayo itakayotusaidia tudumishe uhusiano wetu na Mungu. Hivyo tutanufaika kutokana na vitumbuizo vya kijamii viwezavyo kuonwa kuwa mojawapo ya zawadi nzuri za Mungu.—Mhubiri 5:18.
[Maelezo ya Chini]
a Mnara wa Mlinzi wa Septemba 15, 1984, ulikuwa na shauri lenye usawaziko kuhusu arusi na karamu za arusi. Yule atakayekuwa bwana-arusi pamoja na bibi-arusi wake, pamoja na wengine watakaowasaidia, wanaweza kwa manufaa kupitia habari hiyo kabla ya kufanya mipango yao ya arusi.
Tumejifunza Nini?
◻ Ni maoni gani yenye usawaziko tunayopata katika Biblia kuhusu kuonea shangwe vitumbuizo vya kijamii?
◻ Kwa nini ufikirio utolewe habari ya wakati na namna ya vitumbuizo?
◻ Ni mambo gani ambayo mkaribishaji Mkristo aweza kufanya ili kulinda dhidi ya mitego?
◻ Ikiwa vitumbuizo vinafaa na ni vyenye usawaziko, vinaweza kutimiza nini kwa Wakristo?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Mkaribishaji au mwelekezi kwenye kikusanyiko ana daraka la kuona kwamba wageni hawanaswi katika mtego