Kupenda Fedha Kuna Ubaya Gani?
PAUL na Mary walikuwa na duka kubwa katika jumuiya ya Kiafrika yenye umaskini.a Kwa kufanya kazi kwa bidii kila usiku na mchana, walichuma fedha nyingi sana. Baadaye Mary angeweza kuonea fahari nyumba kubwa mpya iliyojaa fanicha nzuri sana. Kwa habari ya Paul, aliweza kwenda huku na huku katika gari la anasa.
Siku moja Paul alijiwa na kikundi cha watu walioipinga serikali. Walidai hivi: “Tunataka biashara yako ifanye utoaji wa [dola 100] kila mwezi ili kutegemeza mradi wetu.” Wakiwa hawataki kuunga mkono upande mmoja katika ushindani wa kisiasa, Paul na Mary walikataa kwa ujasiri. Kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo, walishukiwa kuwa walipata utegemezo wa kifedha kutoka serikali. Mwisho-juma mmoja, wakati Paul na Mary walikuwa nje ya mji, duka lao liliporwa, na gari na makao yao yenye kupendeza yaliteketezwa.
Huo ni usimulizi wenye kuhuzunisha kwelikweli, lakini je, twaweza kujifunza kutoka kwao? Wengi ambao wamefanya kazi kwa bidii ili kuwa matajiri huenda ikawa hawajapatwa na msiba uliowanyang’anya utajiri wao, lakini namna gani wakati ujao? Kwa nini Biblia husema kwamba “hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu”?—1 Timotheo 6:9.
Maoni ya Fedha Yenye Usawaziko
Kulingana na Biblia, ni lazima Mkristo wa kweli awaandalie washiriki wa familia yake wenye kumtegemea mahitaji ya kimwili. Hali, kama vile ukosefu wa kazi za kuajiriwa au matatizo ya afya, yaweza kufanya hilo liwe gumu nyakati nyingine. Kwa upande ule mwingine, Mkristo anayepuuza kimakusudi kuiandalia familia yake “ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.”—1 Timotheo 5:8.
Katika jumuiya nyinginezo za mashambani, watu hupata riziki kutokana na mashamba yao kwa kupanda chakula chao wenyewe na kufuga wanyama. Wengine hawahitaji fedha sana, wakipata mahitaji ya maisha kwa kubadilishana vifaa na utumishi mbalimbali. Hata hivyo, njia ya kawaida zaidi ambayo wapata riziki huandalia familia zao ni kwa kufanya aina fulani ya kazi ya kuajiriwa ili kupata mishahara. Wanatumia fedha zilizochumwa ili kununua chakula na vitu vingine vinavyochangia hali njema ya familia yao. Kwa kuongezea, fedha zilizowekwa akiba kwa hekima zaweza kuandaa kadiri fulani ya ulinzi katika nyakati za ugumu au msiba. Kwa mfano, zaweza kutumiwa kulipia gharama za kitiba au kufanya marekebisho muhimu kwenye makao ya mtu. Ndiyo sababu Biblia husema halisi kwamba ‘fedha ni ulinzi’ na kwamba “huleta jawabu la mambo yote.”—Mhubiri 7:12; 10:19.
Kwa sababu fedha zinatimiza mambo mengi sana, kuna hatari ya kusitawisha maoni yasiyo halisi juu ya nguvu zazo. Mkristo anahitaji kuwa na ufahamu juu ya mipaka yazo kwa kulinganisha na mambo mengine yenye umaana zaidi. Kwa kielelezo, Biblia hulinganisha thamani ya fedha na hekima ya kimungu, ikisema hivi: “Hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.” (Mhubiri 7:12) Hekima ya kimungu ina faida hiyo juu ya fedha katika njia gani?
Somo Kutoka Wakati Uliopita
Mambo yaliyotukia katika Yerusalemu katika mwaka 66 W.K. yanaonyesha faida za hekima ya kimungu juu ya fedha. Baada ya kuzuia majeshi ya Roma yaliyokuwa yakishambulia, yaonekana Wayahudi katika Yerusalemu waliamini kwamba matarajio ya kibiashara yalikuwa mazuri sasa. Kwa kweli, walianza kutokeza fedha zao wenyewe katika kusherehekea uhuru wao uliopatikana karibuni. Sarafu zao ziliandikwa, katika Kiebrania, usemi kama vile “Kwa uhuru wa Sayuni” na “Yerusalemu Takatifu.” Kila mwaka mpya, walifanyiza sarafu mpya zenye miandiko inayoitambulisha kuwa za “mwaka wa pili,” “mwaka wa tatu,” na “mwaka wa nne.” Waakiolojia wamechimbua hata sarafu chache adimu zenye mwandiko “mwaka wa tano,” ukilingana na mwaka 70 W.K. Je! Wakristo Wayahudi waliona fedha hizo mpya za Kiyahudi kuwa ufananisho ufaao wa uhuru wenye kudumu?
La. Kwa sababu walikumbuka maneno yenye hekima ya Bwana Mkubwa wao. Yesu alikuwa ametabiri shambulio la Roma lililotukia katika 66 W.K. Alikuwa amewashauri wafuasi wake kwamba wakati hilo lilipotukia, walipaswa ‘wakimbilie nje ya Yerusalemu.’ (Luka 21:20-22) Historia inathibitisha kwamba Wakristo Wayahudi walifanya vivyo hivyo. Kwa wazi walikuwa tayari kupoteza majengo, mali, na nafasi za kibiashara kwa sababu ya kuondoka Yerusalemu. Miaka minne baadaye, majeshi ya Roma yalirudi na kulizingira jiji hilo.
“Kulikuwako dhahabu nyingi katika Jiji hilo,” kulingana na shahidi mwenye kujionea mwenyewe, yule mwanahistoria Yosefu. Lakini hesabu kubwa-kubwa za fedha hazikuweza kuliokoa Yerusalemu kutoka katika njaa kuu, iliyozidi kwa utaratibu “kuwa mbaya zaidi” na “kunyafua nyumba na familia nzima-nzima.” Baadhi ya wakaaji walimeza sarafu za dhahabu wakajaribu kulikimbia jiji. Lakini waliuawa na maadui wao, waliopasua matumbo yao ili kuzitoa fedha hizo. “Kwa matajiri,” aeleza Yosefu, “lilikuwa jambo la hatari kubaki katika Jiji hilo kama lilivyokuwa kuliondoka; kwani wengi waliuawa kwa ajili ya fedha zao, kwa masingizio ya kwamba walikuwa watoro.”
Kwa chini ya miezi sita kutoka mwanzo wa kuzingirwa huko, Yerusalemu liliharibiwa, na wakaaji walo zaidi ya milioni moja wakafa kutokana na njaa kuu, ugonjwa wa kipuku, na kwa upanga. Kupenda fedha kulikuwa kumewaondolea wengi ufahamu kukiwatosa katika upotevu na uharibifu, hali kutumia maneno ya hekima kulikuwa kumewawezesha Wakristo Wayahudi waponyoke.
Hilo halikuwa kisa pekee katika historia ambamo fedha zilishindwa kuwasaidia watu katika nyakati za taabu. Kupenda fedha kwaweza kuwa bwana mkubwa mkatili kama nini! (Mathayo 6:24) Isitoshe, kunaweza kukunyang’anya furaha ya sasa.
Mambo ya Kufurahisha Ambayo Fedha Haziwezi Kununua
Kichaa cha kuwa tajiri chaweza kuzuia mtu asione mambo mengi ya kufurahisha ambayo hayahitaji fedha nyingi. Kwa kielelezo, fikiria mahusiano ya familia yenye furaha, marafiki wa kweli, maajabu ya kiasili, machweo yenye kutazamisha, mvua na ngurumo yenye kuvutia, mbingu zenye nyota, na michezo ya wanyama, au maua na miti katika msitu usioharibiwa.
Ni kweli, matajiri wengine wana wakati mwingi zaidi wa kufurahia mambo mengi, lakini wengi wao ni wenye shughuli nyingi wakijaribu kuhifadhi au kuongeza utajiri wao. Ingawa lasikika kuwa jambo la ajabu, mara nyingi furaha huwaepuka hata wale wenye anasa. Hilo hushangaza watafiti wa ki-siku-hizi. “Tutaelezaje uhakika wa kwamba jambo fulani linalotamaniwa na watu wengi sana, na linaloaminiwa kuwa aina fulani ya dawa kwa mambo yote, linapopatikana linakuwa na matokeo ya kinyume yakienea kutoka kuwa yenye kukatisha tamaa na yenye kuhuzunisha sana?” auliza Thomas Wiseman katika kitabu chake The Money Motive—A Study of an Obsession.
Jambo moja liwezalo kumnyang’anya tajiri furaha ni ugumu wa kujua ni nani walio marafiki wake wa kweli. Mfalme Sulemani tajiri alijionea mwenyewe kwamba “mali yakiongezeka, hao walao nao waongezeka.” (Mhubiri 5:11) Matajiri wengi hupatwa pia na wasiwasi wakijaribu kudumisha au kuongeza thamani ya utajiri wao. Mara nyingi hilo huwanyang’anya usingizi wenye kufurahisha. Biblia hueleza hivi: “Usingizi wake kibarua ni mtamu, kwamba amekula kidogo, au kwamba amekula kingi; lakini kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi.”—Mhubiri 5:12.
Kupenda fedha kwaweza kudhuru mahusiano kati ya familia na marafiki kwa sababu kwaweza kumshawishi mtu afanye matendo ya kutofuatia haki na ya uhalifu. Mara nyingi wapendao fedha hugeukia kucheza kamari. Kwa huzuni, kutamani kucheza kamari mara nyingine tu huwatia wengi katika madeni. “Kufikia wakati wanaponijia,” akasema daktari mmoja wa magonjwa ya akili wa Afrika Kusini, “kwa kawaida wale [wenye kichaa cha kucheza kamari] hawasaidiki tena, wamepoteza kazi, biashara, makao, na mara nyingi familia zao zimewaacha.” Onyo la Biblia ni kweli kama nini: “Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele; lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.”—Mithali 28:20.
‘Hujifanyia Mabawa, na Kuruka Mbali’
Sababu nyingine inayofanya kupenda fedha kuwe hatari ni kwamba serikali za kibinadamu zimethibitika kutoweza kushirikiana kikamili au kuhakikisha kwamba fedha zadumisha thamani thabiti ya kimataifa; wala hazijaweza kuzuia kupunguka kwa hali ya kiuchumi, mishuko ya kiuchumi, na mishuko mikubwa katika soko la thamani ya fedha. Upunjaji, wizi, na infleshoni pia hukazia ukweli wa maneno haya yaliyopuliziwa: “Usijitaabishe ili kupata utajiri; acha kuzitegemea akili zako mwenyewe. Je! utavikazia macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, kama tai arukaye mbinguni.”—Mithali 23:4, 5.
Infleshoni. Kwa hakika tatizo hilo halijawa tu katika nchi zenye umaskini. Mapema zaidi katika karne hii, infleshoni yenye kuongezeka kwa kasi ilikumba mataifa yenye viwanda vikubwa vya Ulaya ya kati. Kwa kielelezo, kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, mark moja ya Ujerumani ilikuwa sawasawa na shilingi ya Uingereza, frank ya Ufaransa, au lira ya Italia. Miaka kumi baadaye, shilingi, frank, na lira vilikuwa sawasawa kwa kadiri fulani na mark 1,000,000,000,000. Infleshoni ina matokeo gani juu ya watu katika jamii zenye utajiri? “Ikiwa lile lililoupata ule muungano wa milki za Ujerumani na Austria na Hangari katika miaka ya mapema ya 1920 ndicho kiwango cha kupimia,” asema Adam Fergusson katika kitabu chake When Money Dies, “basi [kuanguka kwa thamani ya fedha] kunatokeza kadiri kubwa sana ya pupa, jeuri, ukosefu wa furaha, na chuki, yenye kuchochewa na hofu, hivi kwamba hakuna jamii iwezayo kuokoka bila kulemaa na kubadilika.”
Katika 1923, Ujerumani ilikadiri upya thamani ya fedha zazo kwa kuondosha sufuri 12 hivi kwamba kwa ghafula mark 1,000,000,000,000 za zamani zikawa sawasawa na mark moja mpya. Hatua hiyo ilikomesha infleshoni lakini ilikuwa na matokeo mengine yenye uharibifu. Fergusson aeleza hivi: “Kuanzishwa upya kwa uthabiti wa fedha, kulikofilisisha wengi, kuwanyang’anya mamilioni riziki yao, na kuzimisha matumaini ya mamilioni wengine, kulitoza kwa njia isiyo ya moja kwa moja gharama mbaya zaidi ambayo ulimwengu mzima ulilazimika kulipa.” Yaonekana hiyo “gharama mbaya” ambayo mwandikaji huyo alikuwa akifikiria ilikuwa kule kutokea kwa Unazi na Vita ya Ulimwengu 2.
Jambo la kwamba akaunti kubwa-kubwa za fedha katika benki zimeshindwa kuwasaidia wengi katika wakati uliopita lapasa kuwa onyo lenye kufikiriwa kwa uzito katika nyakati hizi za ukosefu wa uhakika wa kiuchumi wa ulimwenguni pote. Mwana wa Mungu mwenyewe alionya kwamba fedha zingeshindwa kusaidia, jinsi ambavyo kwa hakika zimeshindwa mara nyingi. (Luka 16:9) Lakini kushindwa kwa fedha kwa kadiri kubwa zaidi na kwa kuenea zaidi kutakuja wakati Yehova Mungu anapotekeleza hukumu juu ya ulimwengu huu mbovu. “Mali hazifaidii kitu siku ya ghadhabu; bali haki huokoa na mauti.”—Mithali 11:4.
Kwa hiyo ni jambo la maana jinsi gani, kwamba kila mmoja wetu ajitahidi kudumisha msimamo mwadilifu pamoja na Marafiki wetu wa kweli Yehova Mungu na Yesu Kristo!
Chanzo cha Furaha ya Kweli
Paul na Mary, waliotajwa mwanzoni, walikuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa miaka mingi walishiriki katika kazi ya kueneza evanjeli ya wakati wote. Hata hivyo, tamaa yao ya kupata utajiri iliwasababisha waache kuhudhuria mikutano ya kutaniko la Kikristo, waliacha kushiriki imani yao katika huduma ya peupe. Lakini wakaamka kiroho. “Sasa naweza kuona jinsi lisivyokuwa jambo la kiakili kutumia wakati na nishati yangu yote kwenye jambo liwezalo kutoweka katika dakika chache,” akasema Mary baada ya kunyang’anywa mali na nyumba yake kuteketezwa. Kwa furaha, wenzi hao wa ndoa walijifunza somo kabla ya hali kufika hatua ya kutorekebika. Naam, dhara kubwa zaidi ambalo kupenda fedha kwaweza kusababisha ni lile la kumnyang’anya mtu uhusiano uliokubaliwa pamoja na Yehova Mungu na Yesu Kristo. Bila Marafiki hao, twaweza kuwa na tumaini gani la kuokoka mwisho wa ulimwengu huu mbovu kuingia katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ulioahidiwa?—Mathayo 6:19-21, 31-34; 2 Petro 3:13.
Kwa hiyo haidhuru iwe unajiona mwenyewe kuwa tajiri au maskini, jilinde na kusitawisha kupenda fedha. Jitahidi kupata na kudumisha ile hazina kuu zaidi—msimamo uliokubaliwa pamoja na Yehova Mungu. Waweza kufanya hivyo kwa kukaza fikira daima juu ya ule mwaliko wa haraka: “Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yao ya kweli hayatumiwi.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Pande zote mbili za sarafu yenye mwandiko “mwaka wa pili” iliyofanyizwa wakati wa uasi wa Kiyahudi
[Hisani]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.