Je! Ulinzi wa Kweli Wawezekana?
MTUNGA insha Ralph Waldo Emerson alijulisha hivi wakati mmoja: “Watu wasiofikiri sana huamini bahati . . . Watu wenye akili nyingi huamini kwamba kitokeacho huwa kimesababishwa.” Naam, mtu anayetia imani katika nguvu za talasimu za kichawi na hirizi za bahati njema huruhusu maisha yake yaongozwe na kani zisizoonekana. Yeye hukatalia mbali hoja na sababu na kufuata hofu za kishirikina, zilizo za kipumbavu.
Hata hivyo, Biblia inaweza kumweka mtu huru na hofu hizo. Hiyo huonyesha kwamba talasimu na hirizi hazina uwezo, wala nguvu. Jinsi gani? Kulingana na The New Encyclopædia Britannica, “inafikiriwa kwamba talasimu hupata nguvu kutokana na uhusiano wazo na kani za kiasili [miongoni mwa mambo mengine].” Kani hizo zaweza kuwa ‘roho za wafu’ au ‘nguvu za bahati.’ Lakini Biblia huonyesha kwa wazi kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Hivyo, hakuna roho za wafu zinazoweza kuwasaidia wala kuwaumiza walio hai; wala hakuna kani yoyote isiyoonekana ya bahati inayoweza kufanya jambo fulani kwa niaba yako.
Katika nyakati za Biblia, Mungu aliwashutumu wale waliomwacha, wale waliosahau mlima wake mtakatifu, wale “[walio]andika meza kwa ajili ya [mungu wa, New World Translation] Bahati [Njema, NW], na kuijazia [mungu wa, NW] Ajali vyombo vya divai iliyochanganyika.” Badala ya kupata ulinzi, watu hao waliounga mkono bahati waliangamizwa. “Mimi nitawaandikia kuuawa kwa upanga,” akasema Yehova Mungu.—Isaya 65:11, 12.
Taifa la Babuloni la kale vilevile lilitia imani katika ulinzi wa nguvu mbalimbali za kifumbo, kwa kuzoea mafumbo ya kichawi. Lakini, hata hivyo, Babuloni lilipatwa na msiba. “Endelea katika ulozi wako na uchawi wako mwingi,” akapinga nabii Isaya. “Labda unaweza kupata msaada kutoka kwao . . . La hasha! zijapokuwa hila zako nyingi huna nguvu.” (Isaya 47:12, 13, The New English Bible) Baadaye taifa hilo lilitoweka kabisa. Imani katika mafumbo ya kishetani ilithibitika kuwa ya bure. Vivyo hivyo, hakuna talasimu ya kichawi, hirizi, wala kago inayoweza kufanya lolote kukusaidia au kukulinda.
Namna ya Ibada ya Sanamu
Bado, huenda watu fulani wasione madhara katika kubeba fuwele, ukwato wa sungura, au nishani ya kidini. Je! hivyo si vipambo tu visivyo na madhara? Sivyo kulingana na Biblia. Hiyo husema kwamba vifaa vya mafumbo ya kishetani ni vyenye madhara pasipo shaka lolote.
Kutumia talasimu ni namna fulani ya ibada ya sanamu—jambo linaloshutumiwa waziwazi katika Neno la Mungu. (Kutoka 20:4, 5) Ni kweli, huenda mtu asihisi kwamba anaabudu talasimu au kago moja kwa moja. Lakini, mtu akiwa tu na moja, je, hilo halidhihirishi mtazamo wenye kicho na wa kiibada kuelekea nguvu za mafumbo ya kishetani zisizoonekana? Na je, si kweli kwamba mara nyingi hirizi zenyewe hupewa uangalifu wa kiibada (kama vile kubusu)? Lakini Biblia huwashauri Wakristo hivi, kwenye 1 Yohana 5:21: “Jilindeni nafsi zenu na sanamu.” Je! hilo lisingetia ndani vifaa vinavyoonwa kuwa hirizi au talasimu?
Mtego wa Mafumbo ya Kishetani
Kupitia utumizi wa talasimu, wengi pia hunaswa na mafumbo ya kishetani. Ni kweli, huenda watu fulani wakabeba fuwele au dawa fulani ya umajimaji wa kichawi kwa sababu za kidesturi hasa kuliko sababu za usadikisho. Lakini kama vile kufanya mzaha unaogusia mapenzi na malaya huenda kukaongoza kwenye kuambukizwa UKIMWI, kufanya mzaha na mafumbo ya kishetani kwaweza pia kuleta maafa. Ni kwa sababu nzuri kwamba Mungu aliwakataza Waisraeli wasizoee uchawi, uaguzi, wala kutabiri matukio mema au mabaya. “Mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA [Yehova, New World Translation],” ndivyo Biblia huonya.—Kumbukumbu la Torati 18:10-14.
Kwa nini kuwe katazo hilo kali? Kwa sababu kani zisizoonekana ambazo ndizo chanzo cha mazoea hayo si roho za wafu (mizimu) wala nguvu za bahati bali ni Shetani Ibilisi na mashetani wake.a Na utumizi wa talasimu unahusiana moja kwa moja na ibada ya mashetani. Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words yasema hivi: “Katika uchawi, utumizi wa dawa za kulevya, kwamba ni za kawaida tu au zenye nguvu, kwa ujumla ulifuatana na maneno fulani ya ulozi ya kuomba nguvu za kisiri, pamoja na uandalizi wa hirizi, talasimu, n.k.”
Kwa hiyo mtu aliye na hirizi ya mafumbo ya kishetani anacheza na uwasiliani-roho. Ajihatarisha kutiishwa chini ya ule uvutano na mwongozo mwovu wa “mungu wa dunia hii”—Shetani Ibilisi. (2 Wakorintho 4:4) Basi, ni kwa sababu nzuri kwamba Biblia hutuamuru tuepuke namna zote za uwasiliani-roho.—Wagalatia 5:19-21.
Kujiweka Huru na Ushirikina
Hata hivyo The World Book Encyclopedia yaonelea hivi: “Labda ushirikina utakuwa sehemu ya maisha maadamu watu wanahofiana na hawana uhakika juu ya wakati ujao.” Lakini Mashahidi wa Yehova wanawasaidia watu wengi wajiweke huru na ushirikina wenye madhara. Mwanamke mmoja wa Afrika Kusini akumbuka hivi: “Nilisumbuliwa na roho waovu, na nyumba yangu ilijaa muti ili kunilinda dhidi yao.” Mashahidi wa Yehova walimsaidia aone hatari za kuchezea mafumbo ya kishetani. Itikio lake lilikuwa nini? “Nilianza kutupa mbali kila kitu nilichomiliki ambacho kilihusiana na roho waovu,” yeye asema. “Afya yangu ilikuwa bora. Niliweka maisha yangu wakfu kumtumikia Yehova nikabatizwa.” Sasa yuko huru na ushirikina na uwasiliani-roho.
Fikiria pia, yule mganga Mnaijeria aliyechanganya uwasiliani-roho pamoja na stadi zake za kuponya. Mara nyingi akitumia matisho na laana, alikuwa kwa kawaida akiwafukuza Mashahidi wa Yehova kwa nguvu kutoka nyumbani kwake walipomtembelea. Hata wakati mmoja alitayarisha dawa ya umajimaji wa pekee, akatamka maneno fulani ya ulozi juu yao, na kuupuliza usoni pa Shahidi mmoja! “Utakufa katika siku saba!” akapaaza sauti. Baada ya siku saba Shahidi huyo alirudi, akimsababisha mganga huyo atoke nje upesi, akiamini kwamba alikuwa ameona kizuka! Sasa uchawi wake ukiwa umefunuliwa kuwa wa bure, alikubali funzo la Biblia na hatimaye yeye mwenyewe akawa Shahidi.
Wewe pia waweza kuwekwa huru na pingu za hofu na ushirikina. Kwa kweli, huenda hilo lisiwe jambo rahisi. Labda umekulia katika utamaduni ambamo utumizi wa talasimu na hirizi ni jambo la kawaida. Wakristo katika Efeso la kale walikabili ugumu huo. Waliishi katika utamaduni uliovutwa sana na uwasiliani-roho. Walifanya nini walipojifunza kweli ya Neno la Mungu? Biblia husema hivi: “Watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu.”—Matendo 19:19.
Kupata Ulinzi wa Mungu
Ukijiweka huru na masalio yote ya mafumbo ya kishetani, je, hutaachwa ukiwa bila ulinzi? Hasha, “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.” (Zaburi 46:1) Ulinzi wa Mungu utadhihirika hasa anapoangamiza huu mfumo mwovu wa mambo. “Bwana [Yehova, NW] ajua kuwaokoa watauwa na majaribu, na kuwaweka wasio haki katika hali ya adhabu hata siku ya hukumu.” —2 Petro 2:9; linganisha Zaburi 37:40.
Kwa sasa, ‘wakati na tukio lisilotazamiwa linatupata sote.’ (Mhubiri 9:11, NW) Mungu haahidi kwamba watumishi wake wataishi maisha yaliyolindwa kama kwamba kwa hirizi au kwamba atawazuia wasipatwe na madhara ya kibinafsi. Hata hivyo, yeye aahidi kulinda hali yetu ya kiroho na uhusiano wetu na yeye. (Zaburi 91:1-9) Jinsi gani? Kwanza, yeye hutupa sisi sheria na kanuni zinazoweza kutunufaisha na kutulinda dhidi ya uvutano wa Shetani wenye kufisidi. (Isaya 48:17) Kwa kupata kwetu kujua njia za Yehova, ‘uwezo wenyewe wa kufikiri utatulinda, utambuzi wenyewe utatuhifadhi’—kwa kielelezo, dhidi ya utendaji mbalimbali usiofaa au wenye madhara.—Mithali 2:11, NW.
Njia nyingine ambayo Mungu hutulinda ni kwa kuandaa “nguvu inayozidi iliyo ya kawaida” katika nyakati za jaribu. (2 Wakorintho 4:7, NW) Na hali zinapotisha kumshinda Mkristo, Yeye hutoa “amani ya Mungu, ipitayo akili zote” kulinda moyo na nguvu za kiakili. (Wafilipi 4:7) Naam, Mkristo ana vifaa vya “kuzipinga hila za Shetani.”—Waefeso 6:11-13.
Unaweza kupataje ulinzi huo? Anza kwa kutwaa ndani ujuzi juu ya Yehova na juu ya Mwana Wake, Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Mashahidi wa Yehova wanaweza kukusaidia sana katika jambo hilo. Unapositawisha uhusiano mchangamfu na Yehova, utaanza kujionea mwenyewe ulinzi wake wenye fadhili. Mungu asema, kama tusomavyo kwenye Zaburi 91:14: “Kwa kuwa amekaza kunipenda nitamwokoa; na kumweka palipo juu, kwa kuwa amenijua Jina langu.”
Kwa kweli, ukiwa mwaminifu kwake, hatimaye Mungu atakubariki kwa kukupa uhai wa milele katika ulimwengu mpya unaokuja. Yehova huhakikisha hivi kuhusu wale wanaoishi wakati huo: “Hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA [Yehova, NW] wa majeshi kimesema hivi.” (Mika 4:4) Ugonjwa na kifo havitakuwako tena. (Ufunuo 21:4) Lakini, hata sasa unaweza kufurahia kadiri fulani ya usalama—ukisitawisha uhusiano wa karibu na Yehova. Kama vile mtunga-zaburi, utaweza kusema hivi: “Msaada wangu u katika BWANA [Yehova, NW], aliyezifanya mbingu na nchi.”—Zaburi 121:2.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata habari zaidi, ona broshua, Roho za Wafu—Je! Zaweza Kukusaidia au Kukuumiza? Je! Ziko Kweli? iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Wakristo katika Efeso waliondolea mbali kila kitu kilichohusiana na mafumbo ya kishetani
[Picha katika ukurasa wa 7]
Chini ya Ufalme wa Mungu, hofu haitakuwako tena