Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 7/1 kur. 2-7
  • Wakristo wa Mapema na Ulimwengu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakristo wa Mapema na Ulimwengu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Katika Nyakati za Kimitume
  • Wakristo Katika Ulimwengu wa Kiroma
  • Raia Wema, na Bado Wenye Kunenwa Vibaya
  • Kudharauliwa Kuwa Farakano Jipya
  • Washtakiwa Juu ya Kugeuza Watu kwa Uchokozi
  • Hakuna Umoja wa Kidini
  • Ukristo wa Mapema na Serikali
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Bila Wazo la Kuridhiana!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wakristo na Jamii ya Kibinadamu Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wanaendelea Kutembea Katika Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 7/1 kur. 2-7

Wakristo wa Mapema na Ulimwengu

KARIBU miaka elfu mbili iliyopita, jambo zuri kupita yote lilitukia katika Mashariki ya Kati. Mwana mzaliwa wa pekee wa Mungu alitumwa kutoka makao yake ya kimbingu kuishi kwa muda mfupi katika ulimwengu wa ainabinadamu. Wanadamu wengi waliitikiaje? Mtume Yohana ajibu hivi: “[Yesu] alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja kwake [Israeli], wala walio wake hawakumpokea.”—Yohana 1:10, 11.

Ulimwengu haukumkubali Yesu, Mwana wa Mungu, hata kidogo. Kwa nini? Yesu alieleza sababu moja aliposema hivi: “Ulimwengu . . . hunichukia mimi, kwa sababu mimi naushuhudia ya kuwa kazi zake ni mbovu.” (Yohana 7:7) Hatimaye, ulimwengu uu huu—uliowakilishwa na baadhi ya viongozi wa dini ya Kiyahudi, mfalme wa Edomu, na mwanasiasa Mroma—ulimwua Yesu. (Luka 22:66–23:25; Matendo 3:14, 15; 4:24-28) Namna gani wafuasi wa Yesu? Je! Ulimwengu ungekuwa tayari zaidi kuwakubali? La. Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwaonya hivi: “Kama mngekuwa wa [sehemu ya, NW] ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa [sehemu ya, NW] ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.”—Yohana 15:19.

Katika Nyakati za Kimitume

Maneno ya Yesu yalitimia. Majuma machache tu baada ya kifo chake, mitume wake walikamatwa, wakatishwa, na kupigwa. (Matendo 4:1-3; 5:17, 18, 40) Muda mfupi baadaye, Stefano mwenye bidii aliburutwa mbele ya Sanhedrini ya Kiyahudi kisha akapigwa kwa mawe hadi kufa. (Matendo 6:8-12; 7:54, 57, 58) Baadaye, mtume Yakobo aliuawa na Mfalme Herode Agripa 1. (Matendo 12:1, 2) Wakati wa safari zake za umishonari, Paulo alinyanyaswa kwa uchochezi wa Wayahudi wa Diaspora.—Matendo 13:50; 14:2, 19.

Wakristo wa mapema waliitikiaje upinzani wa jinsi hiyo? Katika siku za mapema, wakati mamlaka za kidini zilipowakataza mitume wasihubiri kwa jina la Yesu, mitume walitaarifu hivi: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.” (Matendo 4:19, 20; 5:29) Huo uliendelea kuwa mtazamo wao wakati wowote upinzani ulipotokea. Hata hivyo, mtume Paulo aliwashauri Wakristo katika Roma “[wa]itii mamlaka [ya kiserikali] iliyo kuu.” Aliwashauri hivi pia: “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.” (Warumi 12:18; 13:1) Kwa hiyo, Wakristo wa mapema walilazimika kuwa na usawaziko ulio mgumu. Walimtii Mungu akiwa Mtawala wao mkuu. Wakati uleule, walijitiisha kwa mamlaka za kitaifa wakajaribu kuishi kwa amani pamoja na watu wote.

Wakristo Katika Ulimwengu wa Kiroma

Bila shaka huko nyuma katika ulimwengu wa Milki ya Roma ya karne ya kwanza, Wakristo walinufaika kutokana na Pax Romana, au Amani ya Roma, iliyodumishwa na majeshi ya Roma. Kanuni thabiti ya sheria na utaratibu, zile barabara nzuri, na ule usafiri wa baharini uliokuwa na usalama wa kadiri fulani ulifanyiza mazingira yaliyochochea upanuzi wa Ukristo. Yaonekana Wakristo wa mapema walitambua deni lao kwa jamii na wakatii amri ya Yesu ya ‘kumpa Kaisari yaliyo ya Kaisari.’ (Marko 12:17) Akimwandikia maliki wa Roma Antoninus Pius (138-161 C.E.), Justin Martyr alidai kwamba Wakristo, walilipa ushuru zao “kwa utayari zaidi kuliko watu wote.” (First Apology, sura 17) Katika 197 W.K., Tertullian aliwaambia watawala Waroma kwamba watoza ushuru wao “walikuwa na deni la shukrani kwa Wakristo” kwa ajili ya kulipa ushuru zao kwa njia ya kudhamiria. (Apology, sura 42) Hiyo ilikuwa njia moja waliyofuata lile shauri la Paulo kwamba walipaswa kujitiisha kwa mamlaka za juu zaidi.

Zaidi ya hayo, kwa kadiri ambavyo kanuni zao za Kikristo zingeruhusu, Wakristo wa mapema walijaribu kuishi kwa amani pamoja na majirani wao. Lakini hilo halikuwa jambo rahisi. Ulimwengu uliowazunguka ulikuwa hasa wenye kukosa adili na ulijihusisha sana na ibada ya sanamu ya Kigiriki na Kiroma, ambayo karibuni ilikuwa imeongezewa ibada ya maliki. Kwa ujumla dini ya Kiroma ya Kipagani ilikuwa dini ya Taifa, kwa hiyo kukataa hata kidogo kuifuata kungeweza kuonwa kuwa uadui kuelekea Taifa. Wakristo waliathiriwaje na hilo?

Profesa wa Oxford E. G. Hardy aliandika hivi: “Tertullian anataja mambo mengi ambayo hayakuweza kufanywa na Mkristo mwenye kudhamiria, kwani yalihusisha ibada ya sanamu: k.m. kiapo kilichokuwa cha kawaida kwenye mikataba; kumulikwa kwa milango kwenye sikukuu, na kadhalika.; sherehe zote za kidini za Kipagani; michezo na tamasha; kazi ya kufundisha fasihi ya kilimwengu [ya upagani wa zamani]; utumishi wa kijeshi; vyeo vya kiserikali.”—Christianity and the Roman Government.

Naam, ilikuwa vigumu kuishi katika ulimwengu wa Kiroma bila kusaliti imani ya Kikristo. Mtungaji-vitabu aliye Mkatoliki wa Ufaransa A. Hamman aandika hivi: “Haikuwezekana hata kidogo kufanya jambo lolote lisilohusu kijimungu fulani. Msimamo wa Mkristo ulimletea matatizo ya kila siku; aliishi tofauti na jamii kwa ujumla . . . Alikabili matatizo yaliyorudia-rudia akiwa nyumbani, barabarani, sokoni . . . Barabarani, awe ni raia wa Roma au la, Mkristo alipaswa avue kofia yake alipokuwa akipita hekalu au sanamu fulani. Angeweza kufanyaje hivyo bila kutiliwa shaka, na bado angewezaje kufuata amri hiyo bila kufanya tendo la utii? Ikiwa angekuwa na biashara na angehitaji kukopa fedha, alilazimika amwapie mwenye kumkopesha fedha hizo kwa jina la miungu. . . . Ikiwa angekubali cheo cha kiserikali, alitazamiwa atoe dhabihu. Ikiwa angejiandikisha jeshini, angeepukaje kuchukua kiapo na kushiriki katika desturi za utumishi wa kijeshi?”—La vie quotidienne des premiers chrétiens (95-197) (Maisha ya Kila Siku Miongoni mwa Wakristo wa Mapema, 95-197 W.K.).

Raia Wema, na Bado Wenye Kunenwa Vibaya

Karibu 60 au 61 W.K., wakati Paulo alipokuwa katika Roma akingojea kuhukumiwa na Maliki Nero, Wayahudi mashuhuri walisema hivi kuwahusu Wakristo wa mapema: “Kwa maana katika habari za madhehebu hiyo [farakano hilo, NW] imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali.” (Matendo 28:22) Rekodi ya kihistoria yathibitisha kwamba Wakristo walinenwa vibaya—lakini isivyo haki. Katika kitabu chake The Rise of Christianity, E. W. Barnes asimulia hivi: “Katika hati zayo za mapema zenye mamlaka harakati ya Kikristo inawakilishwa kwa ujumla kuwa yenye adili na yenye kutii sheria. Washiriki wayo walitamani kuwa raia wema na waaminifu-washikamanifu. Waliepuka makosa na njia za upagani. Katika maisha ya faragha walijaribu kuwa majirani wenye amani na marafiki wenye kuaminika. Walifundishwa kuwa wenye uzito na wenye kiasi, wenye bidii na wenye kuishi maisha safi. Miongoni mwa ufisadi na ukosefu wa adili ulioenea sana walikuwa wenye kufuatia haki na ukweli, ikiwa walikuwa waaminifu-washikamanifu kwa kanuni zao. Viwango vyao vya ngono vilikuwa vya juu: kifungo cha ndoa kilistahiwa na maisha ya familia yalikuwa safi. Mtu angalifikiri kwamba, wakiwa na sifa hizo wasingeweza kuwa raia wasumbufu. Na bado kwa muda mrefu walidharauliwa, kunenwa vibaya, na kuchukiwa.”

Kama vile ulimwengu wa kale haukumwelewa Yesu, ndivyo ambavyo haukuwaelewa Wakristo na kwa hiyo ukawachukia. Kwa kuwa walikataa kumwabudu maliki na miungu ya kipagani, walishtakiwa juu ya kutokuamini kuwako kwa Mungu. Kama msiba ungetukia, walilaumiwa kuwa walikuwa wamewakasirisha miungu. Kwa sababu hawakuhudhuria michezo ya kuigiza isiyo ya kiadili au maonyesho ya mapigano yenye umwagaji wa damu, walionwa kutokuwa wenye urafiki, hata ‘wenye kuchukia jamii ya kibinadamu.’ Maadui wao walidai kwamba familia zilivunjwa na “farakano” la Kikristo na kwamba kwa sababu hiyo lilihatarisha uthabiti wa kijamii. Tertullian alisema juu ya waume wapagani waliowapendelea wake zao wafanye uzinzi kuliko wao kuwa Wakristo.

Wakristo walichambuliwa kwa sababu walipinga utoaji-mimba, uliozoewa sana wakati huo. Na bado, maadui wao waliwashtaki juu ya kuwaua watoto. Ilidhaniwa kwamba kwenye mikutano yao walikunywa damu ya watoto waliotolewa kuwa dhabihu. Wakati uleule, maadui wao walijaribu kuwalazimisha wale soseji ya damu, wakijua kwamba hilo lilipingana na dhamiri yao. Hivyo wapinzani hao walikanusha shtaka lao wenyewe.—Tertullian, Apology, Sura 9.

Kudharauliwa Kuwa Farakano Jipya

Mwanahistoria Kenneth Scott Latourette aliandika hivi: “Bado wengine walidharau Ukristo kwa ajili ya kuwa na mwanzo wa karibuni na wakautofautisha na ukale wa washindani wao [Dini ya Kiyahudi na dini za kipagani za Kigiriki na Kiroma].” (A History of the Expansion of Christianity, Buku 1, ukurasa 131) Katika miaka ya mwanzo-mwanzo ya karne ya pili W.K., mwanahistoria Mroma Suetonius aliuita Ukristo “ushirikina mpya na mbaya.” Tertullian alithibitisha kwamba jina Kikristo lenyewe lilichukiwa na kwamba Wakristo walikuwa farakano lisilopendwa. Akisema juu ya njia ambayo maofisa wa Milki ya Roma walivyowaona Wakristo katika karne ya pili, Robert M. Grant aliandika hivi: “Maoni ya msingi yalikuwa kwamba Ukristo ulikuwa tu dini isiyofaa kitu, na labda yenye madhara.”—Early Christianity and Society.

Washtakiwa Juu ya Kugeuza Watu kwa Uchokozi

Katika kitabu chake Les premiers siècles de l’Eglise (Karne za Mapema za Kanisa), profesa wa chuo kikuu cha Sorbonne Jean Bernardi aliandika hivi: “[Wakristo] walipaswa watoke nje na kusema kila mahali na kwa kila mtu. Kwenye barabara kuu na katika majiji, kwenye nyanja za umma na nyumbani. Wakiwa wamekaribishwa au la. Kwa maskini, na kwa matajiri waliozuiwa na mali zao. Kwa wadogo na kwa magavana wa mikoa ya Kiroma . . . Walilazimika kusafiri barabarani, kupanda meli, na kwenda hadi miisho ya dunia.”

Je! walifanya hivyo? Yaonekana walifanya hivyo. Profesa Léon Homo asimulia kwamba Wakristo wa mapema walipingwa na watu wote kwa sababu ya “bidii yao ya kugeuza watu.” Profesa Latourette asema kwamba huku Wayahudi walipopoteza bidii yao ya kugeuza watu, “Wakristo, kwa upande ule mwingine, walikuwa wamishonari wenye uchokozi na kwa hiyo walichochea chuki.”

Katika karne ya pili W.K., mwanafalsafa Mroma Celsus alichambua njia za kuhubiri za Wakristo. Alisema kwamba Ukristo uliwafaa wale wasio na elimu na kwamba ungeweza ‘kuwasadikisha tu wajinga, watumwa, wanawake, na watoto wadogo.’ Aliwashtaki Wakristo juu ya kufundisha kwa njia ya kusisitiza sana wale “waliokuwa rahisi kudanganywa,” wakiwalazimisha “waamini bila kufikiria kwa njia ya kusababu.” Alidai kwamba waliwaambia wanafunzi wao wapya hivi: “Msiulize maswali; amini tu.” Hata hivyo, kulingana na Origen, Celsus mwenyewe alikiri kwamba “si wale wasio na elimu na wale wenye cheo cha chini pekee walioongozwa na fundisho la Yesu wafuate dini Yake.”

Hakuna Umoja wa Kidini

Wakristo wa mapema walichambuliwa zaidi kwa sababu walidai kuwa na kweli juu ya Mungu wa kweli. Hawakukubali umoja wa kidini, au kuchanganya imani. Latourette aliandika hivi: “Tofauti na imani nyingi za wakati huo, wao [Wakristo] walikuwa na uadui kuelekea dini nyinginezo. . . . Tofauti na ule uvumilivu mwingi ulioonyeshwa na madhehebu mengine, walitangaza kwamba walikuwa na kweli isiyokanushika.”

Katika 202 W.K., Maliki Septimius Severus alitoa amri iliyowakataza Wakristo wasigeuze watu. Hata hivyo, hilo halikuwazuia wasitoe ushahidi juu ya imani yao. Latourette asimulia tokeo: “Kukataa kwa [Ukristo wa mapema] kutoridhiana na upagani wa wakati huo na pia [kutoridhiana] na desturi nyingi za kijamii na mazoea ya kiadili ya nyakati hizo, [Ukristo wa mapema] ulisitawisha ushikamano na tengenezo lililoupinganisha na jamii. Kujitenga kwenyewe kulikohitajiwa ili kujiunga na [tengenezo] hilo kuliwapa washiriki walo usadikisho uliokuwa chanzo cha nguvu dhidi ya mnyanyaso na [chanzo] cha bidii katika kugeuza wengine.”

Kwa hiyo, rekodi ya kihistoria, yaonyesha wazi. Kwa ujumla, huku Wakristo wa mapema walipokuwa wakijitahidi kuwa raia wema na kuishi kwa amani na watu wote, walikataa kuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19, NW) Walikuwa wenye staha kwa wenye mamlaka. Lakini Kaisari alipowakataza wasihubiri, hawakuwa na la kufanya ila kuendelea kuhubiri. Walijaribu kuishi kwa amani na watu wote lakini walikataa kuridhiana juu ya viwango vya kiadili na ibada ya sanamu ya kipagani. Kwa sababu ya hayo yote, walidharauliwa, kunenwa vibaya, kuchukiwa, na kunyanyaswa, kama vile Kristo alivyokuwa ametabiri wangetendwa.—Yohana 16:33.

Je! kujitenga kwao na ulimwengu kuliendelea? Au, je, baada ya wakati kupita wale waliodai kuzoea Ukristo walibadili mtazamo wao katika jambo hilo?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Msimamo wa Mkristo ulimletea matatizo ya kila siku; aliishi tofauti na jamii kwa ujumla”

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Ukristo [ulidharauliwa] kwa ajili ya kuwa na mwanzo wa karibuni na [kutofautishwa] na ukale wa washindani wao”

[Picha katika ukurasa wa 3]

Kwa sababu Wakristo walikataa kumwabudu maliki wa Roma na miungu ya kipagani, walishtakiwa kuwa wenye kutoamini kuwako kwa Mungu

[Hisani]

Museo della Civiltà Romana, Roma

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wakristo wa karne ya kwanza walijulikana kuwa wahubiri wenye bidii wa ujumbe wa Ufalme

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

Cover: Alinari/Art Resource, N.Y.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki