Usalama Wako Ni Nini?—Ni Nyumba Yako?—Pesa Zako Banki?
—Au Ni Kazi Yako?
1. Yehova atawapa watu mambo gani mazuri wanayotaka, na kwa njia gani?
WATU wote walio na akili nzuri wanataka usalama. Wanataka wawe na pesa za kutosha, mahali pazuri pa kuishi, kazi yenye kuwapa mahitaji yao, wawe bila woga, na kuwa na amani ya akili. Yehova alitia tamaa ya mambo hayo katika mwanamume na mwanamke alipowaumba. Na katika taratibu Yake mpya, wanadamu watakuwa na usalama huo wakiwa chini ya utawala wa ufalme wake wa mbinguni. Mtunga zaburi aliongozwa na Mungu kusema hivi juu Yake: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zab. 145:16) Katika taratibu mpya ya Mungu wanadamu watapewa vitu vizuri wanavyotaka, hata kuliko wanavyotazamia.
2. Ni hasara gani zitakazotokea katika “dhiki kubwa” inayokuja?
2 Lakini hatujaingia bado katika taratibu mpya ya Yehova. Bado tunaishi katika taratibu hii mbovu. Nayo inakaribia sana kwisha. Itakwisha muda mfupi ikiisha kugongana na Mungu katika “dhiki kubwa” inayokuja. (Mt. 24:21) Kwa hiyo, kabla taratibu mpya ya Mungu haijatokea, lazima taratibu ya zamani ya utawala wa kisiasa, wa kibiashara na wa kidini inayoongozwa na Shetani iondolewe. (2 Kor. 4:4; Ufu. 19:11-21) Wakati huo Yehova ataua watu wengi sana wanaokataa kufanya mapenzi yake. Bila shaka mali nyingi zitaharibiwa pia, kama zilivyoharibiwa waovu walipoangamia katika gharika ya siku za Nuhu, na wakati Sodoma na Gomora ilipoharibiwa, na vilevile wakati Yerusalemu ulipoharibiwa mwaka 70 W.K.—Luka 17:26-29; 2 Nya. 36:19.
3. Kwa sababu ya mambo yatakayotukia wakati ujao, tunapaswa kuwa na maoni gani?
3 Ndiyo sababu ni lazima sasa tujiangalie tusitamani mali mno. Tukifikiria mali kupita kiasi, tunaweza kuondolewa katika jambo lililo la maana zaidi, yaani, kufanya mapenzi ya Yehova na kupata kibali yake. Ni kama vile mtume Paulo alivyoandika: “Na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.” (Ebr. 12:1) Tunaweza kukosa imani kwa vyepesi tukijiingiza mno katika mambo ya taratibu hii. Tunapopiga mbio tukaipate zawadi ya uzima wa milele, yatupasa tuvue uzito tusiouhitaji kama mpiga mbio anavyofanya. Paulo anafananisha Mkristo na askari pia, ambaye haachi kazi yake na kuingilia mambo mengine, anaposema: “Ushiriki taabu pamoja nami, kama askari mwema wa Kristo Yesu. Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari.”—2 Tim. 2:3, 4.
KUWA NA MAONI YA KIASI
4. Je! Mungu anataka watu wake waache nyumba zao, kazi zao na pesa zao?
4 Basi, je! inatupasa tuamue kwamba, kwa sababu tumeukaribia sana mwisho wa taratibu hii, Mungu anataka Wakristo waache nyumba zao, kazi zao na pesa zao? Je! haiwapasi tena kutafuta riziki, hasa nyakati zenye matatizo ya pesa, wakati watu wengi wanapokosa kazi? Hapana, tusiamue hivyo, kwa sababu Neno la Mungu linasema hivi pia: “Mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Tim. 5:8) Ili walio na jamaa ‘watunze walio wao,’ inawapasa wafanye kazi wapate pesa zinazoweza kuwapa chakula, mavazi na mahali pa kukaa.
5, 6. Leo ni jambo gani la maana linalopaswa kuangaliwa juu ya mali?
5 Maandiko yanataka kuonyesha kwamba, ingawa mtu anapaswa kutafuta vitu vya lazima, asitafute vitu hivyo tu. Ikiwa anafanya sana kazi za siku, anaweza kudhani hana wakati wala nguvu za kumtafuta Mungu, kujifunza vile anavyotaka, na kufanya mapenzi yake. Kwa hiyo lazima aamue atakayekuwa Mungu wake: Yehova au mali. Yesu alisema, “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili . . . Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.” (Mt. 6:24) Kwa kawaida mtu anayetaka sana mali anafanya kazi nyingi azipate na kuzitunza. Ndiyo sababu matajiri wanaona ni vigumu kufanya mapenzi ya Mungu. Wanakuwa na kazi nyingi sana wakitafuta utajiri na kuutunza. Kwa hiyo Yesu alisema: “Jinsi itakavyokuwa shida wenye mali kuingia katika ufalme wa Mungu!”—Marko 10:23.
6 Baada ya muda fulani, njia yako ya kutumia wakati, maoni unayoendelea kuwa nayo, au maamuzi unayofanya yataonyesha kile unachofanyia kazi katika maisha yako yote, Mungu au mali. Utakachofanyia kazi zaidi ndicho kitakachoamua utapatwa na nini wakati ujao, kama kilivyoamulia Lutu na mke wake. “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. “(Gal. 6:7) Mkulima hawezi kupanda mbegu za magugu akatumainia kupata ngano. Vivyo hivyo, akipanda ngano, hatapata magugu. Kwa hiyo, tukitumaini mali za taratibu hii, tutavunjika moyo zikiharibiwa. Tukimtumaini Mungu, tutapata zawadi zake, sasa na katika taratibu yake mpya.
7. Mtume Paulo alionyeshaje maoni yanayofaa?
7 Wakati huu, ni hekima kuwa na maoni ambayo mtume Paulo alikuwa nayo aliposema hivi: “Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo.” Hata kama Paulo angalipoteza vitu vyote, pamoja na maisha yake, kwa sababu ya kufanya mapenzi ya Mungu, asingalirudi nyuma. Alikuwa na tumaini hakika la kufufuliwa. Alitazamia “ufufuo wa mapema kutoka kwa wafu.” (NW) Paulo alifahamu kwamba jambo la maana maishani si mali, utajiri, madaraka wala cheo alichokuwa nacho zamani. Alikuwa na nia ya kuacha vitu hivyo afuate jambo lililo la maana zaidi, yaani, kufanya mapenzi ya Mungu na kupata upendeleo na baraka zake.—Flp. 3:8, 10, 11.
NYUMBA YAKO INA UBORA GANI?
8, 9. Kwa sababu gani si hekima kupenda sana nyumba au mali?
8 Tunaweza kuona hekima ya kuwa na maoni haya tunapoona vile watu wanaopenda sana mali wanavyohuzunika, kuvunjika moyo na kukasirika wanapozipoteza. Kwa mfano, unaweza kuwa na nyumba ya kupendeza leo, lakini unajuaje kama utakuwa nayo kesho? Pengine hata hutakuwa hai kesho. (Luka 12:16-21) Hata sasa, watu wengi ambao wamekuwa na deni kubwa kwa sababu ya kununua nyumba wanakosa pesa za kulipa kisha wanalazimika kuuza nyumba hizo.
9 Vilevile, kila mwaka nyumba nyingi sana zinabomolewa au kuharibiwa na moto, na nyingine zinaharibiwa na maji mengi au upepo mwingi. Wevi wanazidi kuvunja nyumba za watu na kuiba. Watu wengine wanalipwa na bima hasara waliyopata, lakini wengi hawalipwi. Tena watu wanachafuka sana akili na moyo kwa kutumia maisha yao wakitafuta mali tu. Ni kama vile mama mmoja alivyosema: “Hiyo ni kweli. Ukiendelea kuwa na mali, unaendelea kuwa na wasiwasi.” Vilevile, nyumba za watu zimeharibiwa sana katika sehemu nyingi za ulimwengu wakati wa vita, ghasia na jeuri, bila tumaini la kulipwa hasara walizopata.
10. Mkristo anapata faida gani anapokuwa na maoni yanayofaa? (Luka 14:33)
10 Mtu mwenye nia ya kuwa na mali chache hapati hasara kubwa akizipoteza. Mali chache zinamwezesha kutumia wakati na nguvu zaidi ajifunze habari za Muumba wake na kumtumikia. Anapata nafasi ya kumtumaini sana Yehova na ahadi yake. Moto, watu wenye ghasia au jeuri wanaweza kuharibu nyumba yake, lakini hawawezi kumharibia usalama wa kweli anaopewa na Yehova. Ndiyo sababu Yehova anasema, “Kila anisikilizaye atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.” (Mit. 1:33) Mtu wa namna hiyo anaweza kusema hivi: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, [ Yehova], peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.”—Zab. 4:8.
11. Tunaweza kupata hasara gani wakati wa “dhiki kubwa”?
11 Je! nyumba zetu na mali zetu zitabaki wakati wa “dhiki kubwa”? Wakati huo wa machafuko, je! tudhani kwamba mali zetu hazitaguswa? (Zek. 14:13) Wakati wa “dhiki kubwa” Shetani na majeshi yake watashambulia watumishi wa Yehova “ili kuteka mateka, na kuwinda mawindo.” (Eze 38:12) Hatujui Yehova ataachilia adui zake kadiri gani, lakini inaonekana tutapoteza mali zetu.
12. Tunaweza kutazamia nini?
12 Kwa sababu zote hizo, tunaweza kuona kwamba ni upumbavu kupenda mno vitu kama nyumba na vilivyomo, hata ikiwa vinatufurahisha sana. Yehova hatukatazi kuwa navyo, lakini anajua tunaweza kuingia hatarini tukivipenda sana, kama mke wa Lutu. (Luka 17:31, 32) Badala ya kuvipenda, tunapaswa kuutazamia wakati tutakapokuwa katika taratibu mpya ya Mungu, wakati watumishi wake watakapokuwa salama salimini waweze kujenga nyumba zinazofaa.
JE! PESA, AU KAZI, NDIO USALAMA WAKO?
13. Pesa zina usalama gani? (Mhu. 7:12)
13 Tunahitaji pesa ili kuishi katika taratibu hii na kuwa na vitu vya lazima. Lakini watu wengi wanataka kuwa na pesa nyingi banki, wakidhani zitawapa usalama. Hata hivyo, matukio ya karibuni yanaonyesha kwamba pesa haziwapi watu usalama. Katika Taabu Kuu iliyotokea ulimwenguni: nusu-karne iliyopita, banki nyingi sana zilifungwa, wenye pesa wakapata hasara kubwa sana. Naye mtu mmoja anayeshughulika na uwekevu wa pesa alisema hivi: karibuni: “Banki . . . zimeendelea kuharibika tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Pili.” Vilevile, ubora wa pesa umemalizwa na kupanda kwa bei za vitu, kama jiwe la barafu linavyomalizwa na jua. Wakati wote ambao pesa zimekuwako, zimeleta jambo moja tu: wasiwasi.
14. Kwa sababu gani haifai kupenda pesa? (Mt. 19:21)
14 Kwa hiyo, ingawa pesa zinahitajiwa na zina faida sasa, ni upumbavu kuzitumaini. Hata wakuu wakijaribu sana kutengeneza taratibu za pesa, karibuni zote zitakwisha milele. Kama ilivyotukia zamani, siku itafika karibuni ambayo “watatupa fedha yao katika njia kuu za mji, na dhahabu yao itakuwa kama kitu cha unajisi; fedha yao na dhahabu yao hazitaweza kuwaokoa siku ya ghadhabu ya [Yehova].” (Eze. 7:19) Kwa hiyo, Neno la Mungu linatutolea shauri hili lenye hekima: “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo.” Kwa sababu ya kutokutii shauri hilo na kuendelea kupenda pesa, “wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.” (Ebr. 13:5; 1 Tim. 6:10) Kwa hiyo, mtu anaacha kutafuta faida za ufalme wa Mungu kwa sababu ya kupenda pesa, kisha anapata “maumivu mengi” kwa sababu anazipata na kuzitunza akiisha kufanya kazi nyingi sana.
15. Je! utajiri unatusaidia kupata uzima wa milele? (Zab. 49:16, 17)
15 Pengine matajiri watataka ‘kuishi sikuzote wasilione kaburi,’ wawe na “nyumba zao hata milele,” na kusema ‘mashamba yao yaitwe kwa majina yao.’ (Zab. 49:9, 11) Lakini Mungu ndiye atakayeamua mambo ya wakati ujao. Si pesa, bali ni Yehova atakayeamua ataokoa watu gani au vitu gani katika taabu inayokuja. Katika taratibu yake mpya dunia haitagawanywa kulingana na vile matajiri au wakuu wanaoishi leo wanavyotaka. Yehova atatumia serikali yake ya Ufalme kusimamia mali, kisha watu wake wote watapata faida katika mipaka ya dunia. (Rum. 2:11) Kwa hiyo, shauri hili la Biblia linafaa na ni lenye kuokoa uhai: “Jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi.” (Mt. 6:20) Jambo la maana ni kujiwekea mali nzuri kwa Mungu mbinguni, si kujiwekea pesa nyingi banki.
KUWA BILA WASIWASI
16. Hata nyakati za matatizo ya pesa, Mkristo anaendelea kuwa na maoni gani ya kiasi? (Mt. 6:34)
16 Lakini, leo watu wengi hawatafuti utajiri. Wanataka kupata pesa za kuwatosha tu walipe vitu ambavyo wanatumia. Kuna wasiwasi mwingi kwa sababu matatizo ya pesa yaliyotokea karibuni ulimwenguni pote yamefanya watu wengi waondolewe kazini na kuwa bila malipo. Mtumishi wa Mungu aliye katika hali hiyo amepaswa pia atafute jambo la kufanya. Lakini anapaswa kuwa na kiasi. Anakumbuka kwamba Neno la Mungu linamwambia “tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Mkristo mwenye kiasi anafahamu kwamba “mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mt. 4:4) Kwa hiyo ingawa anajaribu anavyoweza apate kazi ya kumpa mahitaji yake, haiachi imzuie kukutana na Wakristo wenzake kujifunza Neno la Mungu. Wala haiachi imzuie kutumikia watu ambao hawajamjua Yehova wala makusudi yake. Anaweka mbele mambo yaliyo ya maana zaidi yanayohusu Mungu na mapenzi yake.—Flp. 1:10.
17. Mkristo anapata faraja kwa kujua nini, ingawa anapatwa na matatizo ya pesa? (Ebr. 13:5, 6)
17 Mtumishi wa Mungu anayepata matatizo ya pesa yumo katika hali bora zaidi kuliko wale wasiomtumikia Yehova. Anapata faraja kwa sababu Mungu anayetumikia ajua hali yake kuliko yeye mwenyewe, naye anaweza kumtumainia amsaidie wakati wa shida, kama Baba mwenye upendo. Je! kama Mungu hawezi kusaidia watumishi wanaoweka mbele faida zake katika maisha yao, angaliweza kupanga tuwe na mikutano ya kututia nguvu na kuzihubiri habari njema juu ya taratibu mpya inayokuja? Tena, kwa kuwa Mungu mwenyewe asema ‘asiyewatunza walio wake ni mbaya kuliko asiyeamini,’ je! yeye mwenyewe hapaswi kufuata kanuni iyo hiyo? (1 Tim. 5:8) “Kuna udhalimu kwa Mungu? Hasha!” mtume Paulo anasema.—Rum. 9:14.
18, 19. (a) Badala ya kuhuzunika tukifikiria jinsi tutakavyopata hasara ya mali, kwa sababu gani tunapaswa kufurahi kwamba mwisho wa taratibu hii mbovu unakaribia? (b) Kwa hiyo, tutafanya nini wakati huu wa mwisho?
18 Naam, Yehova aliumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kutaka vitu vizuri. Lakini wakati huu wa maana katika vizazi vyote, tunapaswa kuwa na kiasi tunapofikiria mali. Tusiziache zitutawale.. Basi, tunapofikiria “dhiki kubwa” inayokaribia sana, tusiwe kama mkewe Lutu. Tusihuzunike tukifikiria vile tutakavyopoteza mali zetu, kwa maana mawazo hayo mabaya yanaweza kuturusha akili hata tuhatirishe maisha yetu.
19 Badala yake, na tufurahi kwamba mwisho wa taratibu hii mbovu unakaribia. Tunajua kwamba mwisho huo utaliondolea lawama jina la Yehova, na kuokoa watu wanaoitwa kwa jina lake, wanaolitetea kila siku maishani mwao. Kwa sababu ya kushikamana na Yehova, wataingizwa katika taratibu mpya ambamo watakuwa na kazi yenye kupendeza ya kuifanya dunia hii iwe Paradiso, bila maongozi ya Shetani na taratibu yake mbovu, bila utumwa wa dhambi na mauti. (1 Kor. 15:25, 26) Kwa sababu karibuni mambo yatakuwa mazuri sana, lazima watu wote wanaotaka kuendelea kuishi “wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”—1 Tim. 6:17-19.
—Kutoka The Watchtower, April 1, 1977.