Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 10/15 kur. 8-11
  • Tatizo la Kujifunza Kungoja

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tatizo la Kujifunza Kungoja
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hekima ya Kujifunza Kungoja
  • Ugumu Mpya, kwa Wengi
  • Kujifunza Kutoka kwa Wengine
  • Kupiga Vita Vile Vizuri
  • Kujifunza Kungoja Katika Mambo Yote
  • Je, Uko Tayari Kungoja kwa Subira?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Je, Inawezekana Kuwa na Mfumo wa Kiuchumi Wenye Usawa?
    Habari Zaidi
  • Usalama Wako Ni Nini?—Ni Nyumba Yako?—Pesa Zako Banki? —Au Ni Kazi Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Ni Lazima Tumngojee Yehova
    Mwimbieni Yehova Sifa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 10/15 kur. 8-11

Tatizo la Kujifunza Kungoja

LABDA mojawapo masomo magumu zaidi ambayo sisi wanadamu twahitaji kukubali wakati wowote ni kule kujifunza kungojea mambo tunayotaka. Kwa asili watoto wadogo huwa hawana subira. Wanataka chochote kinachowavutia, na wanakitaka saa hiyo! Lakini kama vile huenda ukajua kutokana na yale ambayo umejionea, ni jambo la hakika kwamba hatuwezi kupata kila jambo tunalotaka mara tunapolitaka. Hata kwa habari ya tamaa zilizo halali, ni lazima tujifunze kungojea wakati ufaao wa kuzitosheleza. Wengi hupata kujifunza somo hilo; wengine hawapati kamwe kujifunza.

Watu wanaotaka kupata kibali cha kimungu wana sababu hususa za kujifunza kungoja. Yeremia, mtumishi wa Yehova wa nyakati za kabla ya Ukristo, alikazia hilo: “Ni vema mtu autarajie wokovu wa BWANA [Yehova, NW] na kumngojea kwa utulivu.” Baadaye, mwanafunzi Mkristo Yakobo alisema hivi: “Kwa hiyo ndugu, vumilieni, hata kuja [kuwapo, NW] kwake Bwana.”—Maombolezo 3:26; Yakobo 5:7.

Yehova ana ratiba yake mwenyewe ya kutimiza makusudi ya kimungu. Ikiwa hatuwezi kungoja mpaka wakati wake wa kufanya mambo fulani, tutakuwa wasiotosheka wala kuridhika, jambo ambalo litazuia shangwe. Bila shangwe mtumishi wa Mungu atakuwa dhaifu kiroho, kama vile Nehemia alivyowaambia wananchi wenzake: “Shangwe katika BWANA ndiyo nguvu zenu.”—Nehemia 8:10, The New English Bible.

Hekima ya Kujifunza Kungoja

Ni tamaa ya kiasili kwa waseja kutaka kuoa au kuolewa au kwa waume na wake wasio na watoto kutaka kuwazaa. Zaidi ya hayo, hakuna ubaya wowote katika kutamani kuridhisha mahitaji au tamaa za kimwili zinazofaa. Hata hivyo, kwa sababu ya kuamini kwamba mfumo huu wa mambo utaisha karibuni na kwamba katika ule mfumo mpya unaokuja Mungu ‘ataufumbua mkono wake, na kushibisha kila kilicho hai matakwa yake,’ Wakristo wengi wameamua kungojea kutimiza baadhi ya tamaa hizo kwa wakati ufaao zaidi.—Zaburi 145:16.

Hata hivyo, watu wasio na tumaini hilo la Kikristo lenye msingi mzuri, hawataona sababu ya kuahirisha mambo hayo. Wakiwa bila imani katika Yehova, ambaye “kila kipaji chema na kila zawadi kamilifu” hutoka kwake, wanatilia shaka hekima ya kuahirisha mambo hadi wakati ujao wanaoshuku kuja kwao. Wanaishi kulingana na imani hii: “Na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa.”—Yakobo 1:17, Habari Njema kwa Watu Wote; 1 Wakorintho 15:32; Isaya 22:13.

Katika mataifa yaliyositawi, biashara ya utangazaji hutumia kwa faida yayo ule mbetuko dhahiri kuelekea uradhi wa mara moja. Watu wanatiwa moyo wajibembeleze. Ulimwengu wa biashara wataka tuamini kwamba vifaa na starehe za ki-siku-hizi ni za lazima kabisa. Hoja inayotolewa ni, kwa nini ujinyime vitu hivyo, hasa wakati ambapo kuvipata vyote na kuvipata sasa hivi kumerahisishwa kupitia hati za mkopo, mipango ya kulipa kidogo-kidogo, na mipango ya “nunua sasa—lipa baadaye”? Isitoshe, ‘Wewe wastahili yaliyo bora kabisa; uwe mwenye fadhili kwako mwenyewe! Kumbuka, ama uvifurahie sasa ama labda ukose kamwe kuvifurahia!’ Ndivyo shime zinazopendwa na wengi hudai.

Kwa sasa, makumi ya maelfu ya watu katika nchi zinazositawi wana vitu vya lazima tu—au hata kidogo zaidi. Je! kuna lolote ambalo lingeweza kukazia kwa wazi zaidi ule ukosefu wa ukamilifu na wa haki wa mifumo ya kibinadamu ya kisiasa na ya kiuchumi?

Hekima ya kujifunza kungoja inaonwa kutokana na jambo la kwamba mamilioni ya watu wamejipatia madeni mengi sana bila kutaka—au angalau bila kuona kusudi la kufanya hivyo—ili kuridhisha tamaa za mara iyo hiyo. Hali zisizotazamiwa, kama vile ugonjwa au kutokuwa na kazi ya kuajiriwa, zaweza kumaanisha msiba. Gazeti moja la habari la Kijerumani Frankfurter Allgemeine Zeitung lilieleza kwa nini katika Ujerumani watu wanaoripotiwa kuwa milioni moja hawana makao: “Kwa kawaida, kutokuwa na makao hutangulizwa mara nyingi na kutokuwa na kazi ya kuajiriwa au kuwa na madeni mengi mno.”

Wasiweze kulipa gharama zao, wengi wa watu hao mmoja-mmoja wenye kusikitisha hupatwa na msiba wa kupoteza nyumba na mali zao pia. Mara nyingi sana, ongezeko la mkazo huleta mvutano wa familia. Ndoa zisizo thabiti zinaanza kuzorota. Vipindi vya mshuko wa moyo na matatizo mengine ya afya yanakuwa mambo ya kawaida. Kwa habari ya Wakristo, hali ya kiroho yaweza kuathiriwa vibaya, hilo nalo likiongoza kwenye fikira mbaya na mwenendo usiofaa. Watu ambao mwanzoni walitamani kila kitu kwa njia isiyo ya hekima mwishowe huwa karibu bila chochote.

Ugumu Mpya, kwa Wengi

Yesu alionyesha wazi kwamba twapaswa kujihadhari ili ‘mahangaiko ya dunia, na udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine zisiingie, na kulisonga neno.’ (Marko 4:19) Twapaswa kukumbuka kwamba hakuna mfumo wa kisiasa ambao umeondosha kwa mafanikio mahangaiko ambayo Yesu alisema juu yayo, kutia na yale ya kiuchumi.

Ule Ukomunisti ambao nchi za Ulaya ya Mashariki zimekatalia mbali sasa ulijaribu kusawazisha mambo kupitia uchumi wenye kudhibitiwa na Serikali. Tofauti na ule mfumo wa kiuchumi wenye uhuru wa kufanya biashara, ule mfumo wa wakati uliopita uliwaandalia watu mmoja-mmoja katika mabara hayo usalama fulani wa kiuchumi ambao ubepari hushindwa kutoa mara nyingi. Bado, mahangaiko ambayo Yesu alisema juu yayo yalikuwako kwa namna ya upungufu wa bidhaa za kawaida na kukatizwa kwa uhuru wa kibinafsi.

Kwa sasa, nyingi za nchi hizo zinaanzisha mifumo ya kiuchumi yenye uhuru wa kufanya biashara, hivyo zikitokeza ugumu mpya kwa raia wazo. Ripoti ya hivi karibuni yasema hivi: “Kutokuwa na hali ya kimambo-leo kumeungana na tamaa ya kufikia upesi kiwango cha magharibi cha kununua bidhaa.” Kutimiza hilo “idadi ya watu inayozidi kuongezeka katika Länder [ile sehemu ya Ujerumani iliyokuwa ya kikomunisti] mpya mashariki mwa Ujerumani inajipatia madeni mengi kupita kiasi.” Ripoti hiyo yaongeza hivi: “Sasa hofu na hali ya kukata tamaa vinaenea baada ya ule msisimuko wa kwanza juu ya uhuru mpya wa kiuchumi.” Mahangaiko yanaendelea, lakini sasa yamo kwa namna ya ubepari.

Uhuru mwingi zaidi wa kisiasa na wa kiuchumi umefungulia njia uwezekano mwingi mpya wa kuboreka kiuchumi. Kwa hiyo, huenda watu wengi mmoja-mmoja wakashawishwa kufikiria kwa uzito wazo la kuanza biashara yao wenyewe au kuhamia nchi nyingine yenye fursa bora zaidi za kupata kazi ya kuajiriwa.

Maamuzi kama hayo ni mambo ya kibinafsi. Si vibaya kwa Mkristo kutaka kuboresha hali zake za kiuchumi. Huenda akasukumwa na tamaa ya kuitunza familia yake, akitambua kwamba “ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.”—1 Timotheo 5:8.

Kwa hiyo, haifai kuchambua uamuzi unaofanywa na wengine. Kwa wakati uleule, Wakristo wapaswa kukumbuka kwamba si jambo la hekima kutafuta kitulizo cha kiuchumi kwa kujipatia madeni mengi kupita kiasi ambayo yangeweza kuwanasa. Vilevile isingefaa kutafuta kitulizo cha kiuchumi kwa njia ambayo ingehusisha kupuuza wajibu na masilahi ya kiroho.

Kujifunza Kutoka kwa Wengine

Katika miaka baada ya Vita ya Ulimwengu 2, maelfu ya Wajerumani walihama kutoka Ulaya yenye kukumbwa na vita kwenda kwenye nchi nyingine, hasa Australia na Kanada. Hivyo, wengi waliweza kuboresha hali yao ya kiuchumi, lakini hakuna yeyote kati yao aliyeweza kuepuka kabisa yale mahangaiko ya kiuchumi ambayo Yesu alisema juu yayo. Kusuluhisha matatizo ya kiuchumi kulitokeza matatizo mapya—hamu ya kwenda nyumbani, lugha ya kigeni, kupata kuzoea vyakula vipya, desturi tofauti, kupatana na marafiki wapya, au kukabiliana na mitazamo tofauti.

Mashahidi wa Yehova walikuwa baadhi ya watu hao waliohamia ugenini. Kwa kustahili pongezi, wengi wao walikataa kuruhusu matatizo yaliyo ya kawaida kuhusiana na kuhamia ugenini yaisonge hali yao ya kiroho. Lakini kulikuwako visa vilivyo tofauti. Wengine walinaswa na udanganyifu wa mali. Maendeleo yao ya kitheokrasi yalishindwa kwenda sambamba na hali njema yao ya kiuchumi.

Kwa hakika hilo laonyesha hekima ya kuchanganua hali yetu kwa uangalifu kabla ya kufanya maamuzi ambayo labda si yenye hekima. Mielekeo ya kufuatia vitu vya kimwili itatuzuia tusifanye mengi katika ile kazi ya kufanya wanafunzi ambayo haitarudiwa tena kamwe ambayo Wakristo wamegawiwa kuifanya. Ndivyo ilivyo haidhuru tunakoishi, kwa kuwa hakuna nchi ambayo raia wayo hawana mahangaiko ya kiuchumi.

Kupiga Vita Vile Vizuri

Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole. Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele ulioitiwa.” Alisema hivi kwa Wakristo Wakorintho: “Iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 Timotheo 6:11, 12, UV; 1 Wakorintho 15:58, NW.

Kufuata shauri hilo ndiyo njia iliyo bora zaidi ya kukabiliana kwa mafanikio na ufuatiaji wa vitu vya kimwili, na kwa hakika Mkristo ana mengi ya kufanya! Katika nchi fulani ambamo idadi ya wahubiri wa Ufalme si kubwa, watu wengi mno wamepata kuisikia kweli mara chache sana. Yesu alitabiri hivi kwa usahihi: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache.”—Mathayo 9:37.

Badala ya kuruhusu mahangaiko ya kiuchumi katika nchi hizo yawakengeushe kutoka katika kazi ya kiroho iliyopo, Mashahidi wa Yehova hujifaidi wenyewe na hali hiyo kwa kutumia kikamili fursa zinazopatikana sasa. Wanapokuwa bila kazi ya kuajiriwa kwa muda fulani, wengi wao hupanua utendaji wao wa kuhubiri. Utumishi wao huwapa ile shangwe inayohitajiwa ili kukabiliana na matatizo yao wenyewe ya kiuchumi, zaidi ya kuongezea kile kigelegele cha sifa kwa Yehova.

Mashahidi hao huitanguliza kazi ya kuhubiri na kuweka magumu ya kiuchumi kwenye mahali pa pili, jambo ambalo huonyesha kwa udugu wa ulimwenguni pote kwamba wao humtumaini Yehova kikamili kuwatunza. Ahadi yake ni: “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mathayo 6:33.

Tangu kurudishwa kwa ibada ya kweli katika 1919, Yehova hakuruhusu watu wake wadhoofike. Amewalinda kupitia mnyanyaso mkali na katika sehemu nyingine amewalinda kupitia miongo ya utendaji wa kichinichini. Mashahidi wa Yehova wameazimia kwamba lile ambalo Ibilisi alishindwa kutimiza kupitia mnyanyaso, yeye hatalitimiza kupitia ule mtego wenye hila zaidi wa kufuatia vitu vya kimwili!

Kujifunza Kungoja Katika Mambo Yote

Majumba ya Ufalme makubwa, vikuza-sauti vya bei ya juu, Majumba ya Kusanyiko, na makao ya Betheli yenye kuvutia humletea Mungu utukufu na kutoa ushahidi wa kimya kwamba yeye anawabariki watu wake. Kuhusiana na hilo huenda Mashahidi wa Yehova katika nchi ambamo kazi imepigwa marufuku kwa muda mrefu wakahisi kwamba wana mengi ya kufanya ili kufikia kiwango kilekile cha nchi nyinginezo. Lakini jambo lenye umaana wa kwanza kabisa ni kwamba waendelee kufanya maendeleo kiroho. Maonyesho ya nje-nje ya kuwa na baraka ya Mungu kwa njia ya kimwili yatafuata kwa wakati wayo.

Watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wahitaji kuwa waangalifu, wasije wakaanza kuhisi kwamba wamekuwa bila vitu vya kimwili kwa muda mrefu vya kutosha, kisha waanze ufuatiaji wa masilahi ya kibinafsi. Kutamani kitulizo kutoka katika hali ya ukosefu wa usawa wa kiuchumi na wa kijamii, kwaeleweka, lakini watu wa Yehova hawasahau kwamba watumishi wote wa Mungu wanatamani kupata kitulizo. Vipofu hutamani kuona tena, walio na magonjwa ya kusedeka hutamani kurudishiwa afya, walioshuka moyo hutamani mtazamo mwangavu, na waliofiwa hutamani kuwaona tena wapendwa wao waliokufa.

Kwa sababu ya hali, kila Mkristo hulazimika kwa kadiri fulani kuungojea ulimwengu mpya wa Yehova usuluhishe matatizo yake. Hilo lapaswa litufanye tujiulize wenyewe hivi, ‘Ikiwa nina chakula na nguo, je, nisiridhike na mambo hayo na kuwa na nia ya kungojea kitulizo kutoka katika matatizo ya kiuchumi?’—1 Timotheo 6:8.

Wakristo wanaomtumaini Yehova kikamili waweza kuhakikishiwa kwamba tamaa na mahitaji yao yote yafaayo yataridhishwa hivi karibuni wakiwa tu na nia ya kungoja. Hakuna atakayekuwa amengoja bure. Twarudia maneno haya ya Paulo: “Iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba taabu yenu si ya bure kuhusiana na Bwana.”—1 Wakorintho 15:58, NW.

Kwa hiyo je, kujifunza kungoja kuwapaswa kwa kweli kuwe tatizo kubwa hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kujifunza kungoja kwaweza kuokoa uhai wako

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki