Helo—Mateso ya Milele au Kaburi la Ujumla?
JE! Umeambiwa kwamba wale Mababa wa Kanisa wa mapema, wale wanatheolojia wa enzi za kati, na wale Walioleta Mapinduzi Makubwa ya Kidini walitoa hoja kwamba yale mateso ya helo yalikuwa ya milele? Ikiwa ndivyo, huenda ikakushangaza kujua kwamba baadhi ya wanachuo wa Biblia wenye kuheshimiwa sana wanapinga maoni hayo sasa. Katika Uingereza, mmoja wao, John R. W. Stott, aandika kwamba “Andiko linaelekezea uangamizo, na kwamba ‘mateso ya milele yanayohisiwa’ ni pokeo linalopaswa kujitiisha kwa mamlaka kuu zaidi ya Andiko.”—Essentials—A Liberal-Evanjelical Dialogue.
Ni nini kilichomwongoza akate maneno kwamba fundisho la mateso ya milele halitegemei Biblia?
Somo la Lugha
Hoja yake ya kwanza inahusisha lugha. Yeye aeleza kwamba Biblia inaporejezea hali ya mwisho ya laana (“Gehena”; ona kisanduku, ukurasa 8) mara nyingi inatumia msamiati wa “uangamizo,” “kitenzi [cha Kigiriki] apollumi (kuangamiza) na nomino apòleia (uangamizo).” Je! maneno hayo hurejezea mateso? Stott aonyesha kwamba kitenzi hicho kinapokuwa chenye kutenda na kuelekeza, apollumi humaanisha “-ua.” (Mathayo 2:13; 12:14; 21:41) Hivyo, kwenye Mathayo 10:28 mahali ambapo King James Version hutaja kule kuangamiza kwa Mungu “nafsi na mwili pia katika helo,” wazo la asili ni kuangamiza katika kifo, si katika mateso ya milele. Kwenye Mathayo 7:13, 14, Yesu atofautisha ile ‘njia nyembamba inayoongoza kwenye uzima’ na ile ‘njia pana inayoongoza kwenye maangamizi.’ (Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa sababu nzuri yeye afikia mkataa huu: “Ikiwa kuua ni kuunyima mwili uhai, helo ingeonekana kuwa kunyimwa uhai wa kimwili na wa kiroho pia, yaani, kutoweshwa kwa mtu.”—Essentials, kurasa 315-16.
Kufasiri Masimulizi ya Moto wa Helo
Bado, wanadini wengi watakubaliana na msimamizi wa Southern Baptist Convention Morris H. Chapman, aliyesema hivi: “Mimi huhubiri helo halisi.” Aliongeza hivi: “Biblia huiita ‘ziwa la moto,’ na sidhani kwamba fasili hiyo yaweza kufanyiwa maendeleo.”
Ni kweli, usimulizi wa moto unaotumiwa katika Biblia ungeweza kutokeza picha ya akilini ya mateso. Hata hivyo, kitabu Essentials huonyesha hivi: “Bila shaka ni kwa sababu sisi sote tumepata kuona uchungu mkali wa kuchomeka, kwamba katika akili zetu moto hushirikishwa na ‘mateso yanayohisiwa.’ Lakini kazi kuu ya moto si kusababisha uchungu, bali ni kuangamiza, kama vile meko yote ya kuchomea taka ulimwenguni kote yanavyoshuhudia.” (Ukurasa 316) Kukumbuka tofauti hiyo ya maana kutatusaidia kuepuka kutafuta-tafuta maana fulani katika Maandiko ambayo kwa kweli haimo humo. Baadhi ya vielelezo:
Kuhusu wale wanaotupwa katika Gehena, Yesu alisema kwamba “funza wao hafi, wala moto hauzimiki.” (Marko 9:47, 48) Vikivutwa na maneno katika kitabu cha apokrifa cha Yudithi (“Akitia nyama yao moto na funza, nao watalia na kuumia daima.”—Yudithi 16:17, The Jerusalem Bible), baadhi ya vitabu vya kufafanua Biblia hushikilia kauli kwamba maneno ya Yesu hudokeza mateso ya milele. Hata hivyo, kitabu cha apokrifa cha Yudithi, ambacho hakikupuliziwa na Mungu, si kiwango cha kuamua maana ya maandishi ya Marko. Isaya 66:24, andiko ambalo yaonekana kwamba Yesu alitaja, lasema kwamba moto na funza wanaiangamiza miili iliyokufa (“mizoga,” asema Isaya) ya maadui wa Mungu. Hakuna kidokezo chochote cha mateso ya milele yanayohisiwa katika ama maneno ya Isaya ama yale ya Yesu. Masimulizi ya moto hufananisha uangamizo kamili.
Ufunuo 14:9-11 husema juu ya wengine ambao “[watateswa] kwa moto na kiberiti . . . Na moshi wa maumivu yao hupanda juu hata milele na milele.”a Je! hilo lathibitisha mateso ya milele yanayohisiwa katika moto wa helo? Kwa kweli, fungu hilo la maneno lasema tu kwamba waovu wanateswa, si kwamba wanateswa milele. Andiko hilo lasema kwamba moshi—uthibitisho kwamba moto umefanya kazi yao ya uangamizo—ndio unaoendelea milele, si mateso ya moto.
Ufunuo 20:10-15 lasema kwamba katika “ziwa la moto na kiberiti, . . . watateswa mchana na usiku hata milele na milele.” Linaposomwa mara ya kwanza, hilo laweza kusikika kama uthibitisho wa mateso ya milele yanayohisiwa, lakini sivyo hata kidogo. Kwa nini? Miongoni mwa sababu nyinginezo ni kwamba, mwisho wa “yule mnyama na yule nabii wa uongo” na “mauti na Kuzimu [Hadesi, NW]” utakuwa katika lile linaloitwa “ziwa la moto.” Kama vile huenda ukakata maneno kwa urahisi, yule mnyama, yule nabii wa uwongo, kifo, na Hadesi si watu halisi; kwa hiyo, hawawezi kupatwa na mateso ya milele yanayohisiwa. Badala ya hivyo, aandika G. B. Caird katika A Commentary on the Revelation of St. John the Divine, “ziwa la moto” humaanisha “kutoweka na kusahauliwa kabisa.” Ufahamu wa hilo wapasa kufikiwa kwa urahisi, kwani Biblia yenyewe hutaarifu hivi kuhusu hilo ziwa la moto: “Hii ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto.”—Ufunuo 20:14.
Kutenganisha Mapacha wa Kitheolojia
Zijapokuwa hoja hizo, waamini wengi husisitiza kwamba “uangamizo” halimaanishi vile neno hilo linavyosema bali lamaanisha mateso ya milele. Kwa nini? Kufikiri kwao kunavutwa na pacha la kidini la moto wa helo—lile fundisho la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu. Na kwa kuwa kanisa lao huenda ikawa limeyaendeleza mafundisho hayo kwa muda wa karne nyingi, huenda wakahisi kwamba maandiko yanayosema juu ya uangamizo kwa kweli humaanisha mateso ya milele. Ingawaje, nafsi ya kibinadamu isiyokufa haiwezi kutoweka—ndivyo wengi wanavyosababu.
Lakini ona yale ambayo yule kasisi Mwanglikana Philip E. Hughes aliyosema: “Kushikilia kauli kwamba ni nafsi ya kibinadamu pekee ndiyo isiyokufa kiasili ni kudumisha msimamo usiokubaliwa popote katika fundisho la Andiko, kwani katika masimulizi ya kibiblia asili ya kibinadamu huonwa sikuzote kuwa yenye kufanyizwa kikamili na hali ya kiroho na ya kimwili. . . . Onyo la Mungu mwanzoni, kuhusu ule mti uliokatazwa, ‘Siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa,’ lilielekezwa kwa mwanadamu akiwa kiumbe cha kimwili-kiroho—kama angekula kutoka kwa mti huo, angekufa akiwa mtu wa kimwili-kiroho. Hakuna dokezo lolote kwamba sehemu yake ilikuwa isiyokufa na kwa hiyo kufa kwake kungekuwa kwa sehemu tu.”—The True Image—The Origin and Destiny of Man in Christ.
Vivyo hivyo, mwanatheolojia Clark Pinnock asema hivi: “Wazo hili [kwamba nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa] limekuwa na uvutano juu ya theolojia kwa muda mrefu, mrefu sana lakini si la kibiblia. Biblia haifundishi kutokufa kwa nafsi kiasili.” Ezekieli 18:4, 20 na Mathayo 10:28 huthibitisha hilo. Tena zaidi ya hayo, Yesu mwenyewe alisema juu ya rafiki yake mfu Lazaro kuwa alikuwa “amelala” au kulala usingizi. Yesu alisema kwamba ‘angeenda apate kumwamsha.’ (Yohana 11:11-14) Kwa hiyo mtu wa kibinadamu, au nafsi ya kibinadamu, Lazaro alikuwa amekufa, lakini hata baada ya wakati fulani kupita, angeweza kufufuliwa, kurudishwa kwenye uhai tena. Mambo ya hakika huonyesha hilo. Yesu alifufua Lazaro kutoka kwa wafu.—Yohana 11:17-44.
Mambo hayo huathirije fundisho la mateso ya milele? Huko nyuma katika karne ya 17, mtunga insha William Temple alisema hivi: “Kuna [maandiko] yanayosema juu ya kutupwa katika moto usiofifia. Lakini tusipoyaona hayo kwa maoni yaliyodhaniwa tu kwamba kile kinachotupwa humo hakiangamiki, tutapata wazo, si kwamba kitateketea milele, bali kwamba kitaangamizwa.” Uchanganuzi huo ulio sahihi ungali kweli, kwani ni jambo ambalo Biblia hufundisha hasa.
Bila shaka, una sababu za kushurutisha za kutilia shaka wazo la mateso ya milele yanayohisiwa katika helo. Au labda wataka kupita hatua hiyo ya kutilia shaka tu na kufuata lile shauri la profesa wa theolojia Pinnock, aliyesema hivi: “Imani zote kabisa zinazozunguka [fundisho la] helo, kutia na mateso yasiyokoma, . . . zapasa kuondolewa mbali kwa msingi wa fundisho la hakika.” Naam, adili, haki, na—la maana zaidi—Neno la Mungu, Biblia, hukuambia ufanye vivyo hivyo.
Ukifanya hivyo, utaona kwamba asili ya kweli ya helo ni ya hakika kwelikweli. Waweza kupata habari ya kusaidia juu ya kichwa hiki katika kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duninai.b Tafadhali waombe Mashahidi wa Yehova kitabu hicho unapokutana nao. Soma sura “Inakuaje Wakati wa Kufa?” “Je! Kweli Kuna Mahali Penye Moto wa Mateso?” na “Ufufuo—wa Nani, na Wapi?” Utapata kuona kwamba asili ya kweli ya helo si ya hakika tu bali pia yenye kutoa tumaini pia.
[Maelezo ya Chini]
a Katika fungu hilo la maneno ya Biblia, “[mateso] ya moto” yarejezea hasa mateso ya kiroho, ambayo hata hivyo yana kikomo. Ili kupata maelezo zaidi, ona Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
KUFASILI MANENO
Katika makala hii maneno “helo” na “moto wa helo” kama yalivyotumiwa na wanatheolojia katika Jumuiya ya Wakristo yanarejezea neno la Kigiriki geʹen·na, linalotokea mara 12 katika “Agano Jipya.” (Mathayo 5:22, 29, 30; 10:28; 18:9; 23:15, 33; Marko 9:43, 45, 47; Luka 12:5; Yakobo 3:6) Ingawa tafsiri mbalimbali za Biblia hufasiri neno hilo la Kigiriki kuwa “helo,” tafsiri nyingine huligeuza kuwa “Gehena” (Jehanum). Linalingana na “mauti ya pili, ziwa la moto,” ufananisho wa uangamizo wa milele unaopatikana katika kitabu cha mwisho cha Biblia.—Ufunuo 20:14.
Kuhusu maneno mengine mawili yanayotafsiriwa nyakati nyingine kuwa “helo,” A Dictionary of The Bible (1914), iliyohaririwa na William Smith, husema hivi: “Helo . . . ndilo neno linalotumiwa na watafsiri kwa kawaida na kwa kusikitisha ili kufasiri lile neno la Kiebrania Sheoli. Labda ingalikuwa afadhali kudumisha neno hilo la Kiebrania Sheoli, au vingine kulifasiri sikuzote ‘kaburi’ au ‘shimo’. . . . Katika A[gano] J[ipya], neno Hadesi, kama vile Sheoli, nyakati nyingine humaanisha ‘kaburi’ tu . . . Ni katika maana hiyo kwamba imani husema juu ya Bwana yetu ‘Alikwenda chini ndani ya helo,’ ikimaanisha hali ya wafu kwa ujumla.”
Tofauti na Gehena, inayofananisha uangamizo wa mwisho, Sheoli na Hadesi hurejezea kifo katika kaburi la ujumla la ainabinadamu, kukiwa na taraja la kuinuliwa kwenye uhai tena.—Ufunuo 20:13.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Yesu alimwamsha Lazaro kutoka kwenye usingizi wa kifo