Yehova Akusanya na Kuwapa Watu Wake Vifaa vya Kazi
Katika karne zote, uasi-imani ulikuwa umeenea katika dunia yote. Madhehebu mengi ya makanisa yalikuwa na mafundisho fulani ya Biblia lakini sana sana yakafuata mapokeo ya kibinadamu na desturi nyingi zilizotokana na wapagani. Matazamio juu ya kurudi kwa Kristo kwa ujumla yalisukumiwa nyuma. —Mathayo 13:24-30, 37-43.
Hata hivyo, Yesu alikuwa amesema tuendelee kulinda kwa ajili ya kurudi kwake! Kikundi kimoja kilichokuwa kikifanya hivyo kilikuwa katika Allegheny, Pennsylvania, U.S.A. Katika miaka ya mapema ya 1870 Charles Taze Russell na wengine wa marafiki wake walianza kufanya uchunguzi wa Biblia ulio kamili, usio wa kimadhehebu, kuhusu kurudi kwa Kristo. Pia walianza kutafuta ukweli wa Biblia juu ya mafundisho mengine mengi ya msingi. Huo ulikuwa ndio mwanzo wa utendaji wa kisasa wa Mashahidi wa Yehova.—Mathayo 24:42.
Kikundi hicho kikaja kufahamu kwamba fundisho la Utatu si la Kibiblia bali Yehova pekee ndiye Mungu mwenye nguvu zote na Muumba; Yesu Kristo ni uumbaji Wake wa kwanza na Mwana mzaliwa pekee; na roho takatifu si mtu bali ni kani ya utendaji isiyoonekana ya Mungu. Kikundi hicho kiliona kwamba nafsi inakufa, kwamba tumaini la wafu ni ufufuo, na kwamba adhabu ya kutenda uovu usiotubiwa si mateso ya milele bali ni kuangamizwa kabisa.
Kutoa kwa Yesu uhai wake uwe ukombozi kwa ajili ya wanadamu kulionwa kuwa fundisho la msingi la Biblia. Kwanza, wanaume na wanawake 144,000 waliochaguliwa tangu karne ya kwanza mpaka wakati wetu, watakombolewa kutoka dunia wawe warithi washirika pamoja na Kristo katika Ufalme wa kimbingu. Kisha kupitia ukombozi wa Yesu mabilioni ya wanadamu, ambao wengi wao ni wale watakaofufuliwa, watafikia ukamilifu wakiwa na taraja la uzima wa milele duniani chini ya utawala wa Ufalme.
Russell na washiriki wenzake pia waliona kwamba kuwapo kwa Kristo kulikuwa kusikoonekana, katika roho. Nyakati za Mataifa, ambazo ni kipindi ambacho enzi kuu ya Mungu haikuwa ikionyeshwa kupitia serikali yo yote duniani, zingemalizika mwaka wa 1914. Ndipo Ufalme wa Mungu ungesimamishwa mbinguni. Mafundisho hayo yanashirikishwa na Mashahidi wa Yehova leo.
Russell na wenzi wake walizitangaza kweli hizo kwa urefu na upana kwa njia ya hotuba na vichapo. Katika Julai 1879, Russell alianza kuchapisha gazeti Zion’s Watch Tower (sasa ni Mnara wa Mlinzi). Yeye aliamua kwamba utendaji wa kuhubiri wa Wanafunzi wa Biblia umepasa kutegemea kabisa michango ya kujitolea na kwamba hakuna sadaka za pesa ambazo zingechukuliwa. Pia, ujumbe huo umepasa uenezwe kupitia jitihada za kutokulipwa, za kujitolea kwa wale walioamini. Russell mwenyewe alichanga fedha kutoka mali alizokuwa amekusanya katika biashara kufikia wakati huo.
Wanafunzi wa Biblia walikusanyika pamoja katika madarasa, kama makundi yao yalivyokuwa yakiitwa wakati huo. Walikusanyika kufika mara tatu kila juma, kwa hotuba, kwa kujifunza Maandiko, na mikutano ya kutoa ushuhuda. Kwa ukawaida waliwachagua wanaume wenye madaraka wawe wazee wa kusimamia utendaji wa kiroho wa kila darasa.
Mwaka wa 1884, Shirika Zion’s Watch Tower Tract Society lilianzishwa kisheria likiwa shirika lisilo la faida katika Pennsylvania. Msimamizi wa shirika hilo alipaswa achaguliwe kila mwaka. Jambo hilo lilitoa chombo halali, kisichotegemea maisha ya mtu mmoja ye yote, aendeleze kazi ya elimu ya Biblia. Charles T. Russell alichaguliwa kuwa msimamizi, na afisi yake ilitegemewa kuwa makao makuu.
Jitihada kubwa zilifanywa kupanua kazi kwenye nchi nyingine. Ilifika Kanada na Uingereza katika miaka ya mapema ya 1880. Mwaka wa 1891 Russell alifanya ziara ya kwenda Ulaya na Mashariki ya Kati ili kuchunguza ni jambo gani lingeweza kufanywa ili kusongeza mbele huko kuenezwa kwa ukweli. Mapema katika miaka ya kuanzia 1900, afisi za tawi za Sosaiti zilianzishwa katika Uingereza, Ujeremani, na Australia.
Mwaka wa 1909 makao makuu ya Watch Tower Society yalihamishwa yakapelekwa Brooklyn, New York, ili kupanua kwa njia bora kazi ya kuhubiri katika mataifa yote. Ikawa lazima kuanzisha shirika-jenzi chini ya sheria za tarafa ya New York, Shirika linalojulikana sasa kuwa Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. Mwaka wa 1914 shirika International Bible Students Association lilianzishwa London, Uingereza, ili kusongeza mbele utendaji wa Wanafunzi wa Biblia katika Jumuiya ya Madola ya Uingereza. Kwa sasa mashirika kama 70 yaliyofanywa kisheria katika nchi nyingi kuzunguka ulimwengu yanatimiza makusudi ya Watch Tower Society. Yote ni ya ufadhili, yakitegemezwa na michango ya kujitolea na wafanya kazi wa kujitolea.
Mwaka wa 1916 Charles Taze Russell akafa, na Joseph Franklin Rutherford akamfuata kuwa msimamizi wa Watch Tower Society. Wakati wa miaka ya kumalizia ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Wanafunzi wa Biblia walijaribiwa vikali kwa mateso, yakifikia kikomo cha kufungwa isivyo haki kwa ndugu wanane wenye kutumikia katika vyeo vyenye madaraka kuhusiana na makao makuu ya Sosaiti katika Amerika. Kazi ya Wanafunzi wa Biblia ilionekana imo hatarini. Hata hivyo, mwaka wa 1919 ndugu hao walifunguliwa na wakaondolewa hatia, na sasa ukaanza mpanuko mkubwa zaidi wa kazi ya kuhubiri.
Kupitia makao makuu ya Sosaiti, baraza lenye umoja la Wanafunzi wa Biblia Wakristo wapakwa-mafuta liliendelea kutoa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa kwa ajili ya watu wote mmoja mmoja walioshirikiana na tengenezo hilo. Kama vile kundi la Wakristo wapakwa-mafuta katika karne ya kwanza lilivyokuwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” aliyetajwa na Yesu, ndivyo pia kikundi hicho kilichopakwa mafuta cha Wanafunzi wa Biblia walio wakfu, kinachofanya kazi ya Ufalme, kilivyo jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” katika wakati wetu. Wakati wa kuja kwa Yesu kukagua kundi, aliikuta jamii hiyo ikitoa chakula kuwapa watu wa nyumbani mwake; kisha akaiweka juu ya mali zake zote. —Mathayo 24:45-47; Luka 12:42.
Mara baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ikaonekana waziwazi kwamba Ufalme wa Mungu kupitia Kristo Yesu ulikuwa umesimamishwa katika mbingu mwaka wa 1914. Hivyo sasa maneno haya ya Yesu yangepata utimizo kamili: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Joseph F. Rutherford alichukua hatua ya kwanza kuufanya ujumbe huo wa Ufalme upatikane kwa idadi iliyo kubwa hata zaidi ya watu. —Mathayo 24:14, NW.
Kwa sababu hiyo, Sosaiti ikaamua kujifanyia uchapaji wayo yenyewe ikitumia wafanya kazi wa kujitolea waliokuwa wanaume walio wakfu, ili kuhakikisha kuna utoaji wa daima wa vitabu vya Biblia kwa gharama iliyo ndogo zaidi iwezekanavyo. Wanafunzi wa Biblia wote walitiwa moyo washiriki kwa ukawaida kuzihubiri habari njema za Ufalme. Kutangazwa kwa hotuba za Biblia kwa njia ya redio kulitumiwa katika nchi kadha.
Kabla ya mwaka wa 1918 Wanafunzi wa Biblia walifahamu kwamba kusudi lao la kuhubiri lilikuwa ni kuwakusanya mabaki ya wale waliochaguliwa wakawe pamoja na Kristo Yesu mbinguni na kuuonya ulimwengu juu ya hukumu ya Mungu iliyokuwa inakuja. Si fikira nyingi zilizotolewa juu ya kukusanya wale ambao wangeuokoka mwisho wa mfumo mbovu uliopo waishi duniani. Ndipo tangu mwaka wa 1918 ile hotuba “Mamilioni Wanaoishi Sasa Huenda Wasife Kamwe!” ilipotolewa mahali pote.
Mwaka wa 1923 uchunguzi wa mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi katika Mathayo 25:31-46 ukaonyesha kwamba kabla ya Har–Magedoni watu wenye maelekeo ya uadilifu ambao si sehemu ya Ufalme wa kimbingu wangepata pia kibali ya Mungu na wangeokoka Har–Magedoni. Mwaka wa 1935 uchunguzi zaidi ukaonyesha hao watu walio wa mfano wa kondoo kuwa wanalingana na mkutano mkubwa, wa watu wasiohesabika unaosimuliwa katika Ufunuo 7:9-17. Hao wangepaswa kukusanywa kutoka mataifa yote, na wangekuwa na taraja la kuiokoka Dhiki Kubwa na kupokea uzima wa milele duniani. Ufahamu huo ukatoa kichocheo kikubwa cha kufanya kazi ya kuhubiri. —Yohana 10:16.
Mwaka wa 1931 Wanafunzi wa Biblia walilikubali jina Mashahidi wa Yehova. Kabla ya wakati huo walijulikana kuwa Wanafunzi wa Biblia, Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, Watu wa Mapambazuko ya Miaka Elfu, Watu wa Watch Tower. Hata walibandikwa jina la Wanaruseli na Wanarutherfordi. Hakuna lo lote la majina hayo yalilowatambulisha vya kufaa. Ijapokuwa jina Wakristo, walilopewa wanafunzi wa Yesu kwa uongozi wa kimungu katika karne ya kwanza, hakika lilifaa, hilo pia lilikuwa likitumiwa na vikundi vingi sana vyenye kufuata mafundisho ya uwongo. Ili kujitofautisha wenyewe na mamilioni ya Wakristo wa jina tu, ilibidi kuwe na jina ambalo lingewatambulisha waziwazi wafuasi wa kweli wa Kristo leo.
Uchunguzi wa Maandiko ulionyesha wazi kwamba kama vile Yehova alivyokuwa amewaita watu wa Israeli kuwa mashahidi, vivyo hivyo watu wake katika umalizio wa mfumo wa mambo, ambao wamejiweka wakfu wajulishe jina lake na kusudi lake, wamepaswa waitwe kwa kufaa Mashahidi wa Yehova. Jina hilo limetofautisha kwa kufaa Wakristo walio waabudu wa kweli wa Yehova na wengine wote wanaojidai kuwa Wakristo leo. —Zaburi 83:18; Isaya 43:10-12.
Mwaka wa 1942, wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, Joseph F. Rutherford alikufa, na Nathan H. Knorr akamfuata kuwa msimamizi wa Watch Tower Society. Sasa unabii ulionekana kuwa ukionyesha waziwazi kwamba kungekuwako kipindi cha baada ya vita chenye amani ya kiasi na uhuru wa kiasi ambao ungehusu mpanuko mkubwa wa kazi ya kuhubiri kabla ya mwisho wa mfumo huu. Februari wa 1943 Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower ilianzishwa ili kuzoeza wahudumu wa wakati wote kwa ajili ya kazi ya umisionari katika nchi za kigeni. Baadaye mwaka huo, programu ya mazoezi ya pekee iliongezwa kwenye ratiba ya kila juma ya mikutano ya Mashahidi wa Yehova.
Mwaka wa 1950 Sosaiti ilianza kutoa sehemu za Biblia New World Translation of the Holy Scriptures, tafsiri ya Biblia ya Kiingereza cha kisasa iliyofanywa kutokana na maandishi ya lugha za awali. Biblia hiyo iliyotafsiriwa kwa usahihi, yenye kufahamika kwa urahisi, yenye kuchapishwa kwa bei ya chini katika matbaa za Sosaiti, imekuwa msaada mkubwa katika kazi ya kuhubiri. Leo nakala zaidi ya milioni 40 zimechapishwa katika lugha 11.
Kufikia mwisho wa 1985, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni tatu walikuwa wakishiriki kazi ya kuhubiri katika nchi na visiwa vya bahari zaidi ya 200. Ukumbusho wa kifo cha Kristo, ambao ndio mkutano wenye hudhurio kubwa zaidi ya yo yote iliyofanywa katika makundi yao 49,716 wakati wa mwaka wa 1985, jumla ya watu waliohudhuria ilikuwa 7,792,109.
Kwamba Mungu kweli kweli anatumia Mashahidi wa Yehova inaonyeshwa na kuendelea kwao kuwa watendaji katika utumishi wake, katika umoja wao wa ulimwenguni pote, katika bidii yao ya kuunga mkono jina la Yehova na kuhubiri Ufalme wake, katika viwango vyao safi vya kiadili, katika kukubali kwao Biblia nzima kuwa Neno la Mungu lisilo na makosa, na katika uhuru wao wa kutofuata ushirikina na kuwasiliana na ulimwengu wa roho.
Visehemu vifuatavyo vinaonyesha jinsi wewe unavyoweza kufaidika na kurudishwa huko kwa ibada ya kweli ya Mungu.
• Ni mafundisho gani ya msingi ya Biblia yaliyotofautisha Wanafunzi wa Biblia na madhehebu za makanisa?
• Ni maendeleo gani ya kitengenezo ambayo Wanafunzi wa Biblia waliona kufikia mwaka wa 1918?
• Inaweza kusemwaje kwamba Wanafunzi wa Biblia hao wapakwa mafuta wakawa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” wa Mathayo 24:45-47?
• Ni ufahamu gani wa kusudi la Mungu uliotoa kichocheo kikubwa cha kupanua kazi ya kuhubiri?
• Jina Mashahidi wa Yehova linatimiza kusudi gani?
• Ni mambo gani yanayotoa ushahidi kwamba Mungu kweli kweli anatumia Mashahidi wa Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 8]
C. T. Russell mwaka wa 1879
Toleo la Julai 1879
Kikundi cha kwanza cha Wanafunzi wa Biblia, Pittsburgh, Pa.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Makao Makuu, 1889-1909, Pittsburgh, Pa.
Afisi zilizo kuu, 1909-1918, Brooklyn, N.Y.
Sehemu ya kukaa ya Makao Makuu, 1909-1926, Brooklyn, N.Y.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Makao Makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova, Brooklyn, New York, U.S.A.
Juu kushoto: Majengo yenye afisi
Juu kulia: Majengo ya kukaliwa
Chini kushoto: Majengo ya kiwanda
Chini kulia: Kituo cha usafirishaji
[Picha katika ukurasa wa 11]
Matangazo ya redio yakifanywa na J. F. Rutherford
Matbaa-rotari ya kwanza ya Watchtower Society, ikiendeshwa na wafanya kazi wa kujitolea
Biblia New World Translation, sasa imechapishwa katika lugha 11