Sura ya Kumi na Nane
“Wao Si Sehemu ya Ulimwengu”
1. (a) Kabla ya kuuawa, Yesu alisalije kwa niaba ya wanafunzi wake? (b) Kwa nini ni muhimu sana ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu’?
YESU alisali kwa niaba ya wanafunzi wake usiku uliotangulia kifo chake. Huku akijua kwamba Shetani angewajaribu vikali, Yesu alimwambia Baba yake hivi: “Nakuomba wewe, si uwachukue kutoka ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Kwa nini ni muhimu kujitenga na ulimwengu? Kwa sababu Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu. Wakristo hawangetaka kuwa sehemu ya ulimwengu ambao unatawaliwa na Shetani.—Luka 4:5-8; Yohana 14:30; 1 Yohana 5:19.
2. Yesu hakuwa sehemu ya ulimwengu katika njia zipi?
2 Kutokuwa sehemu ya ulimwengu hakukumaanisha kwamba Yesu hakuwapenda watu. Kinyume chake, aliwaponya wagonjwa, akawafufua wafu, na kuwafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu. Hata alitoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. Lakini hakupenda mielekeo na matendo maovu ya watu ambao walionyesha roho ya ulimwengu wa Shetani. Kwa hiyo, alionya dhidi ya mambo kama vile tamaa ya mambo machafu, kupenda vitu vya kimwili, na kujitafutia umashuhuri. (Mathayo 5:27, 28; 6:19-21; Luka 20:46, 47) Si ajabu kwamba Yesu aliepuka pia siasa za ulimwengu. Ingawa alikuwa Myahudi, yeye hakuunga mkono mapambano ya kisiasa kati ya serikali ya Roma na Wayahudi.
“Ufalme Wangu Si Sehemu ya Ulimwengu Huu”
3. (a) Viongozi wa kidini Wayahudi walitoa shtaka gani kumhusu Yesu mbele ya Pilato, na kwa nini? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu hakutaka kuwa mfalme alipokuwa duniani?
3 Fikiria kilichotukia viongozi wa kidini Wayahudi walipoagiza Yesu akamatwe na kupelekwa kwa gavana Mroma, Pontio Pilato. Kwa kweli viongozi hao walikasirika kwa sababu Yesu alikuwa amefichua unafiki wao. Walimchochea gavana huyo amchukulie Yesu hatua kwa kutoa shtaka hili: “Mtu huyu tulimkuta akipindua taifa letu na kukataza ulipaji wa kodi kwa Kaisari na kusema yeye mwenyewe ni Kristo mfalme.” (Luka 23:2) Kwa wazi, huo ulikuwa uwongo kwa sababu mwaka mmoja mapema Yesu alikataa watu walipotaka kumfanya mfalme. (Yohana 6:15) Alijua kwamba angekuwa Mfalme mbinguni wakati ujao. (Luka 19:11, 12) Isitoshe, angetawazwa na Yehova wala si na wanadamu.
4. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu kulipa kodi?
4 Siku tatu tu kabla ya Yesu kukamatwa, Mafarisayo walijaribu kumtega Yesu ili aseme jambo baya kuhusu kulipa kodi. Lakini alisema: “Nionyesheni dinari [sarafu ya Roma]. Ina sanamu na mwandiko wa nani?” Walipojibu “wa Kaisari,” alisema hivi: “Kwa vyovyote, basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.”—Luka 20:20-25.
5. (a) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake somo gani alipokamatwa? (b) Yesu alielezaje sababu iliyomfanya achukue hatua hiyo? (c) Matokeo ya kesi hiyo yalikuwa nini?
5 Yesu hakuwafundisha kamwe watu waasi mamlaka za ulimwengu. Askari na watu wengine walipokuja kumkamata Yesu, Petro alifuta upanga na kumkata sikio mmojawapo wa watu waliokuwapo. Lakini Yesu akasema: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:51, 52) Siku iliyofuata, Yesu alimweleza Pilato sababu iliyomfanya achukue hatua hiyo: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, mahadimu wangu wangalipigana ili nisikabidhiwe kwa Wayahudi.” (Yohana 18:36) Pilato alikubali kwamba hakukuwa na “msingi wa mashtaka” yaliyoletwa dhidi ya Yesu. Lakini Pilato alishurutishwa na umati, akawaruhusu wamtundike Yesu.—Luka 23:13-15; Yohana 19:12-16.
Wanafunzi Wafuata Mwongozo wa Yesu
6. Wakristo wa awali walionyeshaje kwamba waliepuka roho ya ulimwengu ingawaje waliwapenda watu?
6 Hivyo, wanafunzi wa Yesu walipata kuelewa maana ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu. Walipaswa kuepuka roho na matendo maovu ya ulimwengu, yaliyotia ndani sarakasi na michezo ya kuigiza ya Roma iliyokuwa na ujeuri na matendo machafu. Wanafunzi waliepuka burudani hizo na hivyo walionwa kuwa maadui wa jamii. Lakini hawakuwachukia wanadamu wenzao hata kidogo, badala yake walijitahidi sana kuwasaidia wengine wanufaike na mipango ya Mungu ya wokovu.
7. (a) Wakristo wa awali walitendewaje kwa sababu ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu? (b) Walikuwa na maoni gani kuhusu watawala wa kisiasa na kulipa kodi, na kwa nini?
7 Kama Yesu, wafuasi wake walinyanyaswa mara nyingi na maofisa wa serikali waliokuwa wamepashwa habari za uwongo. Lakini, yapata mwaka wa 56 W.K., mtume Paulo aliwaandikia Wakristo huko Roma, akiwahimiza ‘wajitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa [watawala wa kisiasa], kwa maana hakuna mamlaka ila kwa njia ya Mungu.’ Hiyo haimaanishi kwamba Yehova ndiye anayeteua serikali za ulimwengu, bali anaziruhusu ziwepo hadi Ufalme wake utakapotawala dunia yote. Kwa kufaa, Paulo aliwashauri Wakristo wawaheshimu wenye mamlaka na kulipa kodi.—Waroma 13:1-7; Tito 3:1, 2.
8. (a) Wakristo wanapaswa kujitiisha kwa kadiri gani kwa mamlaka zilizo kubwa? (b) Wakristo wa awali walifuataje mfano wa Yesu?
8 Hata hivyo, ujitiisho kwa watawala wa kisiasa unapasa kuwa wa kadiri, si kamili. Sheria za Yehova na sheria za wanadamu zinapopingana, watumishi wa Yehova wanapaswa kutii sheria Zake. Kitabu On the Road to Civilization—A World History chasema hivi kuhusu Wakristo wa awali: ‘Wakristo walikataa kufanya kazi fulani zilizofanywa na raia Waroma. Waliona kujiunga na jeshi kuwa kinyume cha imani yao. Hawakukubali vyeo vya kisiasa. Hawakumwabudu maliki.’ Mahakama kuu ya Wayahudi ‘ilipowaagiza’ wanafunzi waache kuhubiri, walijibu hivi: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:27-29.
9. (a) Kwa nini Wakristo waliokuwa Yerusalemu walikimbia mnamo mwaka wa 66 W.K.? (b) Waliweka mfano gani bora?
9 Wanafunzi hawakujiingiza kamwe katika mapambano ya kisiasa na ya kijeshi. Wayahudi wa Yudea walimwasi Kaisari mnamo mwaka wa 66 W.K. Jeshi la Roma likazingira Yerusalemu mara moja. Wakristo waliokuwa katika mji huo walifanya nini? Walikumbuka shauri la Yesu kwamba watoke katika mji huo. Waroma walipoondoka kwa muda, Wakristo walivuka Mto Yordani na kukimbilia eneo la milimani huko Pela. (Luka 21:20-24) Wakristo waaminifu leo wanapaswa kuiga mfano wao wa kutounga mkono upande wowote.
Wakristo Hawaungi Mkono Upande Wowote Katika Siku Hizi za Mwisho
10. (a) Mashahidi wa Yehova wanaendelea kufanya kazi gani kwa bidii, na kwa nini? (b) Hawaungi mkono nini?
10 Je, historia inaonyesha kwamba kikundi fulani katika siku hizi za mwisho kimejitahidi kutounga mkono upande wowote katika mapambano ya mataifa kama Wakristo wa awali? Ndiyo, Mashahidi wa Yehova wamefanya hivyo. Katika siku hizi za mwisho, wameendelea kuhubiri kwamba Ufalme wa Mungu ndio tu utakaoleta amani ya kudumu, ufanisi na furaha kwa wale wanaopenda uadilifu. (Mathayo 24:14) Lakini hawaungi mkono kamwe mapambano ya mataifa.
11. (a) Msimamo wa Mashahidi kuhusiana na mambo ya siasa unatofautianaje na wa makasisi? (b) Mashahidi wa Yehova wanaonaje mambo ambayo wengine wanafanya kuhusiana na siasa?
11 Kinyume chake, makasisi wa dini za ulimwengu huu wamejihusisha mno na mambo ya kisiasa. Katika nchi fulani, wamewafanyia kampeni au kuwapinga wagombea-uchaguzi. Baadhi ya makasisi hata wana vyeo vya kisiasa. Wengine wamewachochea wanasiasa waunge mkono miradi ambayo imeidhinishwa na makasisi. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika mambo ya siasa. Wala hawawakatazi wengine wasijiunge na vyama vya kisiasa, kugombea vyeo vya kisiasa, au kupiga kura. Yesu alisema kwamba wanafunzi wake hawangekuwa sehemu ya ulimwengu, kwa hiyo Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika siasa.
12. Matokeo yamekuwa nini kwa sababu dini zimeunga mkono upande fulani katika mapambano ya mataifa?
12 Mataifa yamekuwa yakipigana daima, kama Yesu alivyotabiri. Hata vikundi mbalimbali vimekuwa vikipigana katika nchi ileile. (Mathayo 24:3, 6, 7) Mara nyingi, viongozi wa kidini wamekuwa wakiunga mkono taifa moja au kikundi kimoja vitani, na wamewatia moyo wafuasi wao wafanye vivyo hivyo. Matokeo yamekuwa nini? Waumini wa dini ileile wamewaua waumini wenzao vitani kwa sababu wanatoka katika taifa au kabila jingine. Kufanya hivyo ni kinyume cha mapenzi ya Mungu.—1 Yohana 3:10-12; 4:8, 20.
13. Ushuhuda unaonyesha nini kuhusu msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutounga mkono upande wowote katika mapambano?
13 Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wamekataa katakata kuunga mkono upande wowote katika mapambano. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1939 la Kiingereza, lilisema hivi: “Wote walio upande wa Bwana hawataunga mkono upande wowote mataifa yanayopigana.” Mashahidi wa Yehova katika mataifa yote na chini ya hali zote wanaendelea kudumisha msimamo huo. Hawaruhusu vita na siasa za ulimwengu zinazowagawanya watu ziharibu udugu wao wa ulimwenguni pote. ‘Wanafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.’ Hawajifunzi vita tena kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote wa mapambano.—Isaya 2:3, 4; 2 Wakorintho 10:3, 4.
14. Mashahidi wa Yehova wamepatwa na nini kwa sababu ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu?
14 Wamepatwa na nini kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote katika mapambano? Yesu alisema: “Kwa sababu nyinyi si sehemu ya ulimwengu, . . . ulimwengu huwachukia nyinyi.” (Yohana 15:19) Mashahidi wengi wa Yehova wamefungwa gerezani kwa sababu ya kumtumikia Mungu. Baadhi yao wameteswa kikatili, hata kuuawa kama Wakristo wa karne ya kwanza. Wameteswa kwa sababu Shetani, “mungu wa huu mfumo wa mambo,” huwapinga watumishi wa Yehova ambao si sehemu ya mfumo huu.—2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:12.
15. (a) Mataifa yote yanakabili nini, na Mashahidi wa Yehova wanaweza kuepuka nini? (b) Kwa nini kujitenga na ulimwengu ni jambo muhimu sana?
15 Watumishi wa Yehova wanafurahi kwamba wao si sehemu ya ulimwengu, kwa sababu mataifa yote yanakabili uharibifu kwenye Har–Magedoni. (Danieli 2:44; Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21) Tutaepuka kuangamizwa pamoja na mataifa tukijitahidi kutokuwa sehemu ya ulimwengu. Tukiwa na umoja ulimwenguni pote, sisi ni waaminifu kwa Ufalme wa kimbingu wa Mungu. Ni kweli kwamba tunadhihakiwa na kunyanyaswa kwa sababu sisi si sehemu ya ulimwengu. Hata hivyo, mateso na dhihaka hizo zitakoma hivi karibuni, kwa kuwa ulimwengu huu mwovu unaotawaliwa na Shetani utaharibiwa kabisa. Lakini, wale wanaomtumikia Yehova wataishi milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu utakaotawaliwa na Ufalme wake.—2 Petro 3:10-13; 1 Yohana 2:15-17.
Mazungumzo ya Kurudia
• Yesu alionyeshaje maana ya kutokuwa “sehemu ya ulimwengu”?
• Wakristo wa awali walikuwa na maoni gani kuhusu (a) roho ya ulimwengu, (b) watawala wa ulimwengu, na (c) kulipa kodi?
• Mashahidi wa Yehova wameonyeshaje msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote katika mapambano ya mataifa leo?
[Picha katika ukurasa wa 165]
Yesu alisema kwamba yeye na wafuasi wake hawakuwa “sehemu ya ulimwengu”