Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 7/1 kur. 18-23
  • Kutembea kwa Hekima Kuhusiana na Ulimwengu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutembea kwa Hekima Kuhusiana na Ulimwengu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kushinda Chuki Isiyo na Msingi
  • Wenye Bidii, Si Wenye Uchokozi
  • Wenye Staha na “Tayari kwa Kila Kazi Njema”
  • ‘Kama Yamkini, Mkae Katika Amani na Watu Wote’
  • ‘Kuwatendea Watu Wote Mema’
  • Kuwanyamazisha Wapinzani
  • “Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • “Dumisheni Mwenendo Wenu Ukiwa Bora Miongoni mwa Mataifa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Onyesha kwa Matendo Kwamba Wewe Ni Shahidi wa “Habari Njema”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Wakristo na Ulimwengu wa Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 7/1 kur. 18-23

Kutembea kwa Hekima Kuhusiana na Ulimwengu

“Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje.”—WAKOLOSAI 4:5.

1. Wakristo wa mapema walikabiliwa na nini, na Paulo alitolea kundi katika Kolosai shauri jipi?

WAKRISTO wa mapema walioishi katika majiji ya ulimwengu wa Roma walikabiliwa daima na ibada ya sanamu, utafutiaji anasa usio wa kiadili, na mazoea na desturi za kipagani. Wale walioishi katika Kolosai, jiji katika magharibi-kati mwa Esia Ndogo, bila shaka walikabili ibada ya mama-mungu-mke na uwasiliani-roho wa wenyeji Wafirigia, falsafa ya kipagani ya masetla Wagiriki, na Dini ya Kiyahudi ya ile koloni ya Kiyahudi. Mtume Paulo alishauri kundi la Kikristo ‘lienende kwa hekima’ kuelekea “walio nje” kama hao.—Wakolosai 4:5.

2. Kwa nini Mashahidi wa Yehova leo wanahitaji kuenenda kwa hekima kuelekea wale walio nje?

2 Leo, Mashahidi wa Yehova wanakabili mazoea ayo hayo yasiyofaa, na hata zaidi. Kwa hiyo, wao pia wanahitaji kuonyesha hekima katika uhusiano wao na wale walio nje ya kundi la Kikristo la kweli. Watu wengi katika mashirika ya kidini na ya kisiasa na pia kati ya wasambaza habari huwapinga. Baadhi yao, ama huwashambulia moja kwa moja ama, mara nyingi zaidi, wao hujaribu kwa masingizio, kuiharibu sifa ya Mashahidi wa Yehova na kuchochea chuki isiyo na msingi dhidi yao. Kama vile Wakristo wa mapema walivyoonwa isivyo haki kuwa “farakano,” shupavu na hata lenye hatari, mara nyingi leo Mashahidi wa Yehova ndiyo shabaha ya chuki isiyo na msingi na kufahamiwa kimakosa.—Matendo 24:14, NW; 1 Petro 4:4.

Kushinda Chuki Isiyo na Msingi

3, 4. (a) Kwa nini Wakristo wa kweli hawatapendwa kamwe na ulimwengu, lakini tunapaswa kujaribu kufanya nini? (b) Mtungaji-vitabu mmoja aliandika nini juu ya Mashahidi wa Yehova waliofungwa katika kambi moja ya mateso ya Nazi?

3 Wakristo wa kweli hawatazamii kupendwa na ulimwengu, ambao, kulingana na mtume Yohana, “uko katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Hata hivyo, Biblia huwatia moyo Wakristo wajitahidi kuwavuta watu kwenye upande wa Yehova na ibada yake safi. Tunafanya hivyo kwa kutoa ushahidi moja kwa moja na pia kwa mwenendo wetu mzuri. Mtume Petro aliandika hivi: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”—1 Petro 2:12.

4 Katika kitabu chake Forgive—But Do Not Forget, mtungaji-vitabu Sylvia Salvesen alisema juu ya wanawake Mashahidi waliokuwa wafungwa pamoja na yeye katika kambi moja ya mateso ya Nazi: “Wale wawili, Käthe na Margarethe, na wengine wengi, walinisaidia sana, si kwa imani yao tu bali katika mambo halisi. Walitupatia vitambaa safi vya kwanza tulivyokuwa navyo kwa ajili ya vidonda vyetu. . . . Kwa ufupi tulijipata wenyewe miongoni mwa watu waliotutakia mema, na walioonyesha hisia zao zenye urafiki kwa matendo yao.” Huo ni ushuhuda mzuri kama nini kutoka kwa “walio nje”!

5, 6. (a) Kristo anatimiza kazi gani wakati wa sasa, na hatupaswi kusahau nini? (b) Mtazamo wetu kuelekea watu wa ulimwengu unapaswa uwe nini, na kwa nini?

5 Tunaweza kufanya mengi kukomesha chuki isiyo na msingi kwa ile njia yenye hekima tunayojiendesha kwayo kuelekea walio nje. Ni kweli, tunaishi wakati Mfalme wetu anayetawala, Kristo Yesu, anawatenganisha watu wa mataifa, “kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi.” (Mathayo 25:32) Lakini usisahau kamwe kwamba Kristo ndiye Hakimu; yeye ndiye anayeamua “kondoo” ni nani na “mbuzi” ni nani.—Yohana 5:22.

6 Hilo lapaswa kuathiri mtazamo wetu kuelekea wale ambao si sehemu ya tengenezo la Yehova. Huenda tukawaona kuwa watu walimwengu, lakini wao ni sehemu ya ulimwengu wa ainabinadamu ambao “Mungu aliupenda . . . hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Ni afadhali zaidi kuwaona watu kuwa kondoo wa wakati ujao kuliko kuamua kimbelembele kwamba wao ni mbuzi. Baadhi ya wale walioipinga kweli vikali sana wakati mmoja sasa ni Mashahidi waliojiweka wakfu. Na wengi wao walivutwa kwanza kwa matendo ya fadhili, kabla ya wao kuitikia utoaji ushahidi wowote wa moja kwa moja. Kwa kielelezo, ona picha kwenye ukurasa 18.

Wenye Bidii, Si Wenye Uchokozi

7. Papa alitoa uchambuzi gani, lakini twaweza kuuliza swali gani?

7 Papa John Paul 2 alichambua mafarakano kwa ujumla, na hasa Mashahidi wa Yehova, aliposema hivi: “Ile bidii iliyo kama ya uchokozi ambayo kwayo wengine hutafuta-tafuta wafuasi wapya, wakienda nyumba kwa nyumba, au kuwasimamisha wapita njia kwenye kona za barabara, ni mwigo wa kifarakano wa ile bidii ya kimitume na ya kimishonari.” Yaweza kuulizwa hivi, Ikiwa bidii yetu ni ‘mwigo wa bidii ya kimitume na ya kimishonari,’ bidii ya kweli ya kueneza evanjeli yaweza kupatikana wapi? Kwa hakika si miongoni mwa Wakatoliki wala, miongoni mwa Waprotestanti au washiriki wa makanisa ya Orthodox.

8. Tunapaswa kufanyaje utoaji ushahidi wetu wa nyumba kwa nyumba, kwa kutumaini tokeo gani?

8 Hata hivyo, ili kukanusha shtaka lolote la uchokozi katika utoaji wetu ushahidi, tunapaswa sikuzote kuwa wenye fadhili, wenye staha, na wenye adabu tunapowakaribia watu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “N’nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima.” (Yakobo 3:13) Mtume Paulo atuhimiza ‘tusiwe wagomvi.’ (Tito 3:2) Kwa kielelezo, badala ya kulaumu waziwazi imani za mtu tunayemtolea ushahidi, kwa nini tusionyeshe kupendezwa kwa moyo mweupe na maoni yake? Kisha umwambie mtu huyo habari njema kama zilivyomo katika Biblia. Kwa kuchagua mfikio ufaao na kuonyesha staha inayostahili kwa watu wenye imani nyinginezo, tutawasaidia wawe na mtazamo mzuri zaidi wa akilini ili kusikiliza, na labda watatambua thamani ya ujumbe wa Biblia. Tokeo laweza kuwa kwamba wengine watakuja ‘kumtukuza Mungu.’—1 Petro 2:12.

9. Tunaweza kutumiaje shauri ambalo Paulo alitoa (a) kwenye Wakolosai 4:5? (b) kwenye Wakolosai 4:6?

9 Mtume Paulo alishauri hivi: “Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa wakati.” (Wakolosai 4:5) Akieleza maneno hayo ya mwisho, J. B. Lightfoot aliandika hivi: “Usiruhusu fursa yoyote ipite, ya kusema na kufanya lile liwezalo kuendeleza kusudi la Mungu.” (Italiki ni zetu.) Naam, ni lazima tuwe tayari na maneno na matendo kwa wakati ufaao. Hekima ya jinsi hiyo inahusisha pia kuchagua wakati wa siku unaofaa wa kuwatembelea watu. Ujumbe wetu ukikataliwa, je, ni kwa sababu watu hawauthamini, au ni kwa sababu tulitembelea wakati ambapo yaelekea haukufaa? Paulo aliandika hivi pia: “Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) Hilo lahitaji kufikiria kimbele na upendo wa kweli kwa jirani. Acheni sikuzote tuutoe ujumbe wa Ufalme kwa neema.

Wenye Staha na “Tayari kwa Kila Kazi Njema”

10. (a) Paulo aliwatolea shauri jipi Wakristo walioishi Krete? (b) Mashahidi wa Yehova wameonyeshaje kielelezo kizuri katika kufuata shauri la Paulo?

10 Hatuwezi kuridhiana juu ya kanuni za Biblia. Kwa upande ule mwingine, hatupaswi kubishana isivyohitajiwa juu ya maswali ambayo hayahusishi uaminifu-maadili wa Kikristo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Uwakumbushe watu [Wakristo katika Krete] kunyenyekea kwa wenye uwezo na mamlaka, na kutii, na kuwa tayari kwa kila kazi njema; wasimtukane mtu ye yote, wasiwe wagomvi, wawe wema, wakionyesha upole wote kwa watu wote.” (Tito 3:1, 2) Msomi wa Biblia E. F. Scott aliandika hivi juu ya fungu hilo la maneno: “Wakristo hawakupaswa kutii mamlaka tu, bali ni lazima wawe tayari kwa kazi yoyote njema. Hilo . . . lamaanisha kwamba, ilipokuwa lazima, Wakristo wanapaswa kuwa miongoni mwa watu wa kwanza katika kuonyesha kujali hali njema ya wengine. Daima kungetukia moto, tauni, msiba wa aina mbalimbali, wakati ambapo raia wote wema wangetamani kuwasaidia majirani wao.” Kotekote ulimwenguni kumekuwa pindi nyingi za msiba na Mashahidi wa Yehova wamekuwa miongoni mwa watu wa kwanza kufanya kazi ya kutoa msaada. Wamewasaidia si ndugu zao tu bali pia na wale walio nje.

11, 12. (a) Wakristo wanapaswa kutendaje kuelekea wenye mamlaka? (b) Kujitiisha kwa wenye mamlaka kunatia ndani nini kwa habari ya kujenga Majumba ya Ufalme?

11 Fungu lilo hilo la maneno kutoka kwa barua ya Paulo kwa Tito linakazia umaana wa kufuata mtazamo wenye staha kuelekea mamlaka. Wakristo wachanga wanaoletwa mbele ya mahakimu kwa sababu ya msimamo wao juu ya kutokuwamo wanapaswa kuwa waangalifu hasa kutembea kwa hekima kuelekea wale walio nje. Wanaweza ama kufanyia maendeleo ama kuharibu sifa ya watu wa Yehova kwa sura yao, mwenendo wao, na njia wanayosema na wenye mamlaka hao. Wanapaswa “wapeni . . . astahiliye heshima, heshima,” na kutoa jibu lao kwa staha nyingi.—Warumi 13:1-7; 1 Petro 2:17; 3:15.

12 “[Wenye] mamlaka” wanatia ndani maofisa wa serikali wa mahali fulani. Sasa kwa kuwa Majumba ya Ufalme mengi zaidi yanajengwa, kushughulika pamoja na wenye mamlaka wa mahali fulani hakuwezi kuepukika. Mara nyingi, wazee wanakabili chuki isiyo na msingi. Lakini imeonwa kwamba mahali ambapo waakilishi wa kundi wanapoanzisha uhusiano mzuri na wenye mamlaka na kushirikiana na tume ya kupanga mji, chuki hiyo isiyo na msingi yaweza kukomeshwa. Mara nyingi ushahidi mzuri unatolewa kwa watu ambao hapo mbele walijua kidogo sana au hawakujua lolote juu ya Mashahidi wa Yehova na ujumbe wao.

‘Kama Yamkini, Mkae Katika Amani na Watu Wote’

13, 14. Paulo aliwatolea shauri jipi Wakristo katika Roma, na tunaweza kulitumiaje katika uhusiano wetu na walio nje?

13 Paulo alitoa shauri lifuatalo kwa Wakristo waliokuwa wakiishi katika Roma ya kipagani: “Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”—Warumi 12:17-21.

14 Katika uhusiano wetu na walio nje, ni lazima sisi tukiwa Wakristo wa kweli tukabili wapinzani. Katika fungu la maneno lililo juu, Paulo aonyesha kwamba kijia cha hekima ni kujitahidi kushinda upinzani kwa matendo ya fadhili. Kama vile makaa ya moto, matendo hayo ya fadhili yanaweza kuyeyusha ule uadui na kumvuta mpinzani kwenye mtazamo wenye fadhili zaidi kuelekea watu wa Yehova, labda hata kuchochea kupendezwa kwake na habari njema. Hilo linapotukia, uovu unashindwa na wema.

15. Ni wakati gani Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu hasa kuenenda kwa hekima kuelekea wale walio nje?

15 Kuenenda kwa hekima kuelekea walio nje ni jambo la maana hasa katika nyumba ambamo mwenzi mmoja wa ndoa bado hajaikubali kweli. Kufuata kanuni za Biblia kunatokeza waume bora, wake bora, akina baba bora, akina mama bora, na watoto walio watiifu zaidi na wanaojifunza kwa bidii zaidi shuleni. Mtu asiyeamini anapaswa kuona jinsi kanuni za Biblia zinavyomwathiri mwamini ifaavyo. Hivyo, wengine wanaweza ‘kuvutwa pasipo lile neno, kwa mwenendo wa’ washiriki wa familia waliojiweka wakfu.—1 Petro 3:1, 2.

‘Kuwatendea Watu Wote Mema’

16, 17. (a) Ni dhabihu zipi zimpendezazo Mungu? (b) Tunapaswa ‘kutendaje mema’ kuelekea ndugu zetu na pia wale walio nje?

16 Wema mkubwa zaidi tuwezao kumtendea jirani wetu ni kumletea ujumbe wa uhai na kumfundisha juu ya upatanisho na Yehova kupitia Yesu Kristo. (Warumi 5:8-11) Kwa hiyo mtume Paulo atuambia hivi: “Kwa njia yake yeye [Kristo], na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.” (Waebrania 13:15) Paulo aongeza hivi: “Msisahau kutenda mema na kushirikiana; maana sadaka kama hizi ndizo zimpendezazo Mungu.” (Waebrania 13:16) Kuongezea utoaji ushahidi wetu wa peupe, hatupaswi kusahau “kutenda mema.” Kufanya hivyo kunafanyiza sehemu ya maana sana ya dhabihu zimpendezazo Mungu.

17 Kwa asili, sisi huwafanyia mema ndugu zetu wa kiroho, ambao huenda wakawa na uhitaji kihisiamoyo, kiroho, kimwili, au kimali. Paulo alionyesha hilo alipoandika hivi: “Kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia 6:10; Yakobo 2:15, 16) Hata hivyo, hatupaswi kusahau maneno haya, “Na tuwatendee watu wote mema.” Tendo la fadhili kwa mtu wa ukoo, jirani, au mfanyakazi mwenzetu, laweza kusaidia sana kukomesha chuki isiyo na msingi dhidi yetu na kufanya moyo wa mtu huyo uitikie kweli.

18. (a) Tunapaswa kuepuka hatari zipi? (b) Tunaweza kutumiaje wema wetu wa Kikristo ukiwa utegemezo kwa kazi yetu ya kutoa ushahidi peupe?

18 Ili kufanya hivyo, hatuhitaji kufanya urafiki wa karibu na wale walio nje. Mashirika kama hayo yaweza kuwa yenye hatari. (1 Wakorintho 15:33) Na hatuna nia ya kuwa marafiki na ulimwengu. (Yakobo 4:4) Lakini wema wetu wa Kikristo waweza kutegemeza kuhubiri kwetu. Katika mabara mengine inazidi kuwa vigumu kusema na watu nyumbani kwao. Majengo mengine yenye nyumba kadhaa yamelindwa kwa vifaa vinavyotuzuia tusiwasiliane na wale wanaokaa humo. Katika nchi zilizositawi simu inatoa njia ya kuhubiri. Katika nchi nyingi kutoa ushahidi barabarani kwaweza kufanywa. Bado, katika nchi zote, kuwa mwenye kupendeza, mwenye adabu, mwenye fadhili, na mwenye kusaidia hufungua fursa za kukomesha chuki isiyo na msingi na kutoa ushahidi mzuri.

Kuwanyamazisha Wapinzani

19. (a) Kwa kuwa hatujaribu kujipendekeza kwa watu, tunaweza kutazamia nini? (b) Tunapaswa kujitahidije kufuata kielelezo cha Danieli na kutumia shauri la Petro?

19 Mashahidi wa Yehova si wenye kujipendekeza kwa watu wala wenye kuwahofu watu. (Mithali 29:25; Waefeso 6:6) Wao wanatambua kikamili kwamba ijapokuwa jitihada zao zote za kuwa walipa kodi wenye kielelezo kizuri na raia wema, wapinzani wataeneza uwongo mwovu na kusema kwa njia ya kuwadharau. (1 Petro 3:16) Wakijua hilo, wao wanajaribu kumwiga Danieli, ambaye maadui wake walisema hivi juu yake: “Hatutapata sababu ya kumshitaki Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake.” (Danieli 6:5) Hatutaridhiana kamwe kanuni za Biblia ili kujipendekeza kwa watu. Kwa upande ule mwingine, hatujaribu kuwa mashahidi-wafia-imani. Tunajaribu kuishi kwa amani na kutii shauri hili la kimitume: “Kwa sababu ndiyo mapenzi ya Mungu, kwamba kwa kutenda mema mzibe vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu.”—1 Petro 2:15.

20. (a) Tumesadikishwa juu ya nini, na Yesu alitupa sisi kitia-moyo gani? (b) Tunaweza kuendeleaje kuenenda kwa hekima kuelekea wale walio nje?

20 Tumesadikishwa kwamba msimamo wetu wa kujitenga na ulimwengu unapatana kikamili na Biblia. Unategemezwa na historia ya Wakristo wa karne ya kwanza. Tunatiwa moyo na maneno haya ya Yesu: “Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Sisi hatuhofu. “Naye ni nani atakayewadhuru, mkiwa wenye juhudi katika mema? Lakini mjapoteswa kwa sababu ya haki mna heri. Msiogope kutisha kwao, wala msifadhaike; bali mtakaseni Kristo Bwana mioyoni mwenu. Mwe tayari sikuzote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu.” (1 Petro 3:13-15) Tunapotenda kwa njia hiyo, tutaendelea kuenenda kwa hekima kuwaelekea wale walio nje.

Kwa Njia ya Kupitia

◻ Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanahitaji kuenenda kwa hekima kuelekea wale walio nje?

◻ Kwa nini Wakristo wa kweli hawawezi kutumaini kamwe kupendwa na ulimwengu, lakini wanapaswa kujaribu kufanya nini?

◻ Mtazamo wetu kuelekea watu wa ulimwengu unapaswa uwe nini, na kwa nini?

◻ Kwa nini ‘tutende mema’ si kuelekea ndugu zetu tu bali pia kuelekea wale walio nje?

◻ Kuenenda kwetu kwa hekima kuelekea wale walio nje kunaweza kutusaidiaje katika kazi yetu ya kutoa ushahidi peupe?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kushoto: Wakristo wa kweli katika Ufaransa wakiwasaidia majirani wao baada ya furiko

[Picha katika ukurasa wa 20]

Matendo ya fadhili ya Kikristo yanaweza kusaidia sana kukomesha chuki isiyo na msingi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wakristo wanapaswa wawe “tayari kwa kila kazi njema”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki