Jilinde na Ibada ya Sanamu ya Kila Aina
“Pana mapatano gani kati ya hekalu ya Mungu na sanamu?”—2 WAKORINTHO 6:16.
1. Ni nini lililofananishwa na tabenakulo na mahekalu ya Israeli?
YEHOVA ana hekalu ambalo halina sanamu. Lilifananishwa na tabenakulo la Israeli lililojengwa na Musa na mahekalu yaliyojengwa baadaye katika Yerusalemu. Majengo hayo yaliwakilisha “ile hema ya kweli,” hekalu kuu la kiroho la Yehova. (Waebrania 8:1-5) Hekalu hilo ni mpango wa kumkaribia Mungu katika ibada kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo.—Waebrania 9:2-10, 23.
2. Ni nani wanaokuwa nguzo katika hekalu kuu la kiroho la Mungu, na mkutano mkubwa unafurahia msimamo gani?
2 Kila Mkristo mpakwa-mafuta anakuwa “nguzo katika hekalu la Mungu,” akipokea mahali mbinguni. “Mkutano mkubwa” wa waabudu wengine wa Yehova ‘unatoa utumishi mtakatifu wa Mungu,’ NW, katika mahali palipofananishwa na ua wa Wasio Wayahudi kwenye hekalu lililojengwa upya na Herode. Kwa sababu ya imani katika dhabihu ya Yesu, wana msimamo mwadilifu unaotokeza uhifadhi kupitia “dhiki ile iliyo kuu.”—Ufunuo 3:12; 7:9-15.
3, 4. Kundi la Wakristo wapakwa-mafuta duniani linafananishwa na nini, nalo lapasa liwe huru na uchafuzi gani?
3 Kundi la Wakristo wapakwa-mafuta duniani linafananishwa pia kitamathali na hekalu jingine ambalo halina ibada ya sanamu. Kwa watu wa jinsi hiyo ‘waliotiwa muhuri na roho takatifu,’ mtume Paulo alisema hivi: “Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni. Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana. Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho.” (Waefeso 1:13; 2:20-22) Hao 144,000 waliotiwa muhuri ni “mawe yaliyo hai” ‘wanaojengwa wawe nyumba ya kiroho, ukuhani mtakatifu.’—1 Petro 2:5; Ufunuo 7:4; 14:1.
4 Kwa kuwa makuhani hao wa chini ni “jengo la Mungu,” yeye haruhusu hekalu hilo lichafuliwe. (1 Wakorintho 3:9, 16, 17) “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa,” akaonya Paulo. “Kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu?” Ni lazima Wakristo wapakwa-mafuta, ambao ni mali ya “Yehova Mweza Yote,” (NW) wasijihusishe na ibada ya sanamu. (2 Wakorintho 6:14-18) Ni lazima wale wa mkutano mkubwa pia waepuke ibada ya sanamu ya kila aina.
5. Wakitambua kwamba Yehova anastahili ujitoaji wa pekee, Wakristo wa kweli hufanya nini?
5 Kuna namna za ibada ya sanamu zenye kuonekana wazi sana na zile zilizofichika sana. La, ibada ya sanamu haihusu tu ibada ya vijimungu na vijimungu-vike bandia. Ni ibada kwa kitu chochote au mtu yeyote mwingine isipokuwa Yehova. Akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, yeye ataka na astahili ifaavyo ujitoaji wa pekee. (Kumbukumbu la Torati 4:24) Wakitambua hilo, Wakristo wa kweli hutii maonyo ya Kimaandiko dhidi ya ibada ya sanamu yote. (1 Wakorintho 10:7) Acheni tuchunguze namna fulani-fulani za ibada ya sanamu zipasazo kuepukwa na watumishi wa Yehova.
Ibada ya Sanamu ya Jumuiya ya Wakristo Yatangulia Kufananishwa
6. Ezekieli aliona machukizo gani katika njozi?
6 Alipokuwa uhamishoni katika 612 K.W.K., nabii Ezekieli alikuwa na njozi ya machukizo yaliyozoewa na Wayahudi waasi-imani kwenye hekalu la Yehova katika Yerusalemu. Ezekieli aliona “sanamu ile ya wivu.” Wazee 70 walikuwa wakitoa uvumba katika hekalu. Wanawake walionwa wakimlilia kijimungu bandia. Na wanaume 25 walikuwa wakiliabudu jua. Matendo hayo ya uasi-imani yalikuwa na umaana gani?
7, 8. “Sanamu ile ya wivu” huenda ikawa ilikuwa nini, na kwa nini ilichochea wivu wa Yehova?
7 Ibada ya sanamu ya Jumuiya ya Wakristo ilitangulia kufananishwa na yale machukizo ambayo Ezekieli aliona katika njozi. Kwa mfano, alisema hivi: “Tazama, upande wa kaskazini wa mlango, ilikuwako sanamu ile ya wivu, mahali pale pa kuingilia. [Yehova Mungu] akaniambia, Mwanadamu, je! unayaona wanayoyafanya, yaani, haya machukizo makubwa wanayofanya nyumba ya Israeli hapa, hata niende zangu mbali na patakatifu pangu?”—Ezekieli 8:1-6.
8 Ile sanamu ya wivu ya kuabudiwa huenda ikawa ilikuwa nguzo takatifu iliyowakilisha kijimungu-kike bandia ambacho Wakanaani waliona kuwa ndiye mke wa kijimungu chao Baali. Iwe sanamu hiyo ilikuwa ni nini, ilichochea wivu wa Yehova kwa sababu iligawanya ujitoaji wa pekee wa Israeli kwake katika kuhalifu amri zake: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW], Mungu wako . . . Usiwe na miungu mingine ila mimi. Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu.”—Kutoka 20:2-5.
9. Jumuiya ya Wakristo imechocheaje wivu wa Mungu?
9 Kuabudu ile sanamu ya wivu katika hekalu la Mungu lilikuwa mojayapo machukizo makubwa yaliyokuwa yakifanywa na Waisraeli waasi-imani. Vivyo hivyo, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamechafuliwa na mifano na sanamu yenye kumvunjia Mungu heshima yanayogawanya ule ujitoaji wa pekee wanaodai kumpa Yule wanayedai kumtumikia. Wivu wa Mungu huchochewa pia kwa sababu makasisi hukatalia mbali Ufalme wake kuwa tumaini la pekee la ainabinadamu na kuabudu Umoja wa Mataifa—“chukizo . . . [ambalo] limesimama katika patakatifu,” ambapo halipaswi kusimama.—Mathayo 24:15, 16; Marko 13:14.
10. Ezekieli aliona nini ndani ya hekalu, na hilo linalinganaje na yale yanayoonwa katika Jumuiya ya Wakristo?
10 Akiingia hekaluni, Ezekieli aripoti hivi: “Tazama, kila namna ya wadudu, na wanyama wachukizao, na taswira za vinyago vyote vya nyumba ya Israeli, zimepigwa ukutani pande zote. Na watu sabini wa wazee wa Israeli . . . walikuwa wamesimama na kuzielekea . . . kila mmoja ana chetezo mkononi mwake, na harufu ya moshi wa uvumba ilipaa juu.” Ebu fikiria! Wazee Waisraeli katika hekalu ya Yehova, wakitoa uvumba kwa vijimungu bandia, vilivyowakilishwa na michoro ya ukutani yenye kuchukiza. (Ezekieli 8:10-12) Kwa kulinganisha, ndege na wanyama wa mwituni hutumiwa kufananisha nchi za Jumuiya ya Wakristo, ambazo watu hutoa ujitoaji kwazo. Isitoshe, makasisi wengi wana hatia ya kusaidia kuwaongoza vibaya matungamano ya watu kwa kutetea nadharia zenye kosa kuhusu mageuzi ya mwanadamu kutoka namna za uhai za wanyama, zilizo nusu binadamu badala ya kuunga mkono usimulizi wa Biblia wa kweli wa uumbaji wa Yehova Mungu.—Matendo 17:24-28.
11. Kwa nini wanawake Waisraeli waasi-imani walikuwa wakimlilia Tamuzi?
11 Kwenye mwingilio wa lango la nyumba ya Yehova, Ezekieli aliona wanawake Waisraeli waasi-imani wakimlilia Tamuzi. (Ezekieli 8:13, 14) Wababuloni na Wasiria walimwona Tamuzi kuwa kijimungu cha mimea inayokua katika majira ya mvua na kunyauka katika kipindi cha ukavu. Kunyauka kwa mimea kulifananisha kifo cha Tamuzi, aliyeombolezewa kila mwaka na waabudu wake wakati wa joto jingi zaidi. Mimea ilipotokea tena wakati wa majira ya mvua, ilidhaniwa kwamba Tamuzi alikuwa amerudi kutoka ulimwengu wa chini. Aliwakilishwa na herufi ya kwanza ya jina lake, tau ya kale iliyokuwa namna ya msalaba. Hilo huenda sana likatukumbusha juu ya kule kutolea msalaba staha nyingi mno ya ibada kwa Jumuiya ya Wakristo.
12. Ezekieli aliwaona wanaume Waisraeli waasi-imani 25 wakifanya nini, na ni tendo gani kama hilo linalotukia katika Jumuiya ya Wakristo?
12 Baada ya hapo, katika ua wa ndani wa hekalu, Ezekieli aliona wanaume Waisraeli waasi-imani 25 wakiliabudu jua—uhalifu wa amri ya Yehova kuhusu ibada ya sanamu ya jinsi hiyo. (Kumbukumbu la Torati 4:15-19) Hao waabudu sanamu pia waliielekezea pua ya Mungu tawi la aibu, labda likiwakilisha uume wa kibinadamu. Haishangazi kwamba Mungu hangejibu sala zao, kama vile Jumuiya ya Wakristo itakavyotafuta msaada wake wakati wa “dhiki kubwa,” lakini isiupate. (Mathayo 24:21) Kama vile wale Waisraeli waasi-imani walivyoliabudu jua lenye kutoa nuru wakiwa wamegeuzia hekalu la Yehova visogo vyao, ndivyo Jumuiya ya Wakristo huipa kisogo nuru itokayo kwa Mungu, hufundisha mafundisho bandia, huabudu hekima ya kilimwengu na kuachilia ukosefu wa adili.—Ezekieli 8:15-18.
13. Mashahidi wa Yehova huepuka katika njia zipi zile namna za ibada ya sanamu zilizoonwa katika njozi ya Ezekieli?
13 Mashahidi wa Yehova huepuka namna za ibada ya sanamu zinazozoewa katika Jumuiya ya Wakristo, au Yerusalemu la ufananisho, kama ilivyoonwa kimbele na Ezekieli. Sisi hatuabudu mifano yenye kumvunjia Mungu heshima. Ingawa tunastahi “mamlaka iliyo kuu” ya kiserikali, ujitiisho wetu kwayo ni wa kadiri. (Warumi 13:1-7; Marko 12:17; Matendo 5:29) Ujitoaji wetu wa moyo hupewa kwa Mungu na Ufalme wake. Hatuweki nadharia ya mageuzi mahali pa Muumba na uumbaji wake. (Ufunuo 4:11) Hatuutolei msalaba kicho wala kuabudu utumiaji wa akili, falsafa, au aina nyinginezo za hekima ya kilimwengu. (1 Timotheo 6:20, 21) Sisi hujilinda pia na namna nyinginezo zote za ibada ya sanamu. Baadhi yazo ni zipi?
Aina Nyinginezo za Ibada ya Sanamu
14. Watumishi wa Yehova huchukua msimamo gani kwa habari ya “hayawani-mwitu” wa Ufunuo 13:1, NW?
14 Wakristo hawashiriki na ainabinadamu katika kuabudu “hayawani-mwitu” wa ufananisho. Mtume Yohana alisema hivi: “Nikaona mnyama [hayawani-mwitu, NW] akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba, na juu ya pembe zake ana vilemba kumi . . . Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu.” (Ufunuo 13:1, 8) Hayawani-mwitu wanaweza kuwakilisha “wafalme,” au mamlaka za kisiasa. (Danieli 7:17; 8:3-8, 20-25) Kwa hiyo vile vichwa saba vya hayawani-mwitu huyo wa ufananisho husimamia mamlaka za ulimwengu—Misri, Ashuru, Babuloni, Umedi-Uajemi, Ugiriki, Roma, na muungano wa Uingereza na Amerika. Makasisi wa Jumuiya ya Wakristo huonyesha ukosefu mwingi wa staha kwa Mungu na Kristo kwa kuiongoza ainabinadamu katika kuuabudu mfumo wa kisiasa wa Shetani, “mkuu wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31) Hata hivyo, wakiwa Wakristo wasiokuwamo na waungaji mkono wa Ufalme, watumishi wa Yehova hukatalia mbali ibada ya sanamu ya jinsi hiyo.—Yakobo 1:27.
15. Watu wa Yehova huwaonaje mabingwa wa kilimwengu, na Shahidi mmoja alisema nini kuhusu hilo?
15 Watu wa Mungu huepuka pia kuwaabudu mabingwa wa vitumbuizo na wa michezo. Baada ya kuwa Shahidi wa Yehova, mwanamuziki mmoja alisema hivi: “Muziki wa vitumbuizo na wa dansi waweza kuamsha tamaa zisizofaa . . . Mwanamuziki huimba juu ya furaha na wororo ambao huenda wasikilizaji wengi wakahisi unakosekana katika mwenzi wao wa ndoa. Mara nyingi mwanamuziki anakuja kutambulishwa na yale anayoimba juu yayo. Baadhi ya wanamuziki stadi ninaowajua hupendwa sana na wanawake kwa sababu hiyo. Mara mtu anapozamishwa katika ulimwengu huo wa fantasia, hilo laweza kumwongoza aanze kumwabudu mwanamuziki huyo. Yaweza kuanza kwa njia isiyo yenye kudhuru kwa mtu kuuliza mwanamuziki fulani amtilie sahihi kitu fulani kuwa ukumbusho. Lakini wengine wanakuja kumwona mwanamuziki huyo kuwa mfano mkamilifu, na kwa kumpa staha isiyofaa, wanamfanya awe sanamu. Huenda wakaangika picha ya bingwa huyo ukutani na kuanza kuvaa na kujipamba kama yeye . . . Wakristo wanahitaji kukumbuka kwamba kicho hicho kinafaa kwa Mungu peke yake.”
16. Ni nini kinachoonyesha kwamba malaika waadilifu hukatalia mbali ibada ya sanamu?
16 Naam, ni Mungu tu anayestahili kicho au ibada. Yohana ‘alipoanguka, ili kusujudu mbele ya miguu ya malaika’ aliyemwonyesha mambo ya ajabu, kiumbe wa roho huyo alikataa kuabudiwa katika njia yoyote lakini alisema hivi: “Angalia, usifanye hivi; mimi ni mjoli wako, na wa ndugu zako manabii, na wa wale wayashikao maneno ya kitabu hiki. Msujudie Mungu.” (Ufunuo 22:8, 9) Hofu ya Yehova, au staha nyingi mno kwake, hutufanya tumwabudu yeye peke yake. (Ufunuo 14:7) Hivyo, ujitoaji kimungu wa kweli hutulinda na ibada ya sanamu.—1 Timotheo 4:8.
17. Tunaweza kujilindaje na ukosefu wa adili katika ngono aina ya kuabudu sanamu?
17 Ukosefu wa adili katika ngono ni namna nyingine ya ibada ya sanamu inayokataliwa mbali na watumishi wa Yehova. Wanajua ya kwamba “hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu.” (Waefeso 5:5) Ibada ya sanamu inahusika kwa sababu tamaa ya jambo lenye kufurahisha lisilo halali linakuwa kitu chenye kupewa ujitoaji. Sifa za kimungu zinahatarishwa na tamaa za kingono zisizofaa. Kwa kuelekeza macho na masikio yake kwenye pornografia, mtu anahatarisha uhusiano wowote ambao huenda akawa nao na Mungu mtakatifu, Yehova. (Isaya 6:3) Basi, ili kujilinda na ibada ya sanamu hiyo, ni lazima watumishi wa Mungu waepuke pornografia na muziki wenye kufisidi. Wanahitaji kushikamana na thamani imara za kiroho zinazotegemea Maandiko, na ni lazima waendelee kuvaa “utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”—Waefeso 4:22-24.
Epuka Pupa na Kutamani
18, 19. (a) Pupa na kutamani ni nini? (b) Twaweza kujilindaje na pupa na kutamani aina za kuabudu sanamu?
18 Wakristo hujilinda pia na pupa na kutamani, ambazo ni namna za ibada ya sanamu zinazohusiana kwa ukaribu. Pupa ni tamaa yenye kupita kiasi au yenye uchoyo, na kutamani ni pupa kwa kitu chochote ambacho ni mali ya mtu mwingine. Yesu alionya dhidi ya kutamani na akasema juu ya mwanamume tajiri mwenye kutamani ambaye hakuweza kufaidika na mali yake alipokufa na akawa katika hali yenye kuhuzunisha ya ‘kutojitajirisha kwa Mungu.’ (Luka 12:15-21) Paulo aliwashauri waamini wenzake hivi kwa kufaa: “Vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi [kwa habari ya, NW] . . . kutamani, ndiyo ibada ya sanamu.”—Wakolosai 3:5.
19 Wale ambao huingiwa na kichaa cha kupenda fedha, cha ulafi na ulevi, au cha kujitakia makuu ya nguvu huzifanya tamaa hizo kuwa sanamu zao. Kama vile Paulo alivyoonyesha, mtu mwenye pupa ni mwabudu sanamu naye hataurithi Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 6:9, 10; Waefeso 5:5) Kwa hiyo, watu mmoja mmoja waliobatizwa wanaozoea ibada ya sanamu wakiwa watu wenye pupa wanaweza kutengwa na ushirika wa kundi la Kikristo. Hata hivyo, kwa kutumia Maandiko na kusali kwa bidii, tunaweza kuepuka pupa. Mithali 30:7-9 husema hivi: “Mambo haya mawili nimekuomba [Yehova Mungu]; usininyime [matatu] kabla sijafa. Uniondolee ubatili na uongo; usinipe umaskini wala utajiri; unilishe chakula kilicho kadiri yangu. Nisije nikashiba nikakukana, nikasema, BWANA [Yehova, NW] ni nani? Wala nisiwe maskini sana nikaiba, na kulitaja bure jina la Mungu wangu.” Roho ya aina hiyo inaweza kutusaidia tujilinde na pupa na kutamani aina za kuabudu sanamu.
Jilinde Dhidi ya Kujiabudu Mwenyewe
20, 21. Watu wa Yehova hujilindaje dhidi ya kujiabudu wenyewe?
20 Watu wa Yehova hujilinda dhidi ya kujiabudu mwenyewe. Katika ulimwengu huu ni kawaida kwa mtu kujiabudu mwenyewe na kuabudu nia ya mtu mwenyewe. Tamaa ya umaarufu na utukufu huwasababisha wengi watende katika njia zenye udanganyifu. Wanataka mapenzi yao wenyewe yafanywe, bali si ya Mungu. Lakini tusingeweza kuwa na uhusiano na Mungu ikiwa tungejiruhusu kujiabudu wenyewe kwa kujaribu kwa udanganyifu kusisitiza njia yetu wenyewe na kujaribu kupiga ubwana juu ya wengine. (Mithali 3:32; Mathayo 20:20-28; 1 Petro 5:2, 3) Tukiwa wafuasi wa Yesu, tumekataa mambo ya ulimwengu ya kichinichini.—2 Wakorintho 4:1, 2.
21 Badala ya kutafuta umaarufu, watu wa Mungu hutii onyo hili la upole la Paulo: “Basi, mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Tukiwa watumishi wa Yehova, sisi hatusisitizi njia yetu wenyewe kwa njia ya kuabudu sanamu bali twafanya mapenzi ya kimungu kwa shangwe, tukikubali mwongozo kutoka kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” na kushirikiana kikamili na tengenezo la Yehova.—Mathayo 24:45-47.
Endelea Kujilinda!
22, 23. Tunaweza kujilinda katika njia gani na ibada ya sanamu ya kila aina?
22 Tukiwa watu wa Yehova, sisi hatusujudu mbele ya sanamu za vitu halisi. Sisi hujilinda pia na namna zilizofichika za ibada ya sanamu. Kwa kweli, ni lazima tuendelee kujilinda na ibada ya sanamu ya kila aina. Kwa hiyo tunatii shauri hili la Yohana: “Jilindeni nafsi zenu na sanamu.”—1 Yohana 5:21.
23 Ikiwa wewe ni mmoja wa watumishi wa Yehova, tumia sikuzote dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia pamoja na uwezo wako wa kufahamu. (Waebrania 5:14) Hivyo hutachafuliwa na roho ya ulimwengu ya kuabudu sanamu lakini utakuwa kama wale Waebrania waaminifu watatu na Wakristo waaminifu-washikamanifu wa mapema. Utampa Yehova ujitoaji wa pekee, naye atakusaidia uendelee kujilinda na ibada ya sanamu ya kila aina.
Mawazo Yako Ni Nini?
◻ Mashahidi wa Yehova huepukaje namna za ibada ya sanamu zilizoonwa katika njozi ya Ezekieli?
◻ “Hayawani-mwitu” wa Ufunuo 13:1, NW, ni nini, na watumishi wa Yehova huchukua msimamo gani kumhusu?
◻ Kwa nini kujilinda dhidi ya kuabudu mabingwa wa vitumbuizo na wa michezo?
◻ Tunaweza kujilindaje dhidi ya kujiabudu wenyewe?
◻ Kwa nini tuendelee kujilinda na ibada ya sanamu ya kila aina?
[Picha katika ukurasa wa 26]
Je! wajua jinsi yale machukizo yaliyoonwa katika njozi ya Ezekieli yalivyotangulia kufananisha ibada ya sanamu ya Jumuiya ya Wakristo?
[Hisani]
Sanaa (kushoto juu) yategemea foto ya Ralph Crane/Bardo Museum