Wewe Huonaje Dhambi?
“KWA nini yeye huendelea kuomba msamaha wa dhambi zetu katika sala?” akalalamika mke wa nyumbani mmoja aliyekuwa akijifunza Biblia pamoja na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. “Inasikika kana kwamba mimi ni mhalifu.” Sawa na mwanamke huyo, wengi leo hawatambui dhambi zao isipokuwa iwe wametenda uhalifu.
Hilo ni kweli hasa katika nchi za Mashariki, ambako kimapokeo watu hawana wazo lolote kuhusu dhambi iliyorithiwa kama ifundishwavyo katika dini za Kiyahudi na Kikristo. (Mathayo 3:1-5, 16-19; Warumi 5:12) Kwa kielelezo, wafuasi wa Dini ya Shinto huhusianisha dhambi na uchafu ambao waweza kufutwa mbali kwa urahisi kwa mzungusho mmoja wa fimbo ya kuhani, iliyofungiwa karatasi au katani kwenye ncha yayo. Katika taratibu hiyo, hakuna toba yoyote inayohitajiwa kwa lile lililotendwa. Kwa nini? “Si vitendo viovu tu, bali pia misiba ya asili isiyoweza kudhibitika, iliitwa tsumi [dhambi],” yaeleza Kodansha Encyclopedia of Japan. Misiba ya asili, tsumi zisizosababishwa na watu, ilionwa kuwa dhambi ambazo sherehe za utakasaji zilizifanya zikome zisiwepo tena.
Hilo liliongoza kwenye kufikiri kwamba dhambi yoyote, hata matendo maovu yaliyofanywa kimakusudi (isipokuwa matendo ya uhalifu yaliyostahili kuadhibiwa kisheria) yaliweza kufutwa mbali na sherehe za utakasaji. Chini ya kichwa “Desturi ya Usafishaji wa Kisiasa Katika Japani,” The New York Times lilitaja fikira hiyo kisha likaeleza kwamba wanasiasa katika Japani ambao wamehusika katika mambo ya aibu hujiona wenyewe kuwa “wametakaswa” wanapochaguliwa tena na wapiga kura. Hivyo, hakuna usahihisho wowote wa kweli unaofanywa, na mambo ayo hayo ya aibu yaweza kutukia tena.
Wafuasi wa Dini ya Buddha wanaoamini katika samsara, au kuzaliwa tena, na fundisho la Karma wana maoni tofauti. “Kulingana na fundisho la karman,” yaeleza The New Encyclopœdia Britannica, “mwenendo mzuri huleta tokeo zuri na lenye furaha na hutokeza mbetuko kuelekea matendo mazuri kama hayo, hali mwenendo mbaya huleta tokeo ovu na hutokeza mbetuko kuelekea matendo maovu yenye kurudiwa-rudiwa.” Yaani, mwenendo wenye dhambi hutokeza matunda mabaya. Fundisho la Karma linahusiana na fundisho la kuzaliwa tena, kwani inasemwa kwamba baadhi ya Karma hutokeza matunda katika maisha ya wakati ujao ya kipindi chenye kuachana sana na maisha ambamo tendo hilo lilifanywa.
Fundisho hilo linaathirije waamini walo? Mwanamke mmoja mfuasi wa Dini ya Buddha ambaye kwa moyo mweupe aliamini Karma alisema hivi: “Nilifikiri halikuwa jambo la kiakili kulazimika kuteseka kwa ajili ya jambo fulani nililozaliwa nalo lakini ambalo sikujua lolote juu yalo. Nililazimika kuikubali kuwa ajali yangu. Kukariri sutra na kujitahidi sana kuishi maisha mazuri hakukusuluhisha matatizo yangu. Nikawa mwenye ugomvi na mwenye kutoridhika, nikilalamika sikuzote.” Fundisho la Dini ya Buddha juu ya matokeo ya mwenendo mwovu lilimwacha akihisi hafai kitu.
Dini ya Confucius, ambayo ni dini nyingine ya Mashariki, ilifundisha njia tofauti ya kushughulikia uovu wa kibinadamu. Kulingana na Hsün-tzu, mmoja wa wanafalsafa watatu wakuu wa Dini ya Confucius, asili ya kibinadamu ni ovu na yenye mwelekeo wa kuwa na ubinafsi. Ili kudumisha utaratibu wa kijamii miongoni mwa watu wenye mbetuko ya dhambi, alikazia umaana wa li, linalomaanisha ufaaji, uungwana, na utaratibu wa mambo. Meng-tzu, mwanafalsafa mwingine wa Dini ya Confucius, ingawa alionyesha maoni ya kinyume juu ya asili ya kibinadamu, alitambua kuwako kwa maovu ya kijamii na, akitumaini asili ya watu kuwa nzuri, alitegemea kujifanyia maendeleo ya kibinafsi kuwa ndilo suluhisho la hilo. Kwa vyovyote vile, wanafalsafa wa Dini ya Confucius walifundisha umaana wa elimu na mazoezi ili kupingana na dhambi ulimwenguni. Ingawa mafundisho yao hukubaliana na umuhimu wa li, wazo lao la dhambi na uovu haliko dhahiri hata kidogo.—Linganisha Zaburi 14:3; 51:5.
Wazo la Dhambi Lenye Kufifia Katika Magharibi
Katika Magharibi, maoni kuhusu dhambi yamekuwa ya wazi kabisa kimapokeo, na watu wengi wamekubali kwamba dhambi iko na yapasa kuepukwa. Hata hivyo, mtazamo wa upande wa Magharibi kuelekea dhambi unabadilika. Wengi hukatalia mbali ufahamu wowote wa dhambi, wakiita sauti ya dhamiri “hisia ya hatia,” jambo lipasalo kuepukwa. Zaidi ya miaka 40 iliyopita, Papa Pius 12 aliomboleza hivi: “Dhambi ya karne hii ni kule kupoteza utambuzi wote wa dhambi.” Kulingana na uchunguzi uliotangazwa kwa chapa katika Le Pèlerin la Kikatoliki la kila juma, asilimia 90 yenye kushangaza ya wakaaji wa Ufaransa, ambako watu wengi hudai kuwa Wakatoliki ya Kiroma, hawaamini dhambi tena.
Kwa kweli, Mashariki na Magharibi, sasa yaonekana watu wengi wanaishi katika uradhi uliostareheka bila kusumbuliwa na utambuzi wa dhambi. Hata hivyo, je, hilo lamaanisha kwamba dhambi haiko? Je! twaweza kuipuuza kusiwe dhara? Je! kuna wakati dhambi itatoweka?