Geuzweni Akili na Kutiwa Nuru Katika Moyo
“Basi nasema neno hili, tena nashuhudia katika Bwana, tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo.”—WAEFESO 4:17.
1. Akili na mioyo yetu hutufanyia nini?
AKILI na moyo ni mbili kati ya uwezo mbalimbali wa ajabu zaidi ambao wanadamu wanamiliki. Ingawa utendaji wa moyo na akili ni mwingi sana, kila mtu mmoja mmoja ana akili na moyo tofauti. Utu wetu, usemi, mwenendo, hisiamoyo, na mambo tunayothamini yanaathiriwa sana na njia ambayo akili na mioyo yetu hutenda.
2, 3. (a) Biblia hutumiaje maneno “moyo” na “akili”? (b) Kwa nini ni lazima tuhangaike juu ya yote mbili?
2 Katika Biblia, “moyo” kwa kawaida hurejezea msukumo wa ndani, hisiamoyo, na hisi za kindani, na “akili” hurejezea uwezo wa kusababu na kufikiri. Hata hivyo, vinapatana. Kwa kielelezo, Musa aliwahimiza Waisraeli hivi: “Ukaweke moyoni mwako [“ni lazima ukumbuke akilini mwako,” kielezi-chini, NW] ya kuwa BWANA [Yehova, NW] ndiye Mungu.” (Kumbukumbu la Torati 4:39) Kwa wale waandishi waliokuwa wakikusudia mabaya dhidi yake, Yesu alisema hivi: “Mbona mnawaza maovu mioyoni mwenu?”—Mathayo 9:4; Marko 2:6, 7.
3 Hilo laonyesha kwamba akili na moyo vinahusiana kwa ukaribu. Vinafanya kazi pamoja, nyakati nyingine vikiimarishana katika kufanya kazi vikiwa timu iliyounganika, hata hivyo mara nyingi vikipigana vita viking’ang’ania ukuu. (Mathayo 22:37; linganisha Warumi 7:23.) Kwa sababu hiyo, ili kupata pendeleo la Yehova, si lazima tuhakikishe tu hali ya akili na mioyo yetu bali pia ni lazima tuvizoeze kufanya kazi pamoja kwa upatano, visaidiane. Ni lazima tugeuzwe akili na kutiwa nuru katika moyo.—Zaburi 119:34; Mithali 3:1.
‘Kama Mataifa Yaenendavyo’
4. Shetani amevutaje akili na mioyo ya watu, na tokeo ni nini?
4 Shetani ni stadi wa udanganyo na wa kuvuta kwa hila. Yeye ajua kwamba ili kupata kuwadhibiti watu, ni lazima alenge shabaha akili na mioyo yao. Tangu mwanzo kabisa wa historia ya kibinadamu, amekuwa akitumia mbinu za aina moja au nyingine ili kuvuta akili na mioyo ya watu. Likiwa tokeo, “dunia yote hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Kwa kweli, Shetani amevuta kwa mafanikio sana mioyo na akili za watu wa ulimwengu hivi kwamba Biblia huwasimulia kuwa “kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka.” (Wafilipi 2:15) Mtume Paulo asimulia kwa wazi hali ya moyo na akili ya kizazi hicho chenye ukaidi na kilichopotoka, na maneno yake yanatumika yakiwa onyo kwetu sote leo. Kwa kielelezo, tafadhali soma Waefeso 4:17-19, na kulilinganisha na maneno ya Paulo kwenye Warumi 1:21-24.
5. Kwa nini Paulo aliwaandikia Waefeso shauri lenye nguvu?
5 Twaweza kufahamu kwa nini Paulo aliwaandikia Wakristo katika Efeso maneno hayo yenye nguvu tunapokumbuka kwamba jiji hilo lilikuwa na sifa mbaya kwa ajili ya kuharibika kwalo kiadili na ibada ya sanamu ya kipagani. Ingawa Wagiriki walikuwa na watu wao mashuhuri wenye kufikiri na wanafalsafa, yaonekana kwamba elimu ya Kigiriki iliwapa watu wengi uwezo mkubwa zaidi wa uovu, na utamaduni wao uliwafanya tu wawe stadi zaidi katika maovu yao. Paulo alihangaika sana juu ya Wakristo wenzake walioishi katika mazingira hayo. Alijua kwamba wengi wao walikuwa wamekuwa watu wa mataifa na walikuwa ‘wametembea kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu.’ Lakini sasa walikuwa wameikubali kweli. Akili zao zilikuwa zimegeuzwa, na mioyo yao ilikuwa imetiwa nuru. Zaidi ya hayo yote, Paulo alitaka ‘waenende kama inavyostahili wito wao walioitwa.’—Waefeso 2:2, NW; 4:1.
6. Kwa nini tupendezwe na maneno ya Paulo?
6 Hali ndiyo iyo hiyo leo. Sisi pia huishi katika ulimwengu wenye thamani zilizopotoka, adili zilizofilisika, na mazoea ya dini bandia. Wakati mmoja wengi miongoni mwetu waliishi kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu. Wengine wetu hulazimika kushirikiana kwa ukaribu na walimwengu kila siku. Baadhi yetu huishi katika nyumba ambamo roho ya kilimwengu imeenea. Kwa hiyo, ni lazima tuelewe maana ya maneno ya Paulo na kufaidika kutokana na shauri lake.
Akili Zisizo na Faida na Zilizotiwa Giza
7. Paulo alimaanisha nini kwa usemi “kukosa faida kwa akili zao”?
7 Ili kutoa utegemezo imara kwa himizo lake kwamba Wakristo ‘wasienende kama mataifa waenendavyo,’ Paulo alitaja kwanza “kukosa faida kwa akili zao.” (Waefeso 4:17, NW) Hilo lamaanisha nini? Neno lililotafsiriwa “kukosa faida,” kulingana na The Anchor Bible, “ladokeza utupu, upuzi, ubatili, upumbavu, kukosa kusudi, na fadhaiko.” Hivyo, Paulo alikuwa akionyesha kwamba umaarufu na utukufu wa ulimwengu wa Kigiriki na Kiroma huenda ikawa ulionekana wenye kuvutia lakini kuufuatia kulikuwa kwa kweli jambo lenye utupu, upumbavu, na lisilo na kusudi. Wale waliotamani sana umaarufu na utukufu wasingepata chochote hatimaye ila fadhaiko na kukata tamaa. Kanuni iyo hiyo ni kweli kwa habari ya ulimwengu leo.
8. Jitihada za ulimwengu zinakosa faida katika njia zipi?
8 Ulimwengu una watu wao wenye akili na walio bora ambao wengine huwaendea ili kupata majibu ya maswali magumu kama vile chanzo na kusudi la maisha na mwisho wa ainabinadamu. Lakini wana mwono-ndani na mwongozo gani wa kutoa? Kutoamini kuwapo kwa Mungu, kuamini kwamba habari za Mungu hazijulikani, mageuzi, na mawazo na nadharia nyinginezo nyingi zenye kutatanisha na zenye kupingana ambazo hazitoi mnurisho zaidi kuliko zile desturi na shirikina za wakati uliopita. Mambo mengi ya kilimwengu yanayofuatiwa huonekana pia kutoa kadiri fulani ya uradhi na utimizo. Watu husema juu ya mafanikio na maendeleo katika sayansi, usanii, muziki, michezo, siasa, na kadhalika. Wanafurahia muda wao mfupi wa utukufu. Hata hivyo, habari za historia na vitabu vyenye rekodi za mafanikio ya watu vya leo vimejaa mashujaa waliosahauliwa. Yote hayo ni utupu, upuzi, ubatili, upumbavu, kukosa kusudi, na fadhaiko.
9. Wengi hugeukia ufuatiaji upi unaokosa faida?
9 Kutambua kukosa faida kwa jitihada hizo, wengi hugeukia ufuatiaji wa vitu vya kimwili—wakikusanya fedha na kupata vitu ambavyo fedha zaweza kununua—na kufanya ufuatiaji huo mbalimbali uwe mradi wao maishani. Wanasadiki kwamba furaha hutokana na utajiri, mali, na kutafuta anasa. Hawakazi tu akili zao juu ya hayo bali pia wana nia ya kudhabihu kila kitu—afya, familia, hata dhamiri. Tokeo ni nini? Badala ya kupata utimilifu, ‘wamejichoma kwa maumivu mengi.’ (1 Timotheo 6:10) Haishangazi kwamba Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake waache kuenenda kama mataifa yaenendavyo kwa sababu ya kukosa faida kwa njia hiyo ya kufikiri.
10. Akili za watu wa ulimwengu ‘zimetiwaje giza’?
10 Ili kuonyesha kwamba ulimwengu hauna lolote linalostahili kuonewa kijicho au kuigwa, Paulo aliendelea kusema kwamba “akili zao zimetiwa giza.” (Waefeso 4:18) Bila shaka, ulimwengu una watu wenye akili na wenye ujuzi katika karibu kila uwanja wa jitihada. Hata hivyo, Paulo alisema kwamba walikuwa gizani kiakili. Kwa nini? Maneno yake hayahusu uwezo au stadi zao za kiakili. Neno “akili” yaweza kurejezea pia kitovu cha ufahamu wa kibinadamu, makao ya uelewevu, mtu wa kindani. Wamo gizani kwa sababu hawana nuru ya kuwaongoza au hisi ya mwelekezo katika jitihada zao. Hilo laweza kuonwa katika hisi yao isiyoweza kupambanua mema na mabaya. Huenda watu wakafikiri kwamba mtazamo wa leo wa kutohukumu-hukumu, kukubali chochote kinachosemwa au kutendwa ni kutiwa nuru, lakini, kulingana na Paulo, huo kwa kweli ni mtazamo uliotiwa giza. Kiroho, wanapapasa-papasa katika giza tititi.—Ayubu 12:25; 17:12; Isaya 5:20; 59:6-10; 60:2; linganisha Waefeso 1:17, 18.
11. Ni nini kisababishi cha giza la kiakili ulimwenguni?
11 Kwa nini watu wanaweza kuwa wenye akili, hata wenye akili nyingi sana, katika mambo mengi sana na hata hivyo kuwa katika giza la kiroho? Kwenye 2 Wakorintho 4:4, Paulo alitupatia jibu: “Mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.” Ni baraka yenye thamani kubwa kama nini kwamba wale wanaokubali habari njema tukufu wamekuja kugeuzwa akili na kutiwa nuru katika moyo!
Mioyo Yenye Ujinga na Isiyo na Hisi
12. Ulimwengu ‘umefarikishwa na uhai wa Mungu’ katika njia gani?
12 Ili kutusaidia tuone zaidi kwa nini ni lazima tugeuzwe akili na kutiwa nuru katika moyo, Paulo alielekeza uangalifu wetu kwenye uhakika wa kwamba mwenendo wa ulimwengu ‘umefarikishwa na uzima wa Mungu.’ (Waefeso 4:18) Si kwamba watu hawaamini tena katika Mungu au kwamba wamekuwa wasiomtii Mungu kabisa. Mwandishi mmoja wa safu za magazeti ya habari alieleza jambo hilo hivi: “Badala ya maneno wasiomtii Mungu acheni tubuni neno jipya: kasoro-Mungu. Watu walio kasoro-Mungu hutaka kusifiwa kwa ajili ya kuamini katika Mungu huku wakimweka Yeye katika kisanduku, wakimwondoa Yeye Jumapili asubuhi tu na kutomruhusu Yeye kuathiri maoni yao ya ulimwengu wa kisiasa au maisha zao za kibinafsi katika siku nyinginezo za juma. [Wao] huamini katika Mungu kwa kadiri fulani lakini hawafikiri ana mengi ya kusema kuhusu jamii ya ki-siku-hizi.” Paulo alieleza jambo hilo hivi katika barua yake kwa Warumi: “Walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru.” (Warumi 1:21) Kila siku twaona watu wanaoishi maisha bila kumfikiria Mungu hata kidogo. Kwa hakika, wao hawampi heshima wala shukrani yoyote.
13. Ni nini “uzima [uhai, NW] wa Mungu”?
13 Usemi “uzima [uhai, NW] wa Mungu” ni wenye maana. Unaonyesha zaidi jinsi giza la kiakili na la kiroho linavyoharibu hisi za watu za mambo yenye thamani. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “uhai” hapo si biʹos (ambalo kwalo hutoka maneno kama vile “biolojia,” “biografia”), linalomaanisha njia ya maisha, au mtindo-maisha. Bali, neno ni zo·eʹ (ambalo kwalo hutoka maneno kama vile “zuu,” “zuulojia”). Linamaanisha “uhai ukiwa jambo la asili, uhai katika maana kamili, uhai kama vile Mungu alivyo nao. . . . Mwanadamu amefarikishwa na uhai huo kwa sababu ya lile Anguko [dhambi ya Adamu],” kulingana na Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words. Hivyo, Paulo alikuwa akituambia kwamba giza la kiakili na la kiroho halikuongoza watu wa ulimwengu kwenye uharibifu wa mwili tu bali pia liliwatenganisha na lile tumaini la uhai wa milele ambalo Mungu hutoa. (Wagalatia 6:8) Kwa nini? Paulo aliendelea kutuambia sababu.
14. Ni nini sababu moja kwa nini ulimwengu umefarikishwa na uhai wa Mungu?
14 Kwanza kabisa, alisema kwamba ni “kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao.” (Waefeso 4:18) Fungu la maneno “uliomo ndani yao” lakazia kwamba ujinga huo si kwa sababu ya kukosa fursa bali ni kwa sababu ya kukatalia mbali ujuzi wa Mungu kimakusudi. Fasiri nyinginezo za fungu hilo la maneno ni: “mkatao wao wa asili wa kumjua Mungu” (The Anchor Bible); “bila ujuzi kwa sababu wameifunga mioyo yao wasiupate” (The Jerusalem Bible). Kwa sababu wanakatalia mbali, au kupuuza kimakusudi, ujuzi sahihi wa Mungu, hawana msingi wa kupata aina ya uhai ambao Yehova huwatolea wale wanaozoea imani katika Mwana wake, aliyesema hivi: “Uzima [uhai, NW] wa milele ndio huu, Wakujue wewe Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3; 1 Timotheo 6:19.
15. Ni nini kinachochangia kufarikishwa kwa ulimwengu na uhai wa Mungu?
15 Sababu nyingine kwa nini ulimwengu kwa ujumla umefarikishwa na uhai wa Mungu, kulingana na Paulo, ni “ugumu [ukosefu wa hisi, NW] wa mioyo yao.” (Waefeso 4:18) Hapo “ukosefu wa hisi” humaanisha kwa msingi kufanywa kuwa gumu, kana kwamba kufunikwa kwa ngozi nene-nene. Sote twajua jinsi ngozi nene-nene hukua. Mwanzoni huenda ngozi ikawa nyororo na yenye kuitikia miguso vyepesi, lakini ikifunuliwa kwa mbano au msuguano fulani kwa kurudia-rudia, inafanywa kuwa ngumu na nene, ikifanyiza ngozi nene. Haihisi tena kuwashwa huko. Vilevile, watu hawazaliwi na moyo uliofanywa kuwa mgumu au usio na hisi hivi kwamba kwa asili hawana hisi kumwelekea Mungu. Lakini kwa sababu twaishi ulimwenguni na twafunuliwa kwa roho yao, haichukui muda mrefu kwa moyo kuwa usio na hisi au kufanywa kuwa mgumu ikiwa haulindwi. Ndiyo sababu Paulo alionya hivi: “Angalieni . . . mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi.” (Waebrania 3:7-13; Zaburi 95:8-10) Kwa hiyo, ni jambo la hima kama nini kwamba tubaki tukiwa tumegeuzwa akili na kutiwa nuru katika moyo!
“Wakiisha Ishiwa na Hisi Zote za Adili”
16. Ni nini tokeo la giza la kiakili na kufarikishwa kwa ulimwengu na uhai wa Mungu?
16 Tokeo la giza na kufarikishwa huko linafanyiwa muhtasari na maneno ya Paulo yafuatayo: “Wakiisha kufa ganzi [ishiwa na hisi zote za adili, NW] wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani.” (Waefeso 4:19) Usemi ‘kwisha ishiwa na hisi zote za adili’ humaanisha kihalisi “kwisha kuacha kuhisi maumivu,” maumivu ya adili. Ndivyo moyo usio na hisi huwa. Unapoacha kuhisi maumivu makali ya dhamiri na hisi ya kupaswa kutoa hesabu mbele za Mungu, hakuna kizuizi tena. Hivyo, Paulo alisema kwamba “wanajitia” katika mwenendo mlegevu na uchafu. Hiyo ni hatua ya kimakusudi, ya kujitakia mwenyewe. Maneno “mwenendo mlegevu”, (NW) kama yalivyotumiwa katika Biblia, huonyesha mtazamo wenye ufidhuli, wenye utovu wa haya, unaodharau sheria na mamlaka. Vilevile, “kila namna ya uchafu” haitii ndani upotovu wa kingono tu bali pia mambo mapotovu yanayofanywa kwa kisingizio cha dini, kama vile zile desturi na sherehe za uzazi zilizofanywa kwenye hekalu la Artemi katika Efeso, ambazo wasomaji wa barua za Paulo walifahamu sana.—Matendo 19:27, 35.
17. Kwa nini Paulo alisema kwamba watu ambao wameishiwa hisi zote za adili hutenda dhambi “kwa pupa”?
17 Kana kwamba kujifurahisha bila kizuizi katika mwenendo mlegevu na katika kila namna ya uchafu hakukuwa jambo baya vya kutosha, Paulo aongeza kwamba watu wa jinsi hiyo hutenda “kwa pupa,” (NW). Wakati watu ambao wangali wana kadiri fulani ya hisi za adili wanapotenda dhambi, huenda angaa wakahisi majuto na kujitahidi kutoirudia. Lakini wale ambao ‘wamekwisha ishiwa na hisi zote za adili’ hutenda dhambi “kwa pupa” (“na bado wanaomba kupata zaidi,” The Anchor Bible). Mtangazaji mmoja wa redio alieleza hivi wakati mmoja: “Ukisherehekea kwa kujifurahisha sana, utatamani vitumbuizo zaidi.” Wanatumbukia kwa hamu katika kidimbwi cha upotovu mpaka wadidimie kabisa katika vina vyacho—nao waona hilo kuwa jambo la kawaida. Huo ni ufafanuzi ulio sahihi kama nini wa “mapenzi ya Mataifa”!—1 Petro 4:3, 4.
18. Kwa kutoa muhtasari, Paulo alifafanuaje hali ya kiakili na ya kiroho ya ulimwengu?
18 Hivyo, katika mistari mitatu tu, Waefeso 4:17-19, Paulo afunua hali ya kiadili na ya kiroho ya kweli ya ulimwengu. Aonyesha kwamba mawazo na nadharia zinazoendelezwa na walimwengu wenye kufikiri na ule ufuatiaji mno wa mali na anasa hauna faida hata kidogo. Aonyesha wazi kwamba kwa sababu ya giza la kiakili na la kiroho, ulimwengu umo katika matata ya kiadili, yanayozidi kuwa mabaya. Mwishoni, kwa sababu ya ujinga na ukosefu wa hisi unaojiletea wenyewe, ulimwengu umekuja kufarikishwa na uhai wa Mungu bila tumaini. Kwa hakika, tuna sababu nzuri za kutoenenda kama vile mataifa yaenendavyo!
19. Ni maswali gani ya muhimu ambayo ni lazima bado yachunguzwe?
19 Kwa kuwa giza katika akili na moyo ndilo linalousababisha ulimwengu ufarikishwe na Yehova Mungu, twaweza kuondoleaje mbali giza kutoka kwa akili na mioyo yetu? Naam, twapaswa kufanya nini ili tuenende kama watoto wa nuru na kubaki tukiwa na upendeleo wa Mungu? Hilo litachunguzwa katika makala ifuatayo.
Je! Waweza Kueleza?
◻ Ni nini kilichochochea shauri la Paulo lenye nguvu kwenye Waefeso 4:17-19?
◻ Kwa nini njia za ulimwengu zinakosa faida na zimo gizani?
◻ Ni nini chamaanishwa na usemi “wamefarikishwa na uzima [uhai, NW] wa Mungu”?
◻ Ni nini matokeo ya akili iliyotiwa giza na moyo usio na hisi?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Efeso lilikuwa na sifa mbaya kwa ajili ya upotovu walo wa adili na ibada ya sanamu
1. Mpiganaji Mroma katika Efeso
2. Magofu ya hekalu la Artemi
3. Mahali pa michezo katika Efeso
4. Artemi wa Efeso, kijimungu-kike cha uzazi
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wakuu wa ulimwengu wana mwono-ndani upi wa kutoa?
Nero
[Hisani]
Musei Capitolini, Roma