Ni Aina Gani ya Usalama Unaotamani?
WATU tofauti wana mawazo tofauti kuhusu usalama. Wengine huuona kuwa amani kati ya serikali zenye uwezo wa kijeshi zinazopingana. Kwa mfano, zile serikali zinazoongoza hali ya ulimwengu zikiwa pamoja na nchi za Ulaya zilizojiunga nazo, zimekubali kuchukua hatua nyingi za kupunguza hatari za aksidenti ndogo ndogo ili zisienee kuwa vita ya nyukilia ya ulimwenguni pote. Stockholm International Peace Research Institute Yearbook 1990 huonyesha mshangao juu ya kutopendezwa na hatua za jinsi hiyo kwa mataifa “katika sehemu nyinginezo za ulimwengu.”
Hata hivyo, kwa mamilioni wanaoishi katika nchi maskini, “usalama” humaanisha chakula na utunzi wa kiafya. “Tunapofikiria ‘amani na usalama,’” aeleza mwanasayansi wa siasa Yash Tandon, “mawazo ya ujumla ya utamaduni mkuu wa Magharibi huenea. . . . ‘Usalama’ huonwa kuwa habari ya silaha na upunguzi wa silaha, tofauti na mahangaiko ya usalama ya wale wasio na chakula na makao ambao ni theluthi mbili ya idadi ya watu ulimwenguni.”
Kwa habari ya Biblia, hiyo huahidi kwamba chini ya Ufalme wa Mungu hakutakuwako vita tena. “Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.” (Zaburi 46:9; Isaya 2:4) Ugonjwa wa kimwili utakuwa jambo la wakati uliopita. “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.”—Isaya 33:24.
Chini ya Ufalme huo, ukosefu wa usalama wa kiuchumi hautatisha mtu yeyote tena. “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.”—Isaya 65:21, 22.
Lakini, lenye maana zaidi, Ufalme huo utaondolea mbali kisababishi cha msingi cha ukosefu wa amani na usalama. Ni nani ambaye amesababisha historia ndefu ya mwanadamu ya serikali zisizofanikiwa na zenye uonevu? Ingawa Mungu, kwa sababu nzuri, ameziruhusu kuwako, yule ambaye ni lazima atoe hesabu ni Shetani, kwa kuwa Biblia husema kwamba ‘ulimwengu mzima uko katika uwezo wake.’—1 Yohana 5:19.
Ni kitulizo kama nini basi, wakati chini ya Ufalme wa Mungu, maneno ya Paulo kwa Warumi yatakapotimizwa hatimaye: “Naye Mungu wa amani atamseta Shetani chini ya miguu yenu upesi”! (Warumi 16:20) Ni Ufalme wa Mungu wa kimbingu tu, chini ya Mfalme Yesu Kristo, ambao ungeweza kutimiza jambo kama hilo. Kwa hiyo, ni chini ya Ufalme huo tu kwamba dunia itageuzwa kuwa paradiso.—Mwanzo 1:28; Luka 23:43.
Naam, usalama ulioahidiwa katika Biblia ni wa hali ya juu zaidi na wenye kuenea zaidi ya jambo lolote lililobuniwa na mwanadamu. Kwani, twasoma kwamba “mauti haitakuwapo; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena”! (Ufunuo 21:4) Je! twaweza kuamini ahadi kama hizo? Ndiyo, kwa sababu zinatokana na Muumba mweza yote, Yehova Mungu, atangazaye rasmi pia hivi: “Neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure bali litatimiza mapenzi yangu, nalo [hakika, NW] litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isaya 55:11) Mafanikio ya hakika yanaonekana katika hatua ambazo Yehova Mungu anachukua sasa kuletea ainabinadamu amani, usalama na ufanisi wenye kudumu na wenye kufurahisha katika utetezi wa enzi kuu Yake ya milele.