Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 10/1 kur. 5-8
  • Mesiya Tumaini la Kweli?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mesiya Tumaini la Kweli?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wamesiya wa Karne ya 20
  • Tumaini la Kweli?
  • Mwokozi wa Ainabinadamu
  • Mesiya na Serikali
  • Masihi! Njia ya Mungu ya Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • “Tumempata Mesiya”!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • “Tumempata Masihi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Walimngoja Masihi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 10/1 kur. 5-8

Mesiya Tumaini la Kweli?

Alijiita Musa. Hata hivyo, jina lake la kweli limesahauliwa katika historia. Katika karne ya tano W.K., alisafiri kotekote katika kisiwa cha Krete, akiwasadikisha Wayahudi huko kwamba alikuwa ndiye Mesiya waliokuwa wakimngojea. Aliwaambia kwamba karibuni uonevu wao, uhamisho na utumwa wao ungeisha. Waliamini hilo. Siku ya ukombozi wao ilipowadia, Wayahudi walimfuata “Musa” kwenda kwenye rasi iliyokuwa juu ya Bahari Mediterania. Aliwaambia kwamba walihitaji tu kujirusha wenyewe baharini nayo ingegawanyika mbele yao. Wengi walitii, wakiruka baharini ambayo haikugawanyika. Wengi sana walikufa maji; wengine waliokolewa na mabaharia na wavuvi. Hata hivyo, Musa hakupatikana mahali popote. Mesiya huyo alikuwa amepotelea mbali.

MESIYA ni nini? Maneno “mwokozi,” “mkombozi,” na “kiongozi” huenda yakaja akilini. Watu wengi hufikiri kwamba mesiya ni mtu anayechochea tumaini na ujitoaji katika wafuasi wake, akiahidi kuwaongoza kutoka katika uonevu hadi uhuru. Kwa kuwa historia ya kibinadamu kwa kadiri kubwa ni historia ya uonevu, haishangazi kwamba mesiya wengi wa jinsi hiyo wametokea muda wote wa karne zilizopita. (Linganisha Mhubiri 8:9.) Lakini kama vile yule mwenye kujiita Musa wa Krete, mesiya hao mara nyingi wamewaongoza wafuasi wao kwenye utamausho na msiba kuliko kwenye ukombozi.

“Huyu ndiye Mesiya Mfalme!” Hivyo ndivyo yule rabbi Akiba ben Joseph mwenye kuheshimiwa alivyomsalimu Simeon Bar Kokhba katika mwaka 132 W.K. Bar Kokhba alikuwa mtu mwenye uwezo aliyeongoza jeshi lenye nguvu. Wayahudi wengi wakafikiri kwamba hatimaye, kulikuwako mwanamume ambaye angekomesha uonevu wao wa muda mrefu mikononi mwa Serikali ya Ulimwengu ya Roma. Bar Kokhba alishindwa kufaulu; mamia ya maelfu ya wananchi wenzake walikufa kwa sababu ya kutofaulu huko.

Katika karne ya 12, mesiya mwingine Myahudi alitokea, wakati huu katika Yemen. Wakati khalifa, au mtawala, alipomwomba ishara ya umesiya wake, mesiya huyo alidokeza kwamba khalifa huyo aamuru kichwa chake kikatwe na aache ufufuo wa haraka wa mesiya huyo uwe kama ishara. Khalifa alikubaliana na mpango huo—na huo ukawa mwisho wa mesiya huyo wa Yemen. Katika karne iyo hiyo, mwanamume aliyeitwa David Alroy aliwaambia Wayahudi katika Mashariki ya Kati wajitayarishe kumfuata kwenye mabawa ya malaika ili kurudi kwenye lile Bara Takatifu. Wengi waliamini kwamba alikuwa ndiye mesiya. Wayahudi wa Baghdad walingojea kwa saburi kwenye madari yao, bila kuwa na utambuzi wowote juu ya wevi waliokuwa wakipora mali zao.

Sabbatai Zevi alitokea Smirna katika karne ya 17. Alipiga mbiu ya umesiya wake kwa Wayahudi kotekote Ulaya. Wakristo pia, walimsikiliza. Zevi aliwatolea wafuasi wake ukombozi—yaonekana kwa kuwaacha wazoee dhambi bila kizuizi. Wafuasi wake wa karibu zaidi walifanya karamu za ulafi na ulevi, wakakaa uchi, wakafanya uasherati, na ngono ya watu wa ukoo, kisha wakajiadhibu kwa kujichapa mijeledi, kwa kujivingirisha thelujini wakiwa uchi, na kwa kujizika wenyewe hadi shingoni katika ardhi yenye ubaridi. Aliposafiri kwenda Uturuki, Zevi alikamatwa na kuambiwa kwamba ni lazima aongoke awe Mwislamu au afe. Aliongoka. Wafuasi wake wengi walitamauka. Hata hivyo, kwa muda wa karne mbili zilizofuata, Zevi bado aliitwa mesiya na watu fulani.

Jumuiya ya Wakristo pia imetokeza wamesiya wayo mbalimbali. Katika karne ya 12, mwanamume aliyeitwa Tankelm alikusanya jeshi kubwa la wafuasi akatawala mji wa Antwerp. Mesiya huyo alijiita mungu; hata aliwauzia wafuasi wake maji aliyokuwa ametumia kuogea ili wayanywe yakiwa sakramenti! Mesiya mwingine “Mkristo” alikuwa Thomas Müntzer wa Ujerumani wa karne ya 16. Aliongoza uasi dhidi ya mamlaka ya jumuiya ya sehemu hiyo, akiwaambia wafuasi wake kwamba hilo lilikuwa pigano la Har–Magedoni. Aliahidi kwamba angezikamata risasi za mzinga za maadui katika mikono ya vazi lake. Badala ya hivyo, watu wake walichinjwa-chinjwa, na Müntzer akakatwa kichwa. Mesiya wengineo wengi wa jinsi hiyo walitokea katika Jumuiya ya Wakristo muda wote wa karne zilizopita.

Dini nyingine, pia, zina wamesiya wazo. Uislamu huelekezea yule Mahdi, au yule aliyeongozwa ifaavyo, atakayeleta enzi yenye haki. Katika Uhindu, baadhi ya watu wamedai kuwa waavata, au wale waliozaliwa upya katika miili mingine, ya vijimungu mbalimbali. Na, kama vile The New Encyclopœdia Britannica ionyeshavyo, “hata dini isiyoamini juu ya umesiya kama vile Ubuddha imetokeza imani, miongoni mwa vikundi vya Mahāyāna, katika Buddha wa wakati ujao aitwaye Maitreya ambaye angeshuka kutoka makao yake ya kimbingu na kuwaleta waaminifu kwenye paradiso.”

Wamesiya wa Karne ya 20

Katika karne yetu wenyewe, uhitaji wa mesiya wa kweli umekuwa wenye hima kuliko wakati mwingine wowote; haishangazi basi kwamba wengi wamedai cheo hicho. Katika Kongo ya Afrika ya miaka ya 1920, 1930, na 1940, Simon Kimbangu na mwandamizi wake Andre “Yesu” Matswa waliitwa mesiya. Walikufa, lakini wafuasi wao wangali wakiwatazamia warudi na kuleta mileani (utawala wa miaka elfu) ya Afrika.

Karne hii imeona pia ongezeko la “vidhehebu vya mizigo” katika New Guinea na Melanesia. Washiriki hutazamia kuwasili kwa meli au ndege, inayoendeshwa na wanaume weupe walio kama mesiya ambao watawafanya wawe matajiri na kuleta enzi ya furaha wakati ambapo hata wafu watainuka.

Mataifa yaliyositawi kiviwanda yamekuwa na mesiya wayo pia. Wengine wao ni viongozi wa kidini, kama vile Sun Myung Moon, mwenye kujipiga mbiu kuwa mwandamizi wa Yesu Kristo aliye na lengo la kuusafisha ulimwengu kupitia familia ya wafuasi wake yenye umoja. Viongozi wa kisiasa wamejaribu pia kujitwalia cheo cha kimesiya. Adolf Hitla akiwa mfano wenye kuhofisha zaidi wa karne hii akiwa na maongezi yake yenye majisifu ya Utawala wa Miaka Elfu Moja.

Falsafa na mashirika ya kisiasa yametimiza vilevile cheo cha kimesiya. Kwa mfano, The Encyclopedia Americana huonyesha kwamba nadharia ya kisiasa ya Umaksi-Ulenini inadokeza umesiya. Na lile shirika la Umoja wa Mataifa, linaloitwa na wengi kuwa tumaini la mwisho la amani ya ulimwengu, laonekana kuwa limekuwa aina fulani ya mesiya badala akilini mwa wengi.

Tumaini la Kweli?

Pitio hilo fupi laonyesha tu waziwazi kwamba historia ya harakati za kimesiya kwa kadiri kubwa ni historia ya udanganyo, ya matumaini yaliyotamaushwa na ndoto zisizotimizwa. Basi, si jambo lenye kushangaza kwamba, watu wengi leo wamekuwa wenye kudhihaki tumaini hilo la kuwa na mesiya.

Lakini, kabla ya kuondolea mbali kabisa tumaini la kimesiya, twapaswa kwanza tupate kujua mahali linapotoka. Kwa kweli, “mesiya” ni neno la Biblia. Neno la Kiebrania ni ma·shiʹach, au “mpakwa-mafuta.” Katika nyakati za Biblia, wafalme na makuhani nyakati nyingine waliwekwa rasmi katika vyeo vyao kwa sherehe ya kupakwa mafuta, ambamo mafuta yenye kunukia yalimwagwa kichwani. Kwa hiyo neno ma·shiʹach lilitumiwa kwao kwa kufaa. Kulikuwako pia wanaume waliopakwa mafuta, au kuwekwa rasmi kwenye vyeo vya pekee, bila sherehe yoyote ya kupaka mafuta. Musa anaitwa “Kristo,” au “mpakwa-mafuta,” kwenye Waebrania 11:24-26, kwa sababu alichaguliwa kuwa nabii na mwakilishi wa Mungu.

Fasili hiyo ya mesiya kuwa “mpakwa-mafuta” huwatofautisha mesiya wa Kibiblia na wale mesiya bandia ambao tumezungumzia. Mesiya wa Kibiblia hawakujiweka rasmi wenyewe; wala hawakuchaguliwa na makutano ya wafuasi wenye kuwapenda mno. La, kuwekwa kwao rasmi kulitoka juu, kutoka kwa Yehova Mungu mwenyewe.

Ingawa Biblia husema juu ya wamesiya wengi, inamtokeza mmoja juu zaidi ya wengine. (Zaburi 45:7) Mesiya huyo ndiye mtu mashuhuri katika unabii wa Biblia, ufunguo wa utimizo wa ahadi za Biblia zenye kusisimua zaidi. Na Mesiya huyo kwa kweli hujishughulisha na matatizo tunayokabili leo.

Mwokozi wa Ainabinadamu

Mesiya wa Biblia hushughulikia matatizo ya ainabinadamu kutoka mashina yayo. Wakati wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa walipomwasi Muumba wakichochewa na kiumbe-roho mwenye kuasi, yaani, Shetani, walikuwa kwa kweli wakijitwalia wenyewe haki kamili ya serikali. Walitaka kuwa waamuzi wa lile lifaalo na lisilofaa. Kwa hiyo waliondoka chini ya serikali ya Yehova yenye upendo na ulinzi wakaiingiza familia ya kibinadamu katika mchafuko na huzuni ya kujitawala yenyewe, kutokamilika, na kifo.—Warumi 5:12.

Kwa hiyo, ni jambo lenye upendo kama nini kwamba Yehova Mungu alichagua pindi hiyo yenye giza katika historia ya kibinadamu ili kuiandalia ainabinadamu yote mmweko wa tumaini. Kwa kutamka hukumu juu ya waasi wa kibinadamu, Mungu alitabiri kwamba wazao wao wangekuwa na mwokozi. Akirejezewa kuwa “mbegu,” Mwokozi huyo angekuja kuipindua ile kazi mbaya sana ambayo Shetani alikuwa amefanya huko Edeni; hiyo Mbegu ingemponda yule “nyoka,” Shetani, kichwani, ikimpondaponda asiwepo tena.—Mwanzo 3:14, 15.

Kutoka nyakati za kale, Wayahudi waliona unabii huo kuwa wa Kimesiya. Targamu kadhaa, ambazo ni ufafanuzi mwingi wa Kiyahudi wa Maandiko Matakatifu uliotumiwa kwa kawaida katika karne ya kwanza, zilieleza kwamba unabii huo ungetimizwa “katika siku ya Mfalme Mesiya.”

Haishangazi basi, kwamba kutoka mwanzoni kabisa, wanaume wenye imani walisisimuliwa na ahadi hiyo ya Mbegu, au Mwokozi ambaye angekuja. Ebu wazia hisia za Abrahamu wakati Yehova alipomwambia kwamba hiyo Mbegu ingekuja kupitia ukoo wake mwenyewe, na kwamba “mataifa yote ya dunia”—si wazao wake wenyewe tu—‘wangejibarikia’ kupitia Mbegu hiyo.—Mwanzo 22:17, 18.

Mesiya na Serikali

Unabii mwingi wa baadaye ulilinganisha tumaini hilo na taraja la serikali nzuri. Kwenye Mwanzo 49:10, mwana wa mjukuu wa Abrahamu Yuda aliambiwa hivi: “Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, wala mfanya sheria kati ya miguu yake, hata atakapokuja Yeye [Shilo, New World Translation], mwenye milki, ambaye mataifa watamtii.” Kwa wazi, “Shilo” alitazamiwa kutawala—na angewatawala si Wayahudi tu bali “mataifa.” (Linganisha Danieli 7:13, 14.) Shilo alitambulishwa na Wayahudi wa kale kuwa ndiye Mesiya; kwa kweli, baadhi ya targamu za Kiyahudi ziliweka tu neno “Mesiya” au maneno “mfalme Mesiya” mahali pa neno “Shilo.”

Nuru ya unabii uliopuliziwa roho ilipoendelea kung’aa, mambo zaidi yalifunuliwa juu ya utawala wa Mesiya huyo. (Mithali 4:18) Kwenye 2 Samweli 7:12-16, Mfalme Daudi, mzao wa Yuda, aliambiwa kwamba Mbegu ingetoka katika nasaba yake. Zaidi ya hayo, Mbegu hiyo ingekuwa Mfalme asiye wa kawaida. Kiti chake cha ufalme, au utawala wake, ungedumu milele! Isaya 9:6, 7 huunga mkono jambo hilo: “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme [“serikali,” King James Version] utakuwa begani mwake. . . . Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, tangu sasa na hata milele. Wivu wa BWANA [Yehova, NW] wa majeshi ndio utakaotenda hayo.”

Je! waweza kuwazia serikali ya jinsi hiyo? Mtawala mwadilifu, mwenye haki, anayethibitisha amani na anayetawala milele. Inatofautiana kama nini na ule mfuatano wenye kusikitisha wa historia wa akina mesiya bandia! Tofauti na kuwa kiongozi mdanganyifu, mwenye kujiweka rasmi, Mesiya wa Biblia ni mtawala wa ulimwengu mwenye uwezo na mamlaka yote inayohitajiwa ili kubadili hali za ulimwengu.

Taraja hilo lina umaana mwingi katika nyakati zetu zenye msukosuko. Hakuna wakati mwingine kamwe kama huu, ambapo ainabinadamu imehitaji zaidi sana tumaini la jinsi hiyo. Lakini kwa kuwa mtu aweza kwa urahisi kushikamana na tumaini bandia, ni jambo la muhimu kwamba kila mmoja wetu achunguze swali hili kwa uangalifu: Je! Yesu wa Nazareti alikuwa ndiye Mesiya aliyetabiriwa kama vile wengi huamini? Makala ifuatayo itazungumzia jambo hilo.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Mesiya Katika Brooklyn?

Karatasi za matangazo, bao za matangazo, na matangazo yanayoangaza usiku katika Israeli hivi karibuni vimepiga mbiu hivi “Jiandae kwa ajili ya kuja kwa Mesiya.” Kampeni hiyo ya utangazaji ya dola 400,000 imeanzishwa na Walubavitcha, farakano la Wayahudi la Hasidiki lisilopendelea kamwe mabadiliko. Kuna itikadi iliyoenea sana miongoni mwa kikundi hicho chenye washiriki 250,000 kwamba rabi wao mkuu, Menachem Mendel Schneerson wa Brooklyn, New York, ndiye Mesiya. Kwa nini? Schneerson hufundisha kwamba Mesiya atakuja katika kizazi hiki. Na kulingana na gazeti Newsweek, maofisa Walubavitcha husisitiza kwamba rabi huyo mwenye umri wa miaka 90 hatakufa kabla ya Mesiya kuja. Kwa karne kadhaa farakano hilo limefundisha kwamba kila kizazi hutokeza angalau mwanamume mmoja anayestahili kuwa Mesiya. Kwa wafuasi wake, Schneerson huonekana kuwa ndiye mwanamume huyo, na yeye hajaweka rasmi mwandamizi yeyote. Bado, Wayahudi wengi hawamkubali kuwa ndiye Mesiya, lasema Newsweek. Kulingana na gazeti la habari Newsday, rabi mpinzani mwenye umri wa miaka 96 aitwaye Eliezer Schach amemwita Schneerson “mesiya bandia.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Imani ya kwamba Musa wa Krete alikuwa ndiye mesiya ilisababisha watu wengi wapoteze maisha zao

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki