Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 8/1 kur. 19-22
  • Kupata Kuwajua Wakristo wa Kwanza

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupata Kuwajua Wakristo wa Kwanza
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Barua Zenyewe
  • Watu Wenyewe
  • Mifano Iliyo Myema
  • Mtume Paulo
  • Kitabu Cha Biblia Namba 47—2 Wakorintho
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Kitabu Cha Biblia Namba 46—1 Wakorintho
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Msaada Katika Kufanya Maamuzi Yenye Hekima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • “Endelea Kusema na Usinyamaze”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 8/1 kur. 19-22

Kupata Kuwajua Wakristo wa Kwanza

Paulo Anaandikia Wakorintho

WALIO wengi kati yetu wanafurahia kutuma barua na kuzipokea. Hiyo ni njia nzuri ya kuwasiliana na marafiki na wapendwa walio mbali. Hasa barua zilizoandikwa na Wakristo wa karne ya kwanza zinapendeza sana. Katika barua hizo, tunaweza kufahamu waliishi katika ulimwengu wa namna gani na ni mikazo gani iliyowakabili. Kusoma barua hizo ni njia nzuri ya kupata kuwajua Wakristo wa kwanza.

Kwa mfano, zile barua mbili zilizohifadhiwa katika Biblia zetu ambazo zilizoandikwa na mtume Paulo kwa Wakristo katika Korintho, Ugiriki, zinafunua kwamba huo ulikuwa ulimwengu wenye kusisimua, wenye watu wa namna mbalimbali na matatizo ya namna-namna. Nazo zinatusaidia hasa kufahamiana vizuri zaidi na mtume Paulo, Mkristo mwenye kutokeza sana aliyeipainia (aliyeianzisha) kazi ya kuzihubiri “habari njema” katika sehemu nyingi za Milki ya Roma.

Paulo alifika Korintho mwaka wa 50 WK, miaka kumi na saba tu baada ya kifo cha Yesu. Siku hizo mji huo ulikuwa na shughuli nyingi sana. Ulikuwa mahali pazuri katika uso wa nchi, basi ukawa ni mahali pakuu penye utajiri wa kibiashara. Ulivutia watu wa mataifa yote waliokuwa na hali za kupendeza.

Palikuwa pia mahali pakuu pa michezo. Michezo ya Isthmia, iliyofanywa huko kila miaka miwili, ilichukuliwa kuwa ya pili kwa Michezo ya Olympia katika ubora wayo. Na mji huo ulikuwa wa kidini. Mji wa Korintho ulijulikana hasa kwa sababu ya kumwabudu mungu-mke wa Kigiriki Afrodite, na kwa sababu ya uasherati uliofanywa kuhusiana na ibada ya mungu huyo. Kwa kweli, neno “kukorinthisha” lilimaanisha “kuzoea mambo ya umalaya.”

Barua Zenyewe

Kuhubiri kwa Paulo katika Korintho kulichochea upinzani uliokuwa kawaida kati ya Wayahudi wenye kushikilia sana maoni yao kufa au kupona. Lakini alikaa huko kwa sababu alipata watu wenye mioyo ya kuitikia mahubiri yake. Mwaka mmoja na nusu baadaye, alipoondoka hatimaye, kulikuwa na kundi lililothibitika la Wakristo. Karibu miaka mitatu baada ya hapo, Paulo aliiandika barua ambayo sasa tunaiita Wakorintho wa Kwanza.

Kwa sababu gani mtume aliandika barua hiyo? Kwanza, Wakorintho walikuwa wamempelekea maulizo fulani yaliyohitaji kujibiwa. Lakini jambo la maana zaidi ni kwamba yeye alikuwa amepokea habari zenye kusumbua akili kutoka Korintho. Migawanyiko, mafundisho mabaya, mazoea machafu-machafu na watu wenye kujitakia yao wenyewe ni mambo yaliyokuwa yakielekea kuharibu hali ya kiroho ya kundi changa hilo. Basi Paulo akaiandika barua hiyo yenye mkazo mwingi lakini yenye uchangamshi, ili kurekebisha mambo. Je! Wakorintho waliitikia vizuri? Ndivyo, kwa kadiri fulani. Baada ya muda unaopungua mwaka mmoja aliandika barua yake ya pili kwa Wakorintho, akawasifu kwa sababu ya nia yao iliyokuwa imepata maendeleo.

Kwa kuwa barua hizo ziliongozwa na Mungu, hazijakwisha kazi. Kanuni zilizomo zingali ni zenye mafaa. Kwa hiyo, zisome barua hizo kwa uangalifu ikiwa unataka kukifahamu kiwango cha Kikristo kwa ndoa, namna ya kupanga mikutano ya ibada ya kweli, kanuni ya ukichwa wa Kikristo unaofaa na uhitaji wa wote wa kuwa ‘wamehitimu katika nia moja na shauri moja.’ (1 Wakorintho 1:10) Barua ya kwanza inajulikana sana pia kwa sababu ya maelezo yake mazuri juu ya upendo na kwa sababu ya kueleza na kutetea kwa ustadi tumaini la ufufuo. (1 Wakorintho, sura ya 13 na ya 15) Lakini, kama ilivyokwisha kutajwa, barua hizo zinatusaidia pia kufahamiana vizuri zaidi na Wakristo wa kwanza.

Watu Wenyewe

Wakristo Wakorintho walikuwa watu wa namna gani? Wengine walikuwa na asili ya Kiyahudi, kutia ndani Krispo aliyekuwa afisa-msimamizi wa sinagogi la Kiyahudi wakati Paulo alipofika Korintho mara ya kwanza. (Matendo 18:8) Kulikuwako pia watu wasio Wayahudi, na wengine kati yao walikuwa wamehusika hapo kwanza katika uasherati mchafu sana wa Korintho.​—1 Wakorintho 6:9-11.

Inaonekana kwamba watumwa fulani walipata kuwa Wakristo. Ndivyo na wajane na waseja fulani, na pia watu waliooa au kuolewa ambao wenzi wao wa ndoa hawakuwa wamezikubali habari njema. (1 Wakorintho 7:12-40) Ndiyo kusema, hiki tukizifikiria tofauti zilizohusu wakati na asili ya utamaduni wa Korintho, kundi la Kikristo katika Korintho halionekani kwamba lilikuwa tofauti sana na makundi mengi ya leo yaliyo katika miji mikubwa-mikubwa.

Walakini, waamini katika Korintho walikuwa sana-sana ni wapya katika imani ya Kikristo, nalo jambo hilo lilijionyesha lenyewe. Waliruhusu mwanamume mmoja aendelee kushirikiana nao ingawa alikuwa akifanya zinaa ya maharimu pamoja na mama yake wa kambo. Labda walifikiri kwamba uhuru wa Kikristo uliruhusu watu wafanye mambo ya namna hiyo. Pia, badala ya kuwa wameungana walikuwa wamegawanyika visehemu-visehemu, wakifuata wanadamu badala ya kumfuata Yesu Kristo. Nia mbaya-mbaya zilionekana katika njia ambayo waliadhimisha Chakula cha Jioni cha Bwana, wengine wao hata wakawa ni walevi wakati huo!—1 Wakorintho, sura ya 1, 5, na ya 11.

Tena, waamini fulani Wakorintho walikuwa wakipeleka Wakristo wenzao mahakamani. Wengine, labda kwa sababu ya kuvutwa na falsafa ya Kigiriki, walikuwa wakifundisha kwamba hakuna kitu kama ufufuo. Na wengine walikuwa wenye kiburi, ‘wakawa wanajitutumua,’ wakijiona kuwa bora kwa njia fulani kuliko washiriki wale wengine wote wa kundi.​—1 Wakorintho 4:18, NW; 3:18; 6:1-8; 15:12.

Je! inasikika kama kwamba yalikuwako matatizo mengi? Ndivyo, yalikuwako matatizo mengi? Ndivyo, yalikuwako. Lakini, kumbuka kwamba Paulo alikuwa ameanza kuhubiri katika Korintho miaka mitano tu kabla ya hapo. Ni kweli kwamba Yehova Mungu alikuwa ametoa vipawa (karama) vya pekee vya roho ili kulitia kundi nguvu, lakini Wakorintho walikuwa wamependezwa zaidi na vipawa vya ndimi (lugha). Hiyo ilikuwa ishara yenye kustaajabisha watu wasio Wakristo lakini haikufaa sana katika kulijenga kundi. Kwa hiyo, Paulo aliwatia moyo wasitawishe kipawa cha unabii, ambacho kingewatia zaidi nguvu za kiroho.​—1 Wakorintho 14:1-12.

Makusudi ya kufanya mambo ya Wakristo walio wengi Wakorintho hayakuwa mabaya. Walikuwa wamempelekea Paulo maulizo, kwa hiyo ni wazi walitaka kujua njia inayofaa ya kufanya mambo. Pia, Paulo aliwasifu kwa kusema: “Basi nawasifu, kwa sababu mmenikumbuka katika mambo yote, nanyi mmeyashika yale mapokeo vile vile kama nilivyowatolea.” (1 Wakorintho 11:2) Na wakati alipoandika mashauri thabiti, inaonekana wengi wao waliyakubali kwa utayari, ‘wakahuzunishwa kwa jinsi ya Mungu.’ (2 Wakorintho 7:11) Lakini wengine waliendelea kupinga mamlaka ya Paulo.​—2 Wakorintho 10:10; 11:4-6.

Mifano Iliyo Myema

Katika sehemu zote za vitabu hivyo watu mbalimbali wanatajwa. Paulo anataja mtu fulani aliyeitwa Sosthene, ambaye labda alikuwa Myahudi mashuhuri katika Korintho kabla hajawa Mkristo. (1 Wakorintho 1:1; Matendo 18:17) Washiriki wa nyumba ya Kloe, waliokuwa Wakorintho pia, walimpelekea Paulo ripoti juu ya hali mbaya iliyokuwa ikiendelea katika kundi. Huo ni mfano mwema kama nini wa kufanya yanayofaa kwa ushujaa! (1 Wakorintho 1:11) Watu wa nyumba ya Stefana, waliokuwa ndio Wakristo wa kwanza huko, walikuwa na shughuli nyingi za kuhudumia watakatifu​—mfano mwema wa ukaribishaji. Stefana, pamoja na Fortunato na Akaiko, anapendekezwa kwa Wakorintho na Paulo. “Wajueni sana watu kama hao,” akasema.​—1 Wakorintho 16:18, 15, 17.

Halafu alikuwako Apolo, msemaji mwenye ufasaha na usadikishi. Paulo alimwomba atembelee Korintho, lakini yeye hakutaka kufanya hivyo wakati huo. Labda alikuwa na mambo mengine yaliyompasa kufanya, au labda hakutaka kwenda huko isije ikaongezeka ile roho ya kujigawa madhehebu-madhehebu iliyokuwa imetokea kwa jina lake. (1 Wakorintho 16:12) Tito mwaminifu, ambaye baadaye alimwakilisha Paulo katika Krete, sasa alimwakilisha katika Korintho kisha akaleta habari njema za kwamba walikuwa wamebadili nia yao. (Tito 1:5; 2 Wakorintho 7:14, 15; 12:18) Hata yule kijana Timotheo mwenye kutokeza sana alikuwa amekuwa huko. Alisaidia katika kazi ya kwanza ya kueneza evanjeli katika Korintho, na Paulo alitumainia kwamba Timotheo angerudi huko baada ya muda mfupi. (1 Wakorintho 4:17; 16:10) Ndiyo, jamii ya Kikristo inayofunuliwa katika barua hizo ilikuwa yenye shughuli nyingi. Walikuwa tengenezo la watu wa kweli wenye kuhangaikia kumtumikia Mungu na kuhudumiana.

Mtume Paulo

Na mwenye shughuli kuliko wote alikuwa ni mtume Paulo mwenyewe. Tunamwona akiwahubiri Wakorintho “katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi,” akiwa tofauti sana na vile inavyofikiriwa na wengi kwamba alikuwa na shauku mbaya inayopita kiasi kinachofaa. (1 Wakorintho 2:3) Yajapokuwako matatizo hayo mazito, tunauhisi upendo wa Paulo kwa Wakorintho. Yeye aliwasifu alipoweza na akaonyesha amefurahi wakati alipopata habari za kwamba waliyakubali kwa njia nzuri mashauri yake thabiti.​—1 Wakorintho 4:14; 11:2; 2 Wakorintho 7:8-13.

Mioyo yetu inampenda sana Paulo tunaposoma juu ya magumu yaliyompata katika huduma​—mapigo, zile safari ndefu-ndefu, hatari mbalimbali, na pia “mwiba katika mwili,” ambao labda ulikuwa ni kutaabishwa sana na macho. (2 Wakorintho 12:7-10; 11:21-27) “Baghairi ya mambo ya nje,” anasema Paulo, “yako yanijiayo kila siku, ndiyo maangalizi ya makanisa [makundi] yote.” (2 Wakorintho 11:28) Bila shaka wazee wengi Wakristo watamhurumia kwa matatizo yaliyompata.

Lakini Paulo hakuwa akilalamika. Aliyataja mambo hayo ili atetee tu mamlaka yake kuelekeana na wale “mitume walio bora zaidi.” (2 Wakorintho 12:11-13, NW) Kwa kweli, yeye alifurahi kuvumilia magumu ya namna hiyo, kwa kuwa kufanya hivyo kulionyesha wazi alikuwa akitumikia kwa uwezo wa Mungu, si wake mwenyewe. (2 Wakorintho 12:9, 10) Hivyo yeye ni mfano mwema wa imani yenye matendo.

Paulo aliwaambia Wakorintho hivi: “Basi, nawasihi mnifuate mimi.” (1 Wakorintho 4:16) Hata leo, inafaa tufuate kitia-moyo hicho. Lakini ili tumfuate (tumwige) Paulo ni lazima tupate kumjua yeye​—mwendo wake wa uaminifu, maoni yake na nia zake, na kujitoa kwake atumikie Mungu. Njia nzuri ya kufanya hivyo ni kuzisoma zile barua mbili alizowaandikia Wakristo katika Korintho. Mbona usianze kufanya hivyo sasa?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki