Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • sh sura 15 kur. 344-365
  • Kumrudia Mungu wa Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumrudia Mungu wa Kweli
  • Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Upendo wa Kikristo na Kutokuwamo
  • Mstari Mrefu wa Mashahidi wa Mungu
  • Mwanamume Kijana Akitafuta Mungu
  • Kurudi Kwenye Ukweli wa Biblia
  • Mitihani na Mabadiliko
  • Bidii Iliyofanywa Upya na Jina Jipya
  • Jitihada ya Ulimwenguni Pote ya Kutafuta Watafutaji Mungu
  • Tengenezo la Elimu ya Biblia
  • Mashahidi Wamepangwaje Kitengenezo
  • Kumiminika Kuelekea Mungu wa Kweli
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Yehova Akusanya na Kuwapa Watu Wake Vifaa vya Kazi
    Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote
  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Ufalme Unazaliwa Mbinguni
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
Pata Habari Zaidi
Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
sh sura 15 kur. 344-365

Sura 15

Kumrudia Mungu wa Kweli

“Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:34, 35.

1, 2. Matokeo ya upendo miongoni mwa Wakristo wa kweli yapasa kuwa nini?

KWA maneno hayo, Yesu aliweka mwongozo kwa wale wanaodai kuwa wafuasi wake wa kweli. Upendo wa Kristo ungepaswa kushinda migawanyo yote ya rangi, kabila, na kitaifa. Ungetaka Wakristo wa kweli wawe “si sehemu ya ulimwengu,” sawa na vile Yesu alivyokuwa, naye “si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:14, 16, NW; Warumi 12:17-21.

2 Mkristo anajionyeshaje kuwa “si sehemu ya ulimwengu”? Kwa kielelezo, apaswa kutendaje kwa habari ya msukosuko wa siasa, mapinduzi, na vita vya nyakati zetu? Mtume Mkristo Yohana aliandika, kwa kupatana na maneno ya Yesu yaliyo juu: “Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake. Maana, hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi.” Na Yesu mwenyewe alieleza ni kwa nini wanafunzi wake hawakupigana ili wamwokoe, akisema: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, mahadimu wangu wangepigana . . . Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu si kutoka chanzo hiki.” Hata uhai wa Yesu ukiwa hatarini, mahadimu hao hawakujihusisha katika kusuluhisha mzozo huo kwa kulingana na njia za kupigana za ulimwengu.—1 Yohana 3:10-12; Yohana 18:36, NW.

3, 4. (a) Isaya alitabiri nini kuhusu “sehemu ya mwisho ya hizi siku”? (b) Ni maswali gani yanayohitaji jibu?

3 Miaka zaidi ya 700 kabla ya Kristo, Isaya alikuwa ametabiri kwamba watu wa mataifa yote wangekusanyika kwenye ibada ya kweli ya Yehova na hawangejifunza vita tena. Yeye alisema: “Ni lazima itukie katika sehemu ya kumalizia ya siku kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima . . . na kwao mataifa yote lazima wamiminike. Na vikundi vingi vya watu kwa hakika vitaenda na kusema: ‘Njooni, enyi watu, na twende juu kwenye mlima wa Yehova, kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; na yeye atatuagiza juu ya njia zake, na sisi tutatembea katika vijia vyake.’ Kwa maana toka Sayuni sheria itatoka, na neno la Yehova kutoka Yerusalemu. Na yeye kwa hakika atatoa hukumu miongoni mwa mataifa na kunyoosha mambo juu ya jamii za watu nyingi. Nao watalazimika kufua panga zao kuwa majembe ya plau na mikuki yao kuwa mikasi ya kupogolea. Taifa halitainua upanga dhidi ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.”a—Isaya 2:2-4, NW.

4 Ni ipi kati ya dini zote katika ulimwengu ambayo imekuwa yenye kutokeza katika kutimiza matakwa hayo? Ni nani wamekataa kujifunza vita ijapokuwa magereza, kambi za mateso, na hukumu za kifo?

Upendo wa Kikristo na Kutokuwamo

5. Ni kumbukumbu gani ya kutokuwamo kwa Kikristo ambayo Mashahidi wa Yehova wameimarisha wakiwa watu mmoja mmoja, na kwa nini?

5 Mashahidi wa Yehova wajulikana ulimwenguni pote kwa ajili ya msimamo wao wa kutokuwamo kwa Kikristo wa mtu binafsi kulingana na dhamiri. Wao wamevumilia magereza, kambi za mateso, kuteswateswa, kuhamishwa, na kunyanyaswa katika karne yote ya 20 kwa sababu wamekataa kudhabihu upendo na umoja wao wakiwa kundi la ulimwengu wote la Wakristo waliovutwa kwa Mungu. Katika Ujerumani ya Nazi wakati wa miaka 1933-45, karibu Mashahidi elfu walikufa na maelfu wakafungwa gerezani, kwa sababu ya kukataa kwao kushirikiana na jitihada ya vita ya Hitler. Vivyo hivyo, chini ya Franco katika Hispania iliyokuwa ya Kifashisti hapo kwanza, mamia ya Mashahidi wachanga walienda gerezani na wengi walitumia wastani wa miaka kumi kila mmoja katika magereza ya kijeshi kuliko kujifunza vita. Mpaka wa leo katika nchi kadhaa, Mashahidi wachanga wengi wa Yehova wananyong’onyea katika magereza kwa sababu ya msimamo wao juu ya kutokuwamo kwa Kikristo. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hawaingilii shughuli za kijeshi za serikali. Kutokuwamo kwa Kikristo kwa Mashahidi kusiko na kigeu-geu katika mambo ya kisiasa kumekuwa mojawapo mambo yasiyobadilika ya imani zao katika mapambano na vita vyote vya karne ya 20. Huwatia alama ya kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo na kwawatenganisha na dini za Jumuiya ya Wakristo.—Yohana 17:16; 2 Wakorintho 10:3-5.

6, 7. Mashahidi wa Yehova wamekuja kuelewa nini kuhusu Ukristo?

6 Kwa kushikilia Biblia na kielelezo cha Kristo, Mashahidi wa Yehova huonyesha wanazoea ibada ya Mungu wa kweli, Yehova. Wao watambua upendo wa Mungu kama unavyoonyeshwa katika uhai na dhabihu ya Yesu. Wao waelewa kwamba upendo wa kweli wa Kikristo hutokeza udugu wa ulimwenguni pote usiogawanyika—juu ya migawanyiko ya kisiasa, ya kirangi na kitaifa. Maana yake, Ukristo ni zaidi ya kuwa wa kimataifa; si wa kitaifa, unavuka mipaka ya mataifa, mamlaka, au mapendezi. Huiona jamii ya kibinadamu kuwa familia moja yenye baba mmoja na Muumba mmoja, Yehova Mungu.—Matendo 17:24-28; Wakolosai 3:9-11.

7 Ingawa karibu dini nyingine zote zimehusika katika vita—vya kuua ndugu za mtu na kuua baba na mama za mtu—Mashahidi wa Yehova wameonyesha kwamba wanazingatia unabii wa Isaya 2:4, uliotangulia kunukuliwa. ‘Lakini,’ huenda ukauliza, ‘Mashahidi wa Yehova walitoka wapi? Wanatendaje?’

Mstari Mrefu wa Mashahidi wa Mungu

8, 9. Ni mwaliko gani ambao Mungu ametolea ainabinadamu?

8 Miaka zaidi ya 2,700 iliyopita, nabii Isaya pia alitoa mwaliko ufuatao: “Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu; mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie BWANA [Yehova, NW], naye atamrehemu; na arejee kwa Mungu wetu, naye atamsamehe kabisa.”—Isaya 55:6, 7.

9 Karne nyingi baadaye, mtume Mkristo Paulo alieleza Wagiriki wale katika Athene ‘waliojitoa kwenye hofu ya viabudiwa [vya kingano]:’ “[Mungu] alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili kukaa juu ya uso wote wa dunia, na yeye aliagiza nyakati zilizowekwa na mipaka iliyowekwa ya makao ya watu, ili wao wamtafute Mungu, ikiwa yamkini wapapase-pase kwa ajili yake na kwa kweli wampate yeye, ijapokuwa, hakika, yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:22-28, NW.

10. Twajuaje kwamba Mungu hakuwa mbali na Adamu na Hawa na watoto wao?

10 Hakika Mungu hakuwa mbali na viumbe wake wa kibinadamu Adamu na Hawa. Yeye alinena nao, akiwasilisha amri na matamanio yake. Zaidi ya hayo, Mungu hakujificha kutoka kwa wana wao Kaini na Abeli. Yeye alishauri Kaini mwenye chuki alipoonyesha husuda kuhusu dhabihu ya nduguye kwa Mungu. Hata hivyo, badala ya kubadili namna yake ya ibada, Kaini alionyesha wivu, ukosefu wa uvumilivu wa kidini akamwua kimakusudi nduguye Abeli.—Mwanzo 2:15-17; 3:8-24; 4:1-16.

11. (a) Neno “martyr” lamaanisha nini? (b) Abeli alikuwaje shahidi mfia-imani (martyr) wa kwanza?

11 Abeli, kwa uaminifu wake kwa Mungu mpaka kufa, akawa shahidi mfia-imani (Kiingereza, martyr] wa kwanza.b Pia yeye alikuwa shahidi wa kwanza wa Yehova na mtangulizi wa mstari mrefu wa mashahidi washika maadili katika historia yote. Kwa hiyo Paulo angeweza kutoa taarifa hii: “Kwa imani Habili [Abeli, ZSB] alimtolea Mungu dhabihu iliyo bora kuliko Kaini; kwa hiyo alishuhudiwa kuwa ana haki; Mungu akazishuhudia sadaka zake, na kwa hiyo, ijapokuwa amekufa, angali akinena.”—Waebrania 11:4.

12. Ni nani walio vielelezo zaidi vya mashahidi waaminifu wa Yehova?

12 Katika barua iyo hiyo kwa Waebrania, Paulo aorodhesha mfululizo kamili wa wanaume na wanawake waaminifu, kama vile Nuhu, Abrahamu, Sara, na Musa, ambao, kwa mwendo wao wa ukamilifu, walikuja kufanyiza ‘wingu kubwa la mashahidi [Kigiriki, mar·tyʹron]’ ambao wametumikia kuwa vielelezo na kitia-moyo kwa wengine wanaotaka kujua na kutumikia Mungu wa kweli. Wao walikuwa wanaume na wanawake waliokuwa na uhusiano pamoja na Yehova Mungu. Walikuwa wamemtafuta wakampata.—Waebrania 11:1–12:1.

13. (a) Ni kwa nini Yesu ni udhihirisho wenye kutokeza wa upendo wa Mungu? (b) Ni katika njia gani ya pekee Yesu ni kielelezo kwa wafuasi wake?

13 Wa kutokeza miongoni mwa mashahidi hao ni mmoja aliyeelezwa katika kitabu cha Ufunuo, “Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu.” Bado Yesu ni uthibitisho mwingine ulio wazi wa upendo wa Mungu, kwa maana ni kama Yohana alivyoandika: “Sisi tumeona na kushuhudia ya kuwa Baba amemtuma Mwana kuwa Mwokozi wa ulimwengu. Kila akiriye ya kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu hukaa ndani yake, naye ndani ya Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini.” Kwa kuzaliwa Myahudi, Yesu alikuwa shahidi wa kweli na alifia imani kwa uaminifu akiwa shahidi kwa Baba yake, Yehova. Vivyo hivyo, wafuasi asilia wa Kristo katika enzi zote wangekuwa mashahidi wake na wa Mungu wa kweli, Yehova.—Ufunuo 1:5; 3:14; 1 Yohana 4:14-16; Isaya 43:10-12; Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8.

14. Ni swali gani linalohitaji jibu sasa?

14 Unabii wa Isaya ulionyesha kwamba kumrudia Mungu wa kweli, Yehova, kungekuwa tukio la “sehemu ya mwisho ya zile siku,” au zinazoitwa na sehemu nyingine za Biblia kuwa “siku za mwisho.”c Kwa sababu ya utofautiano na mvurugo wa kidini ambao tumeeleza katika kitabu hiki, swali hili latokea: Ni nani katika hizi siku za mwisho tunamoishi ambao wametafuta kweli kweli Mungu wa kweli, ili wamtumikie “katika roho na kweli”? Ili kujibu swali hilo, ni lazima tuelekeze uangalifu wetu kwenye matukio ya karne ya 19.—Isaya 2:2-4, NW; 2 Timotheo 3:1-5; Yohana 4:23, 24.

Mwanamume Kijana Akitafuta Mungu

15. (a)  Charles Taze Russell alikuwa nani? (b) Baadhi ya shaka zake za kidini zilikuwa zipi?

15 Katika 1870 mwanamume kijana mwenye bidii, Charles Taze Russell (1852-1916), alianza kuuliza maswali mengi juu ya mafundisho ya kimapokeo ya Jumuiya ya Wakristo. Akiwa kijana, alifanya kazi katika duka la vifaa vya jumla la baba yake katika jiji lenye harakati za viwanda la Allegheny (sasa ni sehemu ya Pittsburgh), Pennsylvania, U.S.A. Malezi yake ya kidini yalikuwa ya Kipresbiteri na Kikongrigeshonali. Hata hivyo, alihangaishwa na mafundisho kama vile kuamuliwa kimbele na Mungu na mateso ya milele katika moto wa helo. Sababu zake za kutilia shaka mafundisho hayo ya msingi ya baadhi ya dini za Jumuiya ya Wakristo zilikuwa nini? Yeye aliandika: “Mungu ambaye angetumia uwezo wake kuumba jamii ya kibinadamu ambayo alitangulia kujua na kuandika kwamba yapaswa iteswe milele, hangeweza kuwa mwenye hekima, mwenye haki wala mwenye upendo. Kiwango chake kingekuwa cha chini zaidi ya kile cha wanadamu wengi.”—Yeremia 7:31; 19:5; 32:35; 1 Yohana 4:8, 9.

16, 17. (a) Ni mafundisho gani yaliyopendeza sana kikundi cha funzo la Biblia cha Russell? (b) Ni kutokubaliana gani kukubwa kulikotokea, na Russell alijibuje?

16 Akiwa bado yu katika muda wa kumalizia wa utineja wake, Russell alianzisha kikundi cha funzo la Biblia cha kila juma pamoja na wanaume wengine wachanga. Walianza kuchanganua mafundisho ya Biblia juu ya habari nyinginezo, kama vile kutoweza kufa kwa nafsi na pia dhabihu ya ukombozi ya Kristo na kuja kwake kwa pili. Katika 1877, akiwa na miaka 25, Russell aliuza hisa yake ya biashara ya baba yake yenye kufanikiwa na kuanza kazi-maisha ya kuhubiri wakati wote.

17 Katika 1878 Russell hakukubaliana na mmoja wa washirika wake, aliyekuwa amekataa fundisho la kwamba kifo cha Kristo chaweza kuwa upatanisho wa watenda dhambi. Katika kukanusha kwake Russell aliandika hivi: “Kristo alitimiza mambo mengi mema kwa ajili yetu kwa kifo na ufufuo wake. Yeye alikufa badala yetu; yeye alikufa akiwa wa haki kwa ajili ya wasio haki—wote walikuwa wasio haki. Yesu Kristo kwa neema ya Mungu alionja kifo kwa ajili ya kila mtu. . . . Yeye akawa asili ya wokovu wa milele kwa wote wanaomtii yeye.” Yeye aliendelea hivi: “Kufidia ni kununua ili kirudi. Kristo alinunua nini kirudi kwa ajili ya watu wote? Uhai. Sisi tuliupoteza kwa Adamu wa kwanza kukosa kutii. Kwa uhai wake mwenyewe, Adamu wa pili [Kristo] aliununua ili urudi.”—Marko 10:45; Warumi 5:7, 8; 1 Yohana 2:2; 4:9, 10.

18. (a) Ni nini kilichofuata kutokubaliana juu ya ukombozi? (b) Ni kigezo gani ambacho Wanafunzi wa Biblia walifuata kuhusiana na upaji?

18 Sikuzote akiwa mtetezi thabiti wa fundisho la ukombozi, Russell alikata vifungo vyote na aliyekuwa mshirika wake hapo awali. Katika Julai 1879, Russell alianza kutangaza Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, linalojulikana ulimwenguni pote leo kuwa Mnara wa Mlinzi—Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Katika 1881 yeye, kwa kushirikiana na Wakristo wengine walio wakfu, alianzisha sosaiti ya Biblia isiyotafuta faida. Iliitwa Zion’s Watch Tower Tract Society, ambayo leo yajulikana kuwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, wakala ya kisheria inayotenda kwa niaba ya Mashahidi wa Yehova. Tangu mwanzo wenyewe, Russell alisisitiza kwamba hakungekuwako kutoa sadaka kwenye mikutano ya kundi wala michango ya kuombaomba kupitia vichapo vya Watch Tower. Watu waliojiunga na Russell katika funzo la kina kirefu la Biblia walijulikana kwa usahili kuwa Wanafunzi wa Biblia.

Kurudi Kwenye Ukweli wa Biblia

19. Ni mafundisho gani ya Jumuiya ya Wakristo ambayo Wanafunzi wa Biblia walikataa?

19 Kwa sababu ya funzo lao la Biblia, Russell na washirika wake walikuja kukataa mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo ya “Utatu Mtakatifu Zaidi” wa kifumbo, nafsi ya kibinadamu ambayo kiasili ni isiyoweza kufa, na mateso ya milele katika moto wa helo. Pia wao walikataa uhitaji wa jamii tofauti ya kikasisi iliyozoezwa katika seminari. Wao walitaka kurudia mianzo isiyo ya kujikweza ya Ukristo, kukiwa wazee waliostahili kiroho kuongoza makundi bila ya wazo la mshahara au malipo.—1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9.

20. Wanafunzi wa Biblia hao waligundua nini kuhusu pa·rou·siʹa ya Kristo na 1914?

20 Katika uchunguzi wao wa Neno la Mungu, Wanafunzi wa Biblia hao walipendezwa kwa makini na unabii mbalimbali wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo wenye kuhusiana na “mwisho wa ulimwengu” na “kuja” kwa Kristo. (Mathayo 24:3) Kwa kuyaendea maandishi ya Kigiriki, waligundua kwamba “kuja” kwa Kristo kwa kweli kulikuwa ni “pa·rou·siʹa,” au kuwapo kusikoonekana. Kwa hiyo, Kristo alikuwa amewapa wanafunzi wake habari juu ya uthibitisho wa kuwapo kwake kusikoonekana katika wakati wa mwisho, si kuja kwa kuonekana wakati ujao. Pamoja na funzo hili, wanafunzi wa Biblia hao walikuwa na tamaa yenye makini ya kuelewa tarehe za matukio ya Biblia kuhusiana na kuwapo kwa Kristo. Bila ya kuelewa mambo yote, Russell na washirika wake walitambua kwamba 1914 ungekuwa tarehe ya muhimu sana katika historia ya kibinadamu.—Mathayo 24:3-22; Luka 21:7-33, Int.

21. Ni daraka gani ambalo Russell na waamini wenzake walihisi?

21 Russell alijua kwamba kazi kubwa ya kuhubiri ilipasa kufanywa. Yeye alifahamu maneno ya Yesu yaliyoandikwa na Mathayo: “Tena habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14; Marko 13:10) Kulikuwako uhisiji wa uharaka kwenye utendaji wa Wanafunzi wa Biblia hao kabla ya 1914. Wao waliamini kwamba utendaji wao wa kuhubiri ungefikia upeo katika mwaka huo, na kwa hiyo walihisi wanapaswa kutumia kila jitihada ili kusaidia wengine wajue “habari njema ya ufalme.” Hatimaye, mahubiri ya C. T. Russell yalikuwa yakitangazwa katika maelfu ya magazeti kuuzunguka ulimwengu.

Mitihani na Mabadiliko

22-24. (a) Itikio la Wanafunzi wa Biblia walio wengi lilikuwa nini wakati C. T. Russell alipokufa? (b) Ni nani aliyemfuata Russell kuwa msimamizi wa Watch Tower Society?

22 Katika 1916, akiwa na miaka 64, Charles Taze Russell alikufa ghafula akiwa katika safari ya kuhubiri United States yote. Sasa ingetukiaje kwa Wanafunzi wa Biblia? Je! wangefunga kazi kama kwamba walikuwa wafuasi wa binadamu wa vivi hivi? Wangekabilije mitihani ya Vita ya Ulimwengu 1 (1914-18), ambamo katika machinjo yayo karibuni United States ingehusika?

23 Itikio la wengi wa Wanafunzi wa Biblia liliwakilishwa na maneno ya W. E. Van Amburgh, ofisa mmoja wa Watch Tower Society: “Kazi hii kubwa ya ulimwenguni pote si kazi ya mtu mmoja. Ni kubwa mno kuwa hivyo. Ni kazi ya Mungu nayo haibadiliki. Mungu ametumia watumishi wengi wakati uliopita na Yeye bila shaka atatumia wengi katika wakati ujao. Wakfu wetu si kwa binadamu, wala kwa kazi ya binadamu, bali ni ili kufanya mapenzi ya Mungu, kama ambavyo Yeye atayafunua kwetu kupitia Neno Lake na miongozo ya kimungu. Mungu angali kwenye usukani.”—1 Wakorintho 3:3-9.

24 Katika Januari 1917, Joseph F. Rutherford, mwanasheria na mwanafunzi wa makini wa Biblia, alichaguliwa kuwa msimamizi wa pili wa Watch Tower Society. Yeye alikuwa na utu wenye nguvu na hangeweza kutishwa. Yeye alijua kwamba Ufalme wa Mungu ulipasa kuhubiriwa.—Marko 13:10.

Bidii Iliyofanywa Upya na Jina Jipya

25. Wanafunzi wa Biblia waliitikiaje kazi kubwa katika miaka iliyofuata vita ya ulimwengu ya kwanza?

25 Watch Tower Society ilipanga mikusanyiko katika United States katika 1919 na katika 1922. Baada ya mnyanyaso wa Vita ya Ulimwengu 1 katika United States, ilikuwa karibu ni kama Pentekoste nyingine kwa Wanafunzi wa Biblia maelfu machache wakati huo. (Matendo 2:1-4) Badala ya kuhofu binadamu, walitwaa kwa nguvu hata zaidi mwito wa kwenda na kuwahubiria mataifa. Katika 1919 Watch Tower Society ilitokeza gazeti-jenzi la Mnara wa Mlinzi lililoitwa The Golden Age, linalojulikana ulimwenguni pote leo kuwa Amkeni! Hili limetumika kuwa chombo chenye nguvu nyingi cha kuamsha watu waone umaana wa nyakati tunamoishi na kujenga uhakika katika ahadi ya Muumba ya ulimwengu mpya wenye amani.

26. (a) Wanafunzi wa Biblia walitia mkazo zaidi juu ya daraka gani? (b) Wanafunzi wa Biblia walipata kuelewa kupi kwa Biblia ambako ni wazi zaidi?

26 Wakati wa miaka ya 1920 na 1930, Wanafunzi wa Biblia walitia mkazo zaidi na zaidi kwenye njia ya mapema ya Kikristo ya kuhubiri—nyumba kwa nyumba. (Matendo 20:20) Kila mwaminifu alikuwa na daraka la kutoa ushahidi kwa watu wengi iwezekanavyo kuhusiana na utawala wa Ufalme wa Kristo. Walikuja kuona kwa uwazi kutokana na Biblia kwamba suala kuu mbele ya ainabinadamu lilikuwa lile la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima na kwamba hilo lingesuluhishwa na Yehova Mungu kwa kumponda Shetani na kazi zake zote za uharibifu juu ya dunia. (Warumi 16:20; Ufunuo 11:17, 18) Katika muktadha wa suala hili, ilithaminiwa kwamba wokovu wa binadamu ulikuwa wa pili kwa kutetewa kwa Mungu Mwenye Enzi Kuu aliye na haki. Kwa hiyo, wangepaswa wawepo duniani mashahidi waaminifu wenye nia ya kushuhudia makusudi na mamlaka kuu ya Mungu. Uhitaji huo ulitimizwaje?—Ayubu 1:6-12; Yohana 8:44; 1 Yohana 5:19, 20.

27. (a) Ni tukio gani la maana lililotukia katika 1931? (b) Ni zipi baadhi ya imani za Mashahidi zenye kuwatofautisha?

27 Katika Julai 1931, Wanafunzi wa Biblia walifanya mkusanyiko katika Columbus, Ohio, ambao katika huo maelfu waliokuwapo walipitisha azimio. Katika hilo kwa shangwe walikubali “jina ambalo kinywa cha Bwana Mungu kimetaja,” na wao wakajulisha rasmi: “Sisi twatamani kujulikana na kuitwa kwa jina, lisemalo, ‘mashahidi wa Yehova.’” Tangu tarehe hiyo, Mashahidi wa Yehova wamejulikana ulimwenguni pote si kwa ajili ya imani zao zilizo tofauti tu bali pia kwa ajili ya huduma yao ya bidii ya nyumba kwa nyumba na barabarani. (Ona 356-7.)—Isaya 43:10-12; Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8.

28. Katika 1935 Mashahidi walipata kuelewa kupi ambako ni wazi zaidi juu ya utawala wa Ufalme?

28 Katika 1935 Mashahidi walikuja kuelewa vizuri zaidi juu ya jamii ya Ufalme ya kimbingu, watakaotawala pamoja na Kristo, na raia zao juu ya dunia. Tayari walijua kwamba hesabu ya Wakristo wapakwa mafuta walioitwa wakatawale pamoja na Kristo katika mbingu, ingekuwa 144,000 tu. Kwa hiyo, tumaini la ile ainabinadamu nyingine lingekuwa nini? Serikali yahitaji raia ili istahili kuwapo. Hii serikali, Ufalme wa kimbingu, ingekuwa pia na mamilioni ya raia waaminifu hapa duniani. Wao wangekuwa ule “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” wanaopaaza sauti hivi: “Wokovu una Mungu [Yehova] wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo [Kristo Yesu].”—Ufunuo 7:4, 9, 10; 14:1-3; Warumi 8:16, 17.

29. Ni kazi gani kubwa ambayo Mashahidi waliona wakaikubali?

29 Kuelewa huku juu ya mkutano mkubwa kulisaidia Mashahidi wa Yehova waone kwamba walikuwa na kazi kubwa mbele yao—kutafuta na kufundisha mamilioni wote wale waliokuwa wakitafuta Mungu wa kweli na ambao wangefanyiza “mkutano mkubwa.” Ingetia ndani shughuli ya kimataifa ya kielimu. Ingehitaji wanenaji na wahudumu waliozoezwa. Shule zingehitajiwa. Yote hayo yalionwa kimbele na msimamizi aliyefuata wa Watch Tower Society.

Jitihada ya Ulimwenguni Pote ya Kutafuta Watafutaji Mungu

30. Ni matukio gani ya miaka ya 1930 na 1940 yaliyoathiri Mashahidi?

30 Katika 1931 kulikuwako Mashahidi wanaopungua 50,000 katika mabara yanayopungua 50. Pia matukio ya miaka 1930 na 1940 hayakufanya kuhubiri kwao kuwe rahisi zaidi. Kipindi hiki kiliona kutokeza kwa Ufashisti na Unazi na mfyatuko wa Vita ya Ulimwengu 2. Katika 1942 J. F. Rutherford akafa. Watch Tower Society ingehitaji uongozi wenye sulubu kusudi msukumo mkubwa zaidi utolewe kwenye kuhubiri kwa Mashahidi wa Yehova.

31. Ni nini kilichoanza kufanya kazi katika 1943 ili kupanua kuhubiriwa kwa habari njema?

31 Katika 1942, akiwa na miaka 36, Nathan H. Knorr alichaguliwa kuwa msimamizi wa tatu wa Watch Tower Society. Yeye alikuwa mfanyiza tengenezo mwenye nishati mwenye mwono-ndani ulio wazi katika uhitaji wa kuendeleza mbele kuhubiri habari njema ulimwenguni pote kwa kasi iwezekanayo, hata ingawa mataifa walikuwa wangali wanamenyana katika Vita ya Ulimwengu 2. Kama tokeo, bila kukawia alitekeleza mpango wa shule ya kuzoeza wamisionari, iliyoitwa Watchtower Bible School of Gilead.d Wanafunzi mia wa kwanza, wote wahudumu wa wakati wote, waliandikishwa katika Januari 1943. Walijifunza kindani Biblia na habari za kihuduma zenye kuhusiana kwa karibu miezi sita kabla ya kutumwa kwenye migawo yao, hasa katika nchi za kigeni. Kufikia 1991, madarasa 90 yalikuwa yamehitimu, na maelfu ya wahudumu wametoka Gileadi wakatumikie ulimwenguni pote.

32. Ni maendeleo gani ambayo yamefanywa na Mashahidi wa Yehova tangu 1943?

32 Katika 1943 kulikuwako Mashahidi 126,329 wakihubiri katika nchi 54. Ijapokuwa upinzani wa kikatili wa Unazi, Ufashisti, Ukomunisti, na Aksio Katoliki na pia zile zilizoitwa demokrasia wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, kufikia 1946 Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefikia kilele cha wahubiri wa Ufalme zaidi ya 176,000. Miaka 44 baadaye, kulikuwako zaidi ya milioni nne wenye kutenda katika mabara, visiwa, na maeneo zaidi ya 200. Bila shaka, kitambulisho chao cha wazi kwa jina na tendo kimetumika kufanya wajulikane ulimwenguni pote. Lakini mambo mengine yamehusika ambayo yameongezea sana matokeo yao.—Zekaria 4:6.

Tengenezo la Elimu ya Biblia

33. Ni kwa nini Mashahidi wa Yehova wana Majumba ya Ufalme?

33 Mashahidi wa Yehova hufanya mikutano ya funzo la Biblia la kila juma katika Majumba ya Ufalme yao yanayotumikia makundi zaidi ya 60,000 katika dunia yote. Mikutano hii haitegemei desturi wala hisia za moyo bali juu ya kutwaa maarifa sahihi ya Mungu, Neno lake, na makusudi yake. Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova huja pamoja mara tatu kwa juma ili kuongezea kuelewa kwao Biblia na ili kujifunza kuhubiri na kufundisha ujumbe wayo kwa wengine.—Warumi 12:1, 2; Wafilipi 1:9-11; Waebrania 10:24, 25.

34. Ni nini kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?

34 Kwa kielelezo, mkutano mmoja wa katikati ya juma hutia ndani Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambayo katika hiyo washiriki wa kundi waweza kujiandikisha. Shule hii, yenye kusimamiwa na mzee Mkristo anayestahili, hutumika kuzoeza wanaume, wanawake, na watoto katika ufundi wa kufundisha na kujieleza kwa kulingana na kanuni za Biblia. Mtume Paulo alitoa taarifa hii: “Maneno yenu yawe na neema sikuzote yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.” Katika mikutano yao ya Kikristo, Mashahidi pia hujifunza jinsi ya kueleza ujumbe wa Ufalme “kwa upole na kwa hofu.”—Wakolosai 4:6; 1 Petro 3:15.

35. Ni nini baadhi ya mikutano mingine wanayofanya Mashahidi, na ina manufaa gani?

35 Katika siku tofauti, Mashahidi pia hukutana kwa ajili ya hotuba ya dakika 45 ikifuatwa na mfikirio wa kundi wa saa moja (kwa njia ya maswali na majibu) wa kichwa fulani cha Biblia kinachohusiana na fundisho au mwenendo wa Kikristo. Washiriki wa kundi wako huru kushiriki. Kila mwaka Mashahidi pia huhudhuria mikutano mitatu mikubwa zaidi, makusanyiko na mikusanyiko ya siku moja mpaka nne, ambako maelfu kwa kawaida hujumuika ili kusikiliza hotuba za Biblia. Kama tokeo la mikutano hii na mingineyo isiyo ya malipo, kila Shahidi huongeza maarifa yake juu ya ahadi za Mungu kwa ajili ya dunia hii na kwa ajili ya ainabinadamu zaidi ya kujipatia elimu bora sana katika maadili ya Kikristo. Kila mmoja huvutwa karibu na Mungu wa kweli, Yehova, kwa kufuata mafundisho na kielelezo cha Kristo Yesu.—Yohana 6:44, 65; 17:3; 1 Petro 1:15, 16.

Mashahidi Wamepangwaje Kitengenezo

36. (a) Je! Mashahidi wana jamii ya makasisi wanaolipwa? (b) Basi, ni nani wanaoongoza katika kundi?

36 Kwa kufaa ikiwa Mashahidi wa Yehova wanafanya mikutano na wamepangwa kitengenezo wahubiri, ni lazima wawe na mtu fulani wa kuongoza. Hata hivyo, hawana makasisi wanaolipwa wala hawana kiongozi fulani mwenye karama aliyekwezwa. (Mathayo 23:10) Yesu alisema: “Mmepata bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8; Matendo 8:18-21) Katika kila kundi, kuna wazee na watumishi wa huduma wanaostahili kiroho, wengi wao wakiwa na kazi ya kuajiriwa na wakitunza familia, ambao kwa kujitolea huongoza katika kufundisha na kuelekeza kundi. Hicho hasa ndicho kigezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza.—Matendo 20:17; Wafilipi 1:1; 1 Timotheo 3:1-10, 12, 13.

37. Wazee na watumishi wa huduma huwekwaje?

37 Wazee na watumishi wa huduma huwekwaje? Kuwekwa kwao hufanywa chini ya baraza linaloongoza la wazee wapakwa mafuta kutoka mabara mbalimbali ambalo kazi yalo yalingana na ile ya baraza la mitume na wazee katika Yerusalemu waliokuwa wakiongoza katika kundi la Kikristo la mapema. Kama tulivyoona katika Sura 11, hakuna mtume yeyote mmoja aliyekuwa wa daraja la kwanza juu ya wale wengine. Wao walifikia maamuzi wakiwa baraza, nayo yaliheshimiwa na makundi yaliyotawanyika katika ulimwengu wote wa kale wa Kiroma.—Matendo 15:4-6, 22, 23, 30, 31.

38. Baraza Linaloongoza hufanyaje kazi?

38 Mpango uo huo unafanya kazi kwa ajili ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo. Wao hufanya mikutano ya kila juma kwenye makao makuu yao ya ulimwengu katika Brooklyn, New York, kisha maagizo hupelekwa kwa Halmashauri za Tawi kuuzunguka ulimwengu ambazo zinasimamia utendaji wa kihuduma katika kila nchi. Kwa kufuatia kielelezo cha Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wameweza kueneza visehemu vikubwa vya dunia kwa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kazi hiyo yaendelea kwa kipimo cha tufe lote.—Mathayo 10:23; 1 Wakorintho 15:58.

Kumiminika Kuelekea Mungu wa Kweli

39. (a) Ni kwa nini Mashahidi huchukua msimamo wa kutokuwamo katika masuala ya kisiasa? (b) Mashahidi wamefanikiwaje chini ya marufuku?

39 Wakati wa karne ya 20, Mashahidi wa Yehova wamefanikiwa katika dunia yote. Hiyo imekuwa kweli hata katika mabara ambayo wamekuwa chini ya marufuku au kizuizi. Marufuku hizo ziliwekwa hasa na tawala ambazo zilishindwa kuelewa msimamo wa kutokuwamo wa Mashahidi wa Yehova kuhusu utiifu wa kisiasa na kitaifa wa ulimwengu huu. (Ona kisanduku, ukurasa 347.) Hata hivyo, katika mabara hayo, makumi ya maelfu ya watu wamegeukia Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la kweli kwa ajili ya amani na usalama wa ainabinadamu. Katika mataifa yaliyo mengi ushahidi mkubwa umetolewa, na sasa kuna mamilioni ya Mashahidi wenye kutenda kila mahali.—Ona chati, ukurasa 361.

40, 41. (a) Mashahidi wa Yehova wangojea nini sasa? (b) Ni swali gani ambalo bado litajibiwa?

40 Kwa upendo wao wa Kikristo na tumaini lao la “mbingu mpya na dunia mpya,” Mashahidi wa Yehova wanatazamia wakati ujao ulio karibu kwa ajili ya matukio yenye kutikisa ulimwengu ambayo karibuni lazima yakomeshe ukosefu wa haki, ufisadi, na ukosefu wa uadilifu wote katika dunia hii. Kwa sababu hiyo wao wataendelea kuzuru majirani wao katika jitihada ya moyo mweupe ya kuwaleta watu wenye mioyo minyoofu karibu zaidi na Mungu wa kweli, Yehova.—Ufunuo 21:1-4, NW; Marko 13:10; Warumi 10:11-15.

41 Kwa sasa, kulingana na unabii wa Biblia, wakati ujao umewekea nini ainabinadamu, dini, na dunia hii iliyochafuliwa? Sura yetu ya mwisho itajibu swali hili la muhimu.—Isaya 65:17-25; 2 Petro 3:11-14.

[Maelezo ya Chini]

a Sentensi hizo mbili za mwisho zapatikana kwenye “Ukuta wa Isaya” mbele ya majengo ya UM na pia kwenye sanamu moja katika bustani za UM, na kama ilivyo, utimizo wayo ndio moja la malengo ya UM.

b Neno la Kigiriki mar’tyr, ambalo neno la Kiingereza “martyr” limetolewa (“mtu anayetoa ushahidi kwa kifo chake,” An Expository Dictionary of New Testament Words, cha W. E. Vine), kwa kweli lamaanisha “shahidi” (“mtu anayethibitisha, au anayeweza kuthibitisha, yale ambayo yeye mwenyewe ameona au kusikia au kujua kwa njia nyingine yoyote,” A Greek-English Lexicon of the New Testament, cha J. H. Thayer).

c Kwa mfikirio zaidi wa “siku za mwisho,” ona Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., 1982, sura 18.

d Gileadi, neno linalotokana na Gal·êdh katika Kiebrania, lamaanisha “Rundo la Ushahidi.” Ona pia Insight on the Scriptures, Buku 1, kurasa 882, 942.—Mwanzo 31:47-49.

[Sanduku katika ukurasa wa 347]

Christian Neutrality in Pagan Rome

Kwa kupatana na kanuni za upendo na amani ambazo Yesu alifundisha, na kwa kutegemea funzo lao la kibinafsi la Neno la Mungu, Wakristo wa mapema hawangeshiriki katika vita wala katika kujizoeza hivyo. Yesu alikuwa amesema: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, mahadimu wangu wangepigana kwamba mimi nisitolewe kwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu si kutoka chanzo hiki.”—Yohana 18:36, NW.

Tarehe ya baadaye sana katika 295 W.K., Maximiliano wa Theveste, mwana wa aliyekuwa mwanajeshi Mroma, aliandikishwa kwa ajili ya utumishi wa kijeshi. Wakati prokonso alipomwuliza jina lake, yeye alijibu: “Sasa, kwa nini wataka kujua jina langu? Mimi nina katao la kidhamira juu ya utumishi wa kijeshi: Mimi ni Mkristo. . . . Mimi siwezi kutumika; mimi siwezi kuitenda dhambi dhamiri yangu.” Prokonso huyo alimwonya kwamba angepoteza uhai wake kama hangetii. “Mimi sitatumika. Wewe waweza kunikata kichwa, lakini mimi sitatumikia mamlaka za Ulimwengu Huu; Mimi nitatumikia Mungu wangu.”—An Historian’s Approach to Religion, cha Arnold Toynbee.

Katika nyakati za kisasa, funzo la kibinafsi la Biblia limeongoza Mashahidi wa Yehova mmoja mmoja ulimwenguni pote wafuate miongozo ya dhamiri katika kuchukua msimamo kama huo. Katika nchi fulani fulani wengi walilipa bei ya juu zaidi, hasa katika Ujerumani ya Nazi, ambako walipigwa risasi, wakanyongwa, na kukatwa kichwa wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Lakini umoja wao wa ulimwenguni pote, ukitegemea upendo wa Kikristo, haujapata kuvunjwa kamwe. Hakuna yeyote ambaye amepata kufa katika vita mikononi mwa mmoja wa Mashahidi Wakristo wa Yehova. Jinsi historia ya ulimwengu ingalikuwa tofauti kama kila anayedai kuwa Mkristo angaliishi pia kwa kufuata amri ya Kristo ya upendo!—Warumi 13:8-10; 1 Petro 5:8, 9.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 356, 357]

Wanayoamini Mashahidi wa Yehova

Swali: Nafsi ni nini?

Jibu: Katika Biblia nafsi (Kiebrania, neʹphesh; Kigiriki, psy·kheʹ) ni mtu au mnyama au uhai ambao anafurahia.

“Na Mungu akaendelea kusema: ‘Acha dunia itokeze nafsi zilizo hai kwa kulingana na aina zazo, mnyama wa kufugwa na mnyama anayesonga na hayawani mwitu wa dunia kwa kulingana na aina yake.’ Na Yehova Mungu akachukua hatua ya kufanya mtu kutoka kwa mavumbi ya ardhi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, na mtu akaja kuwa nafsi inayoishi.”—Mwanzo 1:24; 2:7, NW.

Wanyama na binadamu NI nafsi zinazoishi. Nafsi si kitu chenye kuwapo tofauti. Yaweza kufa na inakufa. “Tazama! Nafsi zote—ni mali yangu. Kama nafsi ya baba ndivyo na nafsi ya mwana—ni mali yangu. Nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe itakufa.”—Ezekieli 18:4, NW.

Swali: Je! Mungu ni Utatu?

Jibu: Mashahidi wa Yehova huamini kwamba Yehova ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima asiye na kifani. “Sikiliza, O Israeli: Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” (Kumbukumbu la Torati 6:4, NW) Kristo Yesu akiwa Neno alikuwa kiumbe wa kiroho naye alikuja duniani kwa kutii mapenzi ya Baba yake. Yeye anatii Yehova. “Lakini wakati vitu vyote vitakuwa vimetiishwa kwake [Kristo], ndipo Mwana mwenyewe atajitiisha mwenyewe kwa Yule ambaye alitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu aweze kuwa vitu vyote kwa kila mmoja.”—1 Wakorintho 15:28, NW; ona pia Mathayo 24:36; Marko 12:29; Yohana 1:1-3, 14-18; Wakolosai 1:15-20.

Roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu, au nishati ikitenda kazi, wala si mtu.—Matendo 2:1-4, 17, 18.

Swali: Je! Mashahidi wa Yehova huabudu au kuheshimu sanamu?

Jibu: Mashahidi wa Yehova hawazoei namna yoyote ya ibada ya sanamu, iwe inahusu sanamu, watu, au matengenezo.

“Sisi twajua kwamba sanamu si kitu katika ulimwengu, na kwamba hakuna Mungu ila mmoja. Kwa maana hata ingawa kuna wale ambao huitwa ‘vijimungu,’ wawe katika mbingu au juu ya dunia, sawa na kulivyo ‘vijimungu’ vingi na ‘mabwana’ wengi, kwa kweli kwetu sisi kuna Mungu mmoja aliye Baba, ambaye kutoka kwake vitu vyote vipo, na sisi kwa ajili yake; na kuna Bwana mmoja, Yesu Kristo, ambaye kupitia kwake vitu vyote vipo, na sisi kupitia kwake.”—1 Wakorintho 8:4-6, NW; ona pia Zaburi 135:15-18.

Swali: Je! Mashahidi wa Yehova husherehekea Misa au Komunyo?

Jibu: Mashahidi wa Yehova hawaamini kugeuka kwa divai kuwa damu halisi na mkate kuwa mwili halisi wa Yesu, ambalo ni fundisho la Roma Katoliki. Wao husherehekea Chakula cha Jioni cha Bwana kwenye tarehe inayolingana na Nisani 14 ya Kiyahudi (kwa kawaida katika Machi au Aprili) kuwa ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo. Kwenye mkutano huu wao hupitisha kwenye kundi mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu kuwa wonyesho wa mwili wa Kristo usio na dhambi na damu yake ya kidhabihu. Wale tu wenye tumaini la kutawala na Kristo katika Ufalme wake wa kimbingu ndio hushiriki mifano hiyo.—Marko 14:22-26; Luka 22:29; 1 Wakorintho 11:23-26; Ufunuo 14:1-5.e

[Picha]

Mashahidi wa Yehova hukutana kwa ukawaida katika Majumba ya Ufalme kwa ajili ya funzo la Biblia

Majumba ya Ufalme: Jiji la Ichihara, Japan (ukurasa uliotangulia), na Boituva, Brazil

[Maelezo ya Chini]

e Kwa mfikirio zaidi wa habari hii, ona Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., 1989, kurasa 201-5; 352-6.

[Chati katika ukurasa wa 361]

Nchi Fulani Ambako Mashahidi Huhubiri

Nchi Mashahidi Watendaji

Afrika Kusini 49,000

Argentina 83,000

Australia 53,000

Brazil 293,000

Canada 102,000

Colombia 47,000

El Salvador 18,000

Finland 18,000

Hispania 85,000

Hungary 11,000

India 10,000

Italia 181,000

Japan 148,000

Korea 62,000

Lebanon 2,800

Mexico 305,000

Nigeria 142,000

Poland 97,000

Puerto Rico 24,000

Ufaransa 114,000

Ufilipino 105,000

Ugiriki 24,000

Uingereza 121,000

Ujerumani 154,000

Ureno 37,000

U.S.A 850,000

Venezuela 52,000

Zambia 74,000

33 chini ya marufuku 197,000

Tarakimu za Ulimwengu za 1990 Makundi 63,016 Mashahidi 4,017,000

[Picha katika ukurasa wa 346]

sanamu ya amani ya um hutoa taarifa hii: “sisi tutafua panga zetu kuwa majembe ya plau”; “Ukuta wa Isaya” hutoa andiko hilo la Kibiblia

[Picha katika ukurasa wa 351]

Mashahidi wa Yehova huamini katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo kwa ajili ya dhambi za ainabinadamu

[Picha katika ukurasa wa 363]

Majumba ya Kusanyiko ya Mashahidi wa Yehova: Mtazamo ukiwa angani wa jumba katika East Pennines, Uingereza

Jumba la Kusanyiko, Fort Lauderdale, Florida, U.S.A., linalotumiwa kwa ajili ya programu za Kiingereza, Kihispania, na Kifaransa

[Picha katika ukurasa wa 364]

Makao Makuu ya Ulimwengu ya Watch Tower Society, Brooklyn, New York; (kutoka juu kushoto) maofisi, viwanda, na makao (yenye rangi ya kutokeza)

[Picha katika ukurasa wa 365]

Maofisi ya Tawi ya Watch Tower (kutoka juu kushoto) katika Afrika Kusini, Hispania, na New Zealand

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki