Yehova Ni Nani?
“BWANA [Yehova, New World Translation] ni nani?” Swali hilo liliulizwa miaka 3,500 iliyopita na Farao mwenye kiburi, mfalme wa Misri. Yaonekana ukaidi ulimsukuma aongeze hivi: “Mimi simjui BWANA [Yehova, NW].” Watu wawili waliokuwa wamesimama mbele ya Farao wakati huo walimjua Yehova alikuwa ni nani. Walikuwa wale ndugu wa kimwili Musa na Haruni, wa kabila la Lawi la Israeli. Yehova alikuwa amewatuma wamwombe mtawala wa Misri awaache Waisraeli waende jangwani ili waadhimishe sikukuu ya kidini.—Kutoka 5:1, 2.
Farao hakutaka swali lake lijibiwe. Chini ya mamlaka yake, makuhani waliendeleza ibada ya mamia ya viabudiwa bandia. Kwani, Farao mwenyewe alionwa kuwa mungu! Kulingana na ngano ya Kimisri, yeye alikuwa mwana wa kijimungu-jua Ra na alikuwa umbo jingine la kiabudiwa Horasi, chenye kichwa cha ndege-kipanga. Farao aliitwa kwa majina ya vyeo kama vile “mungu mwenye uweza” na “mwenye umilele.” Kwa hiyo haikushangaza kwamba angeuliza hivi kwa madharau: “BWANA [Yehova, NW] ni nani, hata niisikilize sauti yake?”
Musa na Haruni hawakuhitaji kujibu swali hilo. Farao alijua kwamba Yehova alikuwa ndiye Mungu aliyeabudiwa na Waisraeli, waliokuwa wakiteseka wakati huo katika utumwa wa Kimisri. Lakini Farao na Misri yote wangejifunza karibuni kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli. Vivyo hivyo leo, Yehova atajulisha jina lake na Uungu wake kwa kila mtu duniani. (Ezekieli 36:23) Kwa hiyo tunaweza kupata mafaa kwa kuchunguza jinsi ambavyo Yehova Mungu alivyolikweza jina lake katika Misri ya kale.
Mkuu Kuliko Vijimungu vya Misri
Farao alipouliza kwa ukaidi Yehova alikuwa ni nani, hakutazamia matokeo aliyopatwa nayo. Yehova mwenyewe aliitikia, akileta mapigo kumi juu ya Misri. Mapigo hayo hayakuwa mapigo dhidi ya taifa hilo tu. Yalikuwa mapigo dhidi ya vijimungu vya Misri.
Mapigo hayo yalionyesha ukuu wa Yehova juu ya viabudiwa vya Kimisri. (Kutoka 12:12; Hesabu 33:4) Ebu wazia ghasia iliyokuwako wakati Yehova alipobadili Mto Naili na maji yote ya Misri kuwa damu! Kwa sababu ya muujiza huo, Farao na watu wake walijifunza kwamba Yehova alikuwa mkuu zaidi ya kijimungu wa Naili, Hapi. Kifo cha samaki katika Naili lilikuwa pigo pia kwa dini ya Kimisri, kwani aina fulani za samaki ziliheshimiwa mno.—Kutoka 7:19-21.
Baadaye, Yehova alileta pigo la vyura juu ya Misri. Hilo lililetea sifa mbaya kijimungu-kike-chura cha Kimisri, Hekta. (Kutoka 8:5-14) Pigo la tatu liliwatatanisha makuhani wenye kuzoea mizungu, ambao hawakuweza kuiga muujiza wa Yehova wa kugeuza mavumbi kuwa nzi-waumaji. “Ni chanda cha Mungu!” wakapaaza sauti. (Kutoka 8:16-19) Mungu wa Kimisri Thothi, aliyeonwa kuwa uvumbuzi wa mambo ya uchawi, hakuweza kuwasaidia walaghai hao.
Farao alikuwa akijifunza Yehova alikuwa ni nani. Yehova alikuwa ndiye Mungu ambaye angeweza kutangaza kusudi lake kupitia Musa na kisha kulitimiza kwa kuleta mapigo ya kimuujiza juu ya Wamisri. Yehova angeweza pia kuanzisha na kukomesha mapigo hayo kulingana na mapenzi yake. Hata hivyo, kujua jambo hilo hakukumsukuma Farao ajitiishe kwa Yehova. Badala ya hivyo, mtawala huyo wa Misri mwenye kiburi aliendelea kumkinza Yehova kwa ushupavu.
Katika pigo la nne, mainzi waliiharibu nchi, wakavamia nyumba, na labda kusongamana katika hewa, ambayo yenyewe ilikuwa kitu cha kuabudiwa ikifananishwa na kijimungu Shu au na kijimungu-kike Isisi, malkia wa mbinguni. Neno la Kiebrania kwa mdudu huyo limefasiriwa kuwa “pange,” “nzi wa umbwa,” na “mendemlia.” (New World Translation; Septuagint; Young) Ikiwa mendemlia aitwaye skarabu ndiye alihusika, basi Wamisri walivamiwa na wadudu walioonwa kuwa watakatifu, na watu wasingaliweza kutembea bila kuwaponda-ponda kwa miguu. Hata hivyo, pigo hilo lilimfundisha Farao jambo jipya juu ya Yehova. Ingawa viabudiwa vya Misri havikuweza kuwalinda waabudu wavyo dhidi ya mainzi hao, Yehova angeweza kuwalinda watu wake. Pigo hilo na yote yaliyolifuata yaliwaathiri Wamisri lakini si Waisraeli.—Kutoka 8:20-24.
Pigo la tano lilikuwa tauni juu ya mifugo ya Misri. Pigo hilo liliwafedhehesha Hathori, Apisi, na Nuti kijimungu-kike wa anga mwenye mwili wa ng’ombe. (Kutoka 9:1-7) Pigo la sita lilileta majipu juu ya mwanadamu na mnyama, likiwafedhehesha Thothi, Isisi, na Ptaha, waliohesabiwa kimakosa na uwezo mbalimbali wa kuponya.—Kutoka 9:8-11.
Pigo la saba lilikuwa mvua ya mawe nzito sana, pamoja na moto ukitetemeka miongoni mwa mvua ya mawe. Pigo hilo lilimwaibisha yule kijimungu Reshpu, aliyedhaniwa kuwa bwana-mkubwa wa umeme, na Thothi, aliyesemwa kuwa ndiye aliyeongoza mvua na radi. (Kutoka 9:22-26) Pigo la nane, pigo la nzige, lilionyesha ukuu wa Yehova juu ya kijimungu cha uzazi Mini, aliyedhaniwa kuwa mlinzi wa mimea. (Kutoka 10:12-15) Pigo la tisa, giza la siku tatu juu ya Misri, lilileta madharau juu ya viabudiwa vya Kimisri kama vile vijimungu-jua Ra na Horasi.—Kutoka 10:21-23.
Ijapokuwa mapigo tisa yenye kuleta msiba, bado Farao alikataa kuwaachilia Waisraeli. Ugumu wa moyo wake uligharimu Misri sana wakati Mungu alipoleta pigo la kumi likiwa la mwisho—kifo cha mzaliwa wa kwanza wa mwanadamu na wa mnyama. Hata mzaliwa wa kwanza wa Farao alikufa, ingawa alionwa kuwa mungu. Hivyo Yehova ‘akafanya hukumu juu ya vijimungu vyote vya Misri.’—Kutoka 12:12, 29.
Sasa Farao aliwaita Musa na Haruni akasema hivi: “Ondokeni, tokeni katika watu wangu, ninyi na wana wa Israeli; enendeni, kamtumikieni BWANA [Yehova, NW] kama mlivyosema. Twaeni kondoo zenu na ng’ombe zenu kama mlivyosema, enendeni zenu, mkanibariki mimi pia.”—Kutoka 12:31, 32.
Mhifadhi wa Watu Wake
Waisraeli waliondoka, lakini upesi ikaonekana kwa Farao kwamba walikuwa wakitangatanga bila sababu jangwani. Yeye na watumishi wake sasa wakauliza hivi: “Ni nini jambo hili tulilotenda, kwa kuwaacha Waisraeli waende zao wasitutumikie tena?” (Kutoka 14:3-5) Kupoteza taifa hilo la watumwa kungekuwa pigo zito la kiuchumi kwa Misri.
Farao alikusanya jeshi lake akafuatia Israeli hadi Pi-hahirothi. (Kutoka 14:6-9) Kijeshi, hali ilionekana nzuri kwa Wamisri kwa sababu Waisraeli walikuwa wamenaswa kati ya bahari na milima. Lakini Yehova alitenda kwa kuwalinda Waisraeli kwa kuweka wingu kati yao na Wamisri. Kwenye upande wa Wamisri, “palikuwa na lile wingu na lile giza,” hivyo likizuia shambulio. Kwenye upande ule mwingine, wingu lilikuwa jangavu, ‘likitoa nuru wakati wa usiku’ kwa ajili ya Israeli.—Kutoka 14:10-20.
Wamisri waliazimia kuteka nyara na kuharibu lakini walizuiwa na hilo wingu. (Kutoka 15:9) Lilipoinuka, waliona jambo la ajabu kama nini! Maji ya Bahari Nyekundu yalikuwa yamegawanywa, na Waisraeli walikuwa wakivuka hadi upande ule mwingine kwenye bara kavu! Farao na majeshi yake waliingia bonde la bahari kwa kishindo, wakiazimia kuwakamata na kuwateka wale waliokuwa watumwa wao. Hata hivyo, mtawala wa Misri mwenye kiburi hakuwa amemtazamia Mungu wa Waebrania kuwa na uwezo. Yehova alianza kuwatatanisha Wamisri, akiondoa magurudumu ya magari yao ya vita.—Kutoka 14:21-25a.
“Na tukimbie mbele ya Israeli!” wakapaaza sauti mashujaa wa Misri, “kwa kuwa BWANA [Yehova, NW] anawapigania, kinyume cha Wamisri.” Utambuzi huo ulikuja kwa kuchelewa mno kwa Farao na watu wake. Wakiwa salama kwenye pwani ile nyingine, Musa alinyoosha mkono wake kuelekea bahari, na maji yakarudi, yakiwaua Farao na majeshi yake.—Kutoka 14:25b-28.
Masomo Yaliyopatikana Kupitia Maono
Kwa hiyo, basi, Yehova ni nani? Farao mwenye kiburi alipata jibu kwa swali hilo. Matukio katika Misri yalionyesha kwamba Yehova ndiye Mungu pekee wa kweli, aliye tofauti kabisa na ‘miungu ya mataifa ambayo si kitu.’ (Zaburi 96:4, 5) Kwa uwezo wake wenye kuhofisha, Yehova ‘aliziumba mbingu na nchi.’ Yeye pia ndiye Mkombozi Mkuu, Yule ‘aliyewatoa watu wake, Israeli, katika nchi ya Misri, kwa ishara, na kwa ajabu, na kwa mkono hodari, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa utisho mkuu.’ (Yeremia 32:17-21) Hilo lilithibitisha vizuri kama nini kwamba Yehova anaweza kuwalinda watu wake!
Farao alijifunza masomo hayo kupitia maono machungu. Kwa kweli, somo la mwisho lilimgharimu uhai wake. (Zaburi 136:1, 15) Yeye angalikuwa mwenye hekima zaidi ikiwa angalionyesha unyenyekevu alipouliza, “BWANA [Yehova, NW] ni nani?” Kisha mtawala huyo angaliweza kutenda kulingana na jibu alilopokea. Kwa furaha, watu wengi wanyenyekevu leo wanajifunza Yehova ni nani. Na Yeye ana utu wa aina gani? Yeye ataka nini kwetu? Makala ifuatayo na iongeze uthamini wako kwa ajili ya Yule pekee ambaye jina lake ni Yehova.—Zaburi 83:18.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.