Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je! watu watafufuliwa ikiwa hawakubali Ukristo wa kweli sasa na wanakufa kabla ya mwanzo wa ile dhiki kubwa?
Ni vema kwa sisi sote kukinza mbetuko wowote wa kutenda tukiwa waamuzi, tukitambua kwamba hatimaye, hukumu ya Yehova kupitia Yesu Kristo ndiyo ya maana. (Yohana 5:22; Matendo 10:42; 2 Timotheo 4:1) Lakini Maandiko huandaa habari yenye kusaidia katika kujibu swali lililotangulia.
Kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote ni sehemu ya maana ya ‘ishara ya kuwapo kwa Yesu.’ Ishara hiyo imeonekana wazi tangu mapema katika karne hii. Kazi ya kuhubiri inatokeza kugawanywa kwa watu wa mataifa yote kwa utimizo wa kielezi cha Yesu cha “kondoo” na “mbuzi.” Utendaji huo wa kuhubiri na kugawanya unapomalizika, “dhiki kubwa,” italeta mwisho wa mfumo mbovu wa mambo uliopo.—Mathayo 24:3, NW, 21, 22; 25:31-46.
Yehova, pamoja na Mwana wake, wataamua kama wowote wanaokataa ujumbe wa Ufalme na wanaokufa kabla ya kufyatuka kwa dhiki kubwa wako kwenye kikundi cha mbuzi. Yesu alisema kwamba mbuzi ‘wataingia katika adhabu ya milele.’ Kwa hiyo, twaweza kukata maneno kwamba wale wanaoamuliwa na Mungu kuwa mbuzi hawatapokea ufufuo. Wao wana hukumu inayofanana na ile ya wale ‘watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele’ wakati wa dhiki kubwa.—2 Wathesalonike 1:9.
Lakini namna gani wale ambao huenda ikawa hawakupata ujumbe wa Ufalme kwa kadiri ya kutosha ili wangaliweza kuchukua msimamo wa kiakili kwa ajili ya au dhidi ya kweli kabla ya wao kufa katika ‘siku hizi za mwisho’?—2 Timotheo 3:1.
Wengi wanaokufa wakati kazi ya kuhubiri inapoendelea kabla ya dhiki kubwa kwa hakika watafufuliwa. Hilo laonyeshwa na yale tunayosoma kwenye Ufunuo 6:7, 8 kuhusu wapanda farasi wa ufananisho. Watu wengi wamekufa wakiwa majeruhi wa vita, upungufu wa chakula, na tauni hatari. Kwa kuwa ni “Hadesi” inayodai majeruhi hao wa “Kifo,” hao watafufuliwa wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, wakati Hadesi itakapotoa nje wote waliomo ndani yayo. (Ufunuo 20:13, NW) Wengi wa hao watakaoinuliwa kwenye uhai huenda ikawa walipata kujua ujumbe wa Ufalme kwa kadiri fulani kabla ya kufa.
Twaweza kushukuru kama nini kwamba Yesu hakuwaachia wanadamu waamue ni nani walio na sifa za kikondoo na wale wenye sifa za kimbuzi! Wanadamu wasiokamilika hawawezi kukadiri ifaavyo kadiri ya fursa ambayo mtu alikuwa nayo ya kusikia na kukubali habari njema. Je! twaweza kujua hali yake ya moyoni ilikuwaje au kama alipenda uadilifu kikweli? Je! twaweza kukadiri jinsi ambavyo itikio lake huenda ikawa liliathiriwa na familia yake, dini yake ya kwanza, au mavutano mengine? Bila shaka hatuwezi. Hata hivyo, twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo wanaweza kukadiri mambo hayo na kisha kufikia maamuzi ambayo ni makamilifu, ya haki, na yenye uadilifu.—Kumbukumbu la Torati 32:4; Isaya 11:1-5.
Kwa hiyo, hakuna sababu yoyote ya sisi kukisia kuhusu ni nani miongoni mwa wale ambao wamekufa hivi karibuni watakaofufuliwa au ambao hawatafufuliwa. Hilo ni jambo ambalo hatukupewa mamlaka kufanya. (Linganisha Luka 12:13, 14.) Ni jambo la hekima zaidi kwa sisi kungojea maamuzi ya wale Waamuzi waadilifu Yehova Mungu na Yesu Kristo. Hilo litatupa sisi amani zaidi ya akili tukiwa watumishi wa Yehova. Litatusaidia pia tutolee uangalifu mzuri zaidi lile ambalo tumepewa mgawo kufanya—‘kuenenda, kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi, kuwafundisha kuyashika yote ambayo Yesu aliamuru.’—Mathayo 28:19, 20.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]
Kondoo wa Leicester, Meyers