Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 8/1 kur. 4-8
  • Uwasiliano Si Maongezi tu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwasiliano Si Maongezi tu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuonyesha Mwono-Ndani
  • Kuelewa Hali ya Wakati Uliopita
  • Ikiwa Wakati Uliopita Ulikuwa Wenye Kutendwa Vibaya
  • Kunaswa na Kinyongo
  • Uzoevu Huharibu Uwasiliano
  • Kusuluhisha Matatizo
  • Si Kudumu Tu
  • Iweke Ndoa Yako Katika Hali ya Kuheshimika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mambo Yanayoweza Kukusaidia Kuwasiliana na Mwenzi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Baada ya Siku ya Harusi
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Ndoa Yako-Yaweza Kuokolewa
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 8/1 kur. 4-8

Uwasiliano Si Maongezi tu

EBU wazia umati wa watalii ukitazama mandhari yenye kuvutia sana. Ingawa kikundi chote kinatazama mandhari ileile, kila mtu aiona kwa njia tofauti. Kwa nini? Kwa sababu kila mtu mmoja mmoja anaiona kutoka mahali tofauti. Hakuna watu wawili wanaosimama mahali palepale hasa. Zaidi ya hayo, si kila mtu anayekaza macho kwenye sehemu ileile ya mandhari hiyo. Kila mtu aona sehemu tofauti kuwa yenye kuvutia hasa.

Ndivyo ilivyo ndani ya ndoa. Hata wanapopatana sana, hakuna wenzi wawili wanaoshiriki maoni yaleyale hasa juu ya mambo. Mume na mke wanatofautiana katika mambo kama vile muundo wa kihisiamoyo, maono ya utotoni, na uvutano wa familia. Maoni tofauti yanayotokana na hayo yaweza kuwa chanzo cha mashindano makali. Mtume Paulo alisema hivi kwa unyoofu: “Wale wafungao ndoa watakuwa na maumivu na huzuni.”—1 Wakorintho 7:28, The New English Bible.

Uwasiliano unatia ndani juhudi ya kupatanisha tofauti hizo katika uhusiano wa mwili mmoja. Hilo lataka kufanyiza wakati wa kuongea. (Ona sanduku kwenye ukurasa 7.) Lakini mengi zaidi yanahusika.

Kuonyesha Mwono-Ndani

Mithali moja ya Biblia yasema hivi: “Moyo wake mwenye hekima hufundisha kinywa chake [husababisha kinywa chake kionyeshe mwono-ndani, NW]; huzidisha elimu ya midomo yake.” (Mithali 16:23) Hapa neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘husababisha kuonyesha mwono-ndani’ lamaanisha kuwa mwenye busara, kupima mambo kwa uangalifu akilini. Kwa hiyo, kiini cha uwasiliano wenye matokeo ni moyo, wala si kinywa. Ni lazima mwasilianaji mzuri asiwe msemaji tu; ni lazima awe msikilizaji mwenye hisia-mwenzi. (Yakobo 1:19) Ni lazima atambue hisia na masuala yanayosababisha tabia ya juujuu ya mwenzi wake.—Mithali 20:5.

Jinsi gani? Nyakati nyingine hilo linaweza kutimizwa kwa kuzifikiria hali zenye kuzunguka mapigano. Je! mwenzi wako yuko chini ya mkazo mzito wa kihisiamoyo au wa kimwili? Je! ugonjwa fulani unachangia mtazamo wa mwenzi wako? “Ni shangwe kama nini kupata neno lifaalo hasa kwa pindi ifaayo hasa!” Biblia husema. (Mithali 15:23, Today’s English Version) Kwa hiyo kuzifikiria hali kutakusaidia uitikie kulingana nazo.—Mithali 25:11.

Lakini, mara nyingi kisababishi cha mapigano hutokana na mambo yaliyo nje ya hali zilizopo.

Kuelewa Hali ya Wakati Uliopita

Maono katika utoto huchangia sana namna tunavyofikiri tukiwa watu wazima. Kwa kuwa wenzi wa ndoa wanatoka katika familia tofauti, maoni yenye kupingana hayaepukiki.

Tukio moja lililorekodiwa katika Biblia linaonyesha hilo. Sanduku la agano liliporudishwa Yerusalemu, Daudi alionyesha idili yake peupe. Lakini namna gani mke wake Mikali? Biblia husimulia hivi: “Mikali, binti Sauli, akachungulia dirishani, akamwona mfalme Daudi akiruka-ruka na kucheza mbele za BWANA [Yehova, NW]; akamdharau moyoni mwake.”—2 Samweli 6:14-16.

Mikali alionyesha mtazamo usio na imani wa baba yake Sauli asiyekuwa mwadilifu. Wafafanuzi wa Biblia C. F. Keil na F. Delitzsch wanadokeza kwamba hiyo ndiyo sababu Mikali anaitwa “binti Sauli” katika mstari wa 16 badala ya mke wa Daudi. Kwa vyovyote vile, bishano lililofuata kati yao laonyesha wazi kwamba Daudi na Mikali hawakushiriki maoni yaleyale kuhusu tukio hilo lenye shangwe.—2 Samweli 6:20-23.

Kielelezo hicho kinaonyesha kwamba uvutano mbalimbali wenye hila kutokana na malezi unaweza kumsababisha mume na mke waone mambo kwa njia tofauti sana. Hilo ni kweli hata ikiwa wote wawili wanamtumikia Yehova kwa umoja. Kwa kielelezo, mke ambaye hakupewa utegemezo wa kihisiamoyo wa kutosha alipokuwa mtoto huenda akaonyesha uhitaji usio wa kawaida wa kupata kibali na uhakikishio. Hilo laweza kumtatanisha mume wake. “Ningeweza kumwambia mara mia moja kwamba nampenda,” huenda akasema kwa nguvu “na bado hilo lisingetosha!”

Katika hali hiyo, uwasiliano watia ndani ‘kutoangalia mambo yako mwenyewe, bali kuangalia mambo ya wengine.’ (Wafilipi 2:4) Ili kuwasiliana, ni lazima mume amwone mke wake kulingana na maono ya mke wake ya wakati uliopita kuliko kulingana na maono yake mwenyewe. Na bila shaka, mke anapaswa asukumwe kumfanyia mume wake vivyo hivyo.—1 Wakorintho 10:24.

Ikiwa Wakati Uliopita Ulikuwa Wenye Kutendwa Vibaya

Kupendezwa kibinafsi ni kwa muhimu hasa wakati ambapo mwenzi amenajisiwa au kutendwa vibaya kingono akiwa mtoto—kwa kusikitisha, hilo ni tatizo linaloongezeka leo. Kwa kielelezo, huenda mke akaona kwamba nyakati za kufanya ngono, yeye hawezi kutenganisha hali ya sasa na ile ya wakati uliopita, kutenganisha mwenzi wake na yule aliyemtenda vibaya, au kutenganisha mahusiano ya kingono na kutendwa vibaya kingono. Hilo laweza kufadhaisha, hasa ikiwa mume halioni jambo hilo gumu kutokana na maono ya mke wake.—1 Petro 3:8.

Ingawa huwezi kutangua yale yaliyotukia wakati uliopita wala kuponya kabisa matokeo yayo, unaweza kusaidia sana kumfariji mwenzi mwenye huzuni. (Mithali 20:5) Jinsi gani? “Enyi waume mnapaswa kujaribu kuwaelewa wake mnaoishi nao,” akaandika Petro. (1 Petro 3:7, Phillips) Kuelewa hali ya mwenzi wako ya wakati uliopita ni sehemu muhimu ya uwasiliano. Bila huruma ya kihisia-mwenzi, maneno yako hayatafaa kitu.

Yesu ‘alikuwa na huruma’ alipowakabili wale waliokuwa wakiugua, hata ingawa yeye binafsi hakuwa amepatwa kamwe na maradhi yao. (Mathayo 14:14) Vivyo hivyo, huenda ikawa wewe binafsi hukupuuzwa au kutendwa vibaya kama vile mke wako, lakini badala ya kuona uchungu wake kuwa jambo dogo, kubali hali yake ya wakati uliopita na kumpa utegemezo wako. (Mithali 18:13) Paulo aliandika hivi: “Basi imetupasa sisi tulio na nguvu kuuchukua udhaifu wao wasio na nguvu, wala haitupasi kujipendeza wenyewe.”—Warumi 15:1.

Kunaswa na Kinyongo

Ndoa ni kama chombo bora sana. Inapoharibiwa na uzinzi, madhara yasiyopimika hutokea. (Mithali 6:32) Ni kweli, ikiwa mwenzi asiye na hatia aamua kusamehe, ndoa yaweza kuponywa kupitia mapatano. Lakini nyufa zinabaki, na wakati wa mabishano, huenda kukawa na mwelekeo wa kuzitazama nyufa hizo na kutumia kama silaha hali ya wakati uliopita.

Kinyongo, ni itikio la kawaida kwa ukosefu wa uaminifu wa mwenzi. Lakini ikiwa umemsamehe mwenzi wako, jilinde usiruhusu hasira yenye kubaki-baki iondoe yale mambo mazuri ambayo umetimiza kupitia tendo la msamaha. Iwe kinyongo kinachemka ndani kimyakimya au kinatokezwa bila rehema, kinyongo chenye kuendelea kinawaumiza wenzi wote wawili. Kwa nini? Daktari mmoja adokeza hivi: “Ikiwa unahisi umeumizwa na mwenzi wako, ni kwa sababu ungali unamjali. Kwa hiyo kwa kunyamaza au kwa kujaribu kulipiza kisasi, humwumizi tu mwenzi wako bali unajiumiza mwenyewe pia. Unazidi kuvunja ule uhusiano ambao watamani uwe kamili.”

Naam, huwezi hata kidogo kusuluhisha hitilafu katika ndoa yako bila kuipunguza hasira yako. Kwa hiyo, wakati hisiamoyo zimepoa, zungumza juu ya hisia zako pamoja na mwenzi wako. Eleza kwa nini unahisi uchungu, lile unalohitaji ili kuhisi uhakikishio, na lile utakalofanya ili kuuhifadhi uhusiano huo. Usitumie kamwe hali ya wakati uliopita kama silaha ya kujipatia msimamo wenye nguvu zaidi katika mabishano.

Uzoevu Huharibu Uwasiliano

Ndoa hupatwa na uchungu mwingi wakati mwenzi mmoja anapotumia vibaya vileo au dawa za kulevya. Mwenzi ambaye si mzoevu aweza kuwa katika hali ileile ya Abigaili, kama ilivyoripotiwa katika Biblia. Mume wake Nabali ‘alipokuwa amelewa kabisa’ Abigaili alikuwa akijaribu sana kuyapindua matokeo ya mwenendo wa Nabali usio wenye hekima. (1 Samweli 25:18-31, 36) Ndoa ambamo mwenzi mmoja ana taabu ya uzoevu fulani na yule mwingine anashughulika akijaribu kubadili mwenendo wa mwenzi aliye mzoevu mara nyingi hufanana na nyumba ya Nabali na Abigaili.a

Kwa kueleweka, mtu huhisi kutulizwa sana wakati mzoevu anapoanza kupona. Lakini huo ni mwanzo tu. Ebu wazia tufani mbaya sana inayoharibu mji mdogo. Nyumba zinabomoka, miti inang’olewa, waya za simu zinaanguka chini. Kuna shangwe nyingi wakati dhoruba hiyo inapoisha. Lakini sasa kazi nyingi ya kurekebisha hali inahitajiwa. Ndivyo ilivyo wakati mwenzi anapoanza kupona. Ni lazima mahusiano yaliovunjika yajengwe upya. Ni lazima kutumaini na uaminifu uanzishwe upya. Mawasiliano yanahitaji kuanzishwa tena. Kwa mzoevu anayebadili mwenendo wake, kurekebishwa kupya huko kwa polepole ni sehemu ya “utu mpya” ambao Biblia huwataka Wakristo wasitawishe. Ni lazima huo utu mpya utie ndani “kani itendeshayo akili yako.”—Waefeso 4:22-24, NW.

Funzo la Biblia liliwawezesha Leonard na Elaine waache kutumia vibaya dawa za kulevya, lakini kani itendeshayo akili haikuwa imeanza kutenda kikamili.b Upesi uzoevu mwingine mbalimbali ulitokea. “Kwa miaka 20 tulijaribu kutumia kanuni za Biblia na kuwa na ndoa yenye kuridhisha, lakini tulishindwa sikuzote,” asema Elaine. “Uzoevu wetu mbalimbali ulikuwa umetia mizizi yenye kina kirefu. Hatukuweza kuuondosha kwa kujifunza au kusali.”

Leonard na Elaine walitafuta shauri ili kuelewa visababishi vya uzoevu wao mbalimbali. Habari ya wakati ufaao kutoka kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” juu ya kutendea vibaya watoto, uzoevu wa kileo na kuonyesha wanawake staha imesaidia hasa.c (Mathayo 24:24-27) “Tumesaidiwa kusuluhisha matatizo na kukaribiana tena,” asema Elaine.

Kusuluhisha Matatizo

Rebeka alihisi uchungu mwingi usiovumilika juu ya wake za mwana wake Esau. Akihofu kwamba yule mwana wake mwingine, Yakobo, angefuata kielelezo cha Esau, Rebeka alitoa kufadhaika kwake kwa kumwambia mume wake, Isaka, hivi: “Rohoni mwangu sina raha kwa sababu ya hao binti za Hethi. Kama Yakobo akitwaa mke katika binti za Hethi, kama hawa binti za nchi, maisha yangu yatanifaidia nini?”—Mwanzo 27:46.

Ona kwamba ingawa Rebeka alisema kwa uthabiti juu ya hisia zake, yeye hakumshambulia Isaka binafsi. Yeye hakusema “Ni kosa lako!” au, “Wapaswa kushughulikia jambo hili vema zaidi!” Badala ya hivyo, Rebeka alitumia kiwakilishi-nafsi “mimi” kusimulia jinsi tatizo hilo lilivyomwathiri. Mfikio huo ulivuta hisia-mwenzi ya Isaka, wala si tamaa yake ya kujitetea. Kwa kuwa hakuhisi ameshambuliwa kibinafsi, inaonekana Isaka aliitikia sihi ya Rebeka mara moja.—Mwanzo 28:1, 2.

Waume na wake wanaweza kujifunza kutokana na kielelezo cha Rebeka. Ubishi unapotokea, shambulia tatizo kuliko kushambuliana. Kama vile Rebeka, onyesha kufadhaika kwako kutokana na jinsi tatizo hilo linavyokuathiri. Kusema “Mimi nimefadhaika kwa sababu ya . . .” au, “Mimi nahisi kwamba sijaeleweka kwa sababu ya . . .” kuna matokeo mazuri zaidi kuliko kusema “Wewe unanifadhaisha!” au, “Wewe hunielewi kamwe!”

Si Kudumu Tu

Ndoa ya wenzi wa kwanza wa kibinadamu, Adamu na Hawa, ilidumu kwa karne kadhaa, ikitokeza familia ya wana na binti. (Mwanzo 5:3-5) Lakini hilo halimaanishi kwamba ndoa yao ilistahili kuigwa. Mapema zaidi, roho ya kujitegemea na kupuuza sheria zenye uadilifu za Muumba ziliharibu kifungo chao cha mwili mmoja.

Vivyo hivyo, ndoa yaweza kudumu leo, lakini huenda ikakosa sehemu muhimu za uwasiliano. Njia za kusababu zilizoimarishwa kwa nguvu na vitabia vya kiutu visivyofaa huenda vikahitaji kung’olewa. (Linganisha 2 Wakorintho 10:4, 5.) Hiyo ni taratibu ya kielimu inayoendelea. Lakini jitihada hiyo inastahili. Yehova Mungu anapendezwa sana na mpango wa ndoa, kwa kuwa yeye ndiye Muumba wao. (Malaki 2:14-16; Waebrania 13:4) Kwa hiyo, tukifanya sehemu yetu, twaweza kuwa na uhakika kwamba ataona jitihada zetu na kutuandalia hekima na imara iliyo ya lazima ili kuponya mvunjiko wowote wa uwasiliano katika ndoa.—Linganisha Zaburi 25:4, 5; 119:34.

[Maelezo ya Chini]

a Msaada kwa ajili ya familia ya walevi unazungumziwa katika toleo la Amkeni! (Kiingereza) la Mei 22, 1992, kurasa 3-7.

b Majina yamebadilishwa.

c Ona matoleo ya Amkeni! ya Oktoba 8, 1992, Mei 22, 1992, (katika Kiingereza) na Desemba 8, 1992.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

“Takataka zilipewa wakati mwingi zaidi!”

MUME na mke waliokuwa na matatizo ya ndoa waliombwa wakadiri kiasi cha wakati walichotumia wakiondoa takataka nyumbani kila juma. Jibu lao lilikuwa karibu dakika 35 kwa juma, au dakika 5 kwa siku. Kisha wakaulizwa ni kiasi gani cha wakati walichotumia wakizungumza pamoja. Mume akashtuka. “Takataka zilipewa wakati mwingi zaidi!” akajulisha, akiongeza hivi: “Tunajidanganya wenyewe ikiwa tunafikiri kwamba dakika tano kila siku ni wakati wa kutosha ili kudumisha ndoa. Na kwa hakika si wakati wa kutosha kuifanya ndoa ikue.”

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Weka Sheria za Utaratibu wa Kufuatwa

◻ Zungumza habari moja kwa wakati (1 Wakorintho 14:33, 40)

◻ Onyesha hisia; usitoe mashtaka (Mwanzo 27:46)

◻ Hakuna kupigana (Waefeso 5:28, 29)

◻ Hakuna kuitana majina (Mithali 26:20)

◻ Uwe na lengo la kusuluhisha matatizo, si kushinda (Mwanzo 13:8, 9)

[Picha katika ukurasa wa 4]

Ubishi unapotokea, shambulia tatizo kuliko kushambuliana

[Picha katika ukurasa wa 8]

Onyesha hisia; usitoe mashtaka

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki