Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 12/15 kur. 8-13
  • Yehova, Mfanyi wa Mambo ya Ajabu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova, Mfanyi wa Mambo ya Ajabu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwenye Kuteseka Lakini Mwaminifu-Mshikamanifu
  • Ukaribu na Yehova
  • Wema wa Yehova
  • Kazi za Yehova Zisizoweza Kulinganishwa
  • Ukuu wa Yehova
  • Kutembea kwa Moyo Ulioungamanishwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Yehova Astahili Sifa ya Milele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Ni Nani Atakayemsifu Mfalme?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Yehova Ni Mfano Bora Sana wa Wema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 12/15 kur. 8-13

Yehova, Mfanyi wa Mambo ya Ajabu

“Wewe ni mkuu na unafanya mambo ya ajabu; wewe ndiye Mungu, wewe peke yako.”—ZABURI 86:10 “NW.”

1, 2. (a) Vitu ambavyo mwanadamu amebuni vimeathirije ulimwengu? (b) Ni wapi tuwezapo kupata tumaini la mambo yaliyo bora zaidi?

MWANADAMU wa ki-siku-hizi huenda akajivuna kwamba vitu ambavyo amebuni ni vya ajabu—vyombo vya stimu, mawasiliano ya simu, vidio, magari, kusafiri kwa ndege, na tekinolojia ya kompyuta. Vitu hivyo vimegeuza ulimwengu kuwa ujirani mmoja. Lakini huo ni ujirani ulioje! Badala ya amani, ufanisi, na wingi kwa wote, ainabinadamu imekumbwa na vita vikatili, uhalifu, uharamia, uchafuzi, magonjwa, na umaskini. Na silaha za nyukilia zilizotawanyika kotekote ulimwenguni, ingawa idadi zao zimepunguzwa, zingeweza bado kuiangamiza jamii ya kibinadamu. Wauza kifo, wafanyiza silaha, huendelea kuendesha biashara iliyo kubwa zaidi duniani. Matajiri wanazidi kuwa matajiri, na maskini wanazidi kuwa maskini. Je! yeyote aweza kupata suluhisho?

2 Ndiyo! Kwa kuwa kuna Mtu Fulani anayehakikisha ukombozi, “aliye juu kuliko walio juu,” Yehova Mungu. (Mhubiri 5:8) Alipulizia uandikaji wa zaburi, zinazoandaa faraja nyingi na shauri lenye hekima kwa nyakati za taabu. Miongoni mwao ni Zaburi 86, yenye maandishi ya juu haya sahili (katika NW): “Sala ya Daudi.” Hiyo ni sala uwezayo kufanya iwe yako mwenyewe.

Mwenye Kuteseka Lakini Mwaminifu-Mshikamanifu

3. Katika nyakati hizi, Daudi anatuandalia kielelezo gani chenye kutia moyo?

3 Daudi aliandika zaburi hii alipokuwa akiteseka. Sisi leo, tunaoishi kupitia “siku za mwisho” za mfumo wa Shetani, “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” tunakabili majaribu kama hayo. (2 Timotheo 3:1, NW; ona pia Mathayo 24:9-13.) Kama vile sisi, Daudi alipatwa na wasiwasi na mshuko wa moyo kwa sababu ya matatizo yaliyomwathiri. Lakini hakuruhusu kamwe majaribu hayo yadhoofishe tumaini lake lenye uaminifu-mshikamanifu katika Muumba wake. Alipaza sauti hivi: “Elekeza sikio lako, Ee Yehova. Unijibu, kwa sababu mimi ni mwenye kuteseka na ni maskini. Ee na uilinde nafsi yangu, kwa sababu mimi ni mwaminifu-mshikamanifu. Mwokoe mtumishi wako—wewe ndiye Mungu wangu—anayeamini katika wewe.”—Zaburi 86:1, 2, NW.

4. Twapaswa kuonyeshaje uhakika wetu?

4 Tunaweza kuwa na uhakika, kama Daudi alivyokuwa na uhakika, kwamba “Mungu wa faraja yote,” Yehova, ataligeuza sikio lake kuelekea dunia hii na kusikiliza sala zetu zenye unyenyekevu. (2 Wakorintho 1:3, 4) Tukimtumaini Mungu wetu kabisa, twaweza kufuata shauri hili la Daudi: “Umtwike BWANA [Yehova, NW] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”—Zaburi 55:22.

Ukaribu na Yehova

5. (a) Tafsiri nyinginezo zenye uangalifu zimerekebishaje makosa ya waandishi Wayahudi? (b) Zaburi ya 85 na ya 86 humtukuza Yehova katika njia gani? (Ona kielezi-chini.)

5 Katika Zaburi ya 86, NW, Daudi hutumia msemo “Ee Yehova” mara 11. Sala ya Daudi ni yenye bidii kama nini na ukaribu wake na Yehova ni wa karibu kama nini! Baadaye, utumizi wa jina la Yehova wenye ukaribu jinsi hiyo ulikuja kuwachukiza waandishi Wayahudi, hasa Wasoferi. Walikuza hofu ya kishirikina ya kutumia vibaya jina hilo. Wakipuuza uhakika wa kwamba mwanadamu alikuwa ameumbwa kwa mfano wa Mungu, walikataa kumhesabia Mungu sifa ambazo wanadamu huonyesha pia. Kwa hiyo katika 7 kati ya mara 11 ambazo jina la Mungu linatokea katika maandishi-awali ya Kiebrania ya zaburi hiyo, waliweka jina la cheo ʼAdho-naiʹ (Bwana) mahali pa jina YHWH (Yehova). Twaweza kuwa na shukrani kwamba New World Translation of the Holy Scriptures, pamoja na tafsiri nyinginezo kadhaa zenye uangalifu, zimerudisha jina la Mungu kwenye mahali palo pafaapo katika Neno la Mungu. Likiwa tokeo, uhusiano wetu na Yehova unakaziwa kama upasavyo kukaziwa.a

6. Tunaweza kuonyesha katika njia zipi kwamba jina la Yehova ni lenye thamani kwetu?

6 Sala ya Daudi yaendelea hivi: “Unionyeshe upendeleo, Ee Yehova, kwa sababu mimi huendelea kukuitia mchana kutwa. Uifanye nafsi ya mtumishi wako ishangilie, kwa sababu kwako, Ee Yehova, ninainua nafsi yangu yenyewe.” (Zaburi 86:3, 4, NW) Ona kwamba Daudi aliendelea kumwitia Yehova “mchana kutwa.” Kwa kweli, alisali mara nyingi usiku kucha, kama vile wakati ule alipokuwa mtoro jangwani. (Zaburi 63:6, 7) Vivyo hivyo leo, baadhi ya Mashahidi wanapotishwa na kulalwa kinguvu au na shambulio jingine la kihalifu wamemlilia Yehova kwa sauti kubwa. Nyakati nyingine wameshangaa kwa ajili ya tokeo lenye kufurahisha.b Jina la Yehova ni lenye thamani kubwa kwetu, hata kama lilivyokuwa kwa “Yesu Kristo, mwana wa Daudi,” alipokuwa duniani. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kusali kwa ajili ya utakaso wa jina la Yehova na aliwajulisha maana ya jina hilo.—Mathayo 1:1; 6:9; Yohana 17:6, 25, 26.

7. Tuna vielelezo gani vya kuinua kwa Yehova nafsi yenyewe ya watumishi wake, na twapaswa kuitikiaje?

7 Daudi alimwinulia Yehova nafsi yake, alijiinua mwenyewe kikamili. Anatutia moyo tufanye vivyo hivyo, akisema hivi kwenye Zaburi 37:5: “Umkabidhi BWANA [Yehova, NW] njia yako, pia umtumaini, naye atafanya.” Hivyo ombi letu kwa Yehova ili afanye nafsi yetu ishangilie halitakaa bila kujibiwa. Watumishi wengi wa Yehova wenye kushika uaminifu-maadili huendelea kupata shangwe kubwa katika utumishi wake—yajapokuwa magumu, minyanyaso, na maradhi. Ndugu zetu katika maeneo yenye vita katika Afrika, kama vile Angola, Liberia, Msumbiji, na Zaire, wameendelea kuweka utumishi wa Yehova kwanza maishani mwao.c Kwa kweli amewasababisha washangilie katika mavuno mengi ya kiroho. Kama vile ambavyo wamevumilia, ni lazima sisi pia tuvumilie. (Warumi 5:3-5) Na tuvumiliapo, tunahakikishiwa: “Njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake . . . haitakawia [haitachelewa, NW].” (Habakuki 2:3) Kwa uhakika na tumaini kamili katika Yehova, sisi pia na ‘tufanye haraka ili kuufikilia mwisho.’

Wema wa Yehova

8. Twaweza kuwa na ukaribu gani na Yehova, na yeye ameonyeshaje wema wake?

8 Daudi atoa ombi jingine lenye kuhisiwa moyoni: “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na tayari kusamehe; na fadhili-upendo kwa wale wote wanaokuitia ni nyingi. Sikiliza, Ee Yehova, sala yangu; na uelekezee fikira sauti za haja zangu. Katika siku ya taabu yangu nitakuitia, kwa kuwa utanijibu.” (Zaburi 86:5-7, NW) “Ee Yehova”—tena na tena tunasisi-muliwa na ukaribu wa msemo huo! Huo ni ukaribu uwezao kusitawishwa daima kupitia sala. Daudi alisali hivi pindi nyingine: “Usiyakumbuke makosa ya ujana wangu, wala maasi yangu. Unikumbuke kwa kadiri ya fadhili [fadhili-upendo, NW] zako, Ee BWANA [Yehova, NW], kwa ajili ya wema wako.” (Zaburi 25:7) Yehova ndiye kielelezo bora kabisa cha wema—kwa kuandaa fidia ya Yesu, kwa kuonyesha rehema kwa watenda dhambi wenye kutubu, na kwa kuwamiminia fadhili-upendo Mashahidi wake waaminifu-washikamanifu na wenye kuthamini.—Zaburi 100:3-5; Malaki 3:10.

9. Watenda dhambi wenye kutubu wanapaswa wafikirie kwa uzito uhakikishio gani?

9 Je! tunapaswa kusumbuliwa na makosa ya zamani? Ikiwa sasa tunaifanyia miguu yetu vijia vilivyonyooka, tunachangamshwa tunapokumbuka uhakikishio wa mtume Petro kwa wale waliotubu wa kwamba “nyakati za kuburudishwa” zitatoka kwa Yehova. (Matendo 3:19) Acheni tuendelee kuwa karibu na Yehova katika sala kupitia Mwenye Kutufidi, Yesu, aliyesema hivi kwa upendo: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha [mtapata burudisho kwa nafsi zenu, NW].” Mashahidi waaminifu-washikamanifu wanaposali kwa Yehova leo katika jina la Yesu lenye thamani kubwa, wao kwa kweli hupata burudisho.—Mathayo 11:28, 29; Yohana 15:16.

10. Kitabu cha Zaburi kinatolea fadhili-upendo za Yehova umashuhuri gani?

10 Kitabu cha Zaburi kinarejezea “fadhili-upendo” za Yehova zaidi ya mara mia moja. Fadhili-upendo hizo kwa hakika ni nyingi! Katika mistari yayo minne ya kwanza, Zaburi ya 118, NW, huwasihi watumishi wa Mungu wamshukuru Yehova, ikirudia mara nne, “kwa sababu fadhili-upendo zake ni kwa wakati usiojulikana.” Zaburi ya 136, NW, hukazia ile sifa yenye kupendekeza ya “fadhili-upendo zake” mara 26. Iwe tunakosea katika njia zipi—na kama vile Yakobo 3:2 lisemavyo, “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi”—na tuwe tayari kutafuta msamaha wa Yehova, tukiwa na uhakika juu ya rehema na fadhili-upendo zake. Fadhili-upendo zake ni wonyesho wa upendo wake mwaminifu-mshikamanifu kuelekea sisi. Tukiendelea kufanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu, yeye ataonyesha upendo wake mwaminifu-mshikamanifu kwa kutuimarisha tukabiliane na kila jaribu.—1 Wakorintho 10:13.

11. Utendaji wa wazee unaweza kusaidiaje kuondoa hisia za hatia?

11 Huenda kukawa pindi ambazo tunakwazwa na wengine. Kutendwa vibaya kihisiamoyo au kimwili wakati wa utoto kumewaacha wengine wakiwa na hisia za hatia au za kutofaa kitu kabisa. Mtu aliyetendwa hivyo aweza kumwitia Yehova, akiwa na uhakika kwamba atamjibu. (Zaburi 55:16, 17) Mzee mwenye fadhili aweza kuonyesha kupendezwa na kumsaidia mtu kama huyo akubali uhakika wa kwamba hilo halikuwa kosa la mwenye kutendwa hivyo. Baadaye, mzee akimpigia simu ya kirafiki mara kwa mara hiyo yaweza kumsaidia mtu huyo aweze hatimaye ‘kuuchukua mzigo.’—Wagalatia 6:2, 5.

12. Taabu zimeongezekaje, lakini tunaweza kukabilianaje nazo kwa mafanikio?

12 Kuna hali nyinginezo nyingi zenye kutaabisha ambazo watu wa Yehova wamelazimika kung’ang’ana nazo leo. Tangu Vita ya Ulimwengu 1 katika 1914, maafa makuu yalianza kuikumba dunia hii. Kama ilivyotabiriwa na Yesu, huo ulikuwa “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu.” Taabu zimeongezeka kadiri tumeendelea kuingia “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, 8, NW) “Wakati mchache” wa Ibilisi unapungua kuelekea mwisho wao wa upeo. (Ufunuo 12:12) “Kama simba angurumaye” akitafuta mawindo, Adui huyo mkubwa anatumia kila hila ipatikanayo ili atutenganishe na kundi la kondoo la Mungu na kutuharibu. (1 Petro 5:8) Lakini hatafaulu! Kwani, kama vile Daudi, tunakaza tumaini letu kikamili katika Mungu wetu mmoja, Yehova.

13. Wazazi na watoto wao wanaweza kujinufaishaje kutokana na wema wa Yehova?

13 Bila shaka, Daudi alikazia kikiki moyoni mwa mwana wake Sulemani uhitaji wa kutegemea wema wa Yehova. Hivyo, Sulemani angeweza kumwagiza mwana wake mwenyewe hivi: “Mtumaini BWANA [Yehova, NW] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; mche BWANA [Yehova, NW], ukajiepushe na uovu.” (Mithali 3:5-7) Wazazi leo wanapaswa vilevile wawafundishe watoto wao wadogo jinsi ya kusali kwa kumtumaini Yehova na jinsi ya kukabiliana na mashambulio ya ulimwengu usio na huruma—kama vile mbano wa marika shuleni na vishawishi vya kutenda ukosefu wa maadili. Kuzoea kanuni za Biblia pamoja na watoto wetu kila siku kwaweza kukazia kwenye mioyo yao michanga upendo kwa Yehova na kumtegemea kwa sala.—Kumbukumbu la Torati 6:4-9; 11:18, 19.

Kazi za Yehova Zisizoweza Kulinganishwa

14, 15. Ni zipi baadhi ya kazi za Yehova zisizoweza kulinganishwa?

14 Akiwa na usadikisho wenye kina Daudi asema hivi: “Hakuna aliye kama wewe miongoni mwa miungu, Ee Yehova, wala hakuna kazi zozote zilizo kama zako.” (Zaburi 86:8, NW) Kazi za Yehova ni kuu zaidi, tukufu zaidi, zenye fahari zaidi, kuliko vile binadamu yeyote angeweza hata kuwazia. Kama vile sayansi ya ki-siku-hizi imepata kuona kifupi tu, ulimwengu wote mzima ambao umeumbwa—ukubwa wao, upatano wao, na uzuri wao wa ajabu—umethibitika kuwa wa ajabu mno kuliko chochote kile ambacho Daudi alifahamu. Hata hivyo, hata yeye alisukumwa kusema hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”—Zaburi 19:1.

15 Pia, kazi za Yehova zinaonyeshwa vizuri ajabu katika njia ambayo aliiweka na kuitayarisha dunia, akiandaa kwa ajili ya mchana na usiku, majira, wakati wa kupanda mbegu na kuvuna, na mapendezi mengine mengi kwa ajili ya furaha ya mwanadamu ya wakati ujao. Na sisi wenyewe tumefanywa vizuri ajabu kama nini na kupewa vifaa vya kutumia, ili tuweze kufurahia kazi za Yehova zinazotuzunguka!—Mwanzo 2:7-9; 8:22; Zaburi 139:14.

16. Wonyesho mkuu zaidi wa wema wa Yehova ni nini, ukiongoza kwenye kazi zipi zaidi zisizoweza kulinganishwa?

16 Baada ya wazazi wetu wa kwanza kutomtii Mungu, wakianzisha taabu ambazo zimeikumba dunia hadi siku ya leo, Yehova kwa ajili ya upendo wake alifanya kazi ya ajabu kwa kumtuma Mwana wake duniani ili apige mbiu ya Ufalme wa Mungu na kufa akiwa fidia kwa ajili ya ainabinadamu. Na ajabu kama nini! Kisha Yehova akamfufua Kristo kuwa Mfalme mwenzake aliyechaguliwa. (Mathayo 20:28; Matendo 2:32, 34) Kutoka katika wanadamu waaminifu-washikamanifu Mungu amechagua pia “uumbaji mpya” utakaotawala na Kristo ukiwa “mbingu mpya” wenye fadhili juu ya jamii ya “dunia mpya” itakayotia ndani mabilioni ya wanadamu waliofufuliwa. (2 Wakorintho 5:17; Ufunuo 21:1, 5-7, Habari Njema kwa Watu Wote; 1 Wakorintho 15:22-26) Kazi za Yehova zitasonga mbele hadi upeo mtukufu! Kwa kweli, twaweza kupaza sauti hivi: “Ee Yehova, . . . jinsi wema wako ulivyo mwingi, ambao umewawekea kama hazina wale wanaokuhofu!”—Zaburi 31:17-19, NW.

17. Kwa habari ya kazi za Yehova, Zaburi 86:9 inatimizwaje sasa?

17 Kazi za Yehova za siku hizi zinatia ndani yale ambayo Daudi anaeleza kwenye Zaburi 86:9, NW: “Mataifa yote ambayo umefanya yatakuja yenyewe, nayo yatakuinamia, Ee Yehova, na kulipa jina lako utukufu.” Baada ya kuita kutoka miongoni mwa ainabinadamu wale waliobaki wa uumbaji wake mpya, lile “kundi dogo” la warithi wa Ufalme, Yehova ameendelea kukusanya kutoka miongoni mwa “mataifa yote” “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine,” mamilioni ambayo pia huzoea imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa. Amewajenga hao kuwa tengenezo lenye bidii, jamii pekee ya duniani pote ya wapendao amani duniani leo. Wakiona hayo, malaika wanamsujudia Yehova, wakijulisha wazi hivi: “Baraka na utukufu na hekima na utoaji shukrani na heshima na nguvu na imara ziwe kwa Mungu wetu milele na milele.” Ule mkutano mkubwa pia unalitukuza jina la Yehova, ukimtumikia “mchana na usiku,” ukiwa na tumaini la kuokoka mwisho wa ulimwengu huu na kuishi milele juu ya dunia-paradiso.—Luka 12:32; Ufunuo 7:9-17, NW; Yohana 10:16.

Ukuu wa Yehova

18. Yehova ameonyeshaje kwamba yeye ndiye ‘Mungu peke yake’?

18 Kisha Daudi aelekeza fikira kwenye Uungu wa Yehova, akisema hivi: “Wewe ni mkuu na unafanya mambo ya ajabu; wewe ndiye Mungu, wewe peke yako.” (Zaburi 86:10, NW) Tangu zamani, Yehova amekuwa akionyesha kwamba yeye, kwa kweli, ni ‘Mungu peke yake.’ Farao wa Misri mdhalimu ndiye aliyempinga Musa kwa ukaidi hivi: “BWANA [Yehova, NW] ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui BWANA [Yehova, NW].” Lakini upesi alikuja kujifunza jinsi Yehova alivyo mkuu! Mungu mweza yote alivitahayarisha vijimungu na makuhani wazoeao uchawi wa Misri kwa kupeleka mapigo yenye kuleta msiba mkuu, akiwaua wana wazaliwa wa kwanza wa Misri, na kuharibu Farao na jeshi lake bora katika Bahari Nyekundu. Kwa kweli, hakuna yeyote aliye kama Yehova miongoni mwa miungu!—Kutoka 5:2; 15:11, 12.

19, 20. (a) Wimbo wa Ufunuo 15:3, 4 utafikia upeo wao mtukufu wakati gani? (b) Sisi twaweza kushirikije hata sasa katika kazi ya Yehova?

19 Akiwa Mungu peke yake, Yehova ameendelea kufanya mambo ya ajabu katika kuwaandalia ukombozi waabudu wake watiifu kutoka katika Misri ya ki-siku-hizi—ulimwengu wa Shetani. Amewezesha hukumu zake za kimungu zipigwe mbiu duniani pote zikiwa ushahidi kupitia kampeni ya kuhubiri yenye kuenea zaidi katika historia, hivyo akitimiza unabii wa Yesu kwenye Mathayo 24:14. Hivi karibuni, ni lazima “mwisho” uje, wakati Yehova atakapooneysha ukuu wake kwa kadiri isiyo na kifani kwa kufutilia mbali uovu wote duniani. (Zaburi 145:20) Ndipo wimbo wa Musa na wimbo wa Mwana-Kondoo utakapofikia upeo huu: “Kubwa na za ajabu ni kazi zako, Yehova Mungu, Mweza Yote. Za uadilifu na za kweli ni njia zako, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatahofu wewe, Yehova, na kutukuza jina lako, kwa sababu wewe pekee ni mwaminifu-mshikamanifu?”—Ufunuo 15:3, 4, NW.

20 Kwa upande wetu sisi na tuwe na bidii katika kuongea na wengine juu ya makusudi hayo mazuri ajabu ya Mungu. (Linganisha Matendo 2:11.) Yehova ataendelea kufanya mambo makuu na ya ajabu katika siku yetu na hadi katika wakati ujao, kama vile makala yetu ifuatayo itakavyoeleza.

[Maelezo ya Chini]

a Ufafanuzi mmoja wa Biblia wa 1874 humnukuu Andrew A. Bonar kuwa akisema: “Sifa ya Mungu ya pekee, jina lake tukufu, limefunuliwa kwa wingi, sana sana, katika mwisho-mwisho wa zaburi ya mwisho [ya 85]. Hiyo yaweza kuwa sababu kwa nini inafuatwa na nyingine, ‘Sala ya Daudi,’ ambayo imejaa vivyo hivyo na sifa ya Yehova. Habari ya msingi ya Zaburi hii [ya 86] ni jina la Yehova.”

b Ona ukurasa 28 wa Amkeni! (Kiingereza) Juni 22, 1984 lililotangazwa na Watchtower and Tract Society of New York, Inc.

c Kwa habari zaidi, ona ile chati “Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1992 wa Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote,” itakayotokea katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1993.

Je! Unakumbuka?

◻ Kwa nini tuifanye sala ya Zaburi 86 iwe yetu wenyewe?

◻ Tunaweza kupataje ukaribu na Yehova?

◻ Yehova hutuonyeshaje wema wake?

◻ Ni zipi baadhi ya kazi za Yehova zisizoweza kulinganishwa?

◻ Kuhusiana na ukuu, Yehova ndiye ‘Mungu peke yake’ kwa jinsi gani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Katika “dunia mpya” inayokuja, kazi za ajabu za Yehova zitashuhudiza utukufu na wema wake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki