Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 14 kur. 188-201
  • “Wao Si Sehemu ya Ulimwengu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Wao Si Sehemu ya Ulimwengu”
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtazamo Kuelekea Wanadamu Wenzao
  • Waliojitenga na Walio Tofauti na Babiloni Mkubwa
  • Je, Dini Yapasa Ijihusishe na Siasa?
  • Ulimwengu Ulipoenda Vitani
  • Je, Ni Wonyesho wa Kisiasa wa Ufalme wa Mungu?
  • Rekodi ya Kutokuwamo kwa Kikristo
  • Wakati Mifano ya Kitaifa Ilipopata Kuwa Vitu vya Kuabudiwa
  • Msimamo Wao Wataarifiwa Waziwazi
  • Ulimwengu Ulipokuwa na Sikukuu Zao
  • Kuwasaidia Wanadamu Wenzao
  • “Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kumrudia Mungu wa Kweli
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • “Wao Si Sehemu ya Ulimwengu”
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Wakristo na Jamii ya Kibinadamu Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 14 kur. 188-201

Sura ya 14

“Wao Si Sehemu ya Ulimwengu”

KWA kadiri kubwa dini ya kisasa ni sehemu ya ulimwengu sana, hivyo inashiriki katika miadhimisho ya kilimwengu na huonyesha sana roho yao ya utukuzo wa taifa. Makasisi wayo mara nyingi hukiri uhakika huo, na wengi wao hupenda mambo yawe hivyo. Tofauti sana na hivyo, Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake wa kweli: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yn. 17:16, NW.

Rekodi huonyesha nini kwa habari ya Mashahidi wa Yehova katika jambo hili? Je, wao wametoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba wao si sehemu ya ulimwengu?

Mtazamo Kuelekea Wanadamu Wenzao

Wanafunzi wa Biblia wa mapema walijua vyema kwamba Wakristo wa kweli hawangekuwa wa ulimwengu. The Watch Tower lilieleza kwamba kwa sababu wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta walitakaswa na kuzaliwa kwa roho ili waweze kushiriki katika Ufalme wa kimbingu, walitengwa na ulimwengu kwa tendo hilo la Mungu. Kwa kuongezea, lilitaja kwamba walikuwa chini ya wajibu wa kuepuka roho ya ulimwengu—malengo, kujitakia makuu, na matumaini yao, pamoja na njia zao.—1 Yoh. 2:15-17.

Je, hilo liliathiri mtazamo wa Wanafunzi wa Biblia kuelekea watu ambao hawakushiriki imani zao? Hakika halikuwafanya kuwa wenye kujitenga na watu. Lakini wale waliotumia kikweli yale waliyokuwa wakijifunza kutoka Maandiko hawakutafuta ushirika wa watu wa kilimwengu katika njia ya kwamba wangeshiriki namna yao ya maisha. The Watch Tower lilielekeza watumishi wa Mungu kwenye shauri la Biblia la ‘kufanya lililo jema kuelekea wote.’ Lilishauri pia kwamba wanyanyaswapo wapaswa wajitahidi kuepuka hisi za kulipa kisasi na, badala ya hivyo, kama vile Yesu alivyokuwa amesema, wapaswa ‘kuwapenda adui zao.’ (Gal. 6:10; Mt. 5:44-48, NW) Hasa liliwahimiza wajitahidi kushiriki pamoja na wengine kweli zenye thamani kubwa kuhusu uandalizi wa Mungu kwa ajili ya wokovu.

Yaeleweka, kufanya mambo hayo kungewafanya waonwe na ulimwengu kuwa tofauti. Lakini kutokuwa sehemu ya ulimwengu kwahusu zaidi—mengi zaidi.

Waliojitenga na Walio Tofauti na Babiloni Mkubwa

Ili wawe si sehemu ya ulimwengu, ilikuwa lazima wasiwe sehemu ya mifumo ya kidini iliyokuwa imejihusisha sana katika mambo ya ulimwengu na ambayo ilikuwa imefyonza mafundisho na desturi kutoka Babiloni la kale, adui wa muda mrefu wa ibada ya kweli. (Yer. 50:29) Vita ya ulimwengu ya kwanza ilipolipuka, kwa miongo mingi Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamefunua mizizi ya kipagani ya mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, na moto wa helo. Walikuwa pia wamefunua rekodi ya makanisa ya kujaribu kutumia serikali kwa ajili ya makusudi yayo wenyewe ya ubinafsi. Kwa sababu ya mafundisho na mazoea ya Jumuiya ya Wakristo, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wameihusianisha na “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 18:2, NW) Walitaja kwamba ilichanganya kweli na makosa, Ukristo vuguvugu na mambo halisi ya ulimwengu, na kwamba ule mtajo wa Kibiblia “Babiloni” (unaomaanisha, “Mvurugo”) uliieleza vizuri hali hiyo. Waliwahimiza wapendao Mungu watoke katika “Babiloni.” (Ufu. 18:4, NW) Kwa kusudi hilo, mwishoni mwa Desemba 1917 na mapema katika 1918, waligawanya nakala 10,000,000 za toleo la The Bible Students Monthly lililozungumzia habari kuu “Kuanguka kwa Babiloni,” ambalo lilikuwa ufunuo wenye kupiga sana Jumuiya ya Wakristo. Hilo, nalo, lilitokeza uhasama mkatili kutoka kwa makasisi, ambao walitumia kwa kujifaidi kichaa cha wakati wa vita kujaribu kuponda kazi ya Mashahidi wa Yehova.

Kwa lazima, kutoka katika Babiloni Mkubwa kulihusisha kujiondoa kwa mshiriki wa matengenezo yaliyotetea mafundisho yake bandia. Wanafunzi wa Biblia walifanya hivyo, ijapokuwa kwa miaka mingi waliwaona kuwa ndugu zao Wakristo wale mmoja-mmoja katika makanisa waliodai kuwa wamejitakasa kabisa na kuwa na imani katika fidia. Hata hivyo, Wanafunzi wa Biblia hawakuandika tu barua za kujiondoa katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo bali pia, ilipowezekana, baadhi yao walikuwa wakisoma barua zao wenyewe kwa sauti kubwa kwenye mikutano ya kanisa mahali ambapo ilifaa washiriki kujieleza. Ikiwa hilo halikuwezekana, waliweza kupeleka nakala ya barua yao ya kujiondoa—yenye fadhili ikiwa na ushahidi ufaao—kwa kila mshiriki wa kutaniko.

Je, walikuwa pia wakihakikisha kwamba hawakuchukua pamoja na hilo desturi na mazoea yoyote yasiyo ya kumhofu Mungu ya matengenezo hayo? Hali ilikuwaje katika kipindi kilichoongoza hadi kwenye Vita ya Ulimwengu 1?

Je, Dini Yapasa Ijihusishe na Siasa?

Katika uwanja wa kisiasa, watawala wa mengi ya mataifa makuu, kwa sababu ya mahusiano yao na kanisa la Katoliki au la Protestanti, walikuwa wamedai kwa muda mrefu kuwa wenye kupokea ‘haki ya kutawala kutoka kwa Mungu,’ wakiwa wawakilishi wa Ufalme wa Mungu na kwa upendeleo wa pekee wa Mungu. Kanisa liliipa serikali baraka yalo; nayo serikali ikalipa kanisa utegemezo. Je, Wanafunzi wa Biblia walijiingiza katika jambo hilo pia?

Badala ya kuiga makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, walitafuta kujifunza kutokana na mafundisho na kielelezo cha Yesu Kristo na mitume wake. Funzo lao la Biblia liliwaonyesha nini? Vichapo vya mapema vya Watch Tower hufunua ya kuwa walijua kwamba wakati Yesu alipoulizwa maswali na gavana Mroma Pontio Pilato, alitaarifu hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” Ili kujibu swali kuhusu daraka la Yesu, alimwambia gavana huyo hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yn. 18:36, 37, NW) Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba Yesu alishikamana na mgawo huo bila kuyumbayumba. Wakati Ibilisi alipomtolea falme zote za ulimwengu na utukufu wazo, yeye alikataa. Wakati watu walipotaka kumfanya mfalme, alijiondoa. (Mt. 4:8-10; Yn. 6:15) Wanafunzi wa Biblia hawakuepuka uhakika wa kwamba Yesu alirejezea Ibilisi kuwa “mtawala wa ulimwengu” na akasema kwamba Ibilisi ‘hakuwa na mshiko juu yake.’ (Yn. 14:30, NW) Wangeweza kuona kwamba Yesu hakutafuta kujihusisha mwenyewe au wafuasi wake katika mfumo wa kisiasa wa Roma bali kwamba yeye alijishughulisha kabisa na kujulisha “habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Luka 4:43, NW.

Je, kuamini kwao mambo hayo yaliyoandikwa katika Neno la Mungu kuliwatia moyo wasistahi mamlaka ya serikali? Sivyo kabisa. Badala ya hivyo, kuliwasaidia kuelewa kwa nini matatizo yanayowakabili watawala ni mengi mno, kwa nini kuna uvunjaji-sheria mwingi sana, na kwa nini programu za serikali za kufanya hali ya watu kuwa bora mara nyingi hazifanikiwi. Imani yao iliwafanya kuwa na saburi yajapokuwa magumu, kwa sababu walikuwa na uhakika kwamba kwa wakati wake Mungu angeleta kitulizo cha kudumu kwa njia ya Ufalme wake. Wakati huo walielewa kwamba “mamlaka za juu zaidi,” zirejezewazo kwenye Warumi 13:1-7 (KJ), ilikuwa ni watawala wa kilimwengu. Kupatana na hilo, walihimiza kustahi wakuu wa serikali. Katika kuzungumzia Warumi 13:7, C. T. Russell, katika kitabu The New Creation (kilichotangazwa katika 1904), alitaarifu kwamba Wakristo wa kweli “wangekuwa kiasili ndio wenye moyo mweupe zaidi katika kutambua wakuu wa ulimwengu huu, na wenye kutii zaidi sheria na matakwa ya sheria, isipokuwa mahali ambapo hizo zingepatikana zikihitilafiana na matakwa na amri za kimbingu. Ni watawala wachache wa kidunia ikiwa wako ambao watalaumu utambuzi wa Muumba mkuu zaidi na utii mkuu zaidi kwa amri zake. Kwa hiyo, [Wakristo wa kweli] wapaswa kupatikana miongoni mwa wale wenye kutii sheria zaidi wa wakati huu—si wachochezi, si wagomvi, si walaumuo.”

Wakiwa Wakristo, Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba kazi ambayo wapaswa kuwa wakijitoa kwayo ilikuwa kuhubiri Ufalme wa Mungu. Na, kama ilivyotaarifiwa katika buku la kwanza la Studies in the Scriptures, “hilo likifanywa kwa uaminifu, hakutakuwa na wakati wala mwelekeo wa kugaagaa katika siasa za serikali zilizopo.”

Kwa habari hii walikuwa, kwa kadiri kubwa, kama wale Wakristo wa mapema wanaoelezwa na Augustus Neander katika kitabu The History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries: “Wakristo hawakujihusisha na walikuwa tofauti na serikali, . . . na Ukristo ulionekana ukiweza kuwa na uvutano juu ya maisha za kiraia kwa njia ile tu ambayo, lazima iungamwe, ndiyo safi zaidi, kwa kujitahidi kwa njia yenye kutumika kukaza zaidi na zaidi hisi takatifu ndani ya raia wa taifa.”

Ulimwengu Ulipoenda Vitani

Duniani pote matukio ya Vita ya Ulimwengu 1 yalitahini vikali madai ya wale waliodai kuwa Wakristo. Ilikuwa ndiyo vita yenye kuogofya zaidi iliyopata kupigwa kufikia wakati huo; karibu idadi yote ya watu wa ulimwengu ilihusika kwa njia moja au nyingine.

Papa Benedict 15, ijapokuwa Vatikani iliunga mkono zile Serikali Kuu, alijitahidi kudumisha hali ya kuonekana kutofungamana na upande wowote. Hata hivyo, ndani ya kila taifa makasisi, Wakatoliki na Waprotestanti, hawakudumisha msimamo kama huo wa kutokuwamo. Kuhusu hali katika Marekani, Dakt. Ray Abrams, katika kitabu chake Preachers Present Arms, aliandika hivi: “Makanisa yalichukua umoja wa kusudi usiopata kujulikana kufikia wakati huo katika historia ya kidini. . . . Viongozi hawakupoteza wakati wowote katika kujitayarisha kikamili kwa ajili ya wakati huo wa vita. Katika muda wa saa ishirini na nne baada ya vita kutangazwa, Baraza la Muungano wa Makanisa ya Kristo Katika Amerika lilifanya mipango ya ushirikiano kamili zaidi. . . . Kanisa la Katoliki ya Roma, lilijitayarisha kwa ajili ya utumishi kama huohuo chini ya Baraza la Vita la Katoliki la Kitaifa, likielekezwa na maaskofu wakuu kumi na wanne naye Kardinali Gibbons akiwa msimamizi, lilionyesha ujitoaji huohuo kwa kusudi hilo. . . . Makanisa mengi yalifanya mengi zaidi ya yale yaliyoombwa yafanye. Yakawa vituo vya kuandikisha askari wapya.” Wanafunzi wa Biblia walifanya nini?

Ijapokuwa walijaribu kufanya lile ambalo walihisi kuwa lenye kumpendeza Mungu, sikuzote msimamo wao haukuwa wa kutokuwamo kabisa. Yale waliyofanya yaliongozwa na imani, waliyoshiriki pamoja na wengine waliodai kuwa Wakristo, kwamba “mamlaka za juu zaidi” zilikuwa “zimeagizwa rasmi na Mungu,” kulingana na maneno ya King James Version. (Rum. 13:1) Hivyo, kupatana na mbiu iliyopigwa na rais wa Marekani, The Watch Tower lilihimiza Wanafunzi wa Biblia wajiunge katika kushika Mei 30, 1918, kuwa siku ya sala na dua kuhusiana na matokeo ya vita ya ulimwengu.a

Wakati wa miaka ya vita, hali ambamo Wanafunzi wa Biblia mmoja-mmoja walijikuta zilitofautiana sana. Njia ambayo walizishughulikia ilitofautiana pia. Wakihisi wakiwa na wajibu wa kutii ‘mamlaka zilizopo,’ kama vile walivyowarejezea watawala wa kilimwengu, baadhi yao walikwenda katika mahandaki vitani wakiwa na bunduki na beneti. Lakini wakikumbuka lile andiko, “Usiue,” walikuwa wakipiga silaha zao hewani au kujaribu tu kuangusha silaha kutoka mikononi mwa mpinzani. (Kut. 20:13) Wachache, kama vile Remigio Cuminetti, katika Italia, walikataa kuvaa yunifomu ya jeshi. Serikali ya Italia katika wakati huo haikutoa ruhusa kwa yeyote ambaye kwa sababu ya dhamiri hangetwaa silaha. Alijaribiwa kihukumu mara tano na kufungwa katika magereza na katika hospitali ya wagonjwa wa akili, lakini imani na azimio lake vilidumu bila kutikiswa. Katika Uingereza baadhi ya walioomba wapewe ruhusa walipewa mgawo wa kazi ya maana ya kitaifa au kwenye vikosi vya askari wasiopigana. Wengine, kama vile Pryce Hughes, walichukua msimamo wa kutokuwamo kabisa, bila kujali matokeo kwao binafsi.

Angalau kufikia wakati huo, rekodi ya ujumla ya Wanafunzi wa Biblia haikuwa kabisa kama ile ya Wakristo wa mapema waelezwao katika kitabu The Rise of Christianity, cha E. W. Barnes, aliyeripoti hivi: “Pitio la uangalifu la habari yote ipatikanayo huonyesha kwamba, mpaka wakati wa Marcus Aurelius [maliki Mroma kutoka 161 hadi 180 W.K.], hakuna Mkristo aliyepata kuwa mwanajeshi; na hakuna mwanajeshi, baada ya kuwa Mkristo, aliyeendelea katika utumishi wa kijeshi.”

Lakini, mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu 1, hali nyingine ilizuka iliyotaka vikundi vya kidini vionyeshe msimamo wao wa uaminifu-mshikamanifu.

Je, Ni Wonyesho wa Kisiasa wa Ufalme wa Mungu?

Mkataba wa amani, kutia na Agano la Ushirika wa Mataifa, ulitiwa sahihi katika Versailles, Ufaransa, katika Juni 28, 1919. Hata kabla ya mkataba huo wa amani kutiwa sahihi, Baraza la Muungano wa Makanisa ya Kristo Katika Amerika ulionyeshwa kuwa ukipiga mbiu kwamba Ushirika huo ungekuwa “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Nayo Seneti ya Marekani ilipokea rundo la barua kutoka kwa vikundi vya kidini vikiihimiza ihalalishe Agano la Ushirika wa Mataifa.

Mashahidi wa Yehova hawakuunga mkono. Hata kabla ya mkataba huo wa amani kuthibitishwa (katika Oktoba), J. F. Rutherford alitoa hotuba katika Cedar Point, Ohio, katika Septemba 7, 1919, ambayo alionyesha kwamba si Ushirika wa Mataifa bali Ufalme uliosimamishwa na Mungu mwenyewe ndio tumaini pekee kwa wanadamu wenye kusononeka. Ingawa walikubali kwamba muungano wa kibinadamu ili kufanya ziwe bora hali ungeweza kutimiza mema mengi, Wanafunzi wa Biblia hao hawakuwa wakiupa visogo Ufalme wa Mungu mwenyewe kwa kuubadilisha na mpango wa kisiasa uliosimamishwa na wanasiasa na kubarikiwa na makasisi. Badala ya hivyo, walianza kazi ya kutoa ushahidi wa duniani pote kuhusu Ufalme ambao Mungu alikuwa ameuweka mikononi mwa Yesu Kristo. (Ufu. 11:15; 12:10) Katika The Watch Tower la Julai 1, 1920, ilielezwa kwamba hiyo ndiyo kazi ambayo Yesu alikuwa ametabiri kwenye Mathayo 24:14.

Kwa mara nyingine tena, kufuatia Vita ya Ulimwengu 2, Wakristo walikabiliwa na suala linalofanana na hilo. Wakati huo, lilihusu Umoja wa Mataifa, mwandamizi wa Ushirika ule. Vita ya Ulimwengu 2, ilipokuwa ingali inaendelea, katika 1942, Mashahidi wa Yehova walikuwa tayari wametambua kutoka Biblia, kwenye Ufunuo 17:8, kwamba tengenezo la amani ya ulimwengu lingesimama tena, pia kwamba lingeshindwa kuleta amani ya kudumu. Jambo hilo lilielezwa na N. H. Knorr, wakati huo akiwa msimamizi wa Watch Tower Society, katika hotuba ya mkusanyiko “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Kwa ujasiri Mashahidi wa Yehova walipiga mbiu ya maoni ya hali hiyo ya ulimwengu iliyokuwa ikisitawi. Kwa upande ule mwingine, viongozi Wakatoliki, Waprotestanti, Wayahudi walishiriki hasa katika mazungumzo katika San Francisco katika 1945 ambayo katika hayo Katiba ya UM iliandikwa. Kwa watazamaji wa matukio hayo, ilikuwa wazi ni nani waliotaka kuwa “rafiki ya ulimwengu” na ni nani waliokuwa wakijaribu kuwa “si sehemu ya ulimwengu,” kama Yesu alivyokuwa amesema ndivyo wanafunzi wake wangekuwa.—Yak. 4:4; Yn. 17:14, NW.

Rekodi ya Kutokuwamo kwa Kikristo

Ingawa Mashahidi wa Yehova walitambua upesi baadhi ya masuala yaliyohusu uhusiano wa Mkristo na ulimwengu, mambo mengine yalitaka wakati zaidi. Hata hivyo, Vita ya Ulimwengu 2 ilipokuwa ikiongeza mwendo katika Ulaya, makala yenye maana katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Novemba 1, 1939, iliwasaidia kuthamini maana ya kutokuwamo kwa Kikristo. Wafuasi wa Yesu Kristo, ikataarifu makala hiyo, wana wajibu mbele za Mungu kuwa wenye kujitoa kabisa kwake na Ufalme wake, ile Theokrasi. Sala zao zapaswa kuwa kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, si kwa ajili ya ulimwengu. (Mt. 6:10, 33) Kwa msaada wa yale ambayo Yesu Kristo alifunua kwa habari ya utambulisho wa mtawala asiyeonekana wa ulimwengu (Yn. 12:31; 14:30), makala hiyo ilitoa sababu hivi, mtu ambaye amejitoa kwa Ufalme wa Mungu angewezaje kupendelea upande mmoja au ule mwingine katika pigano kati ya vikundi vya ulimwengu? Je, Yesu hakuwa amesema kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu”? (Yn. 17:16, NW) Msimamo huu wa kutokuwamo kwa Kikristo si ule ambao ulimwengu kwa ujumla ungeelewa. Lakini je, kweli Mashahidi wa Yehova wangeishi kulingana nao?

Kutokuwamo kwao kulitahiniwa vikali wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, kwa kutokeza sana katika Ujerumani. Mwanahistoria Brian Dunn alitaarifu hivi: ‘Mashahidi wa Yehova hawakupatana na Unazi. La maana zaidi ya makatazo ya Nazi kwao lilikuwa kutokuwamo kwao kwa siasa. Hilo lilimaanisha kwamba hakuna mwamini ambaye angechukua silaha, kutumikia katika cheo, kushiriki katika miadhimisho ya umma, au kufanya ishara yoyote ya utii.’ (The Churches’ Response to the Holocaust, 1986) Katika A History of Christianity, Paul Johnson aliongeza hivi: “Wengi walihukumiwa kifo kwa kukataa utumishi wa kijeshi . . . au wakapelekwa Dachau au jela za wenye kichaa.” Ni Mashahidi wangapi katika Ujerumani waliotiwa gerezani? Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani waliripoti baadaye kwamba 6,262 kati yao walikuwa wamekamatwa na 2,074 katika hesabu hiyo walikuwa wametiwa katika kambi za mateso. Waandikaji walimwengu kwa kawaida huonyesha tarakimu za juu zaidi.

Katika Uingereza, ambako wote wanaume na wanawake walitiwa katika jeshi, sheria ilikuwa na mpango wa kutoa ruhusa ya kutoingia jeshini; lakini mahakama nyingi ziliwanyima ruhusa hiyo Mashahidi wa Yehova, na mahakimu walipasisha juu yao hukumu za gerezani zilizozidi jumla ya miaka 600. Katika Marekani, mamia ya Mashahidi wa Yehova wakiwa wahudumu Wakristo walipewa ruhusa ya kutoingia katika utumishi wa kijeshi. Wengine zaidi ya 4,000, walionyimwa ruhusa iliyoandaliwa na Sheria ya Utumishi wa Kuteua, walikamatwa na kutiwa gerezani kwa vipindi vya urefu wa kufika miaka mitano. Katika kila nchi duniani, Mashahidi wa Yehova walishikamana na msimamo uleule wa kutokuwamo kwa Kikristo.

Hata hivyo, mtihani wa uhalisi wa kutokuwamo kwao haukukoma vita ilipokwisha. Ijapokuwa hatari ya 1939-1945 ilikuwa imepita, mapigano mengine yalikuja; na hata katika nyakati za amani ya kadiri, mataifa mengi yalichagua kudumisha utumishi wa kijeshi wa lazima. Mashahidi wa Yehova, wakiwa wahudumu Wakristo, waliendelea kukabili vifungo vya gerezani mahali ambapo hawakupewa ruhusa ya kutoingia utumishi wa kijeshi. Katika 1949, wakati John Tsukaris na George Orphanidis walipokataa kuchukua silaha kupigana na wanadamu wenzao, serikali ya Ugiriki iliamuru wauawe. Vitendo (vya aina mbalimbali) vilivyotendwa juu ya Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki vilikuwa tena na tena vya kikatili sana hivi kwamba baada ya wakati Baraza la Ulaya (Halmashauri ya Haki za Kibinadamu) lilijaribu kutumia mamlaka yalo kwa niaba yao, lakini kwa sababu ya msongo kutoka Kanisa Orthodoksi la Ugiriki, hata kufikia 1992 mahimizo yao yalikuwa yameepukwa kwa werevu, isipokuwa katika visa chache. Hata hivyo, baadhi ya serikali zililiona kuwa jambo lisilofaa kuendelea kuadhibu Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya imani zao za kidini za kidhamiri. Kufikia miaka ya 1990, katika nchi chache, kama vile Sweden, Finland, Poland, Uholanzi, na Argentina, serikali haikuwa ikisonga Mashahidi watendaji washiriki katika utumishi wa kijeshi au utumishi wa lazima wa taifa ulio badala ya wa kijeshi, ingawa kila kisa kilichunguzwa kwa uangalifu.

Katika mahali pamoja baada ya pengine, Mashahidi wa Yehova wamelazimika kukabili hali zilizotatiza kutokuwamo kwao kwa Kikristo. Serikali zilizokuwa zikitawala katika Amerika ya Latin, Afrika, Mashariki ya Kati, Ireland Kaskazini, na kwingineko zimekabili upinzani wa jeuri kutoka kwa majeshi ya kimapinduzi. Likiwa tokeo, serikali na majeshi ya upinzani pia yamesonga Mashahidi wa Yehova waunge mkono kwa tendo. Lakini Mashahidi wa Yehova wamedumisha kutokuwamo kamili. Baadhi yao wamepigwa kikatili, hata kuuawa, kwa sababu ya msimamo waliochukua. Hata hivyo, mara nyingi, kutokuwamo halisi kwa Kikristo kwa Mashahidi wa Yehova kumewapatia staha kutoka kwa maofisa wa pande zote mbili, nao Mashahidi huruhusiwa kuendelea bila kusumbuliwa katika kazi yao ya kuwaambia wengine habari njema juu ya Ufalme wa Yehova.

Katika miaka ya 1960 na ya 1970, kutokuwamo kwa Mashahidi kulipatwa na mitihani ya kinyama kuhusiana na dai la kwamba raia wote wa Malawi wanunue kadi iliyoonyesha uanachama katika chama cha kisiasa chenye kutawala. Mashahidi wa Yehova waliliona jambo hilo kuwa kinyume cha imani zao za Kikristo kushiriki katika hilo. Likiwa tokeo, walipatwa na mnyanyaso usio na kifani katika ukatili wake wenye kuumiza. Makumi ya maelfu walilazimika kutoroka nchi hiyo, na baada ya wakati wengi walirudishwa nchini kwa nguvu wakakabili unyama zaidi.

Wajaponyanyaswa kijeuri, Mashahidi wa Yehova hawajatenda kwa roho ya uasi. Imani zao hazihatarishi serikali yoyote wanayoishi chini yayo. Kwa kutofautisha, Baraza la Makanisa Ulimwenguni limesaidia kifedha mapinduzi, na mapadri Wakatoliki wameunga mkono majeshi ya uviziaji. Lakini ikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova angeshiriki katika vitendo vya kimapinduzi, ingekuwa sawa na kukana imani yake.

Ni kweli kwamba Mashahidi wa Yehova huamini kwamba serikali zote za kibinadamu zitaondolewa na Ufalme wa Mungu. Ndivyo inavyotaarifu Biblia kwenye Danieli 2:44. Lakini, kama vile Mashahidi huonyesha, badala ya kusema kwamba wanadamu wangesimamisha Ufalme huo, andiko hilo hujulisha kwamba “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme.” Vivyo hivyo, wao hueleza kwamba, andiko hilo halisemi kwamba wanadamu wanaruhusiwa na Mungu kutayarishia Ufalme huo njia kwa kuondoa tawala za kibinadamu. Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba kazi ya Wakristo wa kweli ni kuhubiri na kufundisha. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kupatana na staha yao kwa Neno la Mungu, rekodi huonyesha kwamba hapana yeyote wao amejaribu kupindua serikali ya aina yoyote popote ulimwenguni, wala hawajapata kamwe kufanya njama ya kumdhuru mkuu yeyote wa umma. Gazeti la habari la Italia La Stampa lilisema kuhusu Mashahidi wa Yehova hivi: “Wao ndio raia walio waaminifu zaidi ambao yeyote angetamani: wao hawaepi kodi wala kutafuta kuchenga sheria zisizowafaa kwa ajili ya faida yao wenyewe.” Hata hivyo, kwa sababu ya kutambua uzito wa jambo hilo machoni pa Mungu, kila mmoja wao ameazimia kwa imara kuendelea kuwa “si sehemu ya ulimwengu.”—Yn. 15:19; Yak. 4:4, NW.

Wakati Mifano ya Kitaifa Ilipopata Kuwa Vitu vya Kuabudiwa

Adolf Hitler alipoingia mamlakani katika Ujerumani, wimbi la kichaa cha kizalendo lilienea ulimwenguni pote. Ili kuwaandikisha watu katika jeshi, ushiriki katika sherehe za kizalendo ulifanywa kuwa wa lazima. Katika Ujerumani kila mtu alitakwa kutoa salamu iliyoamriwa na kupaaza sauti “Heil Hitler!” Huko kulikuwa kusifu Hitler kuwa mwokozi; kulimaanishwa kuwasilishe wazo la kwamba matumaini yote ya watu yalitegemea uongozi wake. Lakini Mashahidi wa Yehova hawangeweza kujiunga katika hisia kama hizo. Wao walijua kwamba ibada yao lazima imwendee Yehova pekee na kwamba Yeye alikuwa amemtokeza Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa wanadamu.—Luka 4:8; 1 Yoh. 4:14.

Hata kabla Hitler hajawa dikteta katika Ujerumani, Mashahidi wa Yehova, katika kijitabu The Kingdom, the Hope of the World (kilichotangazwa katika 1931), walikuwa wamepitia kielelezo cha Kimaandiko cha wale waandamani watatu Waebrania wenye ujasiri wa nabii Danieli katika Babiloni. Walipoamriwa na mfalme wainame mbele ya taswira muziki fulani upigwapo, Waebrania hao waaminifu walikuwa wamekataa kuridhiana, naye Yehova alikuwa ameonyesha wazi kibali chake kwa kuwakomboa. (Dan. 3:1-26) Kijitabu hicho kilionyesha kwamba sherehe za kizalendo ziliwakabili Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa kukiwa na jaribu kama hilo la uaminifu wao.

Hatua kwa hatua, msukosuko wa sherehe za kizalendo za lazima ulienea kuvuka mipaka ya Ujerumani. Katika Juni 3, 1935, kwenye mkusanyiko katika Washington, D.C., wakati J. F. Rutherford alipoombwa atoe maelezo juu ya kusalimu bendera shuleni, alikazia uaminifu kwa Mungu. Miezi michache baadaye, wakati Carleton B. Nichols, Jr., mwenye miaka minane, wa Lynn, Massachusetts, alipokataa kusalimu bendera ya Marekani na kujiunga katika kuimba wimbo wa kizalendo, jambo hilo liliripotiwa magazetini nchini pote.

Ili aeleze jambo hilo, Ndugu Rutherford alitoa hotuba ya redio katika Oktoba 6 juu ya habari “Kusalimu Bendera,” ambayo alisema hivi: “Kwa watu wengi kusalimu bendera ni sherehe tu na kuna maana kidogo au hakuna maana yoyote. Kwa wale ambao hufikiria jambo hilo kwa maoni ya Kimaandiko, linamaanisha mengi.

“Bendera huwakilisha mamlaka zitawalazo zenye kuonekana. Kujaribu kwa sheria kulazimisha raia au mtoto wa raia asalimu kitu au chochote, au kuimba zile ziitwazo eti ‘nyimbo za kizalendo,’ si haki na ni kosa kabisa. Sheria hutungwa na kufikilizwa ili kuzuia yasitendwe matendo dhahiri ambayo hutokeza dhara kwa mwingine, nazo hazitungwi kwa kusudi la kumlazimisha mtu ahalifu dhamiri yake, na hasa dhamiri hiyo inapoelekezwa kupatana na Neno la Yehova Mungu.

“Kukataa kusalimu bendera, na kusimama kimya, kama vile mvulana huyo alivyofanya, hakungeweza kudhuru yeyote. Ikiwa mtu aamini kwa moyo mweupe kwamba amri ya Mungu hukataza kusalimu bendera, basi kumlazimisha mtu huyo kusalimu bendera kinyume cha Neno la Mungu, na kinyume cha dhamiri yake, humdhuru sana mtu huyo. Serikali haina haki kwa sheria au kwa njia nyingineyo yote kudhuru watu.”

Maelezo zaidi ya sababu za msimamo uliochukuliwa na Mashahidi wa Yehova yaliandaliwa katika kijitabu Loyalty (Uaminifu-Mshikamanifu), kilichotangazwa pia katika 1935. Uangalifu ulielekezwa kwenye maandiko kama yafuatayo: Kutoka 20:3-7, ambalo liliamuru kwamba ibada imwendee Yehova pekee na kwamba watumishi wa Mungu hawakupaswa kufanya au kuinama mbele ya sanamu au mfano wa chochote mbinguni au duniani; Luka 20:25, ambapo Yesu Kristo alielekeza kwamba si vitu vya Kaisari tu vinavyopaswa kurudishiwa Kaisari bali pia vilivyo vya Mungu lazima vitolewe Kwake; na Matendo 5:29 (“NW”), ambapo mitume walitaarifu kwa uthabiti, “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”

Katika Marekani, suala la ufaaji wa kumlazimisha mtu yeyote asalimu bendera lilipelekwa mahakamani. Katika Juni 14, 1943, Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani ilibadili uamuzi wayo yenyewe wa hapo mapema na, katika kesi ya West Virginia State Board of Education v. Barnette, ikaamua kwamba kusalimu bendera kwa kulazimishwa hakupatani na hakikisho la uhuru lililoandikwa katika katiba ya taifa lenyewe.b

Suala lihusulo sherehe za utukuzo wa taifa halikuhusu tu Ujerumani na Marekani. Katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, na Asia, Mashahidi wa Yehova wamenyanyaswa kikatili kwa sababu ya kutoshiriki kwao, hata ingawa wao husimama kwa heshima wakati wa kusalimu bendera au sherehe kama hizo. Watoto wamepigwa; wengi wamefukuzwa shuleni. Kesi nyingi za mahakama zimeshindaniwa.

Hata hivyo, watazamaji wamehisi kushurutishwa wakiri kwamba, katika hili, kama vile katika mambo mengine, Mashahidi wa Yehova wamethibitika kuwa kama Wakristo wa mapema. Hata hivyo, kama ilivyotaarifiwa katika kitabu The American Character: “Kwa idadi iliyo kubwa sana . . . makatao ya Mashahidi yalikuwa yasiyoeleweka kama yalivyokuwa makatao ya Wakristo [katika Milki ya Kiroma] ya kutotoa dhabihu ya kisherehe kwa Maliki wa Kimungu yalivyokuwa kwa Trajan na Pliny.” Hilo lilipasa kutarajiwa, kwa kuwa Mashahidi wa Yehova, kama vile Wakristo wa mapema, waliona mambo si kama vile ulimwengu uyaonavyo bali kulingana na kanuni za Biblia.

Msimamo Wao Wataarifiwa Waziwazi

Baada ya Mashahidi wa Yehova kuwa wamevumilia mitihani mikali ya kutokuwamo kwao kwa Kikristo kwa miaka mingi Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Novemba 1, 1979, lilithibitisha tena msimamo wao. Lilieleza pia sababu ya tendo lililochukuliwa na Mashahidi mmoja-mmoja, liliposema: “Likiwa tokeo la funzo lao la bidii la Neno la Mungu, vijana hao Wakristo waliweza kufanya uamuzi. Hapana mwingine yeyote aliyewafanyia uamuzi huo. Waliweza kuufanya mmoja-mmoja, kwa msingi wa dhamiri ya kila mmoja iliyozoezwa kwa njia ya Biblia. Uamuzi wao ulikuwa kujiepusha na matendo ya chuki na jeuri dhidi ya wanadamu wenzao wa mataifa mengine. Naam, waliamini, na walitaka kushiriki katika utimizo wa unabii wa Isaya ujulikanao sana: ‘Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.’ (Isa. 2:4) Vijana hao wa mataifa yote walifanya hivyo hasa.”

Wakati wa miaka ambayo kushikamana kwao na kutokuwamo kwa Kikristo kulipokuwa kukitahiniwa, kuchunguzwa upya kwa yale ambayo Biblia husema, kwenye Warumi 13:1-7 (NW) juu ya “mamlaka zilizo kubwa” kuliongoza kwenye taarifa iliyo wazi zaidi ya uhusiano wa Mashahidi kwa serikali za kilimwengu. Hiyo ilitangazwa katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ya Januari 1, Februari 1, na Machi 1, 1964, na ikathibitishwa tena katika toleo la Novemba 1, 1990. Makala hizo zilikazia cheo cha Yehova Mungu akiwa “Mkuu Kupita Wote,” wakati huohuo zikionyesha kwamba watawala wa kilimwengu ni “mamlaka zilizo kubwa” kwa kuhusiana tu na wanadamu wengine na katika uwanja wao wa utendaji ambao katika huo Mungu huwaruhusu kutenda katika mfumo wa mambo uliopo. Makala hizo zilionyesha uhitaji wa Wakristo wa kweli kuwastahi kwa kudhamiria watawala hao wa kilimwengu na kuwapa utii katika mambo yote ambayo hayapingani na sheria ya Mungu na dhamiri yao iliyozoezwa kwa njia ya Biblia.—Dan. 7:18; Mt. 22:21; Mdo. 5:29; Rum. 13:5, NW.

Kushikamana imara na viwango hivyo vya Biblia kwa Mashahidi wa Yehova kumewapa sifa ya kuwa wenye kujitenga na ulimwengu, sifa inayowakumbusha watu juu ya Wakristo wa mapema.

Ulimwengu Ulipokuwa na Sikukuu Zao

Mashahidi wa Yehova walipoondolea mbali mafundisho ya kidini yaliyokuwa na mianzo ya kipagani, waliacha pia kushiriki katika desturi nyingi ambazo zilikuwa zimechafuliwa vivyo hivyo. Lakini kwa wakati fulani, sikukuu fulani hazikupewa uchunguzi wa uangalifu ziliohitaji. Mojapo hizo ilikuwa ni Krismasi.

Sikukuu hiyo iliadhimishwa kila mwaka hata na washiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Watch Tower Society kwenye Kao la Betheli katika Brooklyn, New York. Kwa miaka mingi walikuwa wamejua kwamba Desemba 25 haikuwa tarehe sahihi, lakini wakatoa sababu kwamba kwa muda mrefu watu wengi walikuwa wameishirikisha tarehe hiyo na kuzaliwa kwa Mwokozi na kwamba kutendea wengine mema kwafaa siku yoyote. Hata hivyo, baada ya uchunguzi zaidi wa habari hiyo, washiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Sosaiti, pamoja na wafanyakazi kwenye ofisi za tawi za Sosaiti katika Uingereza na Uswisi, waliamua kuacha kushiriki katika miadhimisho ya Krismasi, hivyo hakuna msherehekeo wa Krismasi uliofanywa huko baada ya 1926.

R. H. Barber, mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu aliyefanya uchunguzi kamili wa chanzo cha desturi za Krismasi na tunda zilizokuwa zikizaa, alitoa matokeo yake katika tangazo la redio. Habari hiyo ilitangazwa pia katika The Golden Age la Desemba 12, 1928. Ulikuwa mfichuo kamili wa mianzo yenye kumvunjia Mungu heshima ya Krismasi. Tangu hapo, mianzo ya kipagani ya desturi za Krismasi imepata kujulikana na umma kwa ujumla, lakini ni watu wachache ambao hufanya mabadiliko katika njia yao ya maisha likiwa tokeo. Kwa upande ule mwingine, Mashahidi wa Yehova wana nia ya kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili wawe wenye kukubalika zaidi wakiwa watumishi wa Yehova.

Walipoonyeshwa kwamba kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa kumekuwa kwenye kupendeza zaidi watu wengi kuliko fidia iliyoandaliwa na kifo chake; kwamba kelele za ulevi za sikukuu hiyo na roho ambayo zawadi nyingi zilitolewa hazimheshimu Mungu; kwamba wale wanajimu ambao kutoa zawadi kwao kulikuwa kukiigwa walikuwa kwa kweli wanajimu walioongozwa na mashetani; kwamba wazazi walikuwa wakiwawekea watoto wao kielelezo cha kusema uwongo kwa yale waliyowaambia juu ya Baba Krismasi; kwamba “Mtakatifu Nikolasi” (Baba Krismasi) kwa kweli lilikuwa jina jingine la Ibilisi mwenyewe; na kwamba miadhimisho hiyo ilikuwa, kama vile alivyokiri Kardinali Newman katika kitabu chake Essay on the Development of Christian Doctrine, “vyombo na nyongeza hasa za ibada ya mashetani” ambazo kanisa lilikuwa limekubali—walipojulishwa mambo hayo, Mashahidi wa Yehova waliacha mara hiyo na kwa daima kushiriki sehemu yoyote katika misherehekeo ya Krismasi.

Mashahidi wa Yehova huwa na nyakati za shangwe pamoja na familia na marafiki wao. Lakini hawashiriki katika sikukuu na misherehekeo inayoshirikishwa na miungu ya kipagani (kama ilivyo kwa sikukuu kama vile Ista, Siku ya Mwaka Mpya, Siku ya Mei, na Siku ya Mama). (2 Kor. 6:14-17) Kama vile Wakristo wa mapema,c wao hata hawaadhimishi siku za kuzaliwa. Pia kwa staha wao huepuka kushiriki katika sikukuu za kitaifa ambazo hufanya kumbukumbu ya matukio ya kisiasa au ya kijeshi na huepuka kuwapa heshima ya kiibada mashujaa wa kitaifa. Kwa nini? Kwa sababu Mashahidi wa Yehova si sehemu ya ulimwengu.

Kuwasaidia Wanadamu Wenzao

Kuheshimu mno miungu kulikuwa ndicho kiini cha maisha ya kijamii na ya kitamaduni ya Milki ya Kiroma. Kwa kuwa Wakristo waliepuka kushiriki katika chochote kilichotiwa waa na miungu ya kipagani, watu waliuona Ukristo kuwa dharau kwa njia yao ya maisha; na kulingana na mwanahistoria Tacitus, Wakristo walisemekana kuwa wachukia wanadamu. Akiwasilisha hisia kama hiyo, Minucius Felix, katika maandishi yake, hunukuu Mroma mmoja akisema hivi kwa Mkristo aliyemjua: “Nyinyi hamhudhurii maonyesho; hamshiriki sehemu katika maandamano . . . mwakirihi michezo mitakatifu.” Jamii ya watu wa ulimwengu wa Kiroma ya kale haikuwaelewa sana Wakristo.

Vivyo hivyo leo, wengi katika ulimwengu hawawaelewi Mashahidi wa Yehova. Huenda watu wakasifu viwango vya juu vya kiadili vya Mashahidi lakini wahisi kwamba Mashahidi wapaswa kushiriki pamoja na ulimwengu unaowazunguka katika utendaji wao mbalimbali na kujihusisha katika kusaidia kufanya ulimwengu kuwa mahali bora zaidi. Hata hivyo, wale wapatao kuwajua Mashahidi wa Yehova kwa kushuhudiwa wenyewe hupata kujua kwamba kuna sababu ya Kibiblia kwa kila jambo wafanyalo.

Kuliko kujifungia mbali wenyewe na wengine wa wanadamu, Mashahidi wa Yehova hutumia maisha yao katika kusaidia wanadamu wenzao katika njia ambayo Yesu Kristo aliwekea kielelezo. Wao husaidia watu kujifunza jinsi ya kukabiliana kwa mafanikio na matatizo ya maisha sasa kwa kuwafahamisha kwa Muumba na kwa miongozo ya maisha iliyoonyeshwa katika Neno lake lililopuliziwa. Wao hushiriki pamoja na majirani bila malipo kweli za Biblia ziwezazo kugeuza maoni yote ya mtu juu ya maisha. Kiini cha imani yao ni kujua kwamba “ulimwengu unapilitia mbali,” na kwamba upesi Mungu atajiingiza ili kukomesha mfumo mwovu wa mambo uliopo, na kwamba wakati ujao mtukufu wawangojea wale waendeleao kuwa si wa ulimwengu na kuweka imani yao kamili katika Ufalme wa Mungu.—1 Yoh. 2:17, NW.

[Maelezo ya Chini]

a The Watch Tower, Juni 1, 1918, uku. 17.

b Kwa habari zaidi, ona Sura ya 30, “Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema.”

c The History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries, cha Augustus Neander, uku. 190.

[Blabu katika ukurasa wa 188]

Hawajitengi na watu, lakini hawashiriki namna ya maisha ya ulimwengu

[Blabu katika ukurasa wa 189]

Walijiondoa katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo

[Blabu katika ukurasa wa 190]

“Wakristo hawakujihusisha na walikuwa tofauti na serikali”

[Blabu katika ukurasa wa 194]

Kutokuwamo kwa Kikristo kulitahiniwa

[Blabu katika ukurasa wa 198]

‘Hakuna mwingine aliyewafanyia uamuzi’

[Blabu katika ukurasa wa 199]

Sababu iliyofanya waache kuadhimisha Krismasi

[Sanduku katika ukurasa wa 195]

Si Tisho kwa Serikali Yoyote

◆ Ilipokuwa ikiandika juu ya walivyotendewa Mashahidi wa Yehova katika nchi moja ya Amerika ya Latini, tahariri moja katika “World-Herald” la Omaha, Nebraska, Marekani, ilisema: “Yataka uwazio wa ushupavu wa upande mmoja na hofu isiyo na msingi kuamini kwamba Mashahidi wa Yehova hutokeza tisho la aina yoyote kwa serikali yoyote ya kisiasa; wao si wataka-mapinduzi na ni wapenda amani wakiwa kikundi cha kidini kadiri iwezekanavyo, nao huomba tu kwamba waruhusiwe kufuatia imani yao kwa njia yao wenyewe.”

◆ “Il Corriere di Trieste,” gazeti moja la habari la Italia, lilitaarifu hivi: “Mashahidi wa Yehova wapasa kusifiwa kwa ajili ya imara na ushikamano wao. Tofauti na dini nyinginezo, umoja wao wakiwa kikundi cha watu huwazuia kutosali kwa Mungu yuleyule mmoja, katika jina la Kristo yuleyule mmoja, abariki pande mbili zenye kupingana katika pigano, au kutochanganya siasa na dini ili kutumikia masilahi ya Kiongozi wa Serikali au vyama vya kisiasa. La mwisho lakini lenye umaana uleule, wako tayari kukabili kifo kuliko kuvunja . . . ile amri USIUE!”

◆ Baada ya Mashahidi wa Yehova kuwa wamevumilia marufuku ya miaka 40 katika Chekoslovakia, gazeti la habari “Nová Svoboda” lilisema hivi, katika 1990: “Imani ya Mashahidi wa Yehova huwakataza kutumia silaha dhidi ya wanadamu, na wale waliokataa utumishi wa msingi wa kijeshi na hawakufanya kazi katika migodi ya makaa-mawe walikwenda gerezani, hata kwa miaka minne. Kutokana na hilo tu ni wazi kwamba wana imara kubwa ya kiadili. Tungeweza kutumia watu kama hao wasio na ubinafsi hata katika shughuli za kisiasa za juu kabisa—lakini hatutaweza kamwe kuwaingiza humo. . . . Bila shaka, watambua mamlaka za kiserikali lakini waamini kwamba ni Ufalme wa Mungu tu uwezao kutatua matatizo yote ya kibinadamu. Lakini usikosee—wao hawashikilii mambo bila kutumia akili. Ni watu ambao hujishughulisha sana na wanadamu.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 200, 201]

Mazoea Ambayo Yameachwa Kabisa

Msherehekeo huu wa Krismasi kwenye Betheli ya Brooklyn katika 1926 ulikuwa ndio wao wa mwisho. Wanafunzi wa Biblia walikuja kufahamu hatua kwa hatua kwamba wala mwanzo wa sikukuu hiyo wala mazoea yaliyoshirikishwa nayo hayakumheshimu Mungu

Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia walivaa msalaba na taji kuwa beji ya utambulisho, na ishara hiyo ilikuwa katika jalada la mbele la “Watch Tower” tokea 1891 hadi 1931. Lakini katika 1928 ilikaziwa kwamba si ishara ya kupamba bali utendaji wa mtu akiwa shahidi ndio ulioonyesha kuwa alikuwa Mkristo. Katika 1936 ilionyeshwa kwamba uthibitisho huonyesha kwamba Kristo alikufa juu ya mti, si juu ya msalaba wenye maboriti mawili

Katika kitabu chao “Daily Manna,” Wanafunzi wa Biblia waliweka orodha ya siku za kuzaliwa. Lakini baada ya wao kuacha kuadhimisha Krismasi na wakati walipopata kujua kwamba misherehekeo ya kuzaliwa ilikuwa ikitoa kwa viumbe heshima isivyostahili (hiyo ikawa sababu moja Wakristo wa mapema hawakusherehekea kamwe siku za kuzaliwa), Wanafunzi wa Biblia waliacha zoea hilo vilevile

Kwa miaka ipatayo 35, Pasta Russell alifikiri kwamba ile Piramidi Kubwa ya Gizeh ilikuwa lile jiwe la ushahidi la Mungu, ikiunga mkono vipindi vya wakati wa Biblia. (Isa. 19:19) Lakini Mashahidi wa Yehova wameacha wazo la kwamba piramidi fulani ya Misri ina uhusiano wowote na ibada ya kweli. (Ona “Mnara wa Mlinzi” matoleo ya Novemba 15 na Desemba 1, 1928, Kiingereza)

[Picha katika ukurasa wa 189]

Nakala milioni kumi ziligawanywa

[Picha katika ukurasa wa 191]

Baadhi yao walikwenda katika mahandaki wakiwa na bunduki, lakini wengine, kutia ndani A. P. Hughes wa Uingereza, na R. Cuminetti wa Italia, walikataa kujihusisha kama huko

[Picha katika ukurasa wa 193]

Mashahidi wa Yehova walikataa kukubali Ushirika wa Mataifa au UM kuwa watoka kwa Mungu bali walitetea tu Ufalme wa Mungu kupitia Kristo

[Picha katika ukurasa wa 197]

Carleton na Flora Nichols. Wakati mwana wao alipoepuka kusalimu bendera, hilo likawa habari za taifa zima

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki