Usalama wa Kweli—Sasa na Milele
BILA shaka Yehova Mungu aweza kuandalia watu wake usalama. Yeye ndiye “Mweza Yote.” (Zaburi 68:14, New World Translation) Jina lake la kipekee humaanisha “Yeye Husababisha Iwe.” Hili lamtambulisha kuwa Yule pekee katika ulimwengu wote mzima awezaye kushinda kizuizi chochote ili kutimiza ahadi zake na mapenzi yake. Mungu mwenyewe hutaarifu hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:11.
Mungu huandaa usalama kwa wale wanaomtumaini. Neno lake huhakikisha hilo. “Jina la BWANA ni ngome imara,” akasema Mfalme Sulemani mwenye hekima chini ya upulizio wa kimungu. “Mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Yeye aliendelea kusema hivi: “Amtumainiye BWANA atakuwa salama.”—Mithali 18:10; 29:25.
Usalama kwa Ajili ya Watumishi wa Mungu
Sikuzote Yehova ameandaa usalama kwa wale wanaomtegemea. Kwa kielelezo, nabii Yeremia alipata ulinzi wa Mungu. Wakati majeshi ya Babiloni yalipolizingira Yerusalemu lilioasi imani, ilibidi watu ‘wale mkate kwa kuupima, na kwa kuutunza sana.’ (Ezekieli 4:16) Hali ilikuja kuwa mbaya sana hivi kwamba wanawake fulani waliwachemsha na kuwala watoto wao wenyewe. (Maombolezo 2:20; 4:10) Hata ingawa wakati huo Yeremia alikuwa ametiwa kizuizini kwa sababu ya kuhubiri kwake kusiko na hofu, Yehova alihakikisha kwamba ‘alipewa kila siku mkate mmoja uliotoka katika njia ya waokaji, hata mkate wa mji ulipokwisha.’—Yeremia 37:21.
Yerusalemu lilipoanguka kwa Wababiloni, Yeremia hakuuawa wala kupelekwa Babiloni akiwa mfungwa. Badala ya hivyo, “amiri [Mbabiloni] wa askari walinzi akampa vyakula na zawadi, akamwacha aende zake.”—Yeremia 40:5.
Karne nyingi baadaye Yesu Kristo aliwahakikishia watumishi wa Mungu hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mathayo 6:31-33.
Je, hili lamaanisha kwamba watumishi wa Yehova watapata ulinzi wa kimungu kutokana na misiba yote ya siku hizi? La, halimaanishi hivyo. Waaminifu hawana kinga kamili dhidi ya madhara. Wakristo wa kweli huwa wagonjwa, hupatwa na mnyanyaso, hupatwa na uhalifu, hufa katika aksidenti, na kuteseka kwa njia nyinginezo.
Ingawa Yehova bado haandai usalama kamili kutokana na madhara, ripoti huonyesha kwamba yeye hutumia uwezo wake kuwaandalia watumishi wake na kuwalinda. Wakristo wanakingwa pia kutokana na matatizo mengi kwa sababu wanatumia kanuni za Biblia katika maisha zao. (Mithali 22:3) Na zaidi, wao hufurahia usalama wa ushirika wa ulimwenguni pote wa ndugu na dada wa kiroho wenye upendo, ambao husaidiana katika nyakati za uhitaji. (Yohana 13:34, 35; Warumi 8:28) Kwa kielelezo, kwa kuitikia janga baya la ndugu zao katika Rwanda yenye kukumbwa na vita, Mashahidi wa Yehova katika Ulaya kwa haraka walichanga na kuwapelekea tani 65 za nguo na vilevile dawa, chakula, na ugavi mwingine wenye kugharimu dola bilioni 1,600,000.—Linganisha Matendo 11:28, 29.
Ingawa Yehova huruhusu majaribu yawapate Wakristo wa kweli, wao wana uhakika kwamba yeye atawapa nguvu, usaidizi, na hekima ya kuvumilia. Akiandikia waamini wenzake, mtume Paulo alisema hivi: “Hakuna kishawishi [jaribu] ambacho kimewachukua isipokuwa lililo kawaida kwa wanadamu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mshawishwe [mjaribiwe] kupita kile mwezacho kustahimili, lakini pamoja na kishawishi [jaribu] yeye pia atafanya njia ya kutokea ili nyinyi mweze kukivumilia.”—1 Wakorintho 10:13; The Emphatic Diaglott.
Kile Ambacho Mungu Huwafanyia Watu Wake
Leo, mamilioni ya watu hufurahia kufanya mapenzi ya Mungu. Hawalazimishwi kumtumikia Mungu; wao hufanya hivyo kwa sababu wanamjua na kumpenda. Na kwa sababu Yehova huwapenda watumishi wake waaminifu-washikamanifu, yeye hukusudia kugeuza dunia kuwa paradiso ambamo wanadamu watiifu watafurahia amani, afya, na usalama milele.—Luka 23:43.
Mungu atafanya hili kupitia serikali ya kimbingu, ikiwa na Mfalme wake aliyewekwa rasmi Yesu Kristo, akiwa Mtawala wayo. (Danieli 7:13, 14) Biblia huirejezea serikali hii kuwa “ufalme wa Mungu” na pia “ufalme wa mbinguni.” (1 Wakorintho 15:50; Mathayo 13:44) Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu. Badala ya kuwa na serikali nyingi duniani, kutakuwa na serikali moja tu. Hiyo itatawala kwa uadilifu juu ya dunia yote.—Zaburi 72:7, 8; Danieli 2:44.
Yehova atolea wote mwaliko wa kuishi chini ya huo Ufalme. Njia moja anayofanya hivyo ni kupitia kusambaza sana Biblia, kitabu kinachoeleza kile Ufalme utafanyia jamii ya kibinadamu. Biblia ndiyo kitabu kilichoenezwa zaidi kuliko vyote ulimwenguni, nayo yapatikana sasa, ikiwa nzima au kwa sehemu, katika zaidi ya lugha 2,000.
Yehova Mungu kwa upendo husaidia watu kufahamu kile inachofundisha Biblia kuhusu Ufalme. Yeye hufanya hivyo kwa kuagiza na kutuma watu ili waeleze wengine juu ya Maandiko. Zaidi ya Mashahidi wa Yehova milioni tano sasa wanapiga mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu katika mabara zaidi ya 230.
Usalama wa Kweli kwa Wote?
Je, kila mtu atakubali mwaliko wa kuja kuwa raia wa Ufalme wa Mungu kwa kujipatanisha na viwango vyake vyenye uadilifu? La, kwa sababu watu wengi hawapendezwi na kufanya mapenzi ya Mungu. Wao hukataa jitihada za kuwasaidia kuboresha maisha zao. Kwa kweli, wao hujionyesha wenyewe kuwa kama wale ambao kuwahusu Yesu alisema hivi: “Mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema, na macho yao wameyafumba; wasije wakaona kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaelewa kwa mioyo yao, wakaongoka, nikawaponya [Mungu akawaponya].”—Mathayo 13:15.
Usalama wa kweli wawezaje kuwapo duniani miongoni mwa wale ambao hukataa kuishi kupatana na njia adilifu za Mungu? Hauwezi. Watu wasiomcha Mungu hutisha usalama wa wale wanaotaka kumtumikia Yehova.
Mungu halazimishi watu wabadilike, lakini hata hivyo hatavumilia uovu hadi wakati usio dhahiri. Ingawa Yehova kwa subira huendelea kutuma Mashahidi wake kufundisha watu kuhusu njia na makusudi yake, yeye hataendelea kufanya hivyo zaidi. Yesu Kristo alitabiri hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.
“Mwisho” utamaanisha nini kwa wale wanaokataa viwango vya Mungu? Utamaanisha kupata kwao hukumu ya adhabu na uharibifu. Biblia husema juu ya ‘kulipizwa kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu; watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele.’—2 Wathesalonike 1:6-9.
Hatimaye—Usalama wa Kweli Milele!
Kufuatia uharibifu wa wale wanaokataa njia za Yehova za amani, Ufalme wa Mungu utaleta enzi tukufu ya usalama kwa manufaa ya waadilifu walio duniani. (Zaburi 37:10, 11) Ulimwengu huo mpya utakuwa tofauti kama nini na ule tunamoishi leo!—2 Petro 3:13.
Ukosefu wa chakula na njaa hazitakuwapo tena. Kila mtu atakuwa na kingi cha kula. Biblia husema kwamba “mataifa yote [watafurahia] karamu ya vitu vinono.” (Isaya 25:6) Hakutakuwa na upungufu wa chakula, kwa kuwa ‘kutakuwa na wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.’—Zaburi 72:16.
Watu hawataishi tena katika mabanda na mitaa ya hali ya chini. Chini ya Ufalme wa Mungu, wote watakuwa na nyumba bora zaidi, nao watakula chakula kilichokuzwa kwenye mashamba yao wenyewe. Biblia huahidi hivi: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake.”—Isaya 65:21.
Badala ya ukosefu wa kazi ya kuajiriwa ulioenea sana, kutakuwa na kazi zenye matokeo, nao watu wataona matokeo mazuri kutokana nazo. Neno la Mungu husema hivi: “Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:22, 23.
Chini ya utawala wa Ufalme, watu hawatateseka na kufa kutokana na maradhi. Neno la Mungu latuhakikishia: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
Katika Paradiso ya kidunia ambayo karibuni itakuwa uhalisi, kuteseka na maumivu, huzuni na kifo, zitamalizwa. Ndiyo, hata kifo! Watu wataishi milele katika Paradiso! Biblia hutuambia kwamba Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.
Chini ya utawala wa Yesu Kristo, “Mwana Mfalme wa Amani,” maisha duniani hatimaye yatakuwa salama kikweli. Kwelikweli, usalama wa ulimwenguni pote utakuwapo chini ya utawala wa serikali moja yenye upendo, na uadilifu—Ufalme wa Mungu.—Isaya 9:6, 7, NW; Ufunuo 7:9, 17.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
“Usalama wa binadamu huonyesha uhakika juu ya kesho, . . . [uhakika katika] uthabiti wa hali ya kisiasa na kiuchumi.”—Mwanamke fulani anayeishi Asia
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Kikufanyacho uhisi huna usalama zaidi ya kila kitu ni jeuri na uasi.”—Mwanamume fulani anayeishi Amerika Kusini
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Sikuhisi nikiwa salama wakati wa . . . shambulizi. Nchi ikiwa vitani, watu wanawezaje kuhisi usalama?”—Mwanafunzi wa shule ya msingi katika Mashariki ya Kati
[Blabu katika ukurasa wa 7]
“Nitahisi nikiwa salama wakati nitakapojua kwamba naweza kutembea barabarani usiku bila kulalwa kinguvu.”—Msichana wa shule katika Afrika