Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 8/1 kur. 15-20
  • Usiache Mtu Aharibu Mazoea Yako Yenye Mafaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Usiache Mtu Aharibu Mazoea Yako Yenye Mafaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Shauri Kwao na Kwetu
  • Epuka Kudanganyika
  • Mazoea ya Ujana Pia
  • Hatua Zifaazo Ili Kulinda Mazoea Yetu
  • Kupata Kuwajua Wakristo wa Kwanza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kitabu Cha Biblia Namba 46—1 Wakorintho
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Kitabu Cha Biblia Namba 47—2 Wakorintho
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Jihadhari na Mashirika Mabaya Katika Siku Hizi za Mwisho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 8/1 kur. 15-20

Usiache Mtu Aharibu Mazoea Yako Yenye Mafaa

“Msipotezwe. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” —1 WAKORINTHO 15:33, NW.

1, 2. (a) Mtume Paulo alihisije kuelekea Wakristo Wakorintho, na kwa nini? (b) Tutazungumzia shauri jipi hasa?

UPENDO wa mzazi ni hisia-moyo yenye nguvu kama nini! Unawasukuma wazazi wajidhabihu kwa ajili ya watoto wao, kuwafundisha na kuwashauri. Huenda ikawa mtume Paulo hakuwa baba halisi, lakini aliwaandikia Wakristo katika Korintho hivi: “Ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili.”—1 Wakorintho 4:15.

2 Mapema zaidi, Paulo alikuwa amesafiri kwenda Korintho, ambako alihubiri kwa Wayahudi na Wagiriki. Alisaidia kufanyiza kutaniko la Korintho. Katika barua nyingine Paulo alifananisha utunzaji wake na ule wa mama mlezi, lakini alikuwa kama baba kwa Wakorintho. (1 Wathesalonike 2:7) Kama vile baba halisi mwenye upendo, Paulo aliwaonya kwa upole watoto wake wa kiroho. Unaweza kunufaika kutokana na shauri lake la kibaba kwa Wakristo katika Korintho: “Msipotezwe. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33, NW) Kwa nini Paulo aliwaandikia Wakorintho shauri hilo? Tunaweza kutumiaje shauri hilo?

Shauri Kwao na Kwetu

3, 4. Tunajua nini kuhusu Korintho la karne ya kwanza na wakaaji walo?

3 Katika karne ya kwanza, mwanajiografia Mgiriki Strabo aliandika hivi: “Korintho linaitwa ‘lenye utajiri’ kwa sababu ya biashara yalo, kwa kuwa liko kwenye Isthmasi [shingo-ardhi] na ndilo kuu kati ya bandari mbili, ambazo moja kati yazo huelekea moja kwa moja hadi Esia, na ile nyingine hadi Italia; na hurahisisha shughuli za biashara ya bidhaa kutoka nchi zote mbili.” Baada ya kila miaka miwili Michezo ya Isthmasi iliyokuwa maarufu ilileta halaiki ya watu Korintho.

4 Namna gani watu wa jiji hilo lililokuwa kitovu cha mamlaka ya kiserikali na pia cha ibada ya kuamsha nyege ya Afrodite? Profesa T. S. Evans alieleza hivi: “Labda idadi ya wakaaji [ilikuwa] 400,000 hivi. Jamii [ilikuwa] ya utamaduni wa juu, lakini yenye adili mbaya, hata zenye kuchukiza. . . . Wakaaji Wagiriki wa Achaïa walijulikana kuwa wenye kutoridhika kiakili na kuwa wenye kutafuta-tafuta daima mafundisho mapya. . . . Kujipenda kwao kuliweza kuchochea mafarakano kwa urahisi.”

5. Ndugu Wakorintho walikabili hatari gani?

5 Baada ya wakati fulani hata kutaniko lilianza kugawanywa na wengine ambao bado walikuwa na mbetuko kuelekea makisio yenye kiburi. (1 Wakorintho 1:10-31; 3:2-9) Tatizo kuu lilikuwa kwamba wengine walikuwa wakisema: “Hakuna kiyama ya [ufufuo wa, NW] wafu.” (1 Wakorintho 15:12; 2 Timotheo 2:16-18) Iwe imani yao (au kutokuamini kwao) hasa ilikuwa nini, Paulo alihitaji kuwasahihisha kwa uthibitisho wa wazi kwamba Kristo alikuwa “amefufuka katika wafu.” Hivyo, Wakristo wangeweza kutumaini kwamba Mungu angewapa ‘ushindi kwa Bwana wetu Yesu Kristo.’ (1 Wakorintho 15:20, 51-57) Ikiwa ungalikuwa huko, je, ungalivutwa na roho hiyo ya migawanyiko?

6. Shauri la Paulo kwenye 1 Wakorintho 15:33 liliwahusu nani hasa?

6 Alipokuwa akiandaa uthibitisho imara kwamba wafu watafufuliwa, Paulo aliwaambia hivi: “Msipotezwe. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (NW) Shauri hilo liliwahusu hasa wale walioshirikiana na kutaniko hawakukubaliana na fundisho la ufufuo. Je! walikosa uhakika tu juu ya jambo ambalo hawakuelewa? (Linganisha Luka 24:38.) La. Paulo aliandika kwamba “baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya [ufufuo wa] wafu,” kwa hiyo wale waliohusika walikuwa wanapinga, wakielekea uasi-imani. Paulo alijua vema kwamba wangeweza kuharibu mazoea mazuri na fikira za wengine.—Matendo 20:30; 2 Petro 2:1.

7. Tungeweza kutumia 1 Wakorintho 15:33 katika hali gani moja?

7 Tunaweza kutumiaje onyo la Paulo juu ya mashirika? Yeye hakumaanisha kwamba tunapaswa kukataa kusaidia mtu fulani katika kutaniko anayeiona kuwa vigumu kuelewa mstari au fundisho fulani la Biblia. Kwa kweli, Yuda 22, 23 yatuhimiza kutoa msaada wenye rehema kwa wale wenye mioyo myeupe walio na shaka hizo. (Yakobo 5:19, 20) Hata hivyo, shauri la Paulo la kibaba, lingetumika ikiwa mtu fulani anaendelea kupinga yale tunayojua kuwa kweli ya Biblia au aendelea kutoa maelezo yanayotilika shaka au yasiyofaa. Tunapaswa kujilinda tusishirikiane pamoja na mtu wa aina hiyo. Bila shaka, mtu akiwa mwasi-imani kabisa, wachungaji wa kiroho wangelazimika kuchukua hatua ili kulinda kundi.—2 Timotheo 2:16-18; Tito 3:10, 11.

8. Tunaweza kutendaje kwa utambuzi wakati mtu hakubaliani na fundisho la Biblia?

8 Tunaweza pia kutumia maneno ya Paulo ya kibaba kwenye 1 Wakorintho 15:33 kuhusiana na wale walio nje ya kutaniko wanaoendeleza mafundisho bandia. Tunaweza kuvutwaje tushirikiane pamoja nao? Hilo lingeweza kutukia ikiwa hatutofautishi kati ya wale wanaoweza kusaidiwa kujifunza kweli na wale wanaotokeza ubishi tu ili kuendeleza fundisho bandia. Kwa kielelezo, katika kazi yetu ya kutoa ushahidi, huenda tukakutana na mtu ambaye hakubaliani na jambo fulani lakini aliye na nia ya kulizungumza zaidi. (Matendo 17:32-34) Hilo pekee halipasi litokeze tatizo, kwani tunaieleza kwa furaha kweli ya Biblia kwa yeyote anayetaka kuijua kikweli, hata kurudi ili kumtolea uthibitisho wenye kusadikisha. (1 Petro 3:15) Lakini, huenda wengine wasipendezwe kikweli na kupata kweli ya Biblia.

9. Tunapaswa kuitikiaje imani zetu zinapopingwa?

9 Watu wengi watabishana kwa muda wa saa kadhaa, juma baada ya juma, lakini si kwa sababu wanaitafuta kweli. Wanataka tu kudhoofisha imani ya mtu mwingine huku wakionyesha waziwazi ile ambayo wao wenyewe wanadhania kuwa elimu katika Kiebrania, Kigiriki, au sayansi ya mageuzi. Wanapokutana nao, Mashahidi wengine wamehisi kupingwa na tokeo limekuwa kwamba wameendelea kuwa na ushirika pamoja nao unaokazia imani bandia ya kidini, falsafa, au makosa ya kisayansi. Ni jambo la maana kuona kwamba Yesu hakuruhusu hilo limpate, ingawa angaliweza kushinda ubishi pamoja na viongozi wa kidini waliopata elimu ya Kiebrania au Kigiriki. Alipopingwa, Yesu alijibu kwa ufupi akageuza fikira zake tena kwa wanyenyekevu, kondoo wa kweli.—Mathayo 22:41-46; 1 Wakorintho 1:23–2:2.

10. Kwa nini inafaa kwa Wakristo wenye kompyuta na wanaoweza kupata ujumbe wa kielektroni wajihadhari?

10 Kompyuta za kisasa zimefungua njia nyingine ya kuwa na mashirika mabaya. Kampuni nyingine za kibiashara huwezesha watu wanaotumia kompyuta fulani pamoja na simu kupeleka ujumbe wa kielektroni unaoweza kusomwa na watu kadhaa; hivyo mtu anaweza kuweka ujumbe fulani katika kompyuta uwezao kusomwa na wote wenye kompyuta hiyo. Hilo limeongoza kwenye yale yanayoitwa eti mabishano ya kielektroni juu ya mambo ya kidini. Mkristo aweza kuvutwa kwenye mabishano hayo na aweza kutumia muda wa saa kadhaa pamoja na mtu anayefikiri kwa njia ya uasi-imani ambaye huenda ikawa ametengwa na ushirika wa kutaniko. Mwelekezo kwenye 2 Yohana 9-11 unakazia shauri la Paulo la kibaba juu ya kuepuka mashirika mabaya.a

Epuka Kudanganyika

11. Hali ya kibiashara katika Korintho ilitoa fursa gani?

11 Kama vile ilivyoonyeshwa, Korintho lilikuwa kitovu cha kibiashara, chenye maduka na biashara kadhaa. (1 Wakorintho 10:25) Wengi waliokuja kwa ajili ya Michezo ya Isthmasi wangekaa katika mahema, na wakati huo wafanya biashara wangeuza wakiwa katika vibanda vyenye kuchukulika au vibanda vilivyofunikwa. (Linganisha Matendo 18:1-3.) Hilo lilimwezesha Paulo apate kazi huko akitengeneza mahema. Na angeweza kutumia mahali hapo pa kufanyia kazi ili kueneza habari njema. Profesa J. Murphy-O’Connor aandika hivi: “Akiwa ndani ya duka katika soko lenye shughuli nyingi . . . kwenye barabara yenye halaiki ya watu Paulo aliweza kuongea, si pamoja na wafanyakazi na wateja tu, bali pia na halaiki ya watu waliokuwa nje. Wakati biashara ilipopungua angeweza kusimama mlangoni na kuongea na wale ambao alifikiri wangesikiliza . . . Ni vigumu kuwazia kwamba utu wake wenye bidii na usadikisho mwingi haukumgeuza upesi kuwa ‘mtu wa ujirani mwenye utu wa kutokeza,’ na hilo lingalivuta wale wenye udadisi, si wavivu tu bali pia wale wenye kutafuta kikweli. . . . Wanawake walioolewa pamoja na watumishi wao, waliomsikia, wangetembelea wakijifanya wanakuja kununua vitu. Katika nyakati za mkazo, wakati mnyanyaso au kuudhiwa tu kulipotisha kutokea waamini wangeweza kukutana naye wakiwa wateja. Mahali hapo pa kazi palimwezesha pia awasiliane na ofisa wa manispa.”

12, 13. Shauri katika 1 Wakorintho 15:33 linaweza kutumiwaje ifaavyo kazini?

12 Lakini, Paulo angalitambua uwezekano wa kuwa na “mashirika mabaya” kazini. Sisi pia twapaswa kutambua hivyo. Kwa maana, Paulo alinukuu mtazamo ulioenea miongoni mwa wengine: “Na tule na tunywe maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Alifuatana mara moja na shauri lake la kibaba: “Msipotezwe. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (NW) Mahali pa kufanyia kazi na ule utafutaji wa furaha vinaweza kuunganishwaje kuwa jambo liwezalo kuleta hatari?

13 Wakristo wanataka kuwa na urafiki pamoja na wafanyakazi wenzao, na maono mengi yanaonyesha jinsi jambo hilo linavyoweza kuwa lenye matokeo katika kufungulia njia ya kutoa ushahidi. Hata hivyo, mfanyakazi mwenzetu aweza kufasiri vibaya urafiki wetu, kuwa mwaliko wa kushirikiana pamoja wakati mzuri. Huenda yeye akatoa mwaliko wa kutukia tu wa kwenda kula mlo wa mchana pamoja, kwenda mahali fulani baada ya kazi ili kunywa kileo, au kushiriki tafrija kwenye mwisho-juma. Mtu huyo aweza kuonekana mwenye fadhili na nadhifu, na mwaliko huo waweza kuonekana bila hatia. Lakini, Paulo atushauri hivi: “Msidanganyike [msipotezwe, NW].”

14. Wakristo wengine wamedanganyikaje kupitia mashirika?

14 Wakristo wengine wamedanganyika. Walisitawisha polepole mtazamo mlegevu kuelekea kushirikiana pamoja na wafanyakazi wenzao. Labda ulisitawi kwa sababu ya wote wanapendezwa na michezo ileile au shughuli zilezile zenye kufurahisha. Au mtu fulani kazini asiye Mkristo aweza kuwa mwenye fadhili na mwenye ufikirio isivyo kawaida, jambo ambalo liliongoza kwenye kutumia kiasi cha wakati chenye kuongezeka pamoja na mtu huyo, hata kupendelea ushirika huo kuliko ule wa wengine katika kutaniko. Kisha ushirika huo waweza kuongoza kwenye kukosa mkutano mmoja tu. Ungeweza kumaanisha kuchelewa nje sana jioni moja na kuvunja utaratibu wa kushiriki katika huduma ya shambani asubuhi. Ungeweza kuwa na tokeo la kutazama sinema moja au vidio ya aina ambayo Mkristo angekataa kwa kawaida. ‘Ah, hilo haliwezi kunipata kamwe,’ huenda tukafikiri. Lakini huenda ikawa wengi wa wale ambao wamedanganyika waliitikia njia hiyo mwanzoni. Tunahitaji kujiuliza wenyewe hivi, ‘Nimeazimia kadiri gani kutumia shauri la Paulo?’

15. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani wenye usawaziko kuelekea majirani?

15 Jambo ambalo tumetoka tu kuzungumzia juu ya mahali pa kufanyia kazi linahusu pia ushirika wetu na majirani. Kwa hakika, Wakristo katika Korintho la kale walikuwa na majirani. Katika jumuiya nyingine ni kawaida kuwa na urafiki na kutegemeza sana majirani. Katika maeneo ya mashambani majirani wanaweza kutegemeana kwa sababu ya kuwa mbali na wengine. Mahusiano ya familia ni yenye nguvu hasa katika tamaduni nyingine, hilo likitokeza mialiko mingi kwenye milo. Kwa wazi, maoni yenye usawaziko ni ya maana, kama vile Yesu alivyoonyesha. (Luka 8:20, 21; Yohana 2:12) Katika mahusiano yetu na majirani na watu wa ukoo, je, tuna mwelekeo wa kutenda kama tulivyotenda kabla ya sisi kuwa Wakristo? Badala ya hivyo, je, hatupaswi kufikiria tena mahusiano hayo na kuamua kwa kudhamiria ni mipaka gani inayofaa?

16. Maneno ya Yesu kwenye Mathayo 13:3, 4 yanapasa yaelewekeje?

16 Wakati mmoja Yesu alifananisha neno la Ufalme na mbegu ambazo “zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila.” (Mathayo 13:3, 4, 19) Wakati huo, udongo uliokuwa karibu na njia ulikuja kuwa mgumu wakati miguu mingi ilipotembea huku na huku juu yao. Ndivyo ilivyo na watu wengi. Maisha zao zimejaa na majirani, watu wa ukoo, na wengine wakija na kwenda, wakiwashughulisha. Ni kana kwamba hilo linakanyaga kwa miguu udongo wa mioyo yao, likifanya iwe vigumu kwa mbegu za kweli kumea. Kutoitikia hukohuko kungeweza kusitawi katika mtu ambaye tayari ni Mkristo.

17. Kushirikiana pamoja na majirani na wengine yangeweza kutuathirije?

17 Majirani na watu wa ukoo wengine walimwengu wanaweza kuwa wenye urafiki na wenye kusaidia, ingawa wameendelea kuonyesha kutopendezwa na mambo ya kiroho wala na uadilifu. (Marko 10:21, 22; 2 Wakorintho 6:14) Kuwa kwetu Wakristo hakupasi kumaanisha kwamba tunakuwa bila urafiki, bila kupendezwa na majirani. Yesu alitushauri tuonyeshe kupendezwa kikweli na wengine. (Luka 10:29-37) Lakini shauri lililopuliziwa na la maana vilevile ni lile la Paulo la kuwa waangalifu juu ya mashirika yetu. Tunapotumia lile shauri la kwanza, ni lazima tusisahau hilo la pili. Tusipoweka kanuni zote mbili akilini, mazoea yetu yanaweza kuathiriwa. Mazoea yako yanalinganaje na yale ya majirani au watu wa ukoo wako kuhusiana na ufuatiaji wa mambo yaliyo haki au kutii sheria ya Kaisari? Kwa mfano, huenda wakahisi kwamba wakati wa kulipa kodi, kutoripoti mapato yote au faida zote za biashara ni sawa, hata ni jambo la lazima ili kuendelea kupata riziki. Wanaweza kusema kwa njia ya kuvutia juu ya maoni yao mnapokunywa kahawa kwa ustarehe au wakati wa ziara fupi. Hilo lingeweza kuathirije fikira zako na mazoea yako yenye kufuatia mambo yaliyo haki? (Marko 12:17; Warumi 12:2) “Msipotezwe. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (NW)

Mazoea ya Ujana Pia

18. Kwa nini 1 Wakorintho 15:33 linahusu vijana pia?

18 Vijana hasa wanaathiriwa na yale wanayoona na kusikia. Je! hujaona watoto wakiwa na ishara za mwili au tabia zinazofanana sana na zile za wazazi wao au ndugu na dada zao? Basi, hatupaswi kushangaa kwamba watoto wanaweza kuathiriwa sana na wale wanaocheza nao au wanashule wenzao. (Linganisha Mathayo 11:16, 17.) Ikiwa mwana wako au binti yako yuko karibu na vijana wanaosema bila staha juu ya wazazi wao, kwa nini uwazie kwamba hilo halitawaathiri watoto wako? Namna gani ikiwa mara nyingi wanasikia vijana wengine wakitumia lugha ya matusi? Namna gani ikiwa marika wao shuleni au katika ujirani wanasisimuka juu ya staili mpya ya viatu au mtindo mpya wa vito? Je! tufikiri kwamba Wakristo wachanga hawaathiriwi na uvutano huo? Je! Paulo alisema kwamba 1 Wakorintho 15:33 inawaathiri wale tu ambao wamefikia umri fulani?

19. Wazazi wanapaswa wajaribu kukazia maoni gani kikiki katika watoto wao?

19 Ikiwa wewe ni mzazi, je, unafahamu shauri hilo unapowatolea watoto wako sababu na kufanya maamuzi kuhusu wao? Labda utasaidiwa ukikubali kwamba hilo halimaanishi kwamba vijana wote wengine ambao watoto wako hushirikiana nao katika ujirani au shuleni si watu wazuri. Huenda wengine wakawa wenye kupendeza na wenye adabu, kama majirani, watu wa ukoo, na wafanyakazi wenzako wengine walivyo. Jaribu kuwasaidia watoto wako waone hilo na watambue kwamba una usawaziko katika matumizi yako ya shauri la Paulo lenye hekima, la kimzazi kwa Wakorintho. Wanapotambua njia unayosawazisha mambo, hiyo yaweza kuwasaidia wakuige.—Luka 6:40; 2 Timotheo 2:22.

20. Vijana, mnakabili jambo jipi gumu?

20 Nyinyi mlio wachanga bado, jaribuni kutambua jinsi ya kutumia shauri la Paulo, mkijua kwamba hilo ni jambo la muhimu kwa kila Mkristo, mchanga kwa mzee. Hilo litataka juhudi nyingi, lakini kwa nini usitake kukabiliana nalo? Ng’amua kwamba kwa sababu tu umewajua baadhi ya vijana hao wengine kutoka utoto haimaanishi kwamba hawawezi kuathiri mazoea yako, kwamba hawawezi kuharibu mazoea unayofanyiza ukiwa kijana Mkristo.—Mithali 2:1, 10-15.

Hatua Zifaazo Ili Kulinda Mazoea Yetu

21. (a) Tuna uhitaji upi kuhusiana na ushirika? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba mashirika mengine yanaweza kuwa hatari?

21 Sisi sote twahitaji ushirika. Lakini, ni lazima tuwe macho kwa jambo la kwamba washiriki wetu wanaweza kutuathiri, kwa uzuri au kwa ubaya. Hilo lilithibitika kuwa kweli kwa Adamu na kwa kila mtu katika karne zilizopita baada ya hapo. Kwa kielelezo, Yehoshafati, mfalme mwema wa Yuda, alikuwa na upendeleo na baraka ya Yehova. Lakini baada ya yeye kuruhusu mwana wake amwoe binti ya Mfalme Ahabu wa Israeli, Yehoshafati alianza kushiriki na Ahabu. Ushirika huo mbaya ulikuwa karibu umgharimu Yehoshafati uhai wake. (2 Wafalme 8:16-18; 2 Mambo ya Nyakati 18:1-3, 29-31) Tukifanya machaguo yasiyo na hekima kuhusiana na mashirika yetu, hali yaweza ikawa ya hatari vivyo hivyo.

22. Tunapaswa kuzingatia nini moyoni, na kwa nini?

22 Basi, acheni tuzingatie moyoni lile shauri lenye upendo ambalo Paulo atutolea kwenye 1 Wakorintho 15:33. Hayo si maneno tu ambayo huenda ikawa tumesikia mara nyingi sana hivi kwamba tunaweza kuyakariri. Yanaonyesha ile shauku ya kibaba ambayo Paulo alikuwa nayo kwa ndugu na dada zake Wakorintho, na, kwetu sisi, kwa urefusho. Na bila shaka yana shauri ambalo Baba yetu wa kimbingu huandaa kwa sababu ataka juhudi zetu zifanikiwe.—1 Wakorintho 15:58.

[Maelezo ya Chini]

a Hatari nyingine katika ujumbe huo wa kuwekwa katika kompyuta ni kile kishawishi cha kunakili katika kompyuta yako programu au vichapo vyenye haki ya uchapaji bila ruhusa ya wenye kuzichapisha au ya watunga-vitabu wa awali, jambo ambalo lingepinga sheria za kimataifa za haki ya uchapaji.—Warumi 13:1.

Je! Wakumbuka?

◻ Paulo aliandika 1 Wakorintho 15:33 kwa sababu gani hasa?

◻ Tunaweza kutumiaje shauri la Paulo kazini?

◻ Tunapaswa kuwa na maoni gani yenye usawaziko kuhusu majirani?

◻ Kwa nini 1 Wakorintho 15:33 ni shauri lifaalo hasa kwa vijana?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Paulo alitumia mahali pa kufanyia kazi ili kueneza habari njema

[Picha katika ukurasa wa 18]

Vijana wengine wanaweza kuharibu mazoea yako ya Kikristo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki