Wewe Unaweza Kupataje Usalama wa Kweli?
“Nawe utajifurahisha kwa [Yehova], naye atakupa haja za moyo wako.”—Zab. 37:4.
1. Usalama wa kweli katika mambo yote utapatikana wapi?
TARATIBU mpya ya Mungu itakuwa na usalama kabisa. Unabii wa Mika 4:4 utatimizwa kabisa duniani pote, kwa sababu watu wanaopenda amani “wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.” Naam, “wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zab. 37:11) Ingawa hata leo usalama wa kiroho unaweza kupatikana kwa kiasi kati ya wale wanaomwabudu Yehova, usalama kamili katika pande zote za maisha utapatikana katika taratibu mpya ya Mungu tu. Huo utakuwa wakati mzuri sana, wakati Yehova atakapotumia ufalme wake wa mbinguni alete baraka nyingi za kimwili na usalama usiokwisha, hata maisha ‘yafurahishe sana’ kila siku.
2, 3. Ni baadhi ya faida gani zitakazoletwa na utawala wa Ufalme? (Isa. 32:1, 2)
2 Hakutakuwa tena na watoro wenye kuacha nchi za kwao zinazotawalwa na serikali zenye ukatili na zenye kutumia nguvu. Vijana wala wazee hawataogopa kutenganishwa na vita vyenye kuogofya, kwa sababu “taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Mik. 4:3) Amani itakuwa kila mahali kwa sababu wanadamu wote watabarikiwa na Mkombozi mkuu, ambaye imeandikwa hivi juu yake: “Atawahukumu walioonewa na watu, atawaokoa wahitaji, atamseta mwenye kuonea. . . . Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. Na [atakuwa] na enzi [raia, NW]. . . hata miisho ya dunia.”—Zab. 72:4-8.
3 Usalama huo hautaharibiwa na umaskini, njaa wala ukosefu wa vitu. Neno la Mungu linaahidi kwamba “kutakuwako nafaka tele duniani; juu ya milima kutakuwa na masazo.” (Zab. 72:16, NW) Naam, “mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake.” (Eze. 34:27) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba itakuwa hivyo kwa sababu wakati Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa wa ufalme wa Mungu, alipokuwa duniani alionyesha ana uwezo wa kuwapa watu wengi sana chakula cha kutosha.—Marko 8:19, 20.
JE! UNATAZAMA UPANDE UNAOFAA?
4, 5. (a) Kilicho hatarini leo ni nini? (Linganisha Kumbukumbu la Torati 30:15, 16.) (b) Ni njia gani ya pekee tunavyoweza kupata uzima?
4 Tunapoyafikiria mambo yatakayokuwa katika taratibu mpya ya Mungu, tunavionaje vitu ambavyo watu wa ulimwengu leo wanategemea viwalinde, kama nyumba, pesa zilizo banki, kazi au vitu vinavyowapa starehe? Kwa sababu Yehova aliumba wanadamu wafurahie mambo, je! ni vibaya kuwa na vitu hivyo sasa? Hapana, hatuwezi kusema kwamba vitu hivyo ni vibaya. Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kufurahia vitu vizuri, akilini, moyoni na mwilini. Tena anatuahidi kwamba atatupa vitu vizuri sana katika taratibu yake mpya. Lakini sasa hivi, jambo la maana si kama tuliumbwa tufurahie baraka za kimwili. Leo kilicho hatarini ni maisha yetu wenyewe.
5 Unabii wa Biblia ambao umetimizwa unaonyesha kwamba “siku za mwisho” za taratibu hii mbovu zimeendelea sana. (2 Tim. 3:1-5) Karibuni, Mungu ataleta hukumu kali juu ya taratibu hii, kisha ulimwengu upatwe na dhiki isiyo na kifani. (Dan. 12:1) Hata hivyo, Neno la Mungu linaonyesha kwamba “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” ‘watatoka katika dhiki ile iliyo kuu.’ (Ufu. 7:9, 14) Wataokoka kwa sababu ya kuwa na kibali na ulinzi wa Mungu, si kwa sababu ya mali zo zote walizo nazo. Yesu alisema: “Uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” (Luka 12:15) Njia ya pekee tunavyoweza kupata uzima wa milele katika taratibu mpya ya Mungu ni kumjua Yehova na kupata kibali yake.—Yohana 17:3.
6. Je! sehemu yo yote ya taratibu hii mbovu itatupa usalama? (Zab. 146:3)
6 Hakuna kitu katika ulimwengu huu kitakacholinda watu wakati Mungu atakapozikasirikia taratibu za kibinadamu zilizopo. Tena taratibu zote za kisiasa, za kidini, za kijeshi na za pesa zinazotawala wanadamu sasa zitakwisha. Hazitatoa ulinzi wo wote. (Ufu. 6:16, 17) Kwa hiyo vitu vinavyoonekana kuwa imara na vyenye kulinda watu vitavunjika-vunjika wakati majeshi ya Mungu yatakapoanza kazi ya uharibifu. Nyakati za zamani, watu wengi walitegemea kulindwa na kukimbizwa na farasi wenye nguvu wakati wa matata, Lakini neno la Mungu linasema:’ “Farasi hafai kitu kwa wokovu, wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake.” (Zab. 33:17) Hata leo, watu hawataokolewa na taratibu za kibinadamu zinazoonekana kuwa zenye nguvu, wala mali hazitawaokoa. “Wokovu una [Yehova],” si taratibu yo yote wala cho chote kilichofanywa na wanadamu. “Jina la [Yehova] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.”—Zab. 3:8; Mit. 18:10.
7, 8. Wasafiri wangezionaje mali zilizo katika meli inayozama?
7 Hali ya watu leo inaweza kulinganishwa na hali ya wasafiri walio melini. Vitu ambavyo watu wanapata wanapokuwa melini si vibaya: chakula kilichomo kinaweza kuwa kizuri na kujenga mwili; vibanda vyake vinakuwa na joto zuri na kuwapa watu starehe; watu wanafurahi wanapotumikiwa na kupata faida ya mambo mengine. Lakini inakuwaje meli inapogonga kitu fulani na kuanza kuzama? Kwa mfano, fikiria lililoipata meli “Titanic” yenye sifa mwaka 1912. Encyclopedia moja inasema, “Mafundi walidhani meli hiyo haingeweza kuzama.” Lakini je! meli hiyo “Titanic” pamoja na mali zake zote iliwapa watu usalama wa kweli ilipogonga kilima cha barafu tupu ikazama? Wapi. Watu karibu 1,500 walikufa.
8 Kama wewe ungalikuwa ndani ya “Titanic” hiyo, ungalifanya nini ilipoanza kuzama? Ingawa hapo kwanza usingalidharau mali zilizokuwa melini, bila shaka sasa ungaliziona kuwa ovyo kabisa, sivyo? Jambo la maana ambalo ungalifanya sasa ni kuokoa maisha yako. Ungalimwona mtu kuwa mpumbavu sana, hata pengine udhani ana wazimu, akitumia nguvu zake zote kung’ang’ania vyumba bora vya kulala, vyakula bora, au mali nyinginezo melini, na kumbe baada ya saa chache, vitu vyote hivyo vitazama mawimbini!
9, 10. Kwa sababu ya wakati tunaoishi, inatupasa tuwe na maoni gani juu ya mali? (Flp. 3:7, 8)
9 Karibuni taratibu hii itaingia uharibifuni. Kwa hiyo, haina usalama wo wote wa kweli, kwa sababu haitabakia sehemu yo yote. Ufalme wa Mungu wa mbinguni “utavunja falme hizi zote,” nao peke yake ndio “utasimama milele na milele.” (Dan. 2:44) Na kwa sababu Yesu alitabiri kwamba wakati huo wa hukumu ya Mungu “kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe,” ni wazi kwamba watu wengi sana watakufa, na mali nyingi sana zitaharibiwa.—Mt. 24:21.
10 Mwaka huu wa 1977 ni mwaka wa 63 tangu “wakati wa mwisho” ulipoanza, tukihesabu kutoka vuli ya mwaka wa maana wa 1914. Kulingana na matukio yanayotimiza unabii wa Biblia nyakati zetu, ni wazi kwamba taratibu hii mbovu itamalizwa kabisa. Basi, tutakuwa na maoni gani? Inategemea. Inategemea nini? Inategemea tunachokifanya kiwe lengo letu. Lengo letu likiwa kupata uzima wa milele katika taratibu mpya ya Mungu, tutatumia nguvu zetu zote tumtafute Yehova, tujifunze mapenzi yake. Hatutatafuta sana mali za ulimwengu. Bali, “tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.”—1 Tim. 6:8.
11. (a) Je! matajiri peke yao ndio wanaoweza kupenda mali? (b) Kwa sababu gani ni upumbavu kutafuta mali tu?
11 Yesu alipotoa onyo akasema, “Msijiwekee hazina duniani,” alijua sana kwamba hazina zo zote ambazo zingekuwa katika taratibu hii zingekuwa za muda tu, zisiweze kulinda mtu. (Mt. 6:19) Hakutolea matajiri peke yao shauri hilo; hata maskini wanaweza kutaka sana mali na kuziweka. Malengo ambayo watu wanajiwekea ndiyo yanayoonyesha wazi makusudi yao, hata wawe wana pesa ngapi. Yesu alisema, “Kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.” (Mt. 6:21) Ikiwa nyakati zote mtu anatia bidii azidi kukusanya mali, awe na nyumba kubwa iliyo bora zaidi, pesa nyingi zaidi katika banki, na kazi yenye malipo mengi zaidi, bila kujali matokeo ya kufanya hivyo, anaonyesha wazi anataka vitu vya ulimwengu. Matendo yake yanahakikisha kwamba anafikiria faida za taratibu hii hasa. Lakini mtu huyo haoni mbali, kwa sababu “kila kitu kilichomo katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake—hakitokani na Baba, bali chatokana na ulimwengu. Tena, ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:16, 17, NW.
KUFUNDISHWA NA MATUKIO YA ZAMANI
12. Kosa la watu wa siku za Nuhu lilikuwa nini?
12 Siku zilizokuwa kabla ya gharika, waovu walimdhihaki sana Nuhu na jamaa yake kwa sababu ya kutumia wakati wote wakifanya mapenzi ya Yehova. Bila shaka, ilikuwa lazima wajipatie mahitaji yao ya kila siku na kuwa na mahali pa kukaa, lakini hawakufikiria vitu hivyo nyakati zote. Walimwengu wengine wote walifikiria vitu vya namna hiyo nyakati zote, “wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina.” (Mt. 24:38) Lakini je! kuna ubaya wa kula, au kunywa, au kuoana bila kupita kiasi? Hapana, kwa sababu Yehova mwenyewe ndiye aliyeanza mambo hayo alipoumba mwanamume na mwanamke. Kosa la watu hao lilikuwa kufanya maisha yao yote yategemee mambo hayo, wakakosa kufikiria mapenzi ya Mungu.
13. Je! mali za watu wakati huo ziliwapa usalama? Je! mali za Nuhu zilimpa usalama?
13 Yesu alisema hivi juu ya watu hao: “Wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote.” (Mt. 24:39) Naam, pengine walidhani Nuhu alikuwa “mmashamba” kwa sababu aliacha mali ajenge safina na kuhubiri. Lakini watu hao walipata faida gani kwa kutafuta sana mali na kuwa na anasa? Walipata faida za muda mfupi tu. Walipoteza mali zao na maisha yao, kwa sababu ulimwengu huo uliharibiwa na maji. (2 Pet. 2:5) Vilevile, angalia sana jambo hili: Nuhu pamoja na wanawe na wake zao walipata faida gani katika nyumba zao na mali zao? Hata mali zao hazikuwapa usalama. Usalama ulikuwa safinani. Wao hawakukawia wakati ulipofika wa kuacha nyumba zao. Hawakuwa wakitumaini vitu hivyo viwape usalama, kwa hiyo waliviacha bila ugumu wo wote.—Mwa. 6:22.
14. Watu wote katika Sodoma na Gomora walipata hasara gani, lakini kulikuwa na tofauti gani kati ya Lutu na binti zake? (Luka 9:62)
14 Karne nyingi baadaye, wakati Yehova alipoharibu Sodoma na Gomora kwa sababu ya uovu mwingi sana, je! nyumba na mali zilizokuwa katika miji hiyo zilibaki? Wapi! Wakati Lutu na jamaa yake walipouacha Sodoma, hawakuweza kuchukua vitu vingi. Nyumba yao iliharibiwa pamoja na mali zilizokuwamo. Lakini Lutu na binti zake wawili walijua kwamba maisha yao ndiyo yaliyokuwa ya maana zaidi. Walilifahamu jambo lililohusika. Waliokolewa kwa sababu ya kuyaamini na kuyatii maagizo ya Yehova. Lakini watu wa mji wala mali zao hawakuachiliwa. Kama Yesu alivyosema, siku za Lutu “walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakinunua na kuuza, wakipanda na kujenga; lakini siku ile Lutu aliyotoka Sodoma kulikunya moto na kibiriti kutoka mbinguni vikawaangamiza wote.” Pamoja na nani? Looo, pamoja na mke wa Lutu. Wakati wa kukimbia hakutii, akatazama nyuma alikoacha vitu vyake, akafa.—Mwa. 19:26; Luka 17:28, 29.
15. Kwa sababu gani Yesu alilinganisha siku zetu na za Nuhu na Lutu?
15 Yesu alisema kwamba kama ilivyokuwa siku za Nuhu na za Lutu, ndivyo ingekuwa wakati wa “dhiki kubwa.” Watu wengi duniani hawangetaka habari za Mungu wala mapenzi yake. Kwa hiyo, wangekufa. Sasa, mtu anapokuwa mfu, anaweza kufurahia mali zake ngapi? Hata moja. Lakini wale wanaotaka kuendelea kuishi, wanaomgeukia Mungu awalinde, hawatakufa. Hawatakuwa wamejiacha wanaswe na mambo ya kutafuta mali. Wako tayari kuacha mali zo zote “siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu.” Kwa sababu Yesu alisema: “Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma. Mkumbukeni mkewe Lutu.”—Luka 17:30-32.
16. Je! Wakristo walipata hasara wakati Yerusalemu ulipoharibiwa mwaka 70 W.K.?
16 Ni mali ngapi zitakazoharibiwa katika “dhiki kubwa” inayokuja? Tutajua wakati huo. Lakini katika mifano ya Biblia iliyoonyeshwa sasa hivi, mali nyingi sana ziliharibiwa; hata watu wa Mungu wakapoteza mali zao. Ndivyo ilivyokuwa pia mwaka 70 W.K. wakati majeshi ya Rumi yalipoharibu Yerusalemu. Wakristo walilazimika kuacha nyumba zao mapema, labda wakaenda na vitu vichache tu walivyoweza kuchukua bila ugumu. (Luka 21:20, 21) Ilikuwaje kwa wasiotaka kuondoka? Nyumba zao na mali zao ziliharibiwa na Warumi, na inaonekana walikufa pia. Ingawa Wakristo walioukimbia mji huo walipoteza nyumba zao na mali nyingi, waliokoka wakaendelea kuwa huru. Basi, katika dhiki inayokuja, mali nyingi sana zinaweza kuharibiwa. Wewe ukipoteza mali zako, utaonaje?
17. Kwa sababu gani ni kosa kubwa kutegemea usalama upande usiofaa? (Sef. 1:18)
17 Basi sasa fikiri, unatumaini kitu gani hasa kiwe usalama wako? Je! unatumaini pesa au Mungu? Umeweka wapi akili na moyo wako—juu ya vitu vya taratibu hii au juu ya taratibu mpya ya Mungu? Je! matendo yako na maisha yako yanaonyesha unachotazamia kiwe usalama wako?’Looo, jamani! itakuwa huzuni namna gani kutazamia usalama upande usiofaa katika siku hizi zinazokwisha! Ni kama vile Ayubu 31:24-28 isemavyo: “Ikiwa nimeifanya dhahabu safi, Wewe u tegemeo langu; kama nilifurahi kwa kuwa mali yangu yalikuwa mengi, na kwa sababu mkono wangu umepata vitu vingi; . . . hilo nalo lingekuwa uovu wa kuadhibiwa na waamuzi; kwani ningemwambia uongo Mungu aliye juu.”
18. Wale wanaotegemea usalama katika upande unaofaa wana tumaini gani lenye kufurahisha?
18 Kwa sababu taratibu za kibinadamu zinakaribia sana kuangamia, na mali nyingi sana zinaweza kuharibiwa, ungekuwa upumbavu sana kutoanza kuutazamia uharibifu huo mapema-mapema. Ikiwa unapenda uzima, na unataka kuendelea kuishi, usipende sana kitu cho chote cha kimwili. “Mali hazifaidii kitu siku ya ghadhabu; bali haki huokoa na mauti.” “Azitegemeaye mali zake ataanguka; mwenye haki atasitawi kama jani.” (Mit. 11:4, 28) ‘Wenye haki’ wataingizwa katika taratibu mpya ya Mungu, wafanye kazi yenye kufurahisha ya kufanya dunia nzima iwe Paradiso, makao yenye kupendeza ambamo watafurahia kuishi milele. Kwa sababu watakuwa wamekwisha tegemea upande unaofaa, “watakaa salama salimini, wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Eze. 34:28.
[Picha katika ukurasa wa 396]
Wewe ungetafuta mali zaidi ikiwa meli ulimo ingekuwa ikizama?