“Yaonekana Hatuwezi Kuwasiliana Hata Kidogo!”
MICHAEL, aliye wakili, alipaswa kuwa mwasilianaji mwenye nguvu. Kazi yake ilitaka hivyo. Lakini baada ya miaka 16 ya ndoa, Michael alilazimika kutambua kwamba alipokuja nyumbani kwa mke wake, Adrian, ilionekana kana kwamba stadi zake za kuwasiliana zilitoweka. “Kulalamika, kuchambua-chambua, kusingizia mambo,” Michael akumbuka, “sikuzote Adrian na mimi tulikuwa tunabishana, na nikafikiri hilo lingetumaliza kabisa. Nilijiuliza kama hiyo ilikuwa ndiyo ndoa, shambulio la daima la kutoridhika na uchokozi. Kama hilo lingekuwa ndilo fungu letu kwa maisha yetu yote pamoja, nilitaka kutoroka ndoa hiyo—bila mchezo. Nisingeweza hata kidogo kukabili miaka 20, 30, 40 ya aina hiyo ya uchokozi na mkazo wa daima.”
Maoni ya moyoni kama hayo kwa kweli si ya Michael na Adrian peke yao. Ni ya halisi kwa wenzi wengi ambao uhusiano wao hubadilika-badilika kati ya hali ya kupigana na muda mfupi wa kutopigana. Mazungumzo sahili zaidi hulipuka kuwa vita vya maneno. Wao “wanasikia” mambo yasiyosemwa. Wanasema mambo yasiyomaanishwa. Wanashambulia na kushtaki, na kisha kuingia katika hali ya unyamavu wenye kinyongo. Hawatengani, na bado wao si “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Uhusiano umesimama. Kurudi nyuma kungemaanisha kutengana; kuendelea mbele kungemaanisha kukabili hitilafu moja kwa moja. Ili kuepuka maumivu ya kuchagua lolote kati ya mambo hayo mawili, wenzi hao huamua kutokaribiana kihisiamoyo.
Wenzi hao wanahitaji ‘kupata mwelekezo wenye ustadi’ katika ndoa yao. (Mithali 1:5, New World Translation) Mwelekezo huo unapatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Barua ya pili ya Paulo kwa Timotheo inathibitisha kwamba Biblia “lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza.” (2 Timotheo 3:16) Hivyo ndivyo hali ilivyo katika kusuluhisha mvunjiko wa uwasiliano katika ndoa, kama vile tutakavyoona.