Matumizi Yafaayo na Yasiyofaa ya Picha za Kidini
MANDHARI ni katika St. Petersburg, Urusi. Tarehe ni Agosti 2, 1914. Watu wenye kusisimuka wanaopepeza picha za sanamu wamekusanyika kwenye jumba la kifalme la maliki. Altare imejengwa katikati ya jumba kubwa. Picha ya rangi ya mwanamke mwenye mtoto mikononi mwake yasimama juu ya altare hiyo. Picha hiyo ya sanamu inaitwa “Mama wa Mungu wa Vladimir.” Makutano ya watu huiona kuwa ndiyo hazina iliyo takatifu zaidi katika Urusi.
Kwa kweli, picha hiyo ya sanamu huaminiwa kuwa yafanya miujiza. Katika 1812, wakati majeshi ya Urusi yaliposhambulia Napoléon, Jemedari Kutuzov alisali kabla ya kufanya hivyo. Sasa, baada ya kuingiza nchi yake vitani, Maliki Nicholas wa 2 asimama mbele yayo. Mkono wake wa kulia ukiwa umeinuliwa, yeye aapa hivi: “Ninaapa kwa uzito kwamba sitaleta amani maadamu adui hata mmoja abaki kwenye udongo wa Urusi.”
Majuma mawili baadaye maliki huyo ahiji Mosko kuomba baraka ya Mungu juu ya majeshi yake. Katika Cathedral of the Assumption, yeye apiga magoti na kusali mbele ya kifuniko chenye picha za sanamu zenye vito—kiwambo chenye picha za rangi za Yesu, Mariamu, malaika, na “watakatifu.”
Vitendo hivyo vya kidini vilishindwa kukinga msiba. Katika miaka inayopungua minne, majeshi ya Urusi yalipoteza wanajeshi milioni sita na kupoteza eneo kubwa sana. Tena zaidi ya hayo, maliki huyo, mke wake, na watoto wao watano waliuawa kikatili. Badala ya kutawalwa na umaliki wa muda wa karne nyingi sana, nchi hiyo ilianza kutawalwa na serikali ya mapinduzi iliyopinga dini. Kutumaini picha za sanamu kwa Maliki Nicholas kulithibitika kuwa bure.
Hata hivyo, hadi leo katika Urusi na mabara mengine, mamilioni huendelea kutoa heshima ya kuzidi kwa sanamu za picha. Hilo latokeza maswali ya maana. Mungu huonaje vitendo vya ujitoaji vinavyofanywa mbele ya picha hizo? Na namna gani ile desturi ya kuziangika kwenye kuta za nyumba?
Biblia Husema Nini?
Yesu alipokuwa duniani, alitii Sheria ya Mungu iliyotolewa kupitia Musa. Hiyo ilitia ndani ya pili kati ya zile zinazoitwa Amri Kumi, inayotaarifu hivi: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu.”—Kutoka 20:4, 5.
Kwa hiyo, Yesu hakumwabudu Mungu kwa msaada wa picha au sanamu zilizofanywa kwa mikono ya wanadamu. Badala yake, ibada yake ilipatana na julisho hili la Baba yake: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW]; ndilo jina langu; na utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu.”—Isaya 42:8.
Tena zaidi ya hayo, Yesu alieleza kwa nini Mungu apaswa kuabudiwa bila msaada wa vitu vya kimwili. “Saa inakuja,” akasema “ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24.
Kama vile Yesu, wanafunzi wake wa kweli waliwafundisha wengine njia sahihi ya kuabudu. Kwa kielelezo, wakati mmoja mtume Paulo alisema na umati wa wanafalsafa Wagiriki waliotumia sanamu kuabudu vijimungu vyao visivyoonekana. Aliwaambia juu ya Muumba wa mwanadamu akasema hivi: “Haitupasi kudhani ya kuwa Uungu ni mfano wa dhahabu au fedha au jiwe, vitu vilivyochongwa kwa ustadi na akili za wanadamu.” Baadaye, mtume uyo huyo alieleza kwamba Wakristo “[huenenda] kwa imani, si kwa kuona” na kwamba ni lazima Wakristo “[waikimbie] ibada ya sanamu.”—Matendo 17:16-31; 2 Wakorintho 5:7; 1 Wakorintho 10:14.
Ono moja maishani mwa mtume Petro huonyesha kwamba alikuwa mwepesi wa kusahihisha tendo lolote lililoweza kuongoza kwenye ibada ya sanamu. Wakati afisa wa jeshi la Kiroma Kornelio aliposujudu miguuni pake, Petro alikataa. Alimwinua, akisema: “Simama, mimi nami ni mwanadamu.”—Matendo 10:26.
Kwa habari ya mtume Yohana, yeye aliduwazwa sana na njozi za kimungu hivi kwamba alisujudu miguuni pa malaika mmoja. “Angalia” malaika huyo akashauri. “Usifanye hivi; mimi ni mjoli wako, na wa ndugu zako manabii, na wa wale wayashikao maneno ya kitabu hiki. Msujudie Mungu.” (Ufunuo 22:8, 9) Mtume huyo alithamini shauri hilo. Kwa upendo, aliandika tukio hilo kwa manufaa yetu.
Lakini maono hayo yaliyo juu yanahusianaje na matumizi ya picha za kidini? Ikiwa halikuwa jambo lifaalo kwa Kornelio kumsujudia mmoja wa mitume wa Kristo, namna gani kutoa heshima ya kuzidi kwa picha zisizo hai za “watakatifu”? Na ikiwa halikuwa jambo lifaalo kwa mmoja wa mitume wa Kristo kusujudia malaika aliye hai, basi namna gani kutolea heshima ya kuzidi picha zisizo hai za malaika? Kwa hakika, vitendo hivyo ni kinyume cha onyo hili la Yohana: “Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu.”—1 Yohana 5:21.
Zikiwa Misaada ya Kufundisha Yenye Kupamba
Hiyo haimaanishi kwamba kuwa tu na picha ya mandhari fulani ya Kibiblia ni ibada ya sanamu. Gazeti hili hutumia vizuri picha za matukio ya Kibiblia zikiwa misaada ya kufundisha. Pia, mandhari za matukio ya Kibiblia zaweza kutumiwa ili kupamba kuta za nyumba na majengo. Hata hivyo, Mkristo wa kweli asingetaka kuangika picha inayojulikana kuwa yenye kutolewa na wengine heshima ya kuzidi, wala asingeangika kwenye ukuta wake picha isiyowakilisha Biblia ifaavyo.—Warumi 14:13.
Picha nyingi za sanamu za Jumuiya ya Wakristo huonyesha duara ya nuru kuzunguka vichwa vya Yesu, Mariamu, malaika, na “watakatifu.” Hiyo huitwa halo. Halo ilianzia wapi? “Mwanzo wayo haukuwa wa Kikristo,” yakiri The Catholic Encyclopedia (chapa ya 1987), “kwani ilitumiwa na wasanii na wachongaji wapagani kuwakilisha kwa ufananisho fahari na nguvu kuu za viabudiwa mbalimbali.” Zaidi ya hayo, kitabu The Christians, cha Bamber Gascoigne, kina picha iliyopatikana kutoka katika Capitoline Museum katika Roma ya kijimungu-jua chenye halo. Kijimungu hicho kiliabudiwa na wapagani Waroma. Baadaye, aeleza Gascoigne, “halo ya jua” “iliazimwa na Ukristo.” Naam, halo inahusiana na ibada ya jua ya kipagani.
Je! picha zinazochanganya matukio ya Kibiblia na ufananisho mbalimbali wa ibada ya sanamu ya kipagani zafaa kuangikwa kwenye ukuta wa nyumba ya Mkristo? La. Biblia hushauri hivi: “Pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? . . . Kwa hiyo, tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema Bwana [Yehova, NW], Msiguse kitu kilicho kichafu, nami nitawakaribisha.”—2 Wakorintho 6:16, 17.
Wakati ulipopita, wale waliodai kuwa Wakristo walianza kupuuza shauri hilo. Uasi-imani ulisitawi, kama ilivyokuwa imetabiriwa na Yesu na mitume wake. (Mathayo 24:24; Matendo 20:29, 30; 2 Petro 2:1) Mapema katika karne ya nne W.K., maliki Mroma Konstantino alifanya Ukristo wenye uasi-imani kuwa dini ya Taifa. Sasa mtiririko wa wapagani wakaanza kujijulisha rasmi kuwa “Wakristo.” Zoea la kawaida miongoni mwao lilikuwa ibada ya mifano ya maliki. Walikuwa pia wakiangika picha za wazazi wao wa kale na watu wengine mashuhuri. “Kulingana na ibada ya maliki,” aeleza John Taylor katika kitabu chake Icon Painting, “watu waliabudu picha yake [maliki] iliyochorwa kwa rangi kwenye kitambaa kizito na mbao, na kutoka hapo [ibada ya maliki] hadi kutolea picha za sanamu heshima ya kuzidi haikuwa hatua kubwa.” Hivyo, mahali pa ibada ya picha ya kipagani palichukuliwa na kutoa heshima ya kuzidi kwa picha za Yesu, Mariamu, malaika, na “watakatifu.”
Viongozi wa Kanisa Waliteteaje Hilo?
Kulingana na The Encyclopedia of Religion, viongozi wa kanisa walitumia hoja zilezile za zamani ambazo wanafalsafa wapagani walikuwa wametumia. Watu kama vile Plutarki, Dio Krisostomu, Maksim wa Tiro, Selsio, Porfiri, na Juliano walikiri kwamba sanamu hazina uhai. Lakini wapagani hao walitetea matumizi yao ya sanamu kwa kutoa hoja kwamba hiyo ilikuwa misaada katika kuabudu kwao vijimungu visivyoonekana. Mchunguzi mmoja wa picha za sanamu kutoka Urusi Leonid Ouspenski akiri hivi katika kitabu The Meaning of Icons: “Mababa wa Kanisa walitumia chombo cha falsafa ya Kigiriki, wakigeuza uelewevu na lugha yacho kupatana na theolojia ya Kikristo.”—Linganisha Wakolosai 2:8.
Watu wengi walipata utetezi huo wa kitheolojia wa kutolea mifano heshima ya kuzidi kuwa mgumu kuelewa. “Tofauti kati ya kuabudu picha ya sanamu kwa ajili ya kile ambacho huenda ikawakilisha, au kuiabudu yenyewe . . . ilikuwa kidogo mno kwa yeyote ila wale wenye elimu ya juu sana,” ataarifu John Taylor katika Icon Painting.
Kwa upande ule mwingine, yale ambayo Biblia husema kuhusu mifano ya kidini ni rahisi sana kuelewa. Fikiria Emilia, anayeishi Johannesburg, Afrika Kusini. Alikuwa Mkatoliki mchaji mwenye bidii na alikuwa akipiga magoti na kusali mbele ya picha. Halafu, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alibisha mlangoni pake. Alisisimuka kuona katika Biblia ya Kireno kwamba Mungu ana jina, Yehova. (Zaburi 83:18, Almeida) Wakati wa funzo lake la Biblia, aliuliza hivi: “Ni lazima nifanye nini ili kuepuka kumchukiza Yehova?” Shahidi huyo alielekeza kwenye picha zilizokuwa zimeangikwa ukutani wake akamwomba asome Zaburi 115:4-8. Usiku huo mume wa Emilia alipokuja nyumbani, Emilia alimwambia kwamba alitaka kuondolea mbali picha zake za kidini. Mume wake alikubali. Siku iliyofuata, aliwaambia wana wake wawili, Tony na Manuel, wavunje-vunje picha hizo na kuzichoma. Leo, baada ya miaka 25 hivi, je, Emilia ana majuto yoyote juu ya hilo? La. Kwa kweli, pamoja na familia yake, yeye amewasaidia majirani wengi wake wawe waabudu wa Yehova wenye furaha.
Maono kama hayo yamerudiwa nyakati nyingi. Likiwa tokeo la kazi ya kufanya wanafunzi ya Mashahidi wa Yehova ya ulimwenguni pote, mamilioni wanajifunza kumwabudu Mungu “katika roho na kweli.” Wewe pia waweza kujionea baraka kutokana na njia hiyo bora zaidi ya ibada kwa sababu, kama vile Yesu alivyosema, “Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.”—Yohana 4:23, 24.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Maliki Nicholas wa 2 akiyabariki majeshi yake kwa kutumia picha ya sanamu
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Picha ya C. N.