Onyesha kwa Matendo Kwamba Wewe Ni Shahidi wa “Habari Njema”
“Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], na mtumishi niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye.”—Isa. 43:10.
1. (a) Miungu yote iliyotengenezwa na wanadamu imeshindwa kufanya nini ili kuthibitisha uungu wao? (Isa. 43:8, 9) (b) Mungu wa kweli anatofautianaje na miungu hiyo katika jambo hilo?
HAKUNA ye yote kati ya miungu-waume na miungu-wake waliotengenezwa na wanadamu anayeweza kutokeza hata shahidi mmoja wa kuthibitisha uungu wake. Miungu hao hawakutoa unabii wo wote ukatimizwa kwa usahihi kabisa. Lakini zaidi ya miaka 2,700 iliyopita Mungu Yehova Aliye Juu Zaidi aliweza kuonyesha kwamba taifa zima la Israeli lilikuwa mashahidi wake, aliposema hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . mtumishi niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; . . . nimetangaza habari, nimeokoa, nimeonyesha.”—Isa. 43:10-12.
2. (a) Kama inavyoonekana wazi katika Zaburi 78, Waisraeli walijua nini juu ya ukombozi wa Yehova? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Waisraeli walijua Yehova anatimiza “neno” lake la unabii?
2 Katika Maandiko yao yaliyoongozwa na Mungu, Waisraeli walikuwa na kumbukumbu lenye kuaminika lililoonyesha jinsi Mungu alivyotendea taifa zima. Walijua kwamba Mwenye Nguvu Zote alikuwa ameokoa babu zao utumwani katika Misri na kuwakomboa mikononi mwa adui zao nyakati nyingine. Walijua kwamba alikuwa ametimiza ahadi nyingi kwa kuwapa nchi ya Kanaani iwe urithi. (Zaburi 78) Kitabu cha Biblia cha Yoshua kinasema: “Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo [Yehova] | alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.”—Yos. 21:45.
3. (a) Unabii wa Isaya ulionyesha Waisraeli wangepatwa na nini? (b) Utimizo wa unabii huo ungewezeshaje Waisraeli kutoa ushuhuda?
3 Unabii wa Isaya, ambamo Yehova Mungu aliwaita Waisraeli mashahidi wake, ulikuwa ukitaja wakati ambao taifa hilo lingeingia uhamishoni Babeli kwa sababu ya kukosa uaminifu, halafu Aliye Juu Zaidi angelikomboa kwa kumtumia Koreshi. (Isa. 43:14, 15; 44:24–45:2) Hivyo wangekuwa mashahidi wenye kushuhudia kwa macho yao wenyewe ukombozi mwingine. Lakini Waisraeli hao wangetumikiaje kama mashahidi wa Yehova baada ya kurudishwa? Wasingefanya hivyo kwa kuwahubiri watu wa mataifa mengine, kwa sababu hawakuagizwa hivyo. Lakini wangeweza kutoa ushuhuda kwa maisha yao. Wangeweza kuonyesha kwamba walimtegemea Yehova Mungu kabisa kama Mlinzi na Mwokozi wao, na kumtumaini yeye peke yake ili kuwa na hali njema na furaha wakati ujao.
AGIZO JIPYA LA KUWA MASHAHIDI
4, 5. (a) Kutoa ushuhuda kunahusu nini kwa habari ya wale wanaokuwa wanafunzi wa Yesu Kristo? (Mt. 28:19, 20) (b) Wanafunzi wa Yesu Kristo walikuwa mashahidi wa nani, na jambo hilo linaonekanaje wazi katika Matendo 1:8; 2:32, 33; 4:19, 20; 5:29-32?
4 Masihi au Kristo Yesu alipokuja duniani, njia mpya ya kutoa ushuhuda ilianza kutumiwa. Walioanza kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo walilikubali daraka la kueleza watu mambo ambayo Yehova Mungu alikuwa amemtendea Mwanawe. Kwa mfano, siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., kundi la Wayahudi na waongofu lilistaajabu kuona roho ya Mungu ikifanya kazi juu ya wanafunzi karibu 120 wa Yesu Kristo. Mtume Petro aliwaambia hivi: “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake. Basi yeye, akiisha kupandishwa hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya [roho takatifu] amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisikia.” (Matendo 2:32, 33) Angalia kwamba Petro alikuwa akitoa ushuhuda wa jambo ambalo Yehova Mungu alikuwa amefanya Vilevile alikuwa shahidi wa Yesu, akatoa ushuhuda kwamba huyo alikuwa ndiye Masihi au Kristo halisi. Kwa kufanya hivyo, Petro alikuwa akifuata maneno ambayo Mwana wa Mungu aliwaambia wanafunzi kabla ya kupaa mbinguni: “Mtapokea nguvu, [ikiisha kuwajilia] juu yenu [roho takatifu]; nanyi mtakuwa mashahidi wangu.” (Matendo 1:8) Baadaye watu walioamini wakawa mashahidi wa Yesu waliitwa “Wakristo.” Matendo 11:26 inasema kwamba jambo hilo lilifanyika “kwa majaliwa ya Mungu,” kulingana na tafsiri ya New World.
5 Sasa kundi la Kikristo lililokuwa na Wayahudi wa asili na Mataifa lilikuwa likitoa ushuhuda juu ya “Habari Njema ya Kristo.” Sasa hao ndio watu waliokuwa wakitumiwa na Yehova Mungu kama mashahidi wake. (Flp. 1:27, Zaire Swahili Bible) Nao wanafunzi walijitangaza wazi-wazi kuwa mashahidi. Wakati mitume walipoagizwa na baraza kuu ya Kiyahudi, au Sanhedrin, waache kusema habari za jina la Yesu, wao walisema: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti. Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi. Na sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na [roho takatifu ambayo] Mungu amewapa wote wamtiio.” (Matendo 5:29-32) Kabla ya hapo, mitume Petro na Yohana walikuwa wameiambia baraza iyo hiyo ya hukumu hivi: “Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia.”—Matendo 4:19, 20.
6. (a) Habari njema zilifungulia watu nafasi gani iliyokuwa nzuri sana? (b) Kama inavyoonekana katika Matendo 4:12 na 17:29-31, wanafunzi wa Yesu walijua jambo gani ambalo Wayahudi na wasio Wayahudi walihitaji kujua?
6 Mitume na wanafunzi wale wengine wa Yesu Kristo walifahamu kabisa kwamba walikuwa na wajibu wa kuwa mashahidi wa Mungu na wa Mwanawe. Watu wote walistahili kuzisikia “Habari Njema” za kwamba, kwa kukubali kuwa Yesu ndiye Kristo na kwamba dhabihu yake ina uwezo wa kulipia dhambi, wangeweza kupata uzima wa milele. (Yohana 3:16; 17:3) Mtume Petro aliambia Sanhedrin hivi: “Hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.” (Matendo 4:12) Miaka kadha baadaye, mtume Paulo aliwaambia Waathene hivi: “Haitupasi kudhani ya kuwa Uungu ni mfano wa dhahabu au fedha au jiwe, vitu vilivyochongwa kwa ustadi na akili za wanadamu. Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.” (Matendo 17:29-31) Naam, watu wote, Wayahudi na wasio Wayahudi, walihitaji kuzisikia “Habari Njema” kabla kifo hakijawazuia kuwa mashahidi wa Mungu na wa Kristo, milele.
7. (a) Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na nia ya kuvumilia mambo gani kwa sababu ya kuzitangaza “Habari Njema”? Kwa sababu gani? (b) Tunaweza kujiuliza maulizo gani kupatana na mfano wa mtume Yohana?
7 Kwa hiyo “Habari Njema” zingeweza kuletea wanadamu wenzao hali njema milele. Yalikuwa mapenzi ya Mungu pia watu wote watangaziwe habari hizo. (1 Tim. 2:3, 4) Kwa hiyo, Wakristo waliojitoa waliendelea kutoa ushuhuda kwa sababu ya kupenda sana Mungu na wanadamu wenzao, ingawa wangeweza kunyimwa uhuru na hata kuuawa kwa sababu ya kufanya hivyo. Karibu na mwaka 96 W.K. mtume wa mwisho kuwa hai aliandikia Wakristo katika Asia Ndogo akawaambia: “Mimi Yohana, ndugu yenu na mwenye kushiriki pamoja nanyi katika mateso na ufalme na subira ya Yesu Kristo, nalikuwa katika kisiwa kiitwacho Patmo kwa ajili ya Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu.” (Ufu. 1:9) Je! wewe unaeleza watu “Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu” kama Yohana? Je! una nia ya kuteswa kwa sababu ya kufanya hivyo, huku ukisadiki kwamba watu wanahitaji kuzisikia habari njema maana zinaweza kuwaokoa?
KUTOA USHUHUDA KWA MWENENDO MWEMA
8. Je! kutoa ushuhuda ni kuhubiri tu na ni mfano gani tunaoweza kutoa kuonyesha kwamba sivyo?
8 Ili kufikia mioyo ya watu wanyofu, shahidi Mkristo wa Yehova lazima aishi kupatana na mambo anayofundisha. Maneno matupu ni ya bure tu, ikiwa haweki mfano mwema wa maisha ya Kikristo. Fikiri hivi: Je! ungetaka mtu anayejulikana sana kwa sababu ya kusema uongo na kuzoea mambo ya udanganyifu awe shahidi wa kukutetea? Je! mazoea yake ya udanganyifu yasingeleta mashaka juu ya ukweli wa maneno yake, na hata kama angesema mambo ya kweli, je! ushuhuda ambao angetoa kwa ajili yako usingeharibu kesi yako? Je! watu wasingedhani kwamba tabia zako ni sawa na za mtu huyo anayekutetea?
9. Mtu anayemtolea Yehova ushuhuda anatakiwa awe na mwenendo wa namna gani? Kwa sababu gani?
9 Bila shaka tabia za mtu mwenye kutoa ushuhuda zinaweza kufanya ushuhuda wake uaminiwe au usiaminiwe. Basi: lazima watu wote wanaojitambulisha kuwa mashahidi wa Yehova wawe na maisha manyofu. Mtume Paulo alikazia ubora wa jambo hilo akaandika habari zifuatazo akiwaambia Wayahudi walioijua sheria ya Mungu: “Wewe umfundishaye mwingine, je! hujifundishi mwenyewe? Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe? Wewe Usemaye kwamba mtu asizini, wazini mwenyewe? Wewe uchukiaye sanamu, wateka mahekalu?” (Rum. 2:21, 22) Ikiwa katika maisha mtu hafuati mambo ambayo anatangazia wengine, analetea Mungu lawama kubwa. Mtume Paulo aliendelea kusema hivi: “Jina la Mungu latukanwa katika Mataifa kwa ajili yenu.”—Rum. 2:24.
10, 11. (a) Kwa habari ya maisha ya jamaa, wale wanaojitambulisha kuwa mashahidi wa Aliye Juu Zaidi wanatazamiwa wawe namna gani? (b) Maana yake nini ‘kuwa na dhamiri njema,’ nayo inawezaje kusaidia wapinzani kama inavyoonyeshwa katika 1 Petro 3:16?
10 Kwa hiyo, ili Wakristo waonyeshe kwa matendo kwamba wao ni mashahidi wa Yehova, lazima wawe waume bora na mababa bora, wake bora na mama bora, wana bora na binti bora, wakilinganishwa na watu wengine. (Efe. 5:24–6:4) Watu waliooana wanapaswa wawe wakijitahidi kutatua matatizo yanayotokea katika ndoa zao kwa kutumia mashauri ya Biblia badala ya kuuiga ulimwengu hukumu wakijaribu kujiondoa katika hali isiyopendeza kwa kutengana au kutalikiana. (Mt. 19:4-9; 1 Kor. 7:10, 11)Ingawa huenda Wakristo wa kweli wakachukiwa na kusingizwa kwa sababu ya kumwamini Yehova Mungu na Mwanawe, nyakati zote inawapasa wawe wakitii shauri hili lililoongozwa na Mungu: “Mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema katika Kristo.”—1 Pet. 3:16.
11 Basi inawapasa Wakristo wajihadhari na makosa wasije wakawa na dhamiri mbaya, itakayowalaumu. Mwenendo mwema unaweza kufanya wapinzani wajue kwamba wamekuwa na maoni mabaya juu ya watumishi wa Mungu, Huenda wakaaibika kwa vile walivyowatenda mashahidi vibaya. Huenda wapinzani hao wakajua kwamba hawakuwa na msingi wa kusema maneno ya kudharau Wakristo wa kweli, kuwalaumu kwamba wana unafiki na wanachukia wanadamu, na mambo kama hayo.
12. Kulingana na 1 Petro 2:12, ni jambo gani linaloweza kutokea kwa watu wanaojionea wenyewe matendo mema ya Mkristo?
12 Kabla mtume Petro hajasema maneno tuliyosoma, alionyesha kwamba mwenendo mwema wa Mkristo unaweza kusaidia wapinzani wawe watukuza Mungu. Tunasoma hivi: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze. Mungu siku ya kujiliwa.” (1 Pet. 2:12) Kumbe, mwenendo mwema unaweza kusadikisha wapinzani wakali kwamba wanasingizia watu wanaozoea ibada ya kweli, na huenda wakawa watukuza Mungu, huku wao wenyewe wakimtumikia Aliye Juu Zaidi! Kwa hiyo usivunjike moyo uonyeshwapo upinzani na ubaridi unapojitahidi kueleza wengine “Habari Njema.” Ukiwa na mwenendo mwema unapokuwa katika hali isiyopendeza, huenda watu wanyofu wakafahamu kwamba ibada yako si jambo la vivi hivi tu. Huenda ukawapa hamu ya kutaka kujua habari zaidi.
13, 14. (a) Ni ushuhuda gani bora ambao mke aweza kumpa mume asiyeamini? (b) Ikiwa mke Mkristo anatii shauri lililo katika 1 Petro 3:1, 2, yapasa mume wake asiyeamini aweze kuona nini?
13 Kwa mfano, huenda mke Mkristo akaona kwamba hapati matokeo mazuri anapojitahidi kueleza mume wake asiyeamini “Habari Njema.” Lakini, huenda mwenendo mwema ukampa mumewe ushuhuda wenye nguvu kuliko maneno matupu tu. Ndiyo sababu mtume Petro aliwatia moyo wake Wakristo kwa kuwaambia: “Mutii waume wenu wenyewe; kusudi ikiwa wengine hawatii Neno, wavutwe kwa mwenendo wa wake wao pasipo Neno; wakitazama mwenendo wenu safi, na wa woga.”—1 Pet. 3:1, 2, Zaire Swahili Bible.
14 Yapasa mume asiyeamini aweze kuona kwamba mke wake anakubaliana naye katika mambo yasiyochafua ibada yake. Kutokana na mwenendo mwema wa mke, yapasa mume aweze kuona kwamba imani yake inamwongoza sana afanye mema. Nia yake, maneno na matendo yake yasimpe mumewe sababu ya kumlaumu. Mke akionyesha kwa matendo kwamba mwenendo wake unastahili sifa, huenda mumewe akawa mwamini baadaye. Basi, kuvuta mume “pasipo Neno” hakumaanishi kwamba mke hapaswi kamwe kuongea na mumewe mambo ya kiroho. Lakini, inampasa aepuke ubishi wa kuendelea kung’ang’ana tu amsadikishe mumewe habari za ibada ya kweli hata nyakati ambazo hataki kusikia.
15. Vijana wanawezaje kufanya “Habari Njema” zipendeze zaidi waalimu na wanafunzi wenzao?
15 Vivyo hivyo, vijana wanaokwenda shuleni wanaweza kutumia mwenendo mwema wafanye “Habari Njema” ziwapendeze zaidi waalimu na wanafunzi wenzao. Huenda kijana akawa anadhihakiwa kwa sababu ya imani zake. Lakini akivumilia bila kulipa kisasi, huenda waalimu na hata wanafunzi wenzake wakaanza kuchunguza waone hasa jambo ambalo linamwezesha kuvumilia. Hasa ikiwa ni mtu anayetegemeka, mwenye bidii katika kazi za shule na mwenye kufadhili watu na kuwaheshimu, watu wanaomwona wanaweza kupendezwa naye na kuanza kuchunguza imani zake. Basi tena, mwenendo mwema utafanya ushuhuda mzuri sana utolewe.—Linganisha Tito 2:6-8.
16. Kufuata 1 Petro 2:18 na Tito 2:9, 10 kazini kunawezaje kuwapa watu ushuhuda mzuri?
16 Mkristo anayefanya kazi ya kimwili apaswa atumie kanuni zinazotajwa katika onyo la upole ambalo watumwa wanapewa: “Enyi watumishi, watiini bwana zenu kwa hofu nyingi; sio wao walio wema na wenye upole tu, bali nao walio wakali.” (1 Pet. 2:18) “Watumwa na wawatii bwana zao, wakiwapendeza katika mambo yote: wasiwe wenye kujibu, wasiwe waibaji; bali wauonyeshe uaminifu mwema wote, ili wayapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.” (Tito 2:9, 10) Kwa hiyo, inampasa Mkristo afanye kazi yake kwa uchangamfu na unyamavu, hata ikiwa ameagizwa afanye mambo yasiyo na kiasi. Inampasa aheshimu tajiri wake, wala asibishane naye. Yapasa watazamaji waweze kuona kwamba Mkristo ni mfanya kazi mwaminifu na mwenye bidii, kwamba anajali watu. Akiwa hivyo, watu watajiheshimu sana ibada ya kweli wajuapo kwamba yeye ni mfanya kazi mwema kwa sababu ya dini yake.
17. Inatupasa tuwe na maoni gani juu ya maisha tuliyokuwa nayo kabla hatujaijua kweli?
17 Namna gani maisha yako mwenyewe kama shahidi wa Yehova? Maoni yako ni nini juu ya mwenendo uliokuwa nao kabla hujapata maarifa sahihi ya kweli? Labda wewe ni mmoja wa watu wanaotajwa na mtume Petro: “Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali.” (1 Pet. 4:3) Haifai kabisa kufanya mazoea hayo mapotovu. Wakristo wanapaswa wawe walitosheka na mambo hayo walipokuwa wajinga, wala haiwapasi watake kuyarudia tena.
18. Ikiwa kweli tunataka kufanya matendo ya kuonyesha sisi ni mashahidi wa “Habari Njema,” tunaweza kujiulizaje, na inatupasa tujitahidi kufanya nini?
18 Kwa kuwa sasa unaishi ili kufanya “mapenzi ya Mungu,” je! unapenda sana kusaidia wengine wapate furaha uliyo nayo? (1 Pet. 4:2) Je! moyo wako unazithamini sana “Habari Njema” kiasi cha kukufanya utumie na kutafuta nafasi za kuwapa watu ushuhuda juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo? (Luka 6:45; 8:15) Je! mwenendo wako ni mwema kiasi cha kufanya watu waone ubora wa mambo unayowaambia juu ya Neno la Mungu? Njia ya pekee tunavyoweza kuwa mashahidi waaminifu ni kuitangaza kweli na kuifuata katika maisha yetu. Basi na tuuige mfano wa mtume Paulo aliyeandika hivi: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.”—1 Kor. 9:27.