“Tumempata Mesiya”!
“Kwanza [Andrea] alimpata Simoni, ndugu yake mwenyewe, akamwambia: ‘Tumempata Mesiya,’ (ambalo humaanisha, linapotafsiriwa, Kristo).”—YOHANA 1:41, NW.
1. Yohana Mbatizaji alishuhudia nini kuhusu Yesu wa Nazareti, na Andrea alifikia mkataa gani juu yake?
ANDREA alimtazama kwa makini yule Myahudi aliyeitwa Yesu wa Nazareti. Yesu hakuonekana kuwa mfalme, au mwenye hekima, au rabi. Hakuwa na mavazi ya kifalme, wala mvi, wala mikono miororo na ngozi laini. Yesu alikuwa mchanga—umri wa miaka 30 hivi—mwenye mikono migumu-migumu na ngozi ya rangi kahawanjano ya mfanya kazi za mikono. Kwa hiyo huenda ikawa Andrea hakushangaa alipopata kujua kwamba Yesu alikuwa seremala. Hata hivyo, Yohana mbatizaji alisema hivi juu ya mwanamume huyo: “Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu!” Siku iliyotangulia hiyo, Yohana alikuwa amesema jambo fulani lenye kushtusha hata zaidi: “Huyu ndiye Mwana wa Mungu.” Je! hilo lingekuwa kweli? Andrea alitumia kadiri fulani ya wakati akimsikiliza Yesu siku hiyo. Hatujui ni nini alilosema Yesu; lakini twajua kwamba maneno yake yalibadili maisha ya Andrea. Alimtafuta ndugu yake, Simoni, kwa haraka, na kusema kwa mshangao, “Tumempata Mesiya”!—Yohana 1:34-41, NW.
2. Kwa nini ni jambo la maana kufikiria uthibitisho juu ya kama Yesu alikuwa Mesiya aliyeahidiwa?
2 Andrea na Simoni (ambaye Yesu alimpa jina jipya Petro) baadaye wakawa mitume wa Yesu. Baada ya miaka zaidi ya miwili akiwa mwanafunzi wake, Petro alimwambia Yesu hivi: “Wewe Ndiwe Kristo [Mesiya], Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mathayo 16:16) Mitume na wanafunzi waaminifu walithibitika hatimaye kuwa na nia ya kufa kwa ajili ya imani hiyo. Leo, mamilioni ya watu wanyoofu wamejitoa namna iyo hiyo. Lakini kwa uthibitisho gani? Kwa vyovyote vile, uthibitisho hutofautisha kati ya imani na kuamini tu bila uthibitisho. (Ona Waebrania 11:1.) Basi acheni tuzungumzie sehemu tatu za ujumla za mathibitisho yanayothibitisha kwamba Yesu kwa kweli alikuwa ndiye Mesiya.
Ukoo wa Yesu
3. Gospeli za Mathayo na Luka hueleza mambo gani madogo madogo juu ya ukoo wa Yesu?
3 Ukoo wa Yesu ni uthibitisho wa kwanza ambao Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hutoa ili kuunga mkono Umesiya wake. Biblia ilitabiri kwamba Mesiya angekuja kutoka katika ukoo wa familia ya Mfalme Daudi. (Zaburi 132:11, 12; Isaya 11:1, 10) Gospeli ya Mathayo huanza hivi: “Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu.” Mathayo huunga mkono dai hilo la ujasiri kwa kufuatia nasaba ya Yesu kupitia ukoo wa baba mlezi wake, Yusufu. (Mathayo 1:1-16) Gospeli ya Luka hufuatia ukoo wa Yesu kupitia mama yake wa asili, Mariamu, kurudi nyuma kupitia Daudi na Abrahamu hadi Adamu. (Luka 3:23-38)a Hivyo waandishi wa Gospeli huthibitisha kikamili dai lao la kwamba Yesu alikuwa mrithi wa Daudi, katika maana ya kisheria na ya kiasili pia.
4, 5. (a) Je! watu walioishi wakati wa Yesu walipinga kutoka kwake katika nasaba ya Daudi, na ni kwa nini hilo ni la maana? (b) Marejezo yasiyo ya Kibiblia yanaungaje mkono ukoo wa Yesu?
4 Hata mpinzani mwenye kutilia shaka zaidi wa Umesiya wa Yesu hawezi kukanusha dai la Yesu la kuwa mwana wa Daudi. Kwa nini? Kuna sababu mbili. Moja ni kwamba, dai hilo lilirudiwa-rudiwa sana katika Yerusalemu kwa muda wa miongo mingi kabla ya jiji hilo kuharibiwa katika 70 W.K. (Linganisha Mathayo 21:9; Matendo 4:27; 5:27, 28.) Ikiwa dai hilo lilikuwa bandia, yeyote kati ya wapinzani wa Yesu—naye alikuwa na wengi—angalimthibitisha Yesu kuwa mdanganyi kwa kuchunguza tu ukoo wake katika maandishi ya ukoo katika nyaraka za umma.b Lakini historia haina rekodi yoyote ya yeyote aliyepinga kutoka kwa Yesu katika nasaba ya Mfalme Daudi. Kwa wazi, dai hilo halikuweza kukanushwa. Bila shaka kwa ajili ya masimulizi yao, Mathayo na Luka walinakili moja kwa moja kutoka rekodi za umma, yale majina yaliyohitajiwa ili kuthibitisha nasaba ya Yesu.
5 Ya pili, vyanzo nje ya Biblia huhakikisha kule kukubali kwa watu wengi ukoo wa Yesu. Kwa mfano, Talmudi hurekodi rabi wa karne ya nne akimshutumu Mariamu, mama ya Yesu, ‘kwa sababu ya kufanya ukahaba pamoja na maseremala’; lakini fungu lilo hilo hukubali kwamba “alikuwa mzao wa wana-wafalme na watawala.” Mfano wa mapema zaidi ni ule wa mwanahistoria wa karne ya pili Hegesippa. Alisimulia kwamba wakati Kaisari wa Roma Domishio alipotaka kuwakatalia mbali wazao wowote wa Daudi, baadhi ya maadui wa Wakristo wa mapema waliwashutumu wajukuu wa Yuda, ndugu-nusu wa Yesu, “kuwa wa familia ya Daudi.” Ikiwa Yuda alijulikana kuwa mzao wa Daudi, je, Yesu hakujulikana hivyo pia? Bila shaka ndivyo!—Wagalatia 1:19; Yuda 1.
Unabii Mwingi wa Kimesiya
6. Unabii mwingi wa Kimesiya ni mwingi kadiri gani katika Maandiko ya Kiebrania?
6 Sehemu nyingine ya uthibitisho wa kwamba Yesu alikuwa ndiye Mesiya ni unabii uliotimizwa. Unabii unaohusu Mesiya ni mwingi katika Maandiko ya Kiebrania. Katika kitabu chake The Life and Times of Jesus the Messiah, Alfred Edersheim aliorodhesha mafungu 456 katika Maandiko ya Kiebrania ambayo rabi wa kale waliona kuwa ya kimesiya. Hata hivyo, rabi hao walikuwa na mawazo mengi yasiyofaa juu ya Mesiya; mengi ya mafungu hayo waliyoelekezea si ya kimesiya hata kidogo. Hata hivyo, bado kuna unabii mwingi sana unaomtambulisha Yesu kuwa ndiye Mesiya.—Linganisha Ufunuo 19:10.
7. Ni baadhi ya unabii gani mwingi ambao Yesu alitimiza wakati wa muda wake mfupi duniani?
7 Miongoni mwao ni: mji wa kuzaliwa kwake (Mika 5:2; Luka 2:4-11); ule msiba wa uuaji wa vitoto vingi uliotukia baada ya kuzaliwa kwake (Yeremia 31:15; Mathayo 2:16-18); angeitwa kutoka Misri (Hosea 11:1; Mathayo 2:15); watawala wa mataifa wangeungana ili wamharibu (Zaburi 2:1, 2; Matendo 4:25-28); kusalitiwa kwake kwa vipande 30 vya fedha (Zekaria 11:12; Mathayo 26:15); hata namna ya kifo chake.—Zaburi 22:16, NW, kielezi-chini; Yohana 19:18, 23; 20:25, 27.c
Kuwasili Kwake Kwatolewa Unabii
8. (a) Ni unabii gani unaoelekezea wakati ambapo Mesiye angewasili? (b) Ni mambo gani mawili ambayo ni lazima yajulikane ili kuelewa unabii huo?
8 Acheni tukazie fikira unabii mmoja tu. Kwenye Danieli 9:25, NW, Wayahudi waliambiwa wakati ambapo Mesiya angekuja. Unasomwa hivi: “Nawe imekupasa kujua na kupata ufahamu kwamba tangu kutokea kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Mesiya yule Kiongozi, kutakuwako majuma saba, pia majuma sitini na mbili.” Mwanzoni unabii huo huenda ukaonekana kuwa wa kifumbo. Lakini kwa ujumla, unatuhitaji kutafuta visehemu viwili vya habari: mahali pa kuanzia na muda wa wakati. Kutoa mfano, ikiwa ulikuwa na ramani iliyoelekezea hazina iliyokuwa imezikwa yadi 275 upande wa mashariki wa kisima katika bustani ya starehe ya mji,” huenda ukaiona mielekezo hiyo kuwa yenye kutatanisha—hasa ikiwa hukujua mahali kisima hicho kilipokuwa, au urefu wa ‘yadi’ moja. Je! usingejaribu kupata kujua mambo hayo mawili ya hakika ili kwamba uweze kuipata hazina hiyo? Basi, unabii wa Danieli unafanana na jambo hilo kwa kadiri fulani, isipokuwa kwamba tunatafuta wakati wa kuanzia na kupima wakati unaofuata.
9, 10. (a) Ni wapi mahali pa kuanzia ambapo kutoka hapo majuma yale 69 huhesabiwa? (b) Yale majuma 69 yalikuwa na urefu gani, na tunajuaje hilo?
9 Kwanza, tunahitaji mahali petu pa kuanzia, tarehe ambayo ‘lile neno lilitokea kurudisha na kujenga upya Yerusalemu.’ Halafu, tunahitaji kujua urefu wa wakati kutoka mahali hapo, kupata kujua urefu hasa wa yale majuma 69 (jumla ya 7 na 62). Si vigumu kupata visehemu hivyo viwili vya habari. Nehemia atuambia waziwazi sana kwamba lile neno lilitokea ili kujenga upya ule ukuta uliozunguka Yerusalemu, likilifanya hatimaye kuwa jiji lililorudishwa, “mwaka wa ishirini wa mfalme Artashasta.” (Nehemia 2:1, 5, 7, 8) Hilo laweka mahali petu pa kuanzia katika 455 K.W.K.d
10 Sasa kwa habari ya majuma hayo 69, je, yangeweza kuwa majuma halisi ya siku saba? La, kwani Mesiya hakutokea punde tu baada ya muda wa mwaka mmoja baada ya 455 K.W.K. Hivyo wanachuo wengi wa Biblia na tafsiri nyingi (kutia na ile Tanakh ya Kiyahudi katika kielezi-chini cha mstari huo) hukubali kwamba hayo ni majuma “ya miaka.” Wazo hilo la ‘juma la miaka,’ au mrudio wa miaka saba, lilijulikana kwa Wayahudi wa zamani. Kama vile walivyoadhimisha siku ya sabato kila siku saba, waliadhimisha mwaka wa sabato kila mwaka wa saba. (Kutoka 20:8-11; 23:10, 11) Kwa hiyo majuma 69 ya miaka yangejumuika kuwa miaka 7 mara 69, au miaka 483. Lile tunalobaki nalo tu la kufanya ni kuhesabu. Kutoka 455 K.W.K., kuhesabu miaka 483 kunatupeleka hadi mwaka 29 W.K.—mwaka hasa ambao Yesu alibatizwa akawa ma·shiʹach, Mesiya!—Ona “Majuma Sabini,” Insight on the Scriptures, Buku 2, ukurasa 899.
11. Twaweza kuwajibuje wale wasemao kwamba hiyo ni njia ya ki-siku-hizi tu ya kufasiri unabii wa Danieli?
11 Wengine huenda wakapinga kwamba hiyo ni njia ya ki-siku-hizi tu ya kufasiri unabii huo ili upatane na historia. Ikiwa ndivyo, kwa nini watu katika siku ya Yesu walikuwa wakimtazamia Mesiya atokee wakati huo? Mwanahistoria Mkristo Luka, wanahistoria Waroma Tasito na Suetonio, mwanahistoria Myahudi Yosefo, na mwanafalsafa Myahudi Filo wote waliishi karibu na wakati huo wakashuhudia hali hiyo ya kutazamia. (Luka 3:15) Baadhi ya wanachuo leo husisitiza kwamba ni uonevu wa Kiroma uliowafanya Wayahudi watamani na kutazamia Mesiya katika siku hizo. Lakini, kwa nini Wayahudi walimtazamia Mesiya wakati huo badala ya wakati wa ule mnyanyaso wa Kigiriki wenye ukatili wa karne kadhaa mapema zaidi? Kwa nini Tasito alisema kwamba “unabii mwingi wa kifumbo” ndio uliowaongoza Wayahudi wawatazamie watawala wenye nguvu kuja kutoka Yudea na “kupata milki ya ulimwengu wote mzima”? Abba Hillel Silver, katika kitabu chake A History of Messianic Speculation in Israel, hukiri kwamba “Mesiya alitazamiwa wakati wa robo ya pili ya karne ya kwanza W.K.,” si kwa sababu ya mnyanyaso wa Kiroma, bali kwa sababu ya “orodha ya tarehe za matukio iliyojulikana sana ya siku hiyo,” iliyopatikana kwa sehemu kutoka katika kitabu cha Danieli.
Atambulishwa Kutoka Juu
12. Yehova alimtambulishaje Yesu kuwa ndiye Mesiya?
12 Aina ya tatu ya uthibitisho wa umesiya wa Yesu ni ule ushuhuda wa Mungu mwenyewe. Kulingana na Luka 3:21, 22, baada ya Yesu kubatizwa, alipakwa mafuta kwa kani iliyo takatifu na yenye nguvu zaidi katika ulimwengu wote mzima, roho takatifu ya Yehova Mungu mwenyewe. Na kwa sauti yake mwenyewe, Yehova alikiri kwamba alikuwa amemkubali Mwana wake, Yesu. Kwenye pindi nyinginezo mbili, Yehova alisema moja kwa moja na Yesu kutoka mbinguni, hivyo akionyesha kibali Chake: wakati mmoja, mbele ya mitume wa Yesu watatu, na wakati mwingine, mbele ya umati wa watazamaji. (Mathayo 17:1-5; Yohana 12:28, 29) Zaidi ya hayo, malaika walitumwa kutoka juu ili wathibitishe cheo cha Yesu kuwa ndiye Kristo, au Mesiya.—Luka 2:10, 11.
13, 14. Yehova alionyeshaje kumkubali kwake Yesu kuwa ndiye Mesiya?
13 Yehova alionyesha kumkubali kwake mpakwa-mafuta wake kwa kumpa uwezo wa kutimiza kazi kuu. Kwa mfano, Yesu alitamka unabii mwingi ulioeleza kimbele mambo madogo madogo ya historia—mengine yakifikia siku yetu wenyewe.e Alifanya miujiza pia, kama vile kuyalisha makutano yenye njaa na kuwaponya wagonjwa. Hata aliwafufua wafu. Je! wafuasi wake walibuni tu hadithi za vitendo hivyo vyenye nguvu baadaye? Yesu alifanya mingi ya miujiza yake mbele ya mashahidi wa kujionea wenyewe, nyakati nyingine kukiwa na maelfu ya watu kwa wakati mmoja. Hata maadui wa Yesu hawangeweza kukana kwamba hakufanya kwa hakika mambo hayo. (Marko 6:2; Yohana 11:47) Isitoshe, ikiwa wafuasi wa Yesu walikuwa na mwelekeo wa kubuni masimulizi ya jinsi hiyo, basi kwa nini walitaja waziwazi kasoro zao wenyewe? Kwa kweli, je, wangalikuwa na nia ya kufa kwa ajili ya imani yenye msingi wa ngano tu ambazo walikuwa wamezibuni wao binafsi? La. Miujiza ya Yesu ni mambo ya hakika ya historia.
14 Ushuhuda wa Mungu juu ya Yesu kuwa ndiye Mesiya ulionyeshwa zaidi. Kupitia roho takatifu alihakikisha kwamba uthibitisho wa Umesiya wa Yesu uliandikwa na ukawa sehemu ya kitabu chenye kutafsiriwa na kuenezwa zaidi katika historia yote.
Kwa Nini Wayahudi Hawakumkubali Yesu?
15. (a) Mathibitisho yanayomstahilisha Yesu yakimtambulisha kuwa Mesiya ni mengi kadiri gani? (b) Ni matazamio gani ya Wayahudi yaliyowaongoza wengi wamkatalie mbali Yesu kuwa Mesiya?
15 Kwa ujumla basi, sehemu hizo tatu za uthibitisho hutia ndani mamia ya mambo ya hakika yanayomtambulisha Yesu kuwa ndiye Mesiya. Je! hayo hayatoshi? Ebu wazia ukitoa ombi la kupata leseni ya kuwa dereva au la kupata hadi ya mkopo na unaambiwa kwamba visehemu vitatu vya utambulisho havitoshi—ni lazima ulete mamia yavyo. Hilo ni jambo lisilo la busara kama nini! Kwa hakika basi, Yesu anatambulishwa vya kutosha katika Biblia. Lakini, kwa nini watu wa Yesu mwenyewe walikanusha uthibitisho huo wote kwamba alikuwa ndiye Mesiya? Kwa sababu uthibitisho, ingawa ni wa maana sana kwa imani ya kweli, hauhakikishi kuwako kwa imani. Kwa kusikitisha, watu wengi huamini lile wanalotaka kuamini, hata kukiwa na uthibitisho mwingi sana. Kwa habari ya Mesiya, Wayahudi wengi walikuwa na mawazo hususa sana juu ya lile walilotaka. Walitaka mesiya wa kisiasa, ambaye angekomesha uonevu wa Kiroma na kurudisha Israeli kwenye utukufu uliofanana na ule wa siku za Sulemani kwa njia ya ufanisi wa kimwili. Kwa hiyo, wangeweza kumkubalije mwana huyo wa seremala aliye mnyenyekevu, huyo mtu wa Nazareti ambaye hakuonyesha kupendezwa hata kidogo na siasa au mali? Angewezaje hasa kuwa Mesiya baada ya yeye kuteseka na kufa kwa aibu kwenye mti wa mateso?
16. Kwa nini wafuasi wa Yesu walihitaji kuyarekebisha matazamio yao wenyewe kwa habari ya Mesiya?
16 Wanafunzi wa Yesu mwenyewe walifadhaishwa na kifo chake. Baada ya ufufuo wake mtukufu, wao kwa wazi walitumaini kwamba ‘angewarudishia Israeli ufalme’ wakati uo huo. (Matendo 1:6) Lakini hawakumkatalia mbali Yesu kuwa Mesiya kwa sababu tu tumaini hilo la kibinafsi halikutimizwa. Walizoea imani katika yeye kwa msingi wa uthibitisho wa kutosha uliopatikana, na uelewevu wao ukakua kidato kwa kidato; mafumbo yakafumbuliwa. Walikuja kuona kwamba Mesiya asingeweza kutimiza unabii wote juu yake katika wakati wake mfupi akiwa binadamu kwenye dunia hii. Kwani, unabii mmoja ulikuwa umesema juu ya kuwasili kwake kwa unyenyekevu, akiwa amepanda mwana-punda, hali mwingine ulikuwa umesema juu ya kuja kwake katika utukufu juu ya mawingu! Wote wa aina mbili ungewezaje kuwa kweli? Kwa wazi angehitaji kuja mara ya pili.—Danieli 7:13; Zekaria 9:9.
Sababu Kwa Nini Mesiya Alihitaji Kufa
17. Unabii wa Danieli ulieleweshaje wazi kwamba Mesiya angehitaji kufa, naye angekufa kwa sababu gani?
17 Zaidi ya hayo, unabii wa Kimesiya ulielewesha wazi kwamba Mesiya alihitaji kufa. Kwa mfano, ule unabii wenyewe uliotabiri wakati ambapo Mesiya angewasili ulitabiri hivi katika mstari ufuatao: “Na baada ya yale majuma sitini na mawili [yaliyofuata yale majuma saba], masihi atakatiliwa mbali.” (Danieli 9:26) Neno la Kiebrania ka·rathʹ linalotumiwa hapo kuwa ‘kukatilia mbali’ ni neno lilelile linalotumiwa katika hukumu ya kifo chini ya Sheria ya Musa. Bila shaka ilikuwa ni lazima Mesiya afe. Kwa nini? Mstari wa 24 hutupa sisi jibu: “Ili kukomesha makosa, na kuishiliza dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya uovu, na kuleta haki ya milele.” Wayahudi walijua vema kwamba dhabihu tu, yaani kifo, kingeweza kupatanisha kosa.—Mambo ya Walawi 17:11; linganisha Waebrania 9:22.
18. (a) Isaya sura 53 huonyeshaje kwamba ni lazima Mesiya ateseke na kufa? (b) Unabii huo hutokeza jambo gani linaloonekana kuwa la kinyume?
18 Isaya sura 53 husema juu ya Mesiya kuwa Mtumishi wa Yehova wa pekee ambaye ilikuwa lazima ateseke na kufa ili kufunika dhambi za wengine. Mstari 5 husema hivi: “Alijeruhiwa kwa makosa yetu, alichubuliwa kwa maovu yetu.” Unabii uo huo, baada ya kutuambia kwamba ni lazima Mesiya huyo afe akiwa “toleo la hatia,” hufunua kwamba Mtu uyo huyo “atarefusha siku zake, na katika mkono wake lile lililo penzi la Yehova litafanikiwa.” (Mstari 10, NW) Je, hilo si jambo la kinyume? Mesiya angewezaje kufa na kisha ‘kurefusha siku zake’? Angewezaje kutolewa akiwa dhabihu na baadaye kufanya ‘lile lililo penzi la Yehova lifanikiwe’? Angewezaje kwa kweli kufa na kubaki mfu bila kutimiza ule unabii mwingi wenye maana zaidi kumhusu yeye, yaani kwamba angetawala milele akiwa Mfalme na kuletea ulimwengu mzima amani na furaha?—Isaya 9:6, 7.
19. Ufufuo wa Yesu hupatanishaje ule unabii mwingi kumhusu Mesiya unaoonekana kupingana?
19 Jambo hilo linaloonekana kuwa la kinyume lilisuluhishwa kwa muujiza mmoja wenye kutazamisha. Yesu alifufuliwa. Mamia ya Wayahudi wenye mioyo minyoofu walikuwa mashahidi wa kujionea wenyewe jambo hilo halisi lenye utukufu. (1 Wakorintho 15:6) Mtume Paulo aliandika hivi baadaye: “Huyu [Yesu Kristo], alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake.” (Waebrania 10:10, 12, 13) Naam, ilikuwa baada ya Yesu kufufuliwa kwenye uhai wa kimbingu, na baada ya kipindi cha ‘kungojea,’ kwamba hatimaye angetawazwa kuwa Mfalme na kutenda dhidi ya maadui wa Baba yake, Yehova. Katika daraka lake akiwa Mfalme wa kimbingu, Yesu Mesiya huathiri maisha ya kila mtu anayeishi sasa. Katika njia gani? Makala yetu ifuatayo itazungumzia hilo.
[Maelezo ya Chini]
a Luka 3:23 linaposema: “Yusufu, [mwana, NW] wa Eli,” hilo kwa wazi lamaanisha “mwana” katika maana ya “mwana mkwe,” kwani Eli alikuwa baba ya asili wa Mariamu.—Insight on the Scriptures, Buku 1, kurasa 913-17.
b Mwanahistoria Myahudi Yosefo, alipokuwa akitoa habari za ukoo wake mwenyewe, huonyesha waziwazi kwamba rekodi hizo zilipatikana kabla ya 70 W.K. Yaonekana rekodi ziliharibiwa pamoja na jiji la Yerusalemu, ikifanya madai yote ya Umesiya yaliyofuata yasiweze kuthibitishwa.
c Ona Insight on the Scriptures, Buku 2, ukurasa 387.
d Kuna uthibitisho imara kutoka kwa vyanzo vya kale vya Kigiriki, Kibabuloni, na Kiajemi, unaoonyesha kwamba mwaka wa kwanza wa utawala wa Artashasta ulikuwa 474 K.W.K. Ona Insight on the Scriptures, Buku 2, kurasa 614-16, 900.
e Katika mmoja kati ya unabii huo mwingi yeye, alitabiri kwamba mesiya bandia wangetokea kuanzia siku yake na kuendelea. (Mathayo 24:23-26) Ona makala iliyotangulia.
Ungejibuje?
◻ Kwa nini uchunguze uthibitisho juu ya kama Yesu ndiye Mesiya aliyeahidiwa?
◻ Ukoo wa Yesu huungaje mkono Umesiya wake?
◻ Unabii mwingi wa Biblia husaidiaje kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa ndiye Mesiya?
◻ Yehova alithibitisha kibinafsi kwa njia zipi kwamba Yesu alikuwa ndiye Mesiya?
◻ Kwa nini Wayahudi wengi walimkatalia mbali Yesu kuwa Mesiya, na kwa nini sababu hizo hazikufaa?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Kila mmoja wa ile miujiza mingi ya Yesu ulitokeza uthibitisho zaidi wa Umesiya wake