Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 2/1 kur. 5-7
  • Je! Wema Utapata Kuushinda Uovu Wakati Wowote?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wema Utapata Kuushinda Uovu Wakati Wowote?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupiga Vita Dhidi ya Uovu Katika Dachau
  • Kuushinda Uovu Ulio Ndani Yetu
  • Kumharibu Ibilisi
  • “Hawatafanya Uovu”
  • Ni Nini Kinachotufanya Tuwe Wema au Waovu?
    Amkeni!—2010
  • Wema Wapingana na Uovu—Vita Yenye Kudumu Muda Mrefu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Jinsi Wema Utakavyoshinda Uovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • “Msimlipe Yeyote Uovu Kwa Uovu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 2/1 kur. 5-7

Je! Wema Utapata Kuushinda Uovu Wakati Wowote?

KARIBU miaka elfu mbili iliyopita, Yesu Kristo, mtu asiye na hatia, alikuwa akijaribiwa kwa ajili ya uhai wake. Watu waovu walikuwa wakifanya shauri la kumwua kwa sababu alisema ukweli. Alishtakiwa kimakosa juu ya uhaini, na umati ukafanya ghasia auawe. Gavana Mroma, aliyethamini zaidi umashuhuri wake mwenyewe wa kisiasa kuliko uhai wa seremala mnyenyekevu, alimhukumia Yesu kifo kikatili. Kwa maoni yote ya kijuujuu, ilionekana kwamba uovu ulikuwa umeshinda.

Hata hivyo, usiku wa kabla ya kuuawa kwake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Alimaanisha nini? Kwa sehemu, alimaanisha kwamba uovu ulimwenguni haukuwa umemtia uchungu wala kumfanya alipize kisasi jinsi iyo hiyo. Ulimwengu haukuwa umemfinyanga katika umbo ovu. (Linganisha Warumi 12:2, Philips.) Hata alipokuwa akifa, alisali kwa ajili ya wauaji wake: “Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo.”—Luka 23:34.

Yesu alionyesha—mpaka alipokufa—kwamba uovu waweza kushindwa. Aliwahimiza wafuasi wake wapige vita yao wenyewe dhidi ya uovu. Wanaweza kufanyaje hivyo? Kwa kutii shauri la Kimaandiko la ‘kutomlipa mtu ovu kwa ovu’ na kwa ‘kuushinda ubaya kwa wema,’ kama vile Yesu alivyokuwa amefanya. (Warumi 12:17, 21) Lakini, je, kweli mwendo huo una matokeo?

Kupiga Vita Dhidi ya Uovu Katika Dachau

Else alikuwa mwanamke mmoja Mjerumani aliyefungwa gerezani katika Dachau aliyempa msichana mmoja Mrusi mwenye miaka 14 zawadi yenye thamani kubwa, zawadi ya imani na tumaini.

Dachau ilikuwa kambi ya mateso yenye sifa mbaya ambako maelfu waliuawa kwa gesi yenye sumu na mamia, kutia na msichana huyo Mrusi, walifanyiwa majaribio ya kitiba yenye kuchukiza. Dachau ilionekana kuwa upeo kabisa wa uovu. Ingawa hivyo, hata katika udongo huo ulioonekana kuwa usiozaa, wema ulichipuka na hata kuongezeka.

Else alimsikitikia sana msichana tineja huyo mchanga aliyekuwa pia amelazimishwa kutazama askari wa SS wakimnajisi mama yake kinyama. Else, kwa kuhatarisha uhai wake mwenyewe, alitafuta nafasi za kuongea na msichana huyo kuhusu wema na uovu na kuhusu tumaini la Kimaandiko juu ya ufufuo. Alimfundisha rafiki yake mchanga kupenda badala ya kuchukia. Na msichana huyo Mrusi aliponyoka mambo yenye kuhofisha ya Dachau, kwa sababu ya Else.

Else alifanya aliyoyafanya kwa sababu alitaka kufuata kile kielelezo cha Kristo kisicho cha ubinafsi. Akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alikuwa amejifunza kutolipa ovu kwa ovu, na imani yake ilimsukuma awasaidie wengine wafanye vivyo hivyo. Ingawa aliteseka katika Dachau, alishinda vita ya kiadili dhidi ya utawala mbovu. Naye hakuwa peke yake.

Paul Johnson, katika kitabu chake A History of Christianity, aliandika kwamba “[Mashahidi wa Yehova] walikataa ushirikiano wowote pamoja na utawala wa Nazi ambao walilaumu vikali kuwa ni wenye uovu kabisa . . . Asilimia tisini na saba walipatwa na mateso ya namna fulani.” Je! hilo lilikuwa shindano la bure? Katika kitabu Values and Violence in Auschwitz, mwanasoshiolojia Anna Pawelczynska alisema hivi kuhusu Mashahidi: “Kikundi hiki kidogo cha wafungwa kilikuwa kani thabiti ya kiitikadi na walishinda vita yao dhidi ya Unazi.”

Lakini, kwa wengi wetu, vita ya msingi inapigwa dhidi ya uovu ulio ndani yetu badala ya uovu ulio nje. Ni pigano ndani yetu wenyewe.

Kuushinda Uovu Ulio Ndani Yetu

Mtume Paulo alisimulia vita hiyo katika njia inayofuata: “Si lile jema nilipendalo kufanya ndilo ninalofanya kwa kweli; ni lile ovu nisilotaka kufanya ninalofuliza kufanya.” (Warumi 7:19, The New Testament, ya William Barclay) Kama vile Paulo alivyojua vema, kufanya mema hakutokei kiasili sikuzote.

Eugenioa alikuwa kijana Mhispania aliyepiga vita, kwa muda wa miaka miwili mirefu, dhidi ya mielekeo yake mibovu. “Nililazimika kuwa mkali sana dhidi yangu mwenyewe,” aeleza. “Kutoka miaka yangu ya mapema, nilikuwa na mwelekeo wa kuwa mwenye kukosa adili. Nilipokuwa tineja, nilishiriki katika karamu za ngono za jinsia moja, na kwa kusema wazi, nilifurahia mtindo-maisha wa jinsi hiyo.” Ni nini hatimaye kilichomfanya atake kubadilika?

“Nilitaka kumpendeza Mungu, na nilijifunza kutoka Biblia kwamba yeye hakukubaliana na jinsi nilivyokuwa nikiishi,” Eugenio akasema. “Kwa hiyo niliamua kuwa mtu wa aina tofauti, kufuata miongozo ya Mungu. Kila siku, nililazimika kupiga vita dhidi ya mawazo machafu yasiyofaa, yaliyoendelea kuijaa akili yangu. Niliazimia kushinda pigano hilo, na nilisali bila kukoma ili kupata msaada wa Mungu. Baada ya miaka miwili sehemu ngumu zaidi ilikuwa imepita, ingawa ningali mkali dhidi yangu mwenyewe. Lakini shindano hilo lilifaa. Sasa ninajistahi mwenyewe, nina ndoa nzuri, na zaidi ya yote, nina uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Najua kutokana na ono la kibinafsi kwamba mawazo maovu yaweza kuondoshwa kabla yayo kuzaa matunda—ukijitahidi kwelikweli.”

Wema huushinda uovu kila wakati ambapo wazo ovu linakataliwa mbali, kila wakati tunapokataa kulipa ovu kwa ovu. Hata hivyo, ushindi huo mbalimbali, ingawa ni wa maana, hauondolei mbali vile vyanzo viwili vikuu vya uovu. Hata tukijitahidi jinsi gani, hatuwezi kushinda kabisa udhaifu wetu mbalimbali uliorithiwa, na Shetani bado huzoea uvutano mbovu juu ya ainabinadamu. Kwa hiyo, je, hali hiyo itapata kubadilika wakati wowote?

Kumharibu Ibilisi

Uaminifu wa Yesu hadi kifo ulikuwa ushinde mkuu kwa Shetani. Ibilisi alishindwa katika jaribio lake la kuvunja uaminifu-maadili wa Yesu, na kushindwa huko kulitia alama mwanzo wa mwisho kwa Shetani. Kama vile Biblia hueleza, Yesu alionja kifo ili “kwa njia ya mauti amharibu . . . Ibilisi.” (Waebrania 2:14) Baada ya ufufuo wake Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mathayo 28:18) Na mamlaka hiyo ingetumiwa kubatilisha kazi za Shetani.

Kitabu cha Ufunuo kinasimulia ile siku ambayo Yesu angemwondoa Shetani mbinguni. Mwovu Mkuu huyo, pamoja na mashetani wake, angezuiwa kwenye ujirani wa dunia. Likiwa tokeo, Biblia huonya, uovu ungekuwa mwingi: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”—Ufunuo 12:7-9, 12.

Unabii wa Biblia huonyesha kwamba jambo hilo la kihistoria limetukia tayari—karibu na wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.b Hilo laeleza sababu ya lile ongezeko la uovu lenye kutokeza ambalo tumeshuhudia katika wakati wetu. Lakini hivi karibuni Shetani atazuiwa kabisa asiweze tena kuwa na uvutano juu ya yeyote.—Ona Ufunuo 20:1-3.

Yote hayo yatamaanisha nini kwa ainabinadamu?

“Hawatafanya Uovu”

Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, hivi karibuni Yesu atatumia ‘mamlaka yake juu ya dunia’ ili kupanga programu ya kiroho ya kuelimishwa upya. “Uadilifu ndio wakaaji wa bara lenye kuzaa watajifunza hakika.” (Isaya 26:9, NW) Manufaa zitakuwa wazi kwa kila mtu. Biblia hutuhakikishia hivi: “Hawatadhuru [“hawatafanya uovu,” Interlinear Hebrew/Greek English Bible ya Green] wala hawataharibu . . . maana dunia itajawa na kumjua BWANA [Yehova, New World Translation], kama vile maji yanayoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Hata sasa, mingi ya mielekeo yetu mibovu yaweza kushindwa. Uvutano wa kishetani unapoisha, kwa hakika itakuwa rahisi zaidi sana sana, ‘kuacha mabaya, na kutenda mema.’—1 Petro 3:11.

Tuna kila sababu ya kuwa na uhakika kwamba wema utaushinda uovu kwa sababu Mungu ni mwema, na kwa msaada wake wale wanaotaka kufanya mema wanaweza kuushinda uovu, kama vile Yesu alivyothibitisha kwa kielelezo chake mwenyewe. (Zaburi 119:68) Wale walio na nia ya kupiga vita dhidi ya uovu wanaweza kutazamia kuishi katika dunia iliyosafishwa inayotawalwa na Ufalme wa Mungu, serikali inayoshughulika na kuondolea mbali uovu kabisa kwa wakati wote. Mtunga zaburi asimulia tokeo: “Fadhili na kweli zimekutana, haki na amani zimebusiana. Kweli imechipuka katika nchi, haki imechungulia kutoka mbinguni.”—Zaburi 85:10, 11.

[Maelezo ya Chini]

a Si jina lake halisi.

b Ili kupata maelezo zaidi, ona kurasa 20-2 za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki