Wakristo na Jamii ya Kibinadamu Leo
“Mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu.”—MATHAYO 24:9.
1. Ni nini ambayo ingekuwa alama dhahiri ya Ukristo?
KUJITENGA na ulimwengu kulikuwa alama dhahiri ya Wakristo wa mapema. Kristo alipokuwa akisali kwa Baba yake wa kimbingu, Yehova, alisema hivi juu ya wanafunzi wake: “Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa [si sehemu ya, NW] ulimwengu kama nisivyo wa [sehemu ya, NW] ulimwengu.” (Yohana 17:14) Alipoitwa mbele ya Pontio Pilato, Yesu alisema hivi: “Ufalme wangu sio wa [si sehemu ya, NW] ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Kujitenga na ulimwengu kwa Ukristo wa zamani kunathibitishwa na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na wanahistoria.
2. (a) Je! kungekuwa badiliko lolote katika uhusiano kati ya wafuasi wa Yesu na ulimwengu wakati ulipopita? (b) Je! Ufalme wa Yesu ungekuja kupitia kugeuzwa kwa mataifa?
2 Je! Yesu alifunua baadaye kwamba kungekuwa badiliko katika uhusiano kati ya wafuasi wake na ulimwengu na kwamba Ufalme wake ungekuja kupitia kugeuzwa kwa ulimwengu kwenye Ukristo? La. Hakuna lolote katika yale ambayo wafuasi wake walipuliziwa kuandika baada ya kifo cha Yesu kilichodokeza jambo hilo hata kidogo. (Yakobo 4:4 [lililoandikwa muda mfupi kabla ya 62 W.K.]; 1 Yohana 2:15-17; 5:19 [lililoandikwa karibu 98 W.K.]) Kinyume cha hilo, Biblia hufungamanisha “kuwapo” kwa Yesu na “kuja” kwake kwa baadaye katika mamlaka ya Ufalme, na “umalizio wa mfumo wa mambo,” ukifikia upeo katika “mwisho,” au uharibifu wao. (Mathayo 24:3, 14, 29, 30; Danieli 2:44; 7:13, 14) Katika ile ishara ambayo Yesu alitoa juu ya pa·rou·siʹa, au kuwapo kwake, yeye alisema hivi juu ya wafuasi wake wa kweli: “Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua; nanyi mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu.”—Mathayo 24:9.
Wakristo wa Kweli Leo
3, 4. (a) Ensaiklopedia moja ya Kikatoliki inasimuliaje juu ya Wakristo wa mapema? (b) Mashahidi wa Yehova na Wakristo wa mapema wanasimuliwaje katika maneno ayo hayo?
3 Ni kikundi kipi cha kidini leo ambacho kimejipatia sifa ya uaminifu kwa kanuni za Kikristo na kujitenga na ulimwengu huu, washiriki wacho wakichukiwa na kunyanyaswa? Ni tengenezo jipi la ulimwenguni pote linalolingana kabisa na masimulizi ya kihistoria ya Wakristo wa mapema? Kuhusu hayo, New Catholic Encyclopedia yasema: “Jumuiya ya kale ya Kikristo, ingawa mwanzoni ilionwa kuwa farakano jingine tu ndani ya jamii ya Kiyahudi, ilithibitika kuwa ya pekee katika mafundisho yayo ya kitheolojia, na hasa katika bidii ya washiriki wayo, waliotumikia wakiwa mashahidi wa Kristo ‘katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi’ (Matendo 1.8).”—Buku 3, ukurasa 694.
4 Ebu yaangalia maneno “ilionwa kuwa farakano jingine tu,” “kuwa ya pekee katika mafundisho yayo,” “bidii . . . wakiwa mashahidi.” Na sasa ona jinsi ambavyo ensaiklopedia iyo hiyo inavyosimulia juu ya Mashahidi wa Yehova: “Farakano moja . . . Mashahidi wanasadikishwa sana kwamba mwisho wa ulimwengu utakuja katika muda wa miaka michache sana. Imani hiyo ya wazi sana yaonekana kuwa kani yenye nguvu zaidi inayochochea bidii yao isiyolegea. . . . Wajibu wa msingi wa kila mshiriki wa farakano hilo ni kushuhudia Yehova kwa kutangaza Ufalme Wake unaokaribia. . . . Wao huiona Bibila kuwa chanzo chao pekee cha imani na cha amri ya mwenendo . . . Ili kuwa Shahidi wa kweli ni lazima mtu ahubiri kwa mafanikio katika njia moja au nyingine.”—Buku 7, kurasa 864-5.
5. (a) Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni ya pekee katika njia zipi? (b) Toa vielelezo vinavyoonyesha kwamba imani za Mashahidi wa Yehova zinapatana na Maandiko.
5 Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni ya pekee katika njia zipi? New Catholic Encyclopedia yataja njia chache: “Wao [Mashahidi wa Yehova] wanaulaumu Utatu kuwa ibada ya sanamu ya kipagani . . . Wanamwona Yesu kuwa mkuu zaidi kati ya Mashahidi wa Yehova, ‘mungu’ (ndivyo wanavyotafsiri Yohana 1.1), asiye na cheo cha chini kwa yeyote ila Yehova. . . . Alikufa akiwa mwanadamu akafufuliwa akiwa Mwana wa roho asiyeweza kufa. Tamaa yake na kifo chake ndiyo bei aliyolipa ili kuirudishia ainabinadamu haki ya kuishi milele duniani. Kwa kweli, ule ‘mkutano mkubwa’ (Ufu 7.9) wa Mashahidi wa kweli una tumaini katika Paradiso ya kidunia; ni waaminifu 144,000 tu (Ufu 7.4; 14.1, 4) watakaofurahia utukufu wa kimbingu pamoja na Kristo. Waovu wataharibiwa kabisa. . . . Ubatizo—ambao Mashahidi huzoea kwa kuzamisha . . . [ni] ufananisho wa nje wa wakfu wao kwa utumishi wa Yehova Mungu. . . . Mashahidi wa Yehova wamejulikana na wengi kwa sababu ya kukataa utiaji damu mishipani . . . Adili zao za ndoa na za ngono ni ngumu sana.” Huenda Mashahidi wa Yehova wakawa wa pekee katika njia hizo, lakini msimamo wao juu ya mambo hayo yote unategemea Biblia kwa uthabiti.—Zaburi 37:29; Mathayo 3:16; 6:10; Matendo 15:28, 29; Warumi 6:23; 1 Wakorintho 6:9, 10; 8:6; Ufunuo 1:5.
6. Mashahidi wa Yehova wamedumisha msimamo upi? Kwa nini?
6 Kitabu hicho cha Roma Katoliki kinaongeza kwamba katika 1965 (yaonekana huo ndio mwaka makala hiyo iliandikwa) “Mashahidi hawakuwa bado wameona kwamba walikuwa sehemu ya jamii walimoishi.” Yaonekana mtungaji-kitabu huyo alifikiri kwamba wakati ulipopita na Mashahidi wa Yehova wakawa wengi zaidi na “kuzidi kuwa na sifa za kanisa tofauti na za farakano,” wangekuwa sehemu ya ulimwengu huu. Lakini hilo halikuthibitika kuwa kweli. Leo, kukiwa Mashahidi zaidi ya mara nne kuliko katika 1965, Mashahidi wa Yehova wamedumisha kwa upatano msimamo wao kwa habari ya ulimwengu huu. “Wao si wa [si sehemu ya, NW] ulimwengu,” kama vile Yesu asivyokuwa “[sehemu ya, NW] ulimwengu.”—Yohana 17:16.
Wenye Kujitenga Lakini Si Wenye Uadui
7, 8. Kama ilivyokuwa kweli kuhusu Wakristo wa mapema, ni nini iliyo kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova leo?
7 Akitaja vile yule mteteaji-ukristo wa karne ya pili Justin Martyr alivyowatetea Wakristo wa mapema, Robert M. Grant aliandika hivi katika kitabu chake Early Christianity and Society: “Ikiwa Wakristo wangekuwa wanamapinduzi wangebaki wakiwa wamejificha ili kufikia lengo lao. . . . Wao ni marafiki wema zaidi wa maliki kwa habari ya amani na utaratibu mzuri.” Vilevile, Mashahidi wa Yehova leo wanajulikana kotekote ulimwenguni kuwa raia wanaopenda amani na wenye utaratibu. Serikali, iwe ni za aina gani, zajua kwamba hazina sababu yoyote ya kuwahofu Mashahidi wa Yehova.
8 Mhariri mmoja kutoka Amerika Kaskazini aliandika hivi: “Mawazio yenye ushupavu na yenye kushuku kupita kiasi yangehitajiwa ili kuamini kwamba Mashahidi wa Yehova wanaweza kuleta tisho la aina yoyote kwa utawala wowote wa kisiasa; wao ni wenye kutochochea mapinduzi na wenye kupenda amani kadiri kikundi cha kidini kiwezavyo kuwa.” Katika kitabu chake L’objection de conscience (Katazo la Kudhamiria), Jean-Pierre Cattelain aandika hivi: “Mashahidi ni wenye kujitiisha kikamilifu kwa wenye mamlaka nao hutii sheria kwa kawaida; wanalipa kodi zao na hawajaribu kutilia shaka, kubadili, au kuziharibu serikali, kwani wao hawajihusishi na mambo ya ulimwengu huu.” Cattelain aendelea kuongeza kwamba Serikali inapodai tu uhai wao, ambao wameuweka wakfu kikamili kwa Mungu, ndipo Mashahidi wa Yehova hukataa kutii. Kwa njia hiyo wao wanafanana sana na Wakristo wa mapema.—Marko 12:17; Matendo 5:29.
Waeleweka Vibaya kwa Jamii za Watawala
9. Kuhusu kujitenga na ulimwengu, ni nini tofauti moja kubwa iliyo kati ya Wakristo wa mapema na Wakatoliki wa ki-siku-hizi?
9 Maliki wengi Waroma waliwaelewa vibaya Wakristo wa mapema na wakawanyanyasa. Ukionyesha kwa nini, The Epistle to Diognetus (Waraka kwa Diognetus), unaofikiriwa na wengine kuwa na tarehe ya tangu karne ya pili W.K., wajulisha hivi: “Wakristo wanaishi ulimwenguni, lakini wao hawajihusishi na ulimwengu.” Kwa upande ule mwingine, Baraza la Pili la Vatikani, katika Katiba layo la Kimafundisho juu ya Kanisa, lilisema kwamba Wakatoliki wanapaswa “kuitafuta ufalme wa Mungu kwa kushiriki katika mambo ya kiserikali” na “kufanyia jitihada utakaso wa ulimwengu kutoka ndani.”
10. (a) Wakristo wa mapema walionywaje na jamii za watawala? (b) Mashahidi wa Yehova huonwaje mara nyingi, na itikio lao ni nini?
10 Mwanahistoria E. G. Hardy asema kwamba maliki Waroma waliwaona Wakristo wa mapema kuwa “[watu] wenye idili wa kudharauliwa kwa kadiri fulani.” Mwanahistoria Mfaransa Étienne Trocmé asema juu ya “jinsi maofisa Wagiriki na Waroma wenye elimu nyingi walivyodharau lile waliloona kuwa farakano geni sana la Mashariki [yaani, Wakristo].” Barua kati ya Pliny Mchanga Zaidi, gavana Mroma wa Bithinia, na Maliki Trajan zaonyesha kwamba kwa kawaida jamii za watawala hazikujua asili ya kweli ya Ukristo. Leo vilevile, Mashahidi wa Yehova mara nyingi hueleweka vibaya na hata kudharauliwa na jamii za watawala wa ulimwengu. Hata hivyo, hilo haliwashangazi wala kuwatia hofu Mashahidi.—Matendo 4:13; 1 Petro 4:12, 13.
“Inanenwa Vibaya Kila Mahali”
11. (a) Ni mambo gani yaliyosemwa juu ya Wakristo wa mapema, na ni mambo gani ambayo yamesemwa juu ya Mashahidi wa Yehova? (b) Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika siasa?
11 Ilisemwa hivi juu ya Wakristo wa mapema: “Katika habari za madhehebu hiyo imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali.” (Matendo 28:22) Katika karne ya pili W.K., Celsus mpagani alidai kwamba Ukristo uliwavutia watu wenye hali ya chini sana katika jamii ya kibinadamu. Vivyo hivyo imesemwa juu ya Mashahidi wa Yehova kwamba “kwa ujumla, wao wametoka kati ya wale wenye uhitaji katika jamii yetu.” Mwanahistoria wa kanisa Augustus Neander aliripoti kwamba “Wakristo waliwakilishwa wakiwa wafu kwa habari ya ulimwengu, wasiofaa kwa jambo lolote maishani; . . . na iliulizwa, shughuli za maisha zingekuwaje, ikiwa [watu] wote wangekuwa kama wao?” Kwa sababu Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika siasa, mara nyingi wao pia huonwa kutofaa kitu katika jamii ya kibinadamu. Lakini wangeweza kuwaje wanasiasa wenye bidii na wakati uleule kuwa wateteaji wa Ufalme wa Mungu kuwa tumaini la pekee la ainabinadamu? Mashahidi wa Yehova huzingatia maneno haya ya mtume Paulo: “Shiriki katika kuteseka ukiwa askari-jeshi wa Kristo Yesu. Hakuna askari-jeshi anayetumikia ambaye hujitatanisha na kufuatia mambo ya kiraia, kwa kuwa lengo lake ni kumridhisha yule aliyemwandikisha.”—2 Timotheo 2:3, 4, Revised Standard Version, Chapa ya Ulimwenguni Pote.
12. Mashahidi wa Yehova wanafanana na Wakristo wa mapema katika sehemu gani ya maana ya kujitenga?
12 Katika kitabu chake A History of Christianity, Profesa K. S. Latourette aandika hivi: “Mojawapo masuala ambayo Wakristo wa mapema na ulimwengu wa Kigiriki na wa Kiroma hawakukubaliana nayo lilikuwa juu ya kushiriki katika vita.” Kwa karne za kwanza tatu hakuna maandishi ya Kikristo ambayo yameokoka hadi wakati wetu yaliyowaruhusu Wakristo washiriki katika vita.” Kitabu cha Edward Gibbon The History of the Decline and Fall of the Roman Empire chasema hivi: “Wakristo hawakuweza kuwa wanajeshi, mahakimu, au wakuu, bila kukana wajibu mtakatifu zaidi.” Vivyo hivyo Mashahidi wa Yehova wanafuata msimamo mkali wa kutokuwamo na wanafuata kanuni za Biblia zilizotajwa kwenye Isaya 2:2-4 na Mathayo 26:52.
13. Ni shtaka jipi linalotolewa juu ya Mashahidi wa Yehova, lakini mambo ya hakika huonyesha nini?
13 Mashahidi wa Yehova wanashtakiwa na maadui wao juu ya kuvunja familia. Ni kweli, kuna visa vya familia vinavyogawanyika wakati mshiriki mmoja au wengi zaidi wanapokuwa Mashahidi wa Yehova. Yesu alitabiri kwamba hilo lingetukia. (Luka 12:51-53) Hata hivyo, takwimu zinaonyesha kwamba ndoa zinazovunjika kwa sababu hiyo si za kawaida. Kwa mfano, miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa ndoa 1 kati ya 3 ni zenye mwenzi wa ndoa ambaye si Shahidi. Bado, kiwango cha kutaliki miongoni mwa ndoa hizo zilizochanganyika si cha juu zaidi ya wastani wa kitaifa. Kwa nini? Mitume Paulo na Petro waliwatolea Wakristo waliooana na wenzi wasioamini, shauri lenye hekima, lililopuliziwa, na Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kufuata maneno yao. (1 Wakorintho 7:12-16; 1 Petro 3:1-4) Ndoa iliyochanganyika ikivunjika, karibu sikuzote ni mwenzi asiye Shahidi ambaye huanzisha jambo hilo. Kwa upande mwingine, maelfu mengi ya ndoa yameokolewa kwa sababu wenzi wa ndoa walikuja kuwa Mashahidi wa Yehova wakaanza kutumia kanuni za Biblia maishani mwao.
Wakristo, Si Wanautatu
14. Ni shtaka jipi lililoletwa dhidi ya Wakristo wa mapema, na kwa nini hilo ni kinyume?
14 Ni jambo la kinyume kwamba katika Milki ya Roma, mojawapo mashtaka yaliyoletwa dhidi ya Wakristo wa mapema lilikuwa kwamba wao hawakuamini kuwako kwa Mungu. Dakt. Augustus Neander aandika hivi: “Wale waliokana miungu [ya kipagani], wasioamini kuwako kwa Mungu, . . . ndio jina la kawaida ambalo Wakristo waliitwa miongoni mwa watu.” Ni ajabu kama nini kwamba Wakristo, waliomwabudu Muumba aliye hai wala si miungu mingi, wangeweza kuitwa watu wasioamini kuwako kwa Mungu na wapagani ambao hawakuabudu “miungu, bali kazi ya mikono ya wanadamu; walikuwa miti na mawe.”—Isaya 37:19.
15, 16. (a) Wanadini wengine wamesema nini juu ya Mashahidi wa Yehova, lakini hilo hutokeza swali jipi? (b) Ni nini linaloonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wa kweli?
15 Jambo jingine lililo la kinyume vivyo hivyo ni kwamba leo wenye mamlaka wengine katika Jumuiya ya Wakristo hukana kwamba Mashahidi wa Yehova si Wakristo. Kwa nini? Kwa sababu Mashahidi huukatalia mbali Utatu. Kulingana na fasili ya Jumuiya ya Wakristo yenye kupendelea upande mmoja, “Wakristo ni wale wanaomkubali Kristo kuwa Mungu.” Tofauti na hilo, kamusi ya ki-siku-hizi yafasili nomino “Mkristo” kuwa “mtu anayeamini katika Yesu Kristo na anayefuata mafundisho yake” na “Ukristo” kuwa “dini inayotegemea mafundisho ya Yesu Kristo na ile imani kwamba yeye alikuwa mwana wa Mungu.” Ni kikundi kipi kinachofaana na fasili hiyo kwa ukaribu zaidi?
16 Mashahidi wa Yehova wanakubali ushuhuda wa Yesu mwenyewe kuhusu yeye ni nani. Alisema hivi: “Mimi ni Mwana wa Mungu,” si, “Mimi ni Mungu Mwana.” (Yohana 10:36; linganisha Yohana 20:31.) Wao wanakubali taarifa hii ya Paulo juu ya Kristo, iliyopuliziwa: “Ambaye, akiwa katika umbile la Mungu, hakuhesabu usawa na Mungu kuwa kitu cha kung’ang’aniwa.”a (Wafilipi 2:6, The New Jerusalem Bible) Kitabu The Paganism in Our Christianity chasema hivi: “Yesu Kristo hakutaja kamwe ajabu ya jinsi hiyo [Utatu wenye cheo-sawa], na hakuna popote katika Agano Jipya ambapo neno ‘Utatu’ huonekana. Wazo hilo liliingizwa tu na Kanisa miaka mia tatu baada ya kifo cha Bwana wetu.” Mashahidi wa Yehova wanakubali fundisho la Kibiblia kuhusu Kristo. Wao ni Wakristo, si Wanautatu.
Hakuna Umoja wa Kidini
17. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawashirikiani na harakati ya kutafuta umoja wa kidini, au ya kuchanganya imani?
17 Malalamiko mengine mawili yanayotolewa dhidi ya Mashahidi wa Yehova ni kwamba wao wanakataa kushiriki katika harakati ya kutafuta umoja wa kidini nao wanashiriki katika kule kunakoitwa “kugeuza watu kwa uchokozi.” Wakristo wa mapema walishutumiwa pia juu ya mambo hayo mawili. Bila shaka, Jumuiya ya Wakristo, ikiwa na sehemu zayo za Kikatoliki, Kiorthodox, na Kiprotestanti ni sehemu ya ulimwengu huu. Kama vile Yesu, Mashahidi wa Yehova “si wa [sehemu ya, NW] ulimwengu huu.” (Yohana 17:14) Wangeweza kufanyaje urafiki kupitia harakati za kuchanganya imani na matengenezo ya kidini yanayoendeleza mwenendo na imani zisizo za Kikristo?
18. (a) Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawawezi kuchambuliwa kwa ajili ya kudai kwamba wao pekee ndio huzoea dini ya kweli? (b) Ingawa wanaamini kwamba wana dini ya kweli, wafuasi wa dini ya Roma Katoliki hawana nini?
18 Ni nani aweza kuwachambua Mashahidi wa Yehova kwa haki kwa ajili ya kuamini, kama vile Wakristo wa mapema walivyoamini, kwamba wao pekee ndio wanaozoea dini ya kweli? Hata Kanisa Katoliki, linapodai kinafiki kushirikiana na harakati ya kutafuta umoja wa kidini, lapiga mbiu hivi: “Tunaamini kwamba dini hii moja ya kweli huendelea kuwako katika Kanisa Katoliki na la Kimitume, lililokabidhiwa na Bwana Yesu ile kazi ya kuieneza miongoni mwa watu wote alipowaambia mitume wake: ‘Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi.’” (Baraza la Vatikani 2, “Julisho Juu ya Uhuru wa Kidini”) Lakini, yaonekana kwamba imani ya jinsi hiyo haitoshi ili kuwachochea Wakatoliki wawe na bidii isiyolegea katika kuenenda kufanya wanafunzi.
19. (a) Mashahidi wa Yehova wameazimia kufanya nini, na wakiwa na kusudi gani? (b) Ni nini litakalochunguzwa katika makala ifuatayo?
19 Mashahidi wa Yehova wana bidii ya jinsi hiyo. Wameazimia kuendelea kutoa ushahidi maadamu Mungu awataka wafanye hivyo. (Mathayo 24:14) Kutoa kwao ushahidi ni kwa bidii si kwa uchokozi. Kunachochewa na upendo wa jirani, si na chuki ya ainabinadamu. Wanatumaini kwamba ainabinadamu wengi iwezekanavyo wataokolewa. (1 Timotheo 4:16) Sawa na Wakristo wa mapema, wao hujitahidi ‘kukaa katika amani na watu wote.’ (Warumi 12:18) Jinsi wanavyofanya hivyo itazungumziwa katika makala ifuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Kupata mazungumzo juu ya andiko hili kuhusiana na fundisho la Utatu, ona Mnara wa Mlinzi, Juni 15, 1971, (Kiingereza) kurasa 355-6.
Kwa Njia ya Kupitia
◻ Ni nini lililotia alama Wakristo wa mapema, na Mashahidi wa Yehova wanafananaje nao?
◻ Mashahidi wa Yehova huonyesha wao ni raia wema katika njia zipi?
◻ Jamii za watawala waliwaonaje Wakristo wa mapema, na kuna tofauti yoyote leo?
◻ Usadikisho wa Mashahidi kwamba wao ndio walio na kweli huwasukuma wafanye nini?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Mashahidi wa Yehova wameazimia kuendelea kutoa ushahidi maadamu Mungu awataka wafanye hivyo
[Picha katika ukurasa wa 17]
Pilato alisema: “Tazama, mtu huyu!”—Yule ambaye hakuwa sehemu ya ulimwengu.—Yohana 19:5
[Hisani]
“Ecce Homo” ya A. Ciseri: Florence, Galleria d’Arte Moderna / Alinari/Art Resource, N.Y.